Riwaya: Pumbazo

Riwaya: Pumbazo

Daah Rama anatia huruma,ngoja tuone itaendeleaje,. uko vizuri ndugu Ben R Mtobwa
nashukuru mkuu ila level za Ben Mtobwa ni kubwa mno bado hatujafika level zile mkuu
 
SEHEMU YA 8

mikumi, Tanzania

Baada ya kilio cha dakika kadhaa nilinyanyau macho
yangu na kumtazama Nasra.
“Dada Nasra, mke na mtoto wangu wakiuwawa na
damu yao iwe juu yako…. Sijawahi kuua… sijawahi
hata kufikiria juu ya hilo umeamua kunishtaki kuwa
mimi ni muuaji wa pacha wako? Ukweli wangu kwako
umenilipa haya? Kwanini lakini… eeh kwanini Nasra…
ni kweli nastahili haya…. Nitazame ngozi yangu…
nimechapwa mijeledi nimeliwa na mbu wenye dhiki kuu
ya damu… nimeishi maisha ya hofu. Lakini sikumuua
wala kumjeruhi dada yako… nilimwokoa…” hapo sasa
sikuweza kuendelea kuzungumza nikajikuta katika
kilio tena.
Ule mwonekano wa chuki ukageuka kuwa wa huruma
na hapo akanifikia akanishika mkono tukaondoka.
Huu ulikuwa mwanzo wa safari ndefu ambayo
sikuitarajia kamwe.

MSIMULIZI ANAINGIA.

MAMA JOSE aligutuka kutoka usingizini majira ya saa
nane na nusu.
Usiku wa maneno, hii ni baada ya Jose kuanza kulia.
Mama Jose akakumbuka kuwa Jose hakunyonya vizuri
siku hiyo basi pasi na shaka kile kilio kilikuwa cha
njaa.
Mama Jose akakurupuka na kumkwapua mwanaye wa
pekee huku akitokwa na maneno ya huruma topka kwa
mama kwenda kwa mwana!
Jose alipoisikia sauti ya mama lile deko la kitopto
likaongeza kilio chake.
Mama Jose hakuhangaika akampatia ziwa mwana
akaanza kunyonya kwa fujo.
Baada ya muda akasinzia, ni hapo ndipo mama Jose
akagutuka kuwa pale kitandani mumewe waliyelala
pamoja usiku hakuwepo.
Akamlaza Jose wake na kisha kwa kunyemelea
akaanza kwenda sebuleni.
Wazo lake la kwanza akafikiria kuwa Rama atakuwa
sebuleni akazungumza na simu ya siri.
Siri gani zaidi ya kuzungumza na vimada wake?
Mama Jose alijiwazia huku akizidisha umakini katika
mwendo wake wa kunyata.
Alipokaribia sebule upesi akaufungua mlango ili aweze
kumfumania mumewe.
Holaa! Hakuna mtu….
“Baba Jose….. we Rama….” Mama Jose alianza
kuita,badala ya kupata majibu aliisikia sauti yake
mwenyewe ikijenga mwangwi!
Hapo sasa ule wivu ukatimua mbio, nafasi yake
ikachukuliwa na hofu.
Mama Jose akaufikia mlango.
Akajaribu kuufungua akaukuta umefungwa kwa
funguo.
Hilo halikuwa tatizo kwa sababu alikuwa na funguo
zake za ziada.
Hapo sasa akaiendea taa na kuwasha.
Chumba kile kidogo kikaabnza kumtisha, na akili yake
ikamfikiria yule mwanamke aliyenyongwa vibaya sana
na kisha anakuja kuonekana tena katika mfumo wa
pacha.
Sasa Mama Jose alitimua mbio kali kuelekea chumbani
huku akipiga mayowe.
Mayowe yale yakamwamsha Jose akaanza kusaidiana
naye kupiga mayowe.
Mama Jose akamkumbatia mwanaye huku akifanya
sala kwa kurudiarudia.
Hakutoka kitandani hadi jogoo wa kwanza alipowika
huku akiwa bado bandani.
Kumekucha!
Mama Jose alijisemea huku nafsi yake ikiamini kuwa
mumewe amechukuliwa na jini Nasra ama kwa jina
jingine Hajrati.
Mama Jose akamweka mwanaye mgongoni, wakatoka
nje.
Hata kabla hawajazungumza na majirani mara macho
yake kwa mbali yakaona jambo lililompa tafsiri moja
tu.
Mumewe alikuwa hajachukuliwa na jini bali alikuwa
ameenda kwa kimada.
Alimuona kwa mbali akiongozana na msichana.
“Baba Jose ameniolea mke wa pili…. Uuuuwi sikubali
nasema naondoka mimi….” Alijisemea mama Jose huku
akimweka sawa mwanaye mgongoni.
Akatazama kwa makini zaidi, kweli alikuwa baba Jose
na mwanamke ambaye alikuwa hajamtambua bado.
“Heeh! Tena ameenda kuoa wa dini yake…. Eeh! Baba
Jose si ungesubiri mwanao walau akue kidogo
jamani….” Alizidi kuzungumza huku akisononeka.
Alimwona kwa mbali jinsia ya kike akiwa amejitanda
kichwani huku akiwa amemshika mkono mumewe.
Mapigo ya moyo yakamwenda mbio sana, akaanza
kuugulia uke wenza hata kabla hajatambulishwa rasmi
katika uhalali wa ndoa ile.
Mara ghafla, akaanza kupiga hatua nyuma mama huyu
mwenye shahada ya wivu wa kimapenzi!
Hatua moja ikazaa nyingine, mwishowe akajikuta
amegusa ukuta.. akatokwa nay owe la hofu.
Yowe hili likamfikia mumewe, Rama akaachana na yule
mwanamama aliyejitanda…. Akatimua mbio
kumwelekea mkewe.
Alimkuta Mama Jose akiwa katika uoga mkubwa sana,
macho akiwa ameyakodoa, si kumuelekea Rama bali
binti aliyejitanda ambaye alikuwa anakuja hatua moja
baada ya nyingine.
Rama akaufuata uelekeo wa macho ya Mama Jose
akatambua alichokuwa akikihofia. Lakini wakati
huohuo naye alikuwa katika namna ya pumbazo,
aliyakumbuka maneno ya Sajenti Pilipili kuwa mkewe
amekamatwa, lakini sasa anamuona tena!
“Si kitu mama Jose… kuwa mtulivu. Tena mtulivu
haswa…. Kuna jambo la…” kabla hajasema neno
lolote la ziada mara gari ya polisi ikafunga breki kwa
fujo nyumbani kwake. Wakashuka maaskari
wasiopungua sita…. Hawakusema neno bali
waliwavamia mama na baba Jose, wakamsukuma kando
Rama, akapepesuka na kutua chini kama gunia.
Wakamtwaa mama Jose na Jose akiwa analia katika
mgongo wa mama yake.
Wakamwingiza katika karandinga kisha kama
walivyoingia kwa fujo, wakaondoka hivyohivyo!
Huu ikawa ushuhuda wa kwanza kabisa katika safari
ya Ramadhani!
Mkewe na mtoto walikuwa wametoweka!
Hakujua kilichokuwa kinaendelea…..
Akabaki mkiwa huku akitakiwa kufanya awezavyo
kuhakikisha anamtambua Vonso ilimradi tu aweze tena
kuungana na familia yake.
Kwa sababu Rama aliwahi kuwa polisi kabla, alitambua
wazi kile kilichotokea pale kuwa ni kitisho cha awali ili
atambue wazi kuwa mkewe na mwanaye wapo
matatani na ili kurejesha amani hana budi kupambana.
Hapo akamgeukia Nasra!
“Vonso ni nani kwani?” alimuuliza kiutulivu kabisa
huku akijaribu kuidhibiti ile hali yake ya kutetemeka
kutokana na hofu.
“Ni mimi natakiwa kukuuliza wewe kaka… na sio wewe
kuniuliza mimi?” alijibu kwa ukali kiasi fulani.
Rama hakusema neno badala yake akamkaribisha
ndani.
Alizungumza naye mengi sana akilielezea upya tukio la
kukutana na Hajrati na kisha kuzipata taarifa za kifo
chake kwa kushtukiza.
Na hapa ndipo Nasra alipoinamisha kichwa chake kisha
akakinyanyua na kumtazama Rama machoni moja kwa
moja na kumwelezea jambo ambalo lilizidi kuisogeza
safari yao mbele.
ILIKUWA MNAMO MWAKA 1997, ikiwa ni miaka kadhaa
tangu uchaguzi wa kwanzqa kabisa nchini Tanzania
unaohusisha vyama vingi ulipofanyika.
Pia ile ruksa iliyoasisiwa na mzee Mwinyi ikizidi
kuchukua nafasui yake.
Mwanamama Hadija, mama wa watoto wane alikuwa
amenuia kufanya jambo kwa ajili ya familia yake.
Uzito kimajukumu ulikuwa umemzidi… akawaweka
chini watoto wake japokuwa walikuwa wadogo
akawakabidhi kwa dada yake yaani mama yao mkubwa
na kuaga kuwa anakwenda kufabnya kazi mahali na
atakuwa akiwatumia pesa za matumizi…….
Akawaaga wanawe kwa kuwakumbatia huku akimsihi
dada yake awatunze wanawe kama ambavyo angeweza
kuwatunza watoto wake wa kuwazaa japokuwa
hakuwahi kubarikiwa kupata watoto.
Hadija akawakumbatia kwa mara ya pili watoto wake
wadogo ambao walikuwa pacha, akawaasa wapendane
kwa dhati.
Watoto hawa hawakuelewa lolote lakini huu ulikuwa
mwisho wa kumuona mama yao ambaye katika ukubwa
wao wanaambiwa kuwa alienda nchi za ugenini kufanya
kazi za ndani.
Historia hii ikawa haina uhakika sana ikaenda kushoto
ikarudi kulia kisha kushoto tena ikapinduka na kupotea
katika kumbukumbu zao.
Walichoamini ni kwamba waliwahi kuwa na mama kwa
kutazama picha chache za mama yao alizowahi kupiga
enzi za uhai wake.
Ikawa mwaka na hatimaye miaka mapacha wale hata
kabla ya kufikia makamo ya kuitwa wasichana
wakaanza majukumu ya kufanya kazi kama wasichana,
kazi gani nyingine wangefanya zaidi ya kazi za ndani?
Hawakuiwa na elimu walau ya darasa moja!
Wakatumbukia katika ajira hii kwa ajili ya kumsaidia
mama yao mkubwa ambaye alikuwa anasumbuliwa na
kansa ya matiti akiwa kitandani hajiwezi.
Kansa ambayo ilisababisha mgawanyo, wale watoto
wane kila mmoja akichukuliwa na ndugu ambaye
angeweza kumsaidia.
Mama mkubwa akabaki na pacha mmoja aliyeitwa
Hajrati.
Na alikuwa ni Hajrati aliyemletea mama yake mkubwa
jambo ambalo alihitaji ushauri wa kina.
Hajrati alikuwa amekutana na kijana nadhifu ambaye
alimweleza kuwa kuna kazi amempatia inalipa kwa
kiasi kikubwa sana.
Mama mkubwa akashindwa kukubali kirahisi hadi
alipomwomba Hajrati akutanishwe na huyo kijana.
Kweli kijana akafika akiwa nadhifu vilevile na maneno
yaliyonyooka vyema katika kinywa chake, maneno
matamu ya kuvutia haswa.
Ushawishi ukachukua nafasi hatimaye mipango ikaanza
kufanyika, kijana yule mwema alisema kuwa yeye ni
mwakilishi kutoka kampuni inayohusika na mambo ya
ajira inaenda kwa jina la VONSO ALMEIDA & CO.
Limited. Jina ambalo Hajrat alilikariri kwa sababu ya
kulisema kila siku akiwa anamshawishi mama yake
mkubwa.
Ikapatikana hati ya kusafiria na mambo yote stahiki,
Hajrati akiwaza kupanda ndege na kwenda kufanya
kazi yenye kuingiza kipato kikubwa.
Siku moja kabla hajaondoka alienda kumwaga pacha
wake…… alimkumbatia na kumpa ahadi kedekede.
“Nakupenda Nasra! Nitakutumia nauli na wewe uje
nitakapokuwa…” Hajrati alimwambia pacha wake wa
kufanana.
“Usijali Nasra nawe nitakutafutia kazi sawa…Vonso
anahitaji wafanyakazi wengi ila kwa hatua ya awali
ngoja aende mwenzako” ilisikika sauti ya kijana yule
nadhifu.
Na ule ukawa mwisho wa Nasra kuonana na Hajrati
hadi siku ile alipokuja kufananishwa katika daladala na
hatimaye kufikia hatua ya kushuhudia maiti ya pacha
wake katika namna ya kutisha sana.
Kesi ikamuangukia Rama na sasa Nasra anatakiwa
kushirikiana naye ili waweze kutatua jawabu.
Jawabu juu ya Hajrati aliyetoweka miaka saba
iliyopita na kisha kurejea kimyakimya na kushuhudiwa
akiwa maiti!
Zaidi ya yote jawabu juu ya Vonso na kampuni yake.
 
SEHEMU YA TISA

RAMADHANI alikumbuka kuiwasha simu yake masaa
kadhaa baada ya kuwa amerejea nyumbani akitokea
mahabusu katika namna asizoweza kuzielezea , punde
baada ya kuiwasha alikumbana na ujumbe kutoka
katika nambari mpya lakini iliyoanza kwa
kujitambulisha.
Ulikuwa ni ujumbe kutoka kwa Sajenti Pilipili.
Ujumbe mfupi kabisa uliomkumbusha kuwa familia yake
inahitaji maarifa yake zaidi kuliko kuchanganyikiwa
kwake.
Ujumbe huu ulimchanganya upya Rama, kitendo cha
kusikia juu ya familia yake kilikuwa ni sawa na kuliona
bomu asilolijua na anatakiwa kulitegua na iwapo
atashindwa katika mbinu zake basi litamlipukia.
Rama akaiweka simu yake kando, akaingia jikoni na
kuandaa maakuli kwa ajili yao wawili yeye na Nasra.
Wakati wanapata chakula, kwa mara nyingine Rama
akamuuliza Nasra juu ya mama yake mkubwa ambaye
alimruhusu Hajrati kwenda kusikojulikana kufanya
kazi na kisha kupotea moja kwa moja.
Nasra akamueleza Rama kuwa mama yake mdogo
alipotea katika mazingira ya kutatanisha na akahisiwa
huenda alikufa katika ajali ya treni iliyotokea Dodoma
na kuua watu wapatao mia nane na ushee.
Rama akachukua kalamu na kuandika kitu katika
kitabu chake kidogo.
Kisha wakaendelea kupata chakula, kimyakimya hadi
kila mmoja aliporidhika.
Rama akaagana na Nasra kwa makubaliano ya
kukutana siku inayofuata.
Nasra alipoondoka Rama hakubaki kichwa wazi asiwe
na la kufanya, alikuwa ameingia kazini rasmi.
Akamfuatilia binti yule nyendo zake.

RAMA ANASIMULIA.

UCHUNGU wa mwana hakika aujuaye mzazi, lakini
uchungu wa mwana jumlisha na ule wa mke
unapowekwa pamoja hakika nyongo ya mamba ina
utamu wake.
Tafakuri tupu isingeweza kuwa mbadala wa tatizo
langu, nilitakiwa kuamua... na ipo hivyo katika maisha
ukihitaji kufikia kilele cha mafanikio katika jambo
fulani basi huna budi kunyanyua mguu wako na kupiga
hatua mbele.
Nilijkua kuwa jambo hili haliwezi kuwa jepesi hata
kidogo na nilitambua kuwa serikali yetu isokuwa na
dogo haitakuwa na msalia mtume ikiwa sitapambana
mimi kuusaka ukweli.
Labda ungeweza kunishauri kwa wakati huo niende
mahali kushtaki kuwa sijatendewa haki, lakini ni yupi
namshtaki haswa wakati ile kesi ya mauaji nilikuwa
naimiliki mimi?
Nikaona ni heri nijaribu kuliko kuketi na kusubiri
muujiza.
Nilimfuatilia Nasra na kupafahamu nyumbani
kwake.....
Hiyo ilikuwa siku ya kwanza, sikutaka kujua la ziada
kwa siku ile....
Sikurejea nyumbani mapema, badala yake nilielekea
katika ofisi inayohusika na kusajiri makampuni. Lengo
langu ni kujua juu ya hiyo kampuni ambayo Hajrati
aliwahi kufanya kazi na hatimaye kupotea kwa miaka
kadhaa na kisha kurejea na kukumbwa na umauti.
Nia yangu kuu ni kumjua mkurugenzi ambaye
angenisaidia kujua kampuni ile inahusika na mambo
yapi.
Niliafikiana na wazo langu lile ambalo nililiona kuwa ni
sahihi na ambalo lingenipa mwanga, hatua ya kumjua
tu ambaye anamiliki kampuni ile kwangu ingekuwa
hatua kubwa ya awali.
Kweli nikafika na kuulizia juu ya kampuni ile huku
nikijifanya kuwa nahitaji kusajili kampuni ya jina lile
ikiwa hamna ambaye amewahi kusajili kwa jina lile.
"Kwanini unahitaji kusajili kwa jina hili?" yule bwana
alinitazama kivivu vivu huku akiwa anaendelea
kupekua jina hilo katika kompyuta yake.
"Ni muunganiko wa majina ya wenzangu
tunaoshirikiana.." nilibumba uongo upesi.
Hakujibu kitu... baada ya muda akanieleza kuwa jina
lile halijawahi kutumiwa na mtu yeyote yule hivyo
kama nahitaji kulitumia nifuate taratibu za kusajili
kampuni kisheria.
Majibu yake yalinifanya nikaishiwa nguvu!!
Hajrati alipewa ajira na kampuni ya VONSO ALMEIDA.
CO. LTD halafu leo hii naambiwa kuwa hakuna kampuni
kama ile imewahi kutokea nchini?
Nikamuaga yule bwana na kumweleza kuwa nitarejea
tena nikiwa tayari.
"Una uhakika unahitaji kusajili kampuni kijana?"
alinihoji nikiwa nimesimama nataka kutoka.
Sikuelewa maana ya swali lake, nikatikisa kichwa
kukubali.
"Haya karibu tena sisi tupo kuwahudumia watu kama
wewe."
Nilitoweka nikiwa mnyonge sana, pahali nilipotegemea
kuwa patanipa mwanga mpya pameniingiza katika giza
nene. Kipi kingine ningefanya zaidi ya kurejea
nyumbani kulala niwaze na kuwazua upya?
Nilitembea kwa mwendo mfupi kiasi fulani kabla
sijafika kituoni.
Kama ilivyo kawaida ya jiji la Dar es salaam. Magari ni
mengi lakini watu ni wengi zaidi hivyo vurugu za
kuwania magari huwa haziishi kirahisi.
Nilisubiri likapita gari la kwanza, waliowania
wakawania mi nikawa mtulivu, likapita la pili likiwa
limejaa sana hili sikujishughulisha nalo kabisa.
Nikiwa bado nimesimama pale mara akafika mpiga debe
akilinadi gari aina ya Noah ambalo linapakia kwa bei
mara mbili ya ile ya daladala za kawaida.
Maneno yake ya ushawishi yakanivuta, nikaona ni heri
hasara lakini nisafiri kwa raha.
Nikaufuata uelekeo wa mkono wake, nikaingia katika
Noah.
Walikuwemo abiria wawili, mke na mume. Nikaingia
kimyakimya bila kuwajulia hali.
Mara akafika yule mpigadebe, akaingia na kuufunga
mlango!
Kisha gari likaondoka kwa kasi sana, nikabaki katika
pumbazo nikijiuliza inawezekana vipi gari linaondoka
bila abiria?
Niliwatazama abiria wenzangu ikiwa walikuwa katika
mshangao lakini wao walikuwa na maongezi yao
mengine kabisa jambo hili halikuwagusa kabisa.
Gari lilizidi kwenda huku yule bwna niliyemtambua
kama kondakta akiwa hajihusishi kudai nauli yake wala
kunadi lile gari kila kituo. Alikuwa yu mtulivu
haswa.....
Gari lilitembea kwa kasi ileile hadi maeneo ya
Magomeni, hapo likasimama kisha yule mtu mzima
ambaye alikuwa akizungumza na mwanamke pekee
katika lile gari akanitazama. Jicho lake likaniweka
hatiani kuwa wakati naingia ndani ya lile gari hakuna
niliyekuwa nimemsalimia. Nikakurupuka na kumsalimia.
Badala ya kunijibu aliniuliza umri wangu.
"Miaka Thelathini mzee..." nilimjibu kwa adabu zote.
"Wewe bado ni kijana mdogo sana, je una mke na
watoto...." aliniuliza kwa utulivu sana.
Nikamweleza juu ya kuwa na mke na mtoto mmoja.
Jibu hili nililompa lilipita na kinywani huku likiniachia
kumbukumbu kichwani kuwa mke na mwanangu
hawakuwa mikononi mwangu.
"Tumia muda wako mwingi kujali na kuhudumia familia
yako, achana na mambo ya VONSO.... ni mazito kuliko
unavyodhani... achana nayo. Siku hii ya leo huruma
yangu ipo juu yako.... shuka!!" alizungumza maneno
yale na hata aliposema nishuke, mlango ukafunguka
bila kuguswa na mtu yeyote yule. Sikuuliza swali
nikashuka upesi nikiwa nimekodoa macho nisiamini
nilichokuwa nakisikia.
Niliposhuka gari likaondoka kwa mwendo wa kawaida,
nilipolitazama nikagundua kuwa gari lile halikuwa na
namba za usajili.
NILICHOKA!!
 
mzaramo "siku ya leo huruma yangu ipo juu yako vinginevyo ningekufanya kitu kibaya sana,haya lete episodes nyingi zaidi kwa usalama wako".
 
Mzaramo punguza spidii yakuleta episode
Wenzio tushazoea mdomdo..epsd1 baada ya siku tatu na malamiko juu..
 
Dah.... Kama mimi ndo Rama, hapohapo ningeripoti kwa pilipili
 
Au ningeacha cm mle makusudically ili nikiripoti wai track. Naweka silence kabisa
 
SEHEMU YA KUMI

NILITEMBEA hatua kubwa kubwa huku kila mara
nikigeuka nyuma kutazama ikiwa kuna watu ambao
walikuwa wakinifuata.
Lakini baada ya muda nilijikuta najicheka mwenyewe
huku nikijisonya.
"Sasa kama waliweza kunifuatilia hadi kunipandisha
katika gari lao kisha wakaniacha, sasa hivi nakwepa
kitu gani labda..."
Baada ya kubaini udhaifu wangu walioutumia
kunifuatilia, hapo nikarejea katika unyonge wangu wa
awali nikatembea hadi kituo cha daladala, nikakwea
gari kuelekea nyumbani.
Kichwani mwangu nikiwa sina maswali mengi sana,
nilijua wazi kuwa yule afisa wa kusajiri makampuni
alikuwa yu nyuma ya jambo hili kwa asilimia zake.
Lakini kilichoniumiza kichwa ni kwa nini sasa nimepewa
onyo mapema kiasi kile.
Nilijiuliza pia ikiwa wakuu katika idara ya upelelezi
tena chini ya konkodi Sajenti Pilipili waliweza
kufuatilia hili jambo, ina maana nao waliwahi kupewa
onyo kama nilivyopewa mimi?
Na kama waliwahi kupewa onyo, ina maana basi
wameamua kuniugeuza mimi chambo nijipeleke ili
waupime ukali wa Vonso ama?
Fikra hizi zikanifanya niingiwe na hofu.
Nilipogeuka nje kutazama mazingira ili kujisahaulisha
mawazo yaliyokuwa yananikabili nikatanabai ya
kwamba zamani sana nilishapitishwa katika kituo
nilichotakiwa kushukia.
Nikasimama upesi na kujifanya kuwa sijapitishwa
kituo, nikampigia kelele konda anishushe kituo
kinachofuata.
Konda akatii nikashuka na kuanza kutembea kwa
miguu kurejea nyumbani kwangu!!!
Nikiwa barabarani nikapata wazo la kuwasiliana na
Sajenti Pilipili nimueleze bayana kuwa mtihani alionipa
ulikuwa mgumu sana na laiti kama nikiendelea
kuufanya basi utanigharimu maisha yangu.
Nikajaribu kuwasiliana na ile nambari iliyonitumia
ujumbe, iliita kwa muda kisha ikapokelewa.
"Nikusaidie nini?" iliniuliza kikakamavu.
"Mimi ni Ramadhani.... bila shaka nazungumza na
Afande Pilipili..."
"Tazama nambari uliyopiga kwa makini...." alijibu yule
bwana na kunikatia simu.
Nilibaki kuitazama simu ile huku nikichelewa kuiingiza
mfukoni kana kwamba mpigaji angeendelea
kuzungumza, lakini haikuwa hivyo.
Nilitembea hadi nyumbani, nilipofika niliukuta mlango
upo wazi. Nikasita kuingia kwa muda huku nikijaribu
kuvuta kumbukumbu nikifikiria ni nani ambaye
angeweza kuwa katika chumba changu.
Hata kabla sijapata jawabu mara mlango
ukafunguliwa.
Alikuwa ni Nasra!
Macho yake yalionyesha hofu ya waziwazi, akaingia
ndani huku akinipa ishara nimfuate, nikaingia huku
masikio yangu yakitarajia kupokea kitu ambacho
kitanishtua.
Nasra alifungua mkoba wake na kisha akanionyesha
albamu ya picha, sikumuuliza kitu nikaanza kufunua.
Nusu ya macho yangu yakiangalia picha na nusu
nyingine nikimtazama Nasra na jinsi alivyokuwa
anatetemeka kwa hofu, mikono yake ikiwa haijatulia
sehemu moja.
Nilikuwa naziona picha zake mbalimbali, akiwa sehemu
za starehe na watu mbalimbali.
Nikamaliza kuangalia zile picha nikiwa sijaambulia kitu
chochote.
Hapo nikauvunja ukimya nikamuuliza kulikoni.
"Sijaelewa maana yako..." nilimuuliza.
Akanitazama na kujaribu kusema neno, midomo yake
ikitaka kufunguka na kusema neno lakini anashindwa
kutoa kauli yoyote.
"Nasra kwani hizi picha zina nini... nakuona wewe
ukiwa sehemu mbalimbali..."
"Huyo sio mimi... ni Hajrati... nimetumiwa bahasha na
mama yetu mkubwa siku kadhaa nyuma.... na leo
nimeambiwa kuwa amekutwa amekufa kama.... kama
alivyokutwa Hajrati....." alishindwa kuendelea
akaanza kulia, nikamsogelea na kumbembeleza na
kumsihi kuwa huo haukuwa wakati wa kuomboleza.
Baada ya kutulia kidogo akaniambia nifungue zile picha
kwa nyuma..... hapa nikaanza zoezi la kufungua picha
moja baada ya nyingine. Kuna baadhi hazikuandikwa
kitu chochote na nyingine zilikuwa zimeandikwa
maandishi ya kiarabu ama kichina. Sikuweza kuielewa
lugha ile kwa sababu bila kificho japokuwa niliwahi
kusoma Madrasa na kumaliza Juzuu kadhaa lakini
mambo mengi yalikuwa yananichenga katika kusoma
kiarabu.
"Maandishi haya yanamaanisha nini?" nilimuuliza
Nasra.
Akabaki mdomo wazi, akaniuliza ikiwa sijasoma
madrasa.
"Nasra!! huu si wakati wa kuulizana mambo ya
Madrasa nieleze yana maana gani?" nilikuwa mkali
kidogo baada ya kuona anataka kuniumbua.
Nasra akaanza kunitafsiria maneno yale picha kwa
picha.
Zilikuwa ni picha sita.
1. Ewe Mungu uliye hai litazame chozi langu.
2. Ipo siku dunia itajua na mtasaga meno.
3. Ukipata nafasi ya kuyasoma haya nifikishie ujumbe
kwa raisi.
4. Eeh Tanzania yangu damu yenu inateseka huku.
5. Nina mpango wa kutoroka ukiipata picha hii kabla
yangu basi nimeshindwa
6. Nikifa naomba uwe shuhuda
Maneno haya yalizua utata mkubwa sana, yalikosa
muunganiko sahihi, Nasra alichanganyikiwa na mimi
nikibaki katika kuchanganyikiwa vilevile.
Kwa kauli moja mimi na Nasra tukakubaliana kuwa ni
lazima jambo hili tulifikishe kwa Sajenti Pilipili na
kumwomba msaada wake iwapo itawezekana, wakati
huo nikiwa nimemsimulia Nasra jinsi nilivyotekwa na
kuachiwa ndani ya muda mfupi huku nikisindikizwa na
onyo kali.
Tuliondoka wakati uleule kwa kutumia usafiri wa taksi
hadi kituo kile cha polisi.
Hatukumkuta Afande Pilipili, hivyo tulilazimika
kumngoja kwa muda zaidi hadi alipopigiwa simu.
Alipofika nilichukua jukumu la kumueleza kinaga ubaga
kuanzia mwanzo hadi mwisho juu ya kilichojiri kwangu
na kwa Nasra pia.
Afande akasema kuwa anatambua juu ya kifo ambacho
Nasra alikielezea, ilipofikia suala la yale maandishi
hapa sasa Pilipili alitilia maanani zaidi. Akachukua ile
bahasha na kuitazama kwa makini kuliko umakini
alioutumia kusikiliza maana ya maandishi yale ya
kiarabu.
Baada ya kuitazama ile bahasha alinivuta pembeni
kisha akanitazama machoni.
"Afande unarejea kazini kwa kazi moja maalumu.....
sahau kuhusu kesi sahau kuhusu mkeo ni kwa masilahi
ya taifa letu..." akameza mate kisha akanieleza kuwa
alilosema sio ombi bali narejea kazini bila hiari yangu.
"Kesho asubuhi ufike ofisini kwangu kwa ajili ya.....
aahm ukifika utajua... tutazungumza...." alimalizia
kisha akanyanyua simu yake.
"Naomba unichukulie mtuhumiwa wangu hapa mara
moja..." alipotamka maneno yale kwenye simu
nikaingiwa mchecheto nikitambua kuwa ni mimi
natakiwa kuwekwea rumande, sehemu ambayo
sikuitaka tena asilani.
Punde wakafika askari wawili wasiovaa sare,
wakamchukua Nasra na kuondoka naye.
Nikatambua kuwa alikuwa anaenda kuhifadhiwa kwa
sababu ya usalama wake.
Laiti kama ningekuwa sijawahi kupitia maisha ya
uaskari ningeweza kusema kuwa ule ni unyanyasaji wa
hali ya juu, lakini kwa sababu nimewahi kuwa mmoja
wao nilielewa.
Kama alivyowaza kiusahihi Sajenti Pilipili, ilikuwa
hivyo.
Saa tano usiku alinipigia simu na kuniuliza nipo wapi.
Nikamjibu kuwa nipo kitandani lakini si katika nyumba
yangu. Akaelewa ninachomaanisha, akanieleza kuwa
chumba cha Nasra kimevamiwa na kupekuliwa sana na
watu wanaodhaniwa kuwa ni mtandao mkubwa wa huyo
kiumbe ama yeyote ajiitaye Vonso.
"Upo kazini Ramadhan... na si kazi ndogo ni kubwa na
nzito. Kuwa makini sasa kwa kila hatua yako"
alinieleza na kisha bila kuaga akakata simu.
Nikakiri kimoyomoyo kuwa hakika palikuwa na kazi
kubwa. Nikasimama kutoka kitandani kikakamavu
nikapiga saluti.
Ishara kuwa nimerejea kazini upya!!
Baada ya kupiga saluti ile nikajihisi kama nipo imara
na nina utayari mkubwa sana.
Asubuhi kama tulivyoahidiana na Pilipili, nikakutana
naye ofisini.
Nilipofika kwa katibu muhtasi wake na kujitambulisha,
akanipatia vijana wawili wakaniongoza hadi katika
ukumbi mmoja na kuniambia niingie ndani.
Kwa mawazo yangu nilitarajia kukutana na Pilipili peke
yake, hivyo nikitazamia kuzungumza kwa kujiamini
mbele yake kwani nilikuwa nimeanza kumzoea.
Nikaingia mlango ule wa kwanza, nikapokelewa na
askari wawili, wakanisabahi na kisha wakanisihi
niwafuate.
Nilianza kuingiwa nma hofu, maana tabia za Pilipili
nilizitambua wazi, ni jambo la kawaida kukuua ama
kukutesa huku anacheka. Hapa sasa hofu ikanivamia
upya na kijasho chembamba kikanitoka licha ya hewa
safi iliyotawala katika jengo lile.
Askari wale walinifikisha mahali wakafungua mlango
na kunisihi niingie.....
Macho yangu yakatua katika vazi la kipolisi
lililosheheni nyota lukuki, nikatazama kushoto na
penyewe vilevile.
Ama! nilipagawa.
Sikuwahi kuingia katika kikao kikubwa na kizito kiasi
hiki, niliwashuhudia wakuu wa kazi ambao nilikuwa
nikiwaona magazetini pekee bila ndoto ya kuonana nao
hata siku moja.
Mkuu wa jeshi la polisi alikuwa mbele yangu, niliduwaa
lakini sikusahau kupiga saluti baada ya kuingia pale
ndani. Hakuijibu bali alinipungia mkono niketi.
Hapakuwa na muda zaidi wa kupoteza, maongezi
yakachukua nafasi yake.
Alifungua maongezi yale sajenti Pilipili na kisha
akapokelewa na mkuu wa jeshi la polisi.
Yalizungumzwa mengi sana, na kisha mzizi wa
mazungumzo ukaguswa, VONSO!
Mkuu wa jeshi la polisi akaelezea kuwa jina hilo lipo
katika midomo yao kuanzia mwaka 1990 na suluhu
haijawahi kupatikana. Miaka yote mwanga ulikuwa
mbali lakini sasa mwanga umeanza kupatikana kwa
kiasi fulani. Hivyo ni wakati wa kulitafuta jibu la
miaka mingi!
Na jibu hilo nitatakiwa kulitafuta mimi...... bila
kuchelewa.
Nilitamani kukataa wajibu huu lakini hapakuwa na
kifungu walichokitenga kwa ajili ya mimi kujieleza
ikiwa nipo tayari ama la.
Baada ya ya kukabidhiwa jukumu hilo na watu ambao
nitaweza kuwaomba msaada itakapobidi.
ghafla nikatajiwa tarehe yangu ya kusafiri, safari ya
kwenda nje ya bara la Afrika.
Ambapo waliamini kuwa ndipo jibu lilipojificha.
Nilipagawa jinsi mambo yalivyokuwa yanapelekwa
upesiupesi, lakini kitu ambacho sikuweza kufanya kwa
wakati ule ni kupinga. Kumbukumbu ya mke na
mwanangu mikononi mwa jeshi la polisi ilinitesa.
Kichwani nikajiuliza, ni kitu gani cha ajabu wameona
kwangu hadi kunipa jukumu lile?
Binafsi sikujiona na lolote la ziada, badala yake
nikajipatia jibu tena kuwa jamaa wameamua
kunifanya mimi CHAMBO.....
Baada ya siku tatu nilikuwa navuta na kutoa hewa nje
nikiwa nje ya Afrika.. mahali ambapo watu wa rangi
yangu ni wa kutafuta.
Na huko ndipo nilipokutana na balaa jipya, ajabu ni
kwamba hata huku Vonso alikuwepo lakini
hakujulikana!!
Nikaendelea kubaki katika PUMBAZO!
Mara mapenzi nayo yakaingilia kati.........
 
SEHEMU YA 11

Nilipokelewa nchini Oman na mwanamke refu, alikuwa
amejihifadhi ndani ya juba jeusi na uso wake
ukifichwa katika nikabu iliyofanya nishindwe
kumtambua ikiwa alitabasamu wakati wa kunipokea
lakini hilo halikunizuia kumpokea.
“Asalam aleykum Ramadhani, karibu Muscat! Umekuja
wakati sahihi kabisa na jina lako….” Alinikaribisha na
masikio yangu yakiipokea vyema lafudhi yake ile
ambayo huenda ilikuwa ya Zanzibar.
Nikaijibu salamu yake huku nikikumbuka kuwa mwezi
mtukufu wa Ramadhani ulikuwa njiani!
Aliniongoza hadi katika taksi na kumweleza wapi pa
kutupeleka.
Ama! Jiji hili la Muscat nilikuwa nikiliona tu katika
runinga, lakini kwa macho yangu nilikiri kuwa lilikuwa
jiji lenye hekaheka nyingi.
“Naona huku vazi lenu ni moja… ukinipotea nitapata
tabu kukupata…..”
“Asilimia sabini na tano ya wakazi wa hapa ni waumini
wa dini ya kiislamu….. hili nd’o vazi letu sahihi.”
Alinijibu na kwa hisia nikahisi alikuwa anatabasamu
wakati anazungumza maneno yale.
“Inakuwaje juu ya wanaume kuchagua mabibi zao
sasa… maana nyote mnafanana?” Nilimuuliza na hapa
nikakisikia kicheko chake.
Aliishia kucheka tu na hakutoa jibu.
Safari yetu iliishia katika hoteli ambayo sikujua kama
ni bei ghali ama la kwa sababu mlipaji sikuwa mimi.
“Nimekuwa katika nchi hii kwa miaka minne sasa…
naamini siku moja nitarejea Zanzibar!” alinieleza
wakati tukiwa mapokezi.
“Rama muhudumu atakupa maelekezo zaidi, mimi
siruhusiwi kuingia chumbani kwako pasi na cheti cha
ndoa.” Aliniambia huku akitoa mkono wake na
kunipatia.
Nikahisi kuna kitu ananiachia nami nikakipokea kana
kwamba hakuna lolote lililotokea kati yetu.
Akaniaga na kuahidi kurejea siku ifuatayo kwa ajili ya
kunipa maelekezo zaidi.
Kwa mara ya kwanza nikaingia katika hoteli kwa ajili
ya kulala nikiwa nje ya bara langu, nje ya nchi yangu
ya Tanzania.
Yule binti akaondoka bila kunipatia hata jina lake.
Kuondoka kwa binti yule ukawa mwisho wa
kuzungumza Kiswahili, sasa nikaanza kuhangaishana
na muhudumu anayezungumza kiingereza kibovu
chenye lafudhi ya kiarabu.
Hatimaye nikamalizana naye na kubaki nikiwa
nimejifungia chumbani.
Nilijaribu kujilaza lakini kichwa kilikuwa kizito sana,
jambo la kufanya upelelezi nisioujua mwanzo wake
katika nchi hii ya kigeni liliniweka katika hofu ya
namna yake. Nikasimama na kukizunguka chumba kile
kikubwa, hadi nilipolifikia dirisha na kutazama kwa
umakini mji huu wa Muscat!
Hakuna nilichoambulia zaidi ya maghorofa marefu ya
kifahari na hekaheka za kutosha zilizoonekana kwa
macho.
“Kama Kariakoo vile!” nilijisemea kwa sauti ya chini,
na neno lile likanifanya niuhisi ukiwa wa kupakosa
Tanzania.
Ama hakika nyumbani ni nyumbani.
Macho yangu yaliendelea kutalii, mara yakalifikia
jengo refu sana, jengo hili liliufanya moyo wangu
ushtuke na kuongeza umakini kulitazama.
Jengo lile halikuwa mara ya kwanza kuonekana katika
macho yangu.
Nikabaki kujiuliza ni wapi nimewahi kuliona?
Dar? Arusha? Mbeya? Mwanza au wapi……
Bado sikupata mfanano wa wapi nimewahi kuliona
lakini akili ilinisihi kuwa nimewahi kuliona jengo lile
kabisa, tena si mara moja!!
Nilijaribu kutuliza kichwa sana ili nipate jawabu lakini
mambo yaliniwia magumu.
Mwishowe nikapuuzia na kujiona najiumiza akili kwa
mambo yasiyokuwa na maana.
Yaani nina jukumu la kuzijua hila za Vonso halafu
natumia akili nyingi kujiuliza ni wapi nimeona jengo
fulani.
Nikiwa katika kupuuza kule walau akili ikapata kitu
cha kukumbuka, nikakumbuka juu ya kile alichoniachia
yule mwanadada asiyekuwa na jina.
Nikaipekua suruali yangu nikautoa ujumbe ule.
Alikuwa ameandika kiarabu!
Ebwana eeh!
Nilichachawa na kuingiwa na hatia ya kutotilia
maanani niliyokuwa nafundishwa madrasa…. Sasa
naumbuka.
Itakuwaje kama ni ujumbe wa hatari ama dharula??
Nilijiuliza na hapo nikajikuta namkumbuka Nasra,
pacha wa marehemu Hajrati mtalamu wa lugha ya
kiarabu.
Nikatamani sana kama angekuwepo anipe tafsiri.
Nikakumbuka kuwa nilipoondoka alikuwa yu mikononi
mwa polisi kwa usalama wake.
“Mungu wangu!” mara nikajikuta napiga kelele na
kisha upesiupesi nikakimbia kuelekea kule dirishani,
nikalitazama tena lile jengo.
Hatimaye, hatimaye nilikumbuka ni wapi niliwahi
kuliona lile jengo.
Nililiona katika zile picha za marehemu Hajrati
zilizoambatana na jumbe mbalimbali za kushangaza na
zisizokuwa na majibu.
“Ina maana Hajrati aliwahi kuishi Muscat?” hili
lilikuwa swali la kwanza lenye uhai katika kile
kilichokuwa kimenipeleka kule.
Jumbe zile na maisha yake ya Muscat zinahusiana vipi?
Ina maana Vonso naye yupo Muscat?? Kama yupo
Muscat na afande Pilipili anajua kuiwa yupo Muscat ni
kwanini ameniagiza mimi nije huku, kwanini
asimkamate??
CHAMBO!!! Nageuzwa chambo……
Nilijisemea huku nafsi ikiingiwa na simanzi sana……
nilitamani sasa kumuuliza afande Sajenti Pilipili juu ya
kwanini mimi nipewe jukumu lile. Lakini
nikatambuakuwa atanikumbusha kuwa jeshini hakuna
kuchagua kazi…..
“Kanuni gandamizi sana hii…” nililalamika.
MASAA niliona hayaendi huku nikiishi na ujumbe hatari
kama ule mkononi mwangu nikiwa sielewi maana yake.
Nikakata shauri nimuulize tu muhudumu wa kile
chumba ili niwe na amani.
Nikachukua simu na kupiga nambari iliyoandikwa kwa
kimombo…. RECEPTION!
Mpokeaji akaanza kuzungumza kihindi ama kiarabu, mi
sijui…. Nikamkatisha kiingereza, akabadili lugha bila
kunitaka radhi.
Nikamweleza kuwa nina shida na ninahitaji kuonana
na muhudumu.
Akakata simu bila kusema lolote.
Baada ya dakika sita ama saba, chumba kikagongwa
akaingia yule muhudumu wa kiume mwenye kiingereza
kibovu.
“Nimeukuta huu ujumbe bafuni, je nimeandikiwa mimi
mteja ama ni wa nani? Napenda kujua maana yake
nikiwa kama mteja wenu…” nikampatia kile
kikaratasi.
Akakisoma kisha akanitazama na kukisoma tena.
“Are you sure?” aliniuliza huku akikisoma tena kwa
mara ya tatu. Nikamtazama kwa ghadhabu huku kwa
sauti ya chini nikitokwa na tusi kwa lugha ya Kiswahili.
Alitaka kuondoka na kile kikaratasi, nikamkwapua na
kumuuliza kwa nini anaondoka kana kwamba ameitatua
shida yangu tayari.
“Si kitu, ni uchafu tu….” Alisema huku nikimwona
kama anayejawa na hofu na asiyekuwa na uhakika na
maneno yake. Na hapo akashika hamsini zake aweze
kuondoka. Akaufungua mlango na kutoka kwa kasi
akiniacha katika taharuki ya aina yake.
Sekunde ishirini badaye nikiwa nimeganda vilevile
katika sintofahamu mara mlango ukafunguliwa kwa
nguvu sana, nikaruka pembeni upesi!
Na pale nilipotoka kikapita kiumbe kwa kasi kubwa na
kutua chini kikijibamiza kitandani.
Nikakitazama kiumbe kile na kutambua kuwa alikuwa
ni yule muhudumu aliyekuja kunihudumia.
Nikiwa sijapata pumzi za kusema neno, akaingia
mwanadada akiwa amevalia suruali na fulana ya
kiume.
Akaingia na kuufunga mlango, kisha upesi akamvamia
yule mtu pale chini na kumyanyua.
“What’s wrong..” niliuliza kwa kujitutumua hatimaye
huku nikitoa katika hatia.
“Huyu fala umempa zawadi gani mbona ametoka nje
anachekelea hivyo?” badala ya kujibu kiingereza
alijibu Kiswahili.
Nikashtuka zaidi.
“Naitwa Zainabu niite Zay B… sikujitambulisha awali
eeh….” Aliendelea kuzungumza.
Na hapa nikaitambua sauti yake ile yenye lafudhi ya
kizenji. Alikuwa ni mwanadada aliyenipokea.
“Nilimwita anitafasirie ulichoniandikia…” nilimjibu.
Akanitazama kwa mshangao mdomo wake ukiwa wazi
kabisa. Akataka kusema neno lakini halikutoka.
“Jeshi la Tanzania ndo linafundisha hivyo siku hizi…
kuamini amini watu hovyo katika jambo zito kama
hili….. ama unadhani umekuja huku kwa jambo la
kitoto. Wenzako kumi na ushee kuanzia mwaka 1990
hakuna anayerudi akiwa hai. Tafadhali sana tusifanye
makosa safari hii….” Alinijibu. Majibu yake yakazidi
kunipagawawisha maana ni kweli sikuwa najua
kilichoniweka kule, zaidi ya kufahamu juu ya jina
Vonso.
“Ningechelewa dakika moja zaidi ungekuwa maiti….”
Alinambia na mara ghafla akaizungusha shingo ya yule
muhudumu ikaelekea upande usokuwa wa kawaida.
Huo ukawa mwisho wa uhai wake……
Tukatoweka kwa njia mbili tofauti, mimi kwa njia ya
kawaida mapokezi, na yeye akiruka dirisha.
Tukakutana mbele ya hoteli ile na kutoweka.
MKASA ukaanzia hapo rasmi!!
Huku mimi bado nikiwa sina mwanga, bali kiza kikizidi
kuchukua nafasi.
 
Alaf tatu tu utakuwa umetupunja sana mkuu,weekend hii mkuu tupe walau kaoffer
 
SEHEMU YA 11

Nilipokelewa nchini Oman na mwanamke refu, alikuwa
amejihifadhi ndani ya juba jeusi na uso wake
ukifichwa katika nikabu iliyofanya nishindwe
kumtambua ikiwa alitabasamu wakati wa kunipokea
lakini hilo halikunizuia kumpokea.
“Asalam aleykum Ramadhani, karibu Muscat! Umekuja
wakati sahihi kabisa na jina lako….” Alinikaribisha na
masikio yangu yakiipokea vyema lafudhi yake ile
ambayo huenda ilikuwa ya Zanzibar.
Nikaijibu salamu yake huku nikikumbuka kuwa mwezi
mtukufu wa Ramadhani ulikuwa njiani!
Aliniongoza hadi katika taksi na kumweleza wapi pa
kutupeleka.
Ama! Jiji hili la Muscat nilikuwa nikiliona tu katika
runinga, lakini kwa macho yangu nilikiri kuwa lilikuwa
jiji lenye hekaheka nyingi.
“Naona huku vazi lenu ni moja… ukinipotea nitapata
tabu kukupata…..”
“Asilimia sabini na tano ya wakazi wa hapa ni waumini
wa dini ya kiislamu….. hili nd’o vazi letu sahihi.”
Alinijibu na kwa hisia nikahisi alikuwa anatabasamu
wakati anazungumza maneno yale.
“Inakuwaje juu ya wanaume kuchagua mabibi zao
sasa… maana nyote mnafanana?” Nilimuuliza na hapa
nikakisikia kicheko chake.
Aliishia kucheka tu na hakutoa jibu.
Safari yetu iliishia katika hoteli ambayo sikujua kama
ni bei ghali ama la kwa sababu mlipaji sikuwa mimi.
“Nimekuwa katika nchi hii kwa miaka minne sasa…
naamini siku moja nitarejea Zanzibar!” alinieleza
wakati tukiwa mapokezi.
“Rama muhudumu atakupa maelekezo zaidi, mimi
siruhusiwi kuingia chumbani kwako pasi na cheti cha
ndoa.” Aliniambia huku akitoa mkono wake na
kunipatia.
Nikahisi kuna kitu ananiachia nami nikakipokea kana
kwamba hakuna lolote lililotokea kati yetu.
Akaniaga na kuahidi kurejea siku ifuatayo kwa ajili ya
kunipa maelekezo zaidi.
Kwa mara ya kwanza nikaingia katika hoteli kwa ajili
ya kulala nikiwa nje ya bara langu, nje ya nchi yangu
ya Tanzania.
Yule binti akaondoka bila kunipatia hata jina lake.
Kuondoka kwa binti yule ukawa mwisho wa
kuzungumza Kiswahili, sasa nikaanza kuhangaishana
na muhudumu anayezungumza kiingereza kibovu
chenye lafudhi ya kiarabu.
Hatimaye nikamalizana naye na kubaki nikiwa
nimejifungia chumbani.
Nilijaribu kujilaza lakini kichwa kilikuwa kizito sana,
jambo la kufanya upelelezi nisioujua mwanzo wake
katika nchi hii ya kigeni liliniweka katika hofu ya
namna yake. Nikasimama na kukizunguka chumba kile
kikubwa, hadi nilipolifikia dirisha na kutazama kwa
umakini mji huu wa Muscat!
Hakuna nilichoambulia zaidi ya maghorofa marefu ya
kifahari na hekaheka za kutosha zilizoonekana kwa
macho.
“Kama Kariakoo vile!” nilijisemea kwa sauti ya chini,
na neno lile likanifanya niuhisi ukiwa wa kupakosa
Tanzania.
Ama hakika nyumbani ni nyumbani.
Macho yangu yaliendelea kutalii, mara yakalifikia
jengo refu sana, jengo hili liliufanya moyo wangu
ushtuke na kuongeza umakini kulitazama.
Jengo lile halikuwa mara ya kwanza kuonekana katika
macho yangu.
Nikabaki kujiuliza ni wapi nimewahi kuliona?
Dar? Arusha? Mbeya? Mwanza au wapi……
Bado sikupata mfanano wa wapi nimewahi kuliona
lakini akili ilinisihi kuwa nimewahi kuliona jengo lile
kabisa, tena si mara moja!!
Nilijaribu kutuliza kichwa sana ili nipate jawabu lakini
mambo yaliniwia magumu.
Mwishowe nikapuuzia na kujiona najiumiza akili kwa
mambo yasiyokuwa na maana.
Yaani nina jukumu la kuzijua hila za Vonso halafu
natumia akili nyingi kujiuliza ni wapi nimeona jengo
fulani.
Nikiwa katika kupuuza kule walau akili ikapata kitu
cha kukumbuka, nikakumbuka juu ya kile alichoniachia
yule mwanadada asiyekuwa na jina.
Nikaipekua suruali yangu nikautoa ujumbe ule.
Alikuwa ameandika kiarabu!
Ebwana eeh!
Nilichachawa na kuingiwa na hatia ya kutotilia
maanani niliyokuwa nafundishwa madrasa…. Sasa
naumbuka.
Itakuwaje kama ni ujumbe wa hatari ama dharula??
Nilijiuliza na hapo nikajikuta namkumbuka Nasra,
pacha wa marehemu Hajrati mtalamu wa lugha ya
kiarabu.
Nikatamani sana kama angekuwepo anipe tafsiri.
Nikakumbuka kuwa nilipoondoka alikuwa yu mikononi
mwa polisi kwa usalama wake.
“Mungu wangu!” mara nikajikuta napiga kelele na
kisha upesiupesi nikakimbia kuelekea kule dirishani,
nikalitazama tena lile jengo.
Hatimaye, hatimaye nilikumbuka ni wapi niliwahi
kuliona lile jengo.
Nililiona katika zile picha za marehemu Hajrati
zilizoambatana na jumbe mbalimbali za kushangaza na
zisizokuwa na majibu.
“Ina maana Hajrati aliwahi kuishi Muscat?” hili
lilikuwa swali la kwanza lenye uhai katika kile
kilichokuwa kimenipeleka kule.
Jumbe zile na maisha yake ya Muscat zinahusiana vipi?
Ina maana Vonso naye yupo Muscat?? Kama yupo
Muscat na afande Pilipili anajua kuiwa yupo Muscat ni
kwanini ameniagiza mimi nije huku, kwanini
asimkamate??
CHAMBO!!! Nageuzwa chambo……
Nilijisemea huku nafsi ikiingiwa na simanzi sana……
nilitamani sasa kumuuliza afande Sajenti Pilipili juu ya
kwanini mimi nipewe jukumu lile. Lakini
nikatambuakuwa atanikumbusha kuwa jeshini hakuna
kuchagua kazi…..
“Kanuni gandamizi sana hii…” nililalamika.
MASAA niliona hayaendi huku nikiishi na ujumbe hatari
kama ule mkononi mwangu nikiwa sielewi maana yake.
Nikakata shauri nimuulize tu muhudumu wa kile
chumba ili niwe na amani.
Nikachukua simu na kupiga nambari iliyoandikwa kwa
kimombo…. RECEPTION!
Mpokeaji akaanza kuzungumza kihindi ama kiarabu, mi
sijui…. Nikamkatisha kiingereza, akabadili lugha bila
kunitaka radhi.
Nikamweleza kuwa nina shida na ninahitaji kuonana
na muhudumu.
Akakata simu bila kusema lolote.
Baada ya dakika sita ama saba, chumba kikagongwa
akaingia yule muhudumu wa kiume mwenye kiingereza
kibovu.
“Nimeukuta huu ujumbe bafuni, je nimeandikiwa mimi
mteja ama ni wa nani? Napenda kujua maana yake
nikiwa kama mteja wenu…” nikampatia kile
kikaratasi.
Akakisoma kisha akanitazama na kukisoma tena.
“Are you sure?” aliniuliza huku akikisoma tena kwa
mara ya tatu. Nikamtazama kwa ghadhabu huku kwa
sauti ya chini nikitokwa na tusi kwa lugha ya Kiswahili.
Alitaka kuondoka na kile kikaratasi, nikamkwapua na
kumuuliza kwa nini anaondoka kana kwamba ameitatua
shida yangu tayari.
“Si kitu, ni uchafu tu….” Alisema huku nikimwona
kama anayejawa na hofu na asiyekuwa na uhakika na
maneno yake. Na hapo akashika hamsini zake aweze
kuondoka. Akaufungua mlango na kutoka kwa kasi
akiniacha katika taharuki ya aina yake.
Sekunde ishirini badaye nikiwa nimeganda vilevile
katika sintofahamu mara mlango ukafunguliwa kwa
nguvu sana, nikaruka pembeni upesi!
Na pale nilipotoka kikapita kiumbe kwa kasi kubwa na
kutua chini kikijibamiza kitandani.
Nikakitazama kiumbe kile na kutambua kuwa alikuwa
ni yule muhudumu aliyekuja kunihudumia.
Nikiwa sijapata pumzi za kusema neno, akaingia
mwanadada akiwa amevalia suruali na fulana ya
kiume.
Akaingia na kuufunga mlango, kisha upesi akamvamia
yule mtu pale chini na kumyanyua.
“What’s wrong..” niliuliza kwa kujitutumua hatimaye
huku nikitoa katika hatia.
“Huyu fala umempa zawadi gani mbona ametoka nje
anachekelea hivyo?” badala ya kujibu kiingereza
alijibu Kiswahili.
Nikashtuka zaidi.
“Naitwa Zainabu niite Zay B… sikujitambulisha awali
eeh….” Aliendelea kuzungumza.
Na hapa nikaitambua sauti yake ile yenye lafudhi ya
kizenji. Alikuwa ni mwanadada aliyenipokea.
“Nilimwita anitafasirie ulichoniandikia…” nilimjibu.
Akanitazama kwa mshangao mdomo wake ukiwa wazi
kabisa. Akataka kusema neno lakini halikutoka.
“Jeshi la Tanzania ndo linafundisha hivyo siku hizi…
kuamini amini watu hovyo katika jambo zito kama
hili….. ama unadhani umekuja huku kwa jambo la
kitoto. Wenzako kumi na ushee kuanzia mwaka 1990
hakuna anayerudi akiwa hai. Tafadhali sana tusifanye
makosa safari hii….” Alinijibu. Majibu yake yakazidi
kunipagawawisha maana ni kweli sikuwa najua
kilichoniweka kule, zaidi ya kufahamu juu ya jina
Vonso.
“Ningechelewa dakika moja zaidi ungekuwa maiti….”
Alinambia na mara ghafla akaizungusha shingo ya yule
muhudumu ikaelekea upande usokuwa wa kawaida.
Huo ukawa mwisho wa uhai wake……
Tukatoweka kwa njia mbili tofauti, mimi kwa njia ya
kawaida mapokezi, na yeye akiruka dirisha.
Tukakutana mbele ya hoteli ile na kutoweka.
MKASA ukaanzia hapo rasmi!!
Huku mimi bado nikiwa sina mwanga, bali kiza kikizidi
kuchukua nafasi.
Utamu unakujaa utamu unakata, iko vizuri sana hii mkuu

Napenda sana riwaya za ujasusi kama hizi keep it up
 
Kuna nyakati hutupitia katika maisha yetu nasi
kuzitafsiri kama mkosi lakini ndani yake zimebeba
maajabu ambayo huwezi kuyatambua ikiwa
hautavumilia kile ulichokiita mikosi.

HII NI SEHEMU YA KUMI NA MBILI.

Baada ya kutoweka eneo lile Zay B aliita taksi na
kumpa maelekezo ya wapi anapaswa kutupeleka,
alimwambia jina ambalo sikulishika vizuri zaidi ya
kumsikia yule dereva akimuuliza ikiwa wapite njia ya
mnara wa saa ama kwingineko.
“Pitia mnara wa saa we jamaa” Zay alimwambia kwa
Kiswahili, maksudi kabisa yule mwarabu akaduwaa
akauliza kiingereza ni nini Zay ana maanisha, kwa
pamoja bila kupeana taarifa tukajikuta tunacheka
huku nikipata muda wa kuitazama sura ya mwarabu
yule jinsi ilivyokuwa imebadilika kwa hasira, ndevu
zake aina ya mustachi zikimfanya azidi kuchekesha.
Sisi tuliendelea kuzungumza Kiswahili. Mimi nikiwa
mjibu maswali na Zay B akiwa ananiuliza mambo
kedekede juu ya Tanzania yetu!!
Ilifurahisha hakika, na kwa wakati huo nikajikuta
nikisahau juu ya hatari ya kumfuatilia Vonso kadri
nilivyoonywa na yule mzee wa Tanzania.
“Ule kule ndo mnara mashuhuri wa Oman, mnara ule ni
mkongwe haswa na ni kivutio kwa watalii….” Akasita
akiniacha nikiutazama mnara ule kisha akaendelea.
“Sijui kinachowavutia kipi sasa hapo… si huu ni kama
ule mnara wa saa wa Arachuga ama Mbeya…” akasita
akiniacha nikicheka kutokana na kauli yake kisha
akaendeleza vijembe.
“Bora nikashangae sanamu la posta limeshika bunduki
miaka lukuki lakini halipigi risasi hata moja kuliko huu
mnara….” Hapa tena tukacheka kwa pamoja.
Mwarabu akazidi kukunja sura, mustachi nao
ukasisimka na kusimama.
Alifurahisha!!!
Hatimaye akatushusha baada ya kufika, Zay B
akamlipa. Nikamwambia Zay ampe na nyongeza.
Zay akanipa habari kuwa nchini Oman hakuna uswahili
wa namna hiyo, iwe kwa wahudumu wa mahoteli ama
hao madereva wa taksi, Bakhshishi ni kitu
kisichokubalika kabisa.
Kauli hii ikanifanya niipende nchi ya Oman hasahasa
jiji hili la Muscat. Maana Tanzania yangu rushwa
imegeuzwa kuwa bakhshishi
Sikujua kabisa kuna nyakati huja na furaha tele na
kisha kugeuka ghafla!!
____

MSIMULIZI ANATOKA KATIKA PUMZIKO! ANAINGIA

ZAY B pamoja na Ramadhani waliingia katika mgahawa
kwa ajili ya kupata chakula.
Ramadhani hakutaka kuonekana ‘wakuja’, akaishika
karatasi iliyokuwa na orodha ya vyakula na bei zake.
Macho yake yakiwa yanaibia kumtazama Zay,
akiutathmini urembo wa mwanamke yule mwenye
mikono yenye uwezo wa kuua.
Rama alitumia kidole chake akawa anashuka chini hadi
akalifikia neno ‘MISHKAK’
Badala ya kuchagua chakula Rama akaanza kucheka.
“Hawa majamaa nao wanaita Mishkaki… eti ili
kujitofautisha wameondoa ile ‘i’ wanaita Mishkak...
watu bwana”….. Zay aliyekuwa amejikaza asicheke
akajikuta anacheka kwa sauti ya juu kidogo.
Uchangamfu wa Rama ulikuwa umemkosha, hakujua
Rama alikuwa amepagawa na urembo wake tayari.
“Vipi nikuagizie SHUWA?” Zay alimuuliza Rama huku
akiwa anamalizia kicheko.
“SHUWA?? CHURAAA? Sijakusikia vizuri….” Rama
alihoji kimasikhara.
“SHUWA…. Hii ni nyama inaokwa taratibu hadi siku
mbili chini ya ardhi kwa moto mdogo kabisa…..inapen
dwa japokuwa nasikia inaleta kitambi.” Alitoa maelezo
yale.
“Sitaki SHUWA wana Chura… niletee Mishkak…”
alijibu Rama huku akigeza lafudhi ya kiarabu.
Zay B akampungia mkono muhudumu, akampa
maelekezo pamoja na pesa.
Baada ya dakika arobaini na tano, Rama alikuwa
anashambulia mishkaki pamoja na Zay B huku kila
mmoja akiwa na kinywaji baridi.
Wakiwa katikati ya mlo, simu ya Zay iliita. Akaipokea
na kusikiliza kwa sekunde kadhaa…
“Simu muhimu afande… nikukute maeneo hayahaya..”
alisema Zay akimwambia Rama, sasa hakuwa na
tabasamu lolote usoni.
Akatoweka akimwacha Rama akimsindikiza kwa macho
yaliyochanganyika nusu mshangao na nusu matamanio.
Baada ya kumaliza chakula, Rama alitoka nje ya
mgahawa na kuangaza huku na kule huku akipiga mluzi
kana kwamba ni mwenyeji sana.
Mara akajikuta akilikumbuka tukio la usiku ule, tukio
la kukutana na Hajrati na sasa yu Muscat Oman kwa
upelelezi.
Kitendo cha kumkumbuka Hajrati akakumbuka ladha ya
ile bia yake ya mwisho kabisa.
Mawazo haya yakamletea kiu kikali cha bia.
Rama akaamua kuitafuta pombe, alipita mitaa kadhaa
huku akijitahidi kukumbuka njia ya kwenda mgahawani
na jina lake.
Hatimaye akafika alipohitaji, akaagiza chupa mbili za
bia.
“Leseni ipo wapi? Maana sura yako ni ngeni hapa”
akaulizwa kiingereza na muhudumu huku akimsaili
vyema.
Leseni?? Rama akashtushwa!
Leseni kwake huja ikiwa anaendesha gari, sasa hapa ni
baa anaulizwa leseni.
Akamwomba yule bwana amweleze vyema
anachomaanisha.
Muhudumu yule mkarimu, akamweleza kuwa nchini
Oman pombe ni haramu kwa waumini wa dini ya kislamu
na hairuhusiwi kabisa lakini kwa watalii na wasiokuwa
waislamu basi umri wa kunywa pombe ni miaka 21 na
kuendelea tena katika baa ambazo zina leseni ya kuuza
pombe, na mnywaji pia awe ameruhusiwa kunywa
pombe.
Rama akatulia kwa sekunde kadhaa kisha akatokwa na
tusi zito la nguoni kwa lugha mama ya Kiswahili huku
akimlaani yeyote yule aliyepitisha sharia ile ya kikatili
dhidi ya wapenda pombe kama yeye.
Aikainama kwa muda huku akilisikia koo likizidi
kukauka, akamuita yule bwana aliyekuwa anataka
kuondoka.
“Nisaidie walau chupa moja tu nakuomba…..”
alibembeleza.
Yule bwana kwa kumsaidia akamuelekeza katika baa
isiyofuata sheria mtaa unaofuata.
Looh! Amakweli kimfaacho mtu chake, Rama hakujali
kuhusu kupotea akakatiza mitaa na kufika alipotakiwa
kufika.
Kweli akaipata huduma, akanywa pombe chupa tatu.
Ile anaifungua chupa ya nne, likazuka balaa.
Alikuja mtu kuketi pahali alipokuwa amekaa, kama
alivyokuja hajrati usiku ule, sema huyu hakuomba
kuketi pamoja na Rama.
Akamsabahi Rama naye akajibu.
Huku akimimina ile pombe katika glasi yake.
“Samahani naweza kuona leseni yako ya unywaji
pombe?” yule bwana akamuuliza.
Rama hadi wakati huo aliichukulia Oman kama
Tanzania kuwa mikwara ni mingi kuliko vitendo.
Akatabasamu tu huku akiipeleka glasi mdomoni.
Mara akadakwa mkono na kuzuiwa kuinywa, akaulizwa
tena swali lilelile.
Safari hii akajibu.
“Sina leseni ila ni mnywaji mzuri tu!”
Ile anamalizia jibu lile yule mtu akapuliza kipyenga,
ghafla watu kadhaa wakamzingira Ramadhani ambaye
alikuwa hajaijua vyema Oman.
Mmoja kati ya watu waliomzunguka alikuwemo yule
dereva taksi mwenye mustachio.
Sasa alikuwa anatabasamu wakati huio Rama
akifungwa pingu.
Ilikuwa bahati kubwa sana kwa Rama alikana kuwa
yeye sio muislamu, na hili lilimsaidia kupatiwa hukumu
ya mtu wa kawaida.
Alikaa rumande siku tatu, siku ya nne akasimamishwa
mahakamani.
Akasomewa vifungu vya sheria.
Nchini Oman ukinywa pombe, ama kuuza kilevi bila
kuwa na kibali unapelekwa jela miezi sita, ama unalipa
faina ya reali mia tatu ama vyote kwa pamoja.
Miezi sita ikamuangukia Rama, reali 300 hakuwa nazo
na wala hakuulizwa kama hanazo.
Bora hata angekuwa ni mwarabu angefikiriwa lakini ni
mweusi tena kutoka Tanzania akashangaa anaingia
jela bila kupewa nafasi ya kutafuta wakili wala
kuujulisha ubalozi wake juu ya kinachomsibu.
Rama akiwa na masaa yasiyozidi sabini na mbili katika
jiji la Muscat nchini Oman, akajikuta hajajua jina la
mtaa hata mmoja badala yake akalijua jina la gereza
kuu lililo katika jiji hilo.
Gereza la SUMAYIL (Sumayil Central Prison).
Lazima alijue kwa sababu ilikuwa ni nyumba yake.
Kama Zay B alivyobaki na pumbazo siku ilipopita bila
kumwona Rama kisha zikawa siku tatu, hivyohivyo kwa
sajini Pilipili na wenzake akiwemo inspekta jenerali
mkuu wa polisi.
Wote hawa waliingia katika pumbazo baada ya
kufikishiwa taarifa za Rama kutoweka.
Heri yao walikumbwa na jinamizi hili la pumbazo
wakiwa mtaani, Ramadhani alikuwa ni mfungwa halali
kabisa.
Kifungo cha miezi sita!
Harakati za kuutafuta mwili wa Rama zikaanza
kufanyika chinichini bila kuushirikisha ubalozi wa
Tanzania nchini Oman.
Wangeanza vipi kuushirikisha ubalozi ikiwa ubalozi
ulishawakanya kabisa kujihusisha na harakati za
kumnyamazisha Vonso?
Wangejibu nini? Kwamba hawakuelewa maana ya
‘mwacheni Vonso?’ ama ni kiherehere kimewaponza?
Sajini Pilipili akageuka kuwa mpole na mtulivu kama
maji yaliyotiwa katika mtungi na kuachwa kama
yalivyo ama mwanaume aliyekamatwa ugoni.
Jeuri yake ikayeyuka, na sasa akajikuta yu upande wa
hatia dhidi ya mke wa Rama pamoja na mtoto wake.
Ataanza vipi kuwaeleza kuwa Ramadhani amepoteza
maisha lakini hata nguo yake aliyokuwa ameivaa
haijaonekana?
Wangeanza vipi kuipokea taarifa hii na kuielewa kisha
maisha yaendelee.
Sajenti pilipili alichanganyikiwa, akampigia simu
inspeikta Zay B na kumuuliza kama kuna lolote ambalo
amesikia juu ya mtu mweusi kuuwawa.
Akajibu ndio!
Pilipili akapata matumaini mapya kabla Zay B hajaua
Tumaini lile kwa kuelezea kuwa aliyeuwawa sio
Ramadhan.
Pilipili akakata simu na kujitupa kitandani!
 
Back
Top Bottom