SEHEMU-35














Kachero Yasmine nyumbani kwa "Maso Maso" mafichoni alipo, alikuwa anaishi maisha ya fawaishi, maisha ya gharama ambayo hakutaraji kama kuna siku ataishi hivyo. Ilikuwa ni nyumba yenye kila kitu zaidi ya hoteli ya nyota tano, laini hakuipata furaha hata chembe ya hardali.
Sekunde ziliyeyuka kama kama plastiki kwenye moto, na dakika zilikatika, yakaja masaa, zikaja siku leo ilikuwa inatimia wiki moja kamili. Alikuwa hana raha hata kidogo kwanza hajui hatima yake itakuwaje kwenye kasri lile alilofungiwa ndani. Lakini tayari pia wameshapotezana mawasiliano na mkuu wake wa kazi Kachero Manu. "Sijui Kachero Manu anapitia madhila gani huko alipo au pengine ameshapoteza uhai wake. Na kama yupo hai na yeye pia ana hofu na mimi kwa vyovyote vile ukimya wangu atadhania nimepoteza maisha au nimetekwa na maadui" alikuwa anazidi kuwaza Kachero Yasmine mawazo yasiyo na kikomo mpaka kichwa kikawa kinamgonga kwa maumivu wakati mwingine.
Mawazo mengine yalikuwa yanamjia kuhusu huyu mumewe feki "Maso Maso", ile saba ya bila tendo la ndoa kutokana na hedhi feki aliyomdanganya ndio leo inakatika. Akaanza kuyarudia kichwani mwake majadiliano yao na mumewe alipomwambia yupo kwenye siku zake jinsi alivyohuzunika na kutaka hata kulazimisha tendo la ndoa kwa nguvu.
Sasa Kachero Yasmine aliwaza sekeseke la siku ile mpaka akamtuliza kijana wa watu kwa maneno ya Mwenyezi Mungu mpaka akapoa sasa leo akija atambeba kwa mbeleko gani, hatokuwa na jinsi nyingine bali kukubali kuliwa mzigo tu.
Kwa mara ya kwanza tokea aajiriwe na Idara ya Usalama akaanza kumwaga machozi kama mtoto mdogo, akawa hawezi kujizuia baada ya kuona hatari ya kutumika kingono bila ridhaa yake. Kilichokuwa kinamuumiza zaidi ni sawa anaweza kumpa tendo la ndoa, je iwapo katika harakati hizo akinasa ujauzito je.
"Wallahi nitatoa mimba hiyo siwezi kupata mtoto na gaidi, uso wangu nitauweka wapi mimi Yarrabi toba" alikuwa anaendeleza fikra nzito Kachero Yasmine. "Lakini nikitoa hiyo mimba na kukiua kiumbe kisicho na hatia nitamchukiza MwenyeziMungu na huenda ikawa ndio uzazi wangu wa pekee hapa dunia" alikuwa anawaza huku yupo juu ya kitanda bila kupata muafaka.
Akiwa kwenye lindi hilo la mawazo akasikia sauti ya kengele inayomjulisha muda wa wakati wa mlo wa usiku upo tayari mezani. Chakula cha usiku kilikuwa kinaliwa kila ifikapo saa 1:00 usiku juu ya alama. Akakurupuka kutoka kitandani na kujiandaa kwenda kula maana tayari njaa ilikuwa inamtafuta vilivyo.
Kuna kitu kimoja katika uchunguzi wake kilikuwa hajakipatia majibu ndani ya nyumba ile. Kulikuwa na lundo la watumishi, na chakula kinachopikwa ni kingi sana. Kwanza akawa anajiuliza kuna umuhimu gani wa kuwa na idadi kubwa ya watumishi wakati nyumba nzima kabla hajaja yeye anaishi "Maso Maso" pekee na masuria wake!.
"Hiki chakula kinachopokea ni chakula watu zaidi ya 50 na kuendelea na ni chakula cha watu wenye hadhi yao, yanapikwa mabiriani humu, mapilau na kila anuwai ya vyakula vitamu" alikuwa anatengeneza majawabu ya kukisia ya dhana alizojitengenezea.
"Hiki chakula kitakuwa kinasafirishwa kwa njia za panya maana sijawahi kuona namna vyakula vinavyosafirishwa wala wakati vyombo vinaporejeshwa" alizidi kutengeneza majibu ya dhana zake. Akaelekea mesini kwenda kujipakulia mlo wake. Akawa ni mwenye kula chapuchapu arudi zake chumbani huku hofu ikitawala moyoni mwake akiombea mumewe "Maso Maso" asirudi haraka kama alivyoahidi kurudi baada ya kupita juma moja.
Matarajio yake yalikuwa huenda akapata baadhi ya ufumbuzi wa kero zake. Alivyomaliza kula tu akapitiliza bafuni kwenda kupiga mswaki kuondosha mabaki ya chakula mdomoni mwake. Alipoingia bafuni akachukua mswaki wake akaelekea kwenye kioo cha kwenye sinki na kuanza kusafisha meno yake.
Kwa bahati mbaya maji maji yenye ya mdomoni yaliyochanganyika na dawa ya meno yakadondokea kwenye kioo na kuchafua muonekano wa kioo kile. Kwa kawaida usafi unafanywa na watumishi lakini hakupenda asubirie mpaka asubuhi ndio kisafishwe, hasa akichukulia yeye ni mtoto wa kike.
Akaamua kuchukua kitambaa safi akakiloweka kwenye sabuni akaanza kusugua kwenye kioo. Kwa mshangao mkubwa alikiona kile kioo kikubwa kinacheza cheza kuonyesha hakijashikizwa kiuimara ukutani. "Hii ni kuharibika au imefanywa hivi makusudi! " alijiuliza Kachero Yasmine.
Akaamua akichomoe kwanza aone, akakiona kinachomoka bila shida yoyote. Kilikuwa kimeshikizwa na pini mbili zilizoingizwa kwenye chuma kidogo kilichoungwa kwenye fremu ya kioo kile. Akakuta kuna duara kubwa linalotosha kabisa kupitisha kiwiliwili cha binadamu likiwa limefungwa na mbao laini.
Akaisogeza pembeni shimo likawa lipo wazi. Akarudi katika mlango wa bafuni na kuubana na ufunguo ili kutoruhusu mtu kuingia. Akapanda juu ya sinki kiuangalifu na kudumbukia kwenye hilo shimo huku akitanguliza miguu yake. Miguu ilipofika chini tu ikawa tayari imekanyaga ngazi na kushukia chini.
Akawa anateremka kwa umakini mkubwa kutokana na kiza kilichopo. Alipoteremka kama hatua 22 hivi akaona kuna kizuizi tena cha dirisha kubwa ambalo limefunikwa na pazia. Akafika mpaka hapo na kupekenyua lile pazia kiasi kidogo. Hamadi..! akaona kwa chini yake kama meta 50 kwenda chini kuna taa zinawaka huku kuna barabara nzuri ya lami imepita. Ilikuwa ni barabara nyembamba yenye uwezo wa kuruhusu bodaboda mbili kupishana. Wakati yupo pale pale kwenye kidirisha anapiga chabo akaona bodaboda mbili zinapita.
Zikiwa zimebeba majungu ya vyakula mbalimbali. Haraka haraka akafunga lile pazia na kurudi juu kwa kasi huku anatweta kwa uoga haamini alichokiona. Akarudi mpaka bafuni akakirudishia kile kioo vizuri. Alipotoka tu nje ya bafu na kuingia chumbani kwake, kengele ikaanza kulia. Akashtuka sana sio kawaida kupigiwa kengele akiwa ameshaingia ndani kupumzika hasa baada ya kupata mlo wa usiku. Akaipuuzia labda watakuwa wamekosea, wakati anajiandaa apande kitandani sasa ikaanza kulia tena mara hii ikiwa ni mfululizo.
Akakurupuka na kwenda kuitika wito kwa kufungua mlango. "Seyyidati samahani kwa usumbufu usiku huu kuna gari limekuja kukufuata limetumwa na mumeo unatakiwa umfuate alipo ubebe vitu vyako vya muhimu tu vingine uviache, huo ndio ujumbe wangu kwako mtukufu Seyyidati" alileta ujumbe mmoja wa watumishi kwa nyumba ile na kuaga akaondoka zake.
Akaurejesha mlango na kuuegemea mlango kwa mgongo wake. Akavuta pumzi ndefu kwa muda, alikuwa yupo pwetepwete kwanza akimshukuru Mungu kwa kuigundua njia ya siri dakika za majeruhi bila kushtukiwa. Lakini pia sasa alikuwa anaogopa kuwa lazima sasa ataenda kushiriki tendo la ndoa na "Maso Maso".
"Ukitaka kuoga lazima uyavulie nguo maji hamna jinsi, tutaona huko huko" alijipa moyo na kuanza kufungasha virago vyake. Baada ya nusu saa akawa yupo tayari kwa safari, akaingia na msafara ukaanza kuelekea sehemu asipokujua. Ila alikuwa amejiandaa kuwa makini kusoma vibao na alama za kumtambulisha eneo hilo, lakini kikubwa alikuwa anaangalia muda anaoondoka pale nyumbani kwa "Maso Maso".
Alipoingia ndani ya gari vioo vya giza "tinted" vikateremshwa akawa haoni anapotoka wala anapopelekwa. "Hawa mbwa ni kiboko aisee wamejipanga hawataki kufanya makosa, tutaonana huko huko. Ni kama vile wananitoa kikaangoni huku na kuniweka motoni huko wanakonipeleka. Unapojitwika wajibu si vyema kulalama, maadamu ni kazi niliyoichagua mwenyewe ngoja nikapambane" alijisemea Kachero Yasmine moyoni mwake. Huku injini ya gari inaunguruma kukata mitaa.












