MKE WA RAIS
Mwandishi: Ibrahim Masimba
*********
Alihitaji kumtumia msichana yule, alihitaji kumtumia katika kuijua kambi iitwayo victoria. Aliuhitaji msaada wa mwanamke yule. Lakini angemuamini vipi mwanamke ambaye anahisi anamfuatilia yeye. Ugongwaji wa mlango kule hotelini na kule kumuona pale kulimpa hisia tofauti. Hisia ambazo hakupenda kuzidharau. Huyu ni mmoja wao na ananifuatilia mimi. Yalikuwa maneno aliyoyatamka wakati akiivuka barabara kuelekea upande wa zinapopaki tax. Alitembea akiangalia eneo lote kwa jicho la tatu, alitizama kuhakikisha kuwa hakuna mtu yoyote anayemfuatilia. Akaifikia tax na kuingia pasipokutoa salamu. Muda huo huo dereva naye akaingia pasipo kutoa salamu. Dereva akaiwasha gari na kukanyaga mafuta. Gari ikaanza kutembea kwa mwendo wa kawaida. Wakati huo ilikuwa yapata majira ya saa tatu na nusu usiku. Gari ikatembea pasipo abiria kusema wapi anapoelekea. Hilo lilikuwa aina ya tabia nyingine, hakuwahi kupakia abiria mkorofi kama huyu. Akageuka kutizama nyuma alipokaa abiria wake akitegemea kuulizwa chochote, lakini akapigwa na mshangao ambao hakuutegemea, licha ya kumuona mtu akiingia ndani ya gari yake lakini kwa wakati huu alishangaa zaidi baada ya kutokumuona mtu. Kusema kweli hilo hakuwa amelitegemea. Hakuwa amejiandaa kwa tukio hilo. Akabaki kuduwaa. Punde akaliona gari aina ya marcedes Benz likimpita kisha likasimama kwa mbele. Kabla hajajua nini cha kufanya akawaona watu watatu wenye silaha wakiisogelea gari yake. Hawakuwa watu wa utani na hawakuonyesha umasihara. Watu wale wakaifikia gari yake kisha bila kuuliza mdomo wa bastola ukaelekezwa kwake, harafu wale wawili wakaufungua mlango wa nyuma kwa kasi bastola mkononi. Lakini mshangao uliompata dereva mara ya kwanza,ndio mshtuko ambao waliupata hawa watu. Walipoteza umakini kwa sekunde karibia kumi wakishangazwa na kutoweka kwa mtu wao katika mazingira tatanishi. Bastola tatu zikaelekezwa kichwani kwa dereva akitakiwa kusema wapi alipo mtu ambaye aliingia ndani ya gari. Lakini hata yeye alikuwa ameshangazwa na uyeyukaji wa abiria wake, abiria alieingia bila salamu na kuketi siti ya abiria, kisha kuyeyuka mfano wa kivuri. Angejibu nini? Jibu angelitoa wapi? Akaendelea kutetemeka huku midomo ya bastola tatu ikimtizama. Hapakuwa na masihara tena, lakini hata swali liliporudiwa hakuwa na majibu. Kidole cha mmoja kati yao kikashuka taratibu kwenye kitufe cha kuruhusu risasi.. lakini kabla hajafyatua wakaisikia sauti, sauti kutoka nyuma yao, sauti ambayo iliwagutusha na kuendelea kupoteza umakini. Ilikuwa sauti ya Muddy, tena ikitokea nyuma yao. Wote wakageuka kwa pamoja, wote wakageuka huku bastola zimetangulia, lakini walikuwa wamechelewa, kwani hawakuipata nafasi hiyo, hawakuipata nafasi ya kufyatua.. punde walikuwa wakianguka chini kila mmoja akivuja damu. Risasi kutoka kwenye bastola yenye kiwambo cha kuzuia mlio zilitosha kuwamaliza watu wale. Muddy hakuchelewa wala hakutaka kuwapekua, akaingia ndani ya tax ile ile akiamulu dereva Ampeleke VICTORIA BASE.
Kuitaja Victoria Base kukaleta mshtuko machoni kwa dereva yule, mshtuko ambao ulikuwa wazi machoni mwake. Hilo likamvutia Muddy, likamvutia kwa kuwa alihisi sasa amepata mtu wa kumpeleka.
"Boss huko ni hatari haparuhusiwi kufika mtu yoyote wala gari." Hatimaye aliongea dereva kwa sauti yenye woga ndani yake.
"Endesha gari, mimi na wewe tutakuwa watu wa kwanza kufika huko." Akajibu Mudy pasipokuonyesha masihara.
"Boss unaongea kwa kuwa hupajui huko. Hivi umeshawahi kuwasikia CIA na Hata KGB? Akajibu dereva yule huku akimuangalia Mohamed.
Kufikia hapo Mudy akatambua kuwa mtu alienae alikuwa mtu sahihi kwake. Alikuwa mtu sahihi wa kumpeleka Victoria Base ama Kumueleza ukweli kuhusu sehemu hiyo.
"Hapana siwajui na wasikia tu. Lakini kwa nini hiyo sehemu iogopewe hivyo kunakitu gani?" Akauliza Muddy huku akijifanya hajui kitu.
" wewe ni nani kwanza? Maana nilichokishuhudia pale nyuma tulipopita ni hatari. Nahisi hata wewe unaweza kuwa jasusi wa CIA, MOSSAD ama FSB."akajibu mtu yule.
"Mimi ni mtu wa kawaida sana. Natamani kufika huko kwa kuwa nashangaa watu wengi wanaogopa kufika huko." Akajibu Mohammed akionyesha ni mtu wa kawaida kabisa.
""Unadhani huko nyuma watu walikuwa wakiogopa? Siku hizi tu ndio watu wanaogopa hasa baa.....kabla hajaimalizia kauli ile Muddy akashangaa kuiona damu ikiruka... Dereva alikuwa amepigwa Risasi kupitia kwenye kioo. Gari akaanza kuyumba huku na huko, muddy hakuwa mpuuzi, akaufungua mlango na chupa akiangukia kando ya barabara. Muda mfupi baada ya kuruka akaiona gari ikienda kugonga ukingo wa barabara, kisha kulipuka.
Muddy aliiangalia gari ikiwaka moto, kisha akaamua kuondoka. Alihitaji kufika Victoria Base lakini kwanza alihitaji kwenda kuonana na mwanamke yule, mwanamke ambaye alihisi alikuwa nyuma ya matukio yote. Alihitaji kurudi pale hotelini, kurudi kwa njia nyingine na akiwa mwingine kabisa. Alihitaji kumjua yule mwanamke, na alitaka kuijua victoria Base.. akageuka kuelekea huko, huku maneno ya dereva Tax yakimpa mwanga ingawa aliuawa kabla ya kuyamalizia