Riwaya: Msako wa mwehu

Riwaya: Msako wa mwehu

SEHEMU-34


Lengo la Kachero Manu hakutaka kuacha hata chembe ya ushahidi kwa sababu alijua huko wanakokwenda kuna kufa au kupona. Hisia zake mpaka akaamua amfuatilie huyo Mzee wa kiarabu zilimtuma kuwa baadhi ya washirika wa "Al-shabaab" wameanza kutafuta maficho hasa baada ya nyaraka za siri zilizonaswa na Kachero Manu kule Simba Hoteli, Dodoma, zenye majina yao kutua mikononi mwa serikali. "Wewe Juma nakukubali aisee umejuana nae vipi mtu muhimu kama huyu, ambaye ana utajiri chekwachekwa" alidodoswa Juma na Kachero Manu wakati tayari ameshajaza mafuta pomoni kwenye tenki la pikipiki sasa walikuwa wanakata msitu kuelekea huko mashambani.
Juma Mavideo alikuwa analikimbiza pikipiki kwa mwendo wa kasi hakujibu swali la Kachero Manu, akawa anakanyaga mafuta na alikuwa analimudu ingawa alikuwa 'chordo chupa na kizibo chake' ananuka pombe ya ngomani balaa.
"Hapo mbele kwenye kona hapo pana mti wa msufi mkubwa, gari yao siku moja iliharibika, ilikuwa usiku kama saa 4 hivi sasa kuna fundi wao alitoka Mjini nikapewa kazi ya kumleta, kwa sababu mie hamna kijana anavijua vichochoro vyote vya Amboni kama mimi" alijibu Juma swali aliloulizwa kwa mbwembwe zote huku anaikamua pilipiki vilivyo.
Ghafla kutokea mbele yao ikawa inasikika sauti ya gari linakuja uelekeo wa kutokea mbele yao. "Ingiza porini haraka, huenda watu wabaya wanataka kutupora madini" alitoa amri Kachero Manu na Juma Mavideo akatii bila shuruti, wakalisweka pembeni haraka haraka, Juma akazima pikipiki yake na taa zake. Punde si punde likajitokeza gari linatembea mwendo wa pole pole limeshusha vioo, ndani kuna msichana amejifunga mtandio kichwani na mwanaume anayeliendesha gari. Waliweza kuwatambua vizuri kwa sababu dereva aliwasha taa ya ndani ya gari kana kwamba kwamba kuna kitu yule msichana alikuwa anatafuta ndani ya gari.
"Kaka kaka hili ndio gari lenyewe linalombeba yule mwarabu" alikuwa ananong'ona Juma kumwambia Kachero Manu, huku anatetemeka mwili mzima kule kichakani walipojisweka. Kachero Manu akatikisa kichwa kuonyesha kukubaliana nae huku ametingwa na ananakiri namba za gari hiyo ya polisi.
Baada ya gari lile kupita safari yao ikawa inaendelea tena, huku wanatumia matairi ya lile gari kama ndio dira ya wanaoelekea. Ilikuwa ni safari ya mwendo mrefu takribani masaa mawili, mpaka wakawa wamekaribia kufika. Juma akazima bodaboda ghafla pale yalipoishia yale matairi ya lile gari.
Akaanza sasa kumsomesha Kachero Manu, "sasa kaka yangu mpaka hapa ndio mwisho wa safari yangu, hapo mbele kuna nyumba moja nadhani ukiuliza hapo utapata jibu wapi anapoishi. Unajua analetwa na gari ya manjagu sasa wale jamaa hawana udugu wala urafiki unaweza bambikiziwa kesi ya wizi au mauaji ili wakufyedede vizuri".
Kachero Manu akabaki anatabasamu tu, akistaajabishwa na uoga wa Juma Mavideo wa ghafla, maana safari yao nzima akiongea yeye tu kujisifu ujanja, sasa ametepeta kama chapati za maji. "Mie nakupa nusu saa tu vinginevyo nasepa zangu, bado uhai naupenda mke wangu ndio kwanza nipo nae mwaka wa pili hata mahari yangu haijajilipa vizuri bado. Maadamu umeamua kujifunga bogi mie nakutakia kila kheri" aliongea kwa sauti kubwa Bwana Juma kusisitiza Kachero Manu asichelewe kurejea huko anakokwenda.
Kachero Manu akawa anatokomea kwenye uoni wa upeo wa Juma kuelekea alipoelekezwa, kikubwa alichoshukuru hawakukanyaga chechele wakapotea njia bali wamefika salama wanapopakusudia. Jukumu la Juma lilishaisha tayari, sasa imebaki kazi yake.

Kachero Manu akaanza kutembea kupita kwenye mafukutu ya nyasi zilizoshonana kwa msaada wa mbalamwezi huku akichukua tahadhari kubwa. Mpaka alivyotembea kama dakika 5 akaanza kuona mwangaza kwa mbali unatoka kwenye nyumba iliyoonekana kuwa ni ya kibanda cha miti, iliyokaa kiungani kwa kujitenga.
Akazidi kukisogelea kibanda kile kwa umakini mkubwa. Mbele yake akauona mti mkubwa ulio karibu na nyumba ile. Akajificha kwenye mti mmoja huku akitafuta mbinu ya kuingia kwenye kibanda kile. Alipoona kimya hamna michakato yoyote inayoendelea pale akachomoka kwa kasi kwa mwendo wa kunyata kuzungukia upande wa kushoto wa nyumba. Akafanikiwa kufika mlango wa nyuma. Akaweka sikio lake kwenye uwazi mdogo sana wa baina ya mbao na mbao pale mlangoni. Akawa anasikilizia kama kuna lolote linaloendelea. Akaona kimya kimetamalaki kwa kiasi kikubwa.
Giza la nje lilikuwa msaada mkubwa kwake, mwanga uliokuwa unaangaza ni wa mbalamwezi tu. Akaachana na mlango na kuanza kuzunguka na kiambaza kuchungulia kwenye madirisha ya chumba tofauti tofauti. Chumba zote tatu zilikuwa vina giza isipokuwa kimoja tu kulikuwa na mwangaza wa koroboi.
Kilikuwa ni chumba kina pipa moja kubwa la plastiki lilikuwa lina maji kiasi. Pia kulikuwa na vyombo vichache vya kupikia. Akaamua aingilie kupitia dirisha hilo. Haikuwa kazi ngumu kulinyofoa dirisha hilo kutokana na kuwa ilikuwa ni nyumba ya udongo na miti. Akachidikia chumbani, wakati anashangaa mle chumbani anafikiria kitu cha kufanya, akasikia michakato ya viatu ya mtu anayekuja kwenye kile chumba.
Kachero Manu akafanya maamuzi ya kupiga mbizi kwenye pipa lile la maji. Kweli Bwana yule mtu aliingia chumba kile kile akaenda mpaka vyombo akaviparanganyua na kuchukua kitu anachokitaka, akajifanya anaondoka zake na kufunga mlango. Kachero Manu alipiga mbizi kwa zaidi ya dakika 10, kisha akaibuka na kuruka nje ya pipa hilo. Ile anatua chini tu, akapigwa na gunia zito la mchanga kisogoni mwake. Lilikuwa ni pigo takatifu ambalo kama angepigwa mtu tefutefu asiye na mazoezi kama Kachero Manu lazima angefuata njia ya marahaba, malaika wangempokea kaburini. Akaanza kuyumbayumba kama mlevi aliezidiwa na pombe, kisha akaanza kuona nyota nyota na huku kuna watu warefu wasio na mwisho wamevaa nguo nyeupe wengi sana.
Ambao wanaimba nyimbo za mapambio huku wakimzunguka duara. Akajiona mwishoni anazama kwenye shimo refu sana yenye kiza kinene. Alichokuwa hakifahamu Kachero Manu ni kuwa kulikuwa na mlinzi mmoja yupo juu ya mti anafanya doria ya eneo zima, kwa bahati mbaya hakumuona na huyo ndio aliyepanga shambulizi dhidi yake. Kachero Manu akapoteza fahamu akiwa ndani ya nyumba ya mtu asiyemfahamu.
 
SEHEMU-35



Kachero Yasmine nyumbani kwa "Maso Maso" mafichoni alipo, alikuwa anaishi maisha ya fawaishi, maisha ya gharama ambayo hakutaraji kama kuna siku ataishi hivyo. Ilikuwa ni nyumba yenye kila kitu zaidi ya hoteli ya nyota tano, laini hakuipata furaha hata chembe ya hardali.
Sekunde ziliyeyuka kama kama plastiki kwenye moto, na dakika zilikatika, yakaja masaa, zikaja siku leo ilikuwa inatimia wiki moja kamili. Alikuwa hana raha hata kidogo kwanza hajui hatima yake itakuwaje kwenye kasri lile alilofungiwa ndani. Lakini tayari pia wameshapotezana mawasiliano na mkuu wake wa kazi Kachero Manu. "Sijui Kachero Manu anapitia madhila gani huko alipo au pengine ameshapoteza uhai wake. Na kama yupo hai na yeye pia ana hofu na mimi kwa vyovyote vile ukimya wangu atadhania nimepoteza maisha au nimetekwa na maadui" alikuwa anazidi kuwaza Kachero Yasmine mawazo yasiyo na kikomo mpaka kichwa kikawa kinamgonga kwa maumivu wakati mwingine.
Mawazo mengine yalikuwa yanamjia kuhusu huyu mumewe feki "Maso Maso", ile saba ya bila tendo la ndoa kutokana na hedhi feki aliyomdanganya ndio leo inakatika. Akaanza kuyarudia kichwani mwake majadiliano yao na mumewe alipomwambia yupo kwenye siku zake jinsi alivyohuzunika na kutaka hata kulazimisha tendo la ndoa kwa nguvu.
Sasa Kachero Yasmine aliwaza sekeseke la siku ile mpaka akamtuliza kijana wa watu kwa maneno ya Mwenyezi Mungu mpaka akapoa sasa leo akija atambeba kwa mbeleko gani, hatokuwa na jinsi nyingine bali kukubali kuliwa mzigo tu.
Kwa mara ya kwanza tokea aajiriwe na Idara ya Usalama akaanza kumwaga machozi kama mtoto mdogo, akawa hawezi kujizuia baada ya kuona hatari ya kutumika kingono bila ridhaa yake. Kilichokuwa kinamuumiza zaidi ni sawa anaweza kumpa tendo la ndoa, je iwapo katika harakati hizo akinasa ujauzito je.
"Wallahi nitatoa mimba hiyo siwezi kupata mtoto na gaidi, uso wangu nitauweka wapi mimi Yarrabi toba" alikuwa anaendeleza fikra nzito Kachero Yasmine. "Lakini nikitoa hiyo mimba na kukiua kiumbe kisicho na hatia nitamchukiza MwenyeziMungu na huenda ikawa ndio uzazi wangu wa pekee hapa dunia" alikuwa anawaza huku yupo juu ya kitanda bila kupata muafaka.
Akiwa kwenye lindi hilo la mawazo akasikia sauti ya kengele inayomjulisha muda wa wakati wa mlo wa usiku upo tayari mezani. Chakula cha usiku kilikuwa kinaliwa kila ifikapo saa 1:00 usiku juu ya alama. Akakurupuka kutoka kitandani na kujiandaa kwenda kula maana tayari njaa ilikuwa inamtafuta vilivyo.
Kuna kitu kimoja katika uchunguzi wake kilikuwa hajakipatia majibu ndani ya nyumba ile. Kulikuwa na lundo la watumishi, na chakula kinachopikwa ni kingi sana. Kwanza akawa anajiuliza kuna umuhimu gani wa kuwa na idadi kubwa ya watumishi wakati nyumba nzima kabla hajaja yeye anaishi "Maso Maso" pekee na masuria wake!.
"Hiki chakula kinachopokea ni chakula watu zaidi ya 50 na kuendelea na ni chakula cha watu wenye hadhi yao, yanapikwa mabiriani humu, mapilau na kila anuwai ya vyakula vitamu" alikuwa anatengeneza majawabu ya kukisia ya dhana alizojitengenezea.
"Hiki chakula kitakuwa kinasafirishwa kwa njia za panya maana sijawahi kuona namna vyakula vinavyosafirishwa wala wakati vyombo vinaporejeshwa" alizidi kutengeneza majibu ya dhana zake. Akaelekea mesini kwenda kujipakulia mlo wake. Akawa ni mwenye kula chapuchapu arudi zake chumbani huku hofu ikitawala moyoni mwake akiombea mumewe "Maso Maso" asirudi haraka kama alivyoahidi kurudi baada ya kupita juma moja.
Matarajio yake yalikuwa huenda akapata baadhi ya ufumbuzi wa kero zake. Alivyomaliza kula tu akapitiliza bafuni kwenda kupiga mswaki kuondosha mabaki ya chakula mdomoni mwake. Alipoingia bafuni akachukua mswaki wake akaelekea kwenye kioo cha kwenye sinki na kuanza kusafisha meno yake.
Kwa bahati mbaya maji maji yenye ya mdomoni yaliyochanganyika na dawa ya meno yakadondokea kwenye kioo na kuchafua muonekano wa kioo kile. Kwa kawaida usafi unafanywa na watumishi lakini hakupenda asubirie mpaka asubuhi ndio kisafishwe, hasa akichukulia yeye ni mtoto wa kike.
Akaamua kuchukua kitambaa safi akakiloweka kwenye sabuni akaanza kusugua kwenye kioo. Kwa mshangao mkubwa alikiona kile kioo kikubwa kinacheza cheza kuonyesha hakijashikizwa kiuimara ukutani. "Hii ni kuharibika au imefanywa hivi makusudi! " alijiuliza Kachero Yasmine.
Akaamua akichomoe kwanza aone, akakiona kinachomoka bila shida yoyote. Kilikuwa kimeshikizwa na pini mbili zilizoingizwa kwenye chuma kidogo kilichoungwa kwenye fremu ya kioo kile. Akakuta kuna duara kubwa linalotosha kabisa kupitisha kiwiliwili cha binadamu likiwa limefungwa na mbao laini.
Akaisogeza pembeni shimo likawa lipo wazi. Akarudi katika mlango wa bafuni na kuubana na ufunguo ili kutoruhusu mtu kuingia. Akapanda juu ya sinki kiuangalifu na kudumbukia kwenye hilo shimo huku akitanguliza miguu yake. Miguu ilipofika chini tu ikawa tayari imekanyaga ngazi na kushukia chini.
Akawa anateremka kwa umakini mkubwa kutokana na kiza kilichopo. Alipoteremka kama hatua 22 hivi akaona kuna kizuizi tena cha dirisha kubwa ambalo limefunikwa na pazia. Akafika mpaka hapo na kupekenyua lile pazia kiasi kidogo. Hamadi..! akaona kwa chini yake kama meta 50 kwenda chini kuna taa zinawaka huku kuna barabara nzuri ya lami imepita. Ilikuwa ni barabara nyembamba yenye uwezo wa kuruhusu bodaboda mbili kupishana. Wakati yupo pale pale kwenye kidirisha anapiga chabo akaona bodaboda mbili zinapita.
Zikiwa zimebeba majungu ya vyakula mbalimbali. Haraka haraka akafunga lile pazia na kurudi juu kwa kasi huku anatweta kwa uoga haamini alichokiona. Akarudi mpaka bafuni akakirudishia kile kioo vizuri. Alipotoka tu nje ya bafu na kuingia chumbani kwake, kengele ikaanza kulia. Akashtuka sana sio kawaida kupigiwa kengele akiwa ameshaingia ndani kupumzika hasa baada ya kupata mlo wa usiku. Akaipuuzia labda watakuwa wamekosea, wakati anajiandaa apande kitandani sasa ikaanza kulia tena mara hii ikiwa ni mfululizo.
Akakurupuka na kwenda kuitika wito kwa kufungua mlango. "Seyyidati samahani kwa usumbufu usiku huu kuna gari limekuja kukufuata limetumwa na mumeo unatakiwa umfuate alipo ubebe vitu vyako vya muhimu tu vingine uviache, huo ndio ujumbe wangu kwako mtukufu Seyyidati" alileta ujumbe mmoja wa watumishi kwa nyumba ile na kuaga akaondoka zake.
Akaurejesha mlango na kuuegemea mlango kwa mgongo wake. Akavuta pumzi ndefu kwa muda, alikuwa yupo pwetepwete kwanza akimshukuru Mungu kwa kuigundua njia ya siri dakika za majeruhi bila kushtukiwa. Lakini pia sasa alikuwa anaogopa kuwa lazima sasa ataenda kushiriki tendo la ndoa na "Maso Maso".
"Ukitaka kuoga lazima uyavulie nguo maji hamna jinsi, tutaona huko huko" alijipa moyo na kuanza kufungasha virago vyake. Baada ya nusu saa akawa yupo tayari kwa safari, akaingia na msafara ukaanza kuelekea sehemu asipokujua. Ila alikuwa amejiandaa kuwa makini kusoma vibao na alama za kumtambulisha eneo hilo, lakini kikubwa alikuwa anaangalia muda anaoondoka pale nyumbani kwa "Maso Maso".
Alipoingia ndani ya gari vioo vya giza "tinted" vikateremshwa akawa haoni anapotoka wala anapopelekwa. "Hawa mbwa ni kiboko aisee wamejipanga hawataki kufanya makosa, tutaonana huko huko. Ni kama vile wananitoa kikaangoni huku na kuniweka motoni huko wanakonipeleka. Unapojitwika wajibu si vyema kulalama, maadamu ni kazi niliyoichagua mwenyewe ngoja nikapambane" alijisemea Kachero Yasmine moyoni mwake. Huku injini ya gari inaunguruma kukata mitaa.
 
Back
Top Bottom