Riwaya: Mfalme Anataka Kuniua

Abtali mwerevu

JF-Expert Member
May 5, 2013
637
432
Msisitizo: Riwaya imekamilika, kila siku itakuwa inatumwa sehemu moja mpaka itakapoisha. Hakuna longolongo, hakuna kuchelewesha wala hakuna kununua.

Mfalme Anataka Kuniua | Sehemu ya Kwanza
Mwandishi: Mwalimu Makoba


Mako alijibanza katika kichaka cha kijani. Mbele alitazama kundi kubwa la swala. Akapiga hesabu haraka yupi amkamate. Aliona swala watatu waliokuwa na watoto, hao hakutaka kuwakamata, asingependa kuwatenga swala wale wadogo na mama zao. Basi alitazama kwa makini akagundua uwepo wa swala mzee kuliko wengine, huyo akamuwekea lengo la kumkamata.

Alichomoka katika chaka alilojificha kwa kasi kama Simba. Swala walikimbia, naye akamkimbiza mmoja aliyekuwa mzee, alitamani kwenda kumgeuza kitoweo, wadogo aliwaacha wafurahie dunia. Swala mzee alikimbia kama gari jipya, nayo mbuga ikatulia ikimtazama Mako na swala.

Kona ya kwanza ilikatwa, Mako naye akakata, kona ya pili, chenga, kona ya tatu, hola, kona ya nne, imo! Swala akakamatwa. Mako aliwinda bila silaha, yeye alikimbiza wanyama kama wafanyavyo wanyama wengine wala nyama.

Wakati yote hayo yakitokea, Malkia wa nchi ya Kanakantale alikuwa akishuhudia. Siku hiyo, yeye na wasaidizi wake, alikwenda porini kujionea wanyama. Alishangazwa mno kushuhudia mtu akiwinda bila kutumia silaha yoyote.

Malkia alisogea mpaka alipo Mako, Mako alisimama na kumpa ishara ya heshima kwa kupiga mguu wa kulia mara tatu ardhini.

“Jina lako nani?” aliuliza Malkia.

“Naitwa Mako.”

Japo haikutarajiwa, lakini Malkia alivutiwa mno na Mako. Mako alikuwa mwanamume mwenye urefu wa futi tano na nchi saba, rangi yake maji ya kunde, nywele kipilipili, tumbo limejengeka vyema, mikono imejaa misuli nayo miguu ipo imara.

Malkia alilishika tumbo la Mako, kisha akauliza swali, “Unawezaje kumkamata mnyama bila silaha?”

“Mimi hutumia mbinu anazotumia Simba au chui. Wanyama hawa huwinda bila silaha,” alijibu Mako akimchinja mnyama wake. “Malkia wangu,” aliongeza Mako, “chukua mguu, kampikie supu mfalme na wewe usisahau kula kidogo.

Mako aliondoka na kumuacha malkia akiwa na wasaidizi wake. Bila shaka nao waliondoka hapo baadae.

Mako alitembea mpaka alipofika katika mji wa Kanakantale, mji huu ulikuwa makao makuu ya nchi ya Kanakantale. Alipita katika familia duni, akagawa nyama vipande vipande. Vipande vilivyobaki alikwenda kula yeye na familia yake. Kitendo cha kugawia masikini sehemu ya mawindo, kilimfanya apendwe sana na watu wa mji wa Kanakantale. Mako hakuwa mchoyo, hakuwa na makuu.

Kwa upande wa pili, malkia hakutulia siku hiyo. Muda wote alimuwaza Mako. Kila akitoka chumba hiki akiingia kile mawazo yake yalikuwa kwa mtu mmoja.

Hata ule mguu aliopewa ampikie mfalme supu, hakufanya hivyo, aliuchukua, akawaagiza watumishi wake wauchome, nao wakakaa pamoja wakila nyama choma. Wakati wa kula, Malkia alipeleleza habari za Mako, nao wakasimulia mikasa yake.

“Malkia wangu, ninao mkasa mmoja wa Mako, naomba nikusimulie.” alisema dada wa kazi akilitafuna pande la nyama choma.

“Nisimulie.” alijibu Malkia akipaka chumvi katika pande la nyama lililometameta kwa yale mafuta yake.

Dada akakaa vizuri, wanawake wanne wakamtazama huku wakimsikiliza masikio yamewasimama kama sungura. Basi akasimulia mkasa mmoja wa Mako.

Inaendelea Kesho Saa Tisa Mchana...
 
Mfalme Anataka Kuniua | Sehemu ya Pili

“Katika kijiji kimoja cha kijani, waliishi watu wenye furaha. Furaha yao ilidumu kwa miaka mingi mpaka walipovamiwa na simba mmoja mzee. Simba huyu mzee, alikuwa katili kwa wanakijiji, kijiji kikakosa amani na furaha yao ikateketea kama fedha za mlevi ziteketeavyo baa.

Simba mzee alianza unyama wake kwa kumuua mzee maarufu wa kijiji aliyependwa na watu wote. Inasemekana kuwa mzee alikuwa katika shamba lake akipalilia mahindi, ndipo alipovamiwa na simba mzee ambaye alimrukia shingoni na kumuua kisha akamla mpaka aliposhiba na kuacha sehemu ndogo ya mwili.

Simba mzee hakuishia hapo, aliwatafuna watoto wawili mapacha waliokuwa wakichoma viazi pembezoni mwa nyumba yao. Basi baada ya tukio hilo, habari ya simba huyo ikaenea kwa wanakijiji na kila mmoja akajifungia katika nyumba yake akiogopa kutoka kwa hofu ya yule simba mzee.

Kwa kuwa wanakijiji walijifungia ndani, simba yule mzee alipohisi njaa, akawinda watu asiwaone, akaanzisha kioja kipya, alianza kubomoa nyumba za watu na kuwatafuna wote aliowakuta humo.

Tukio la kwanza alivunja nyumba ya mganga wa kijiji, mganga alijifungia ndani kwake yeye na wanae, nao wakawa wamewasha moto ili waweze kuonana usiku ule, simba alivunja mlango wao, akaingia na kuwatafuna wote, hata mganga alitafunwa, kweli mganga hajigangi!

Nyumba ya pili ilikuwa ni nyumba ya mpiga ngoma wa kijiji, tukio hili husikitisha sana, kwani mpiga ngoma alikuwa na mke wake, mtoto wake mmoja wa kiume mwenye mwaka mmoja na mama yake mzazi, wote wakatafunwa na simba yule.

Wanakijiji waligundua kuwa, milango yao haikuwa imara kuweza kumzuia simba kuingia atakapo, lakini hawakuwa na namna yoyote ya kufanya, isipokuwa kukaa hivyo wakiomba miungu wasije uawa na Simba mzee. Pia walitamani kupeleka taarifa kwa mkuu wa wilaya ili atume jeshi lije kumwondoa Simba yule, lakini hakupatikana mwanamume aliyeweza kutoka ndani ya nyumba yake kwa hofu ya yule Simba. Basi kijiji kikawa kimya kama hakina watu. Inasemekana kwa sababu ya ule ukimya, hata hatua za sisimizi ziliweza kusikika!

Bwana Mako aliishi katika kijiji hicho, nyumba yake ilijitenga na nyumba za wanakijiji wengine, aliijenga katika kilima. Ungeziona, ungezani nyumba yake ni askari mkuu na zile zingine ni askari wadogo nao wanaamrishwa mguu pande mguu sawa!

Bwana Mako alishtushwa na ukimya wa kijiji, mwanzo alidhani labda shughuli zimewachosha hivyo kwa sababu ya uchovu hawana nguvu ya kupiga kelele.

Lakini baada ya siku kadhaa akahisi hatari, akaamua kuteremka kilimani ilipokuwa nyumba yake na kwenda kwa wanakijiji wengine.

Alitembea katika hali ile ya ukimya mpaka alipozifikia nyumba za wanakijiji wengine.

“Wanakijiji kulikoni, mbona kimya na mmejifungia ndani ya nyumba zenu?” aliuliza. “Tatizo nini ndugu zangu?”

Hakuna aliyejibu, wanakijiji walikaa kimya kwa hofu, pengine walidhani simba yule angetokea na kummeza Bwana Mako mara moja. Naye Bwana Mako kuona watu wako kimya, aliamua kusogea katika dirisha la fundi cherehani wa kijiji.

“Fundi, fundi,” alinong’ona. “Nieleze, tatizo nini?”

“Simba ndugu yangu,” alijibu, “anatafuna watu kama atafunavyo swala.”

Bwana Mako alipopata taarifa hizo, alisogea katikati ya nyumba zote.

Inaendelea Kesho...
 
Mfalme Anataka Kuniua | Sehemu ya Tatu

“Ndugu zangu,” alisema kwa sauti kubwa, “Wanaume msijifungie ndani, njooni nje twende tukapambane na huyu Simba. Mkiendelea kubaki ndani hakuna atakayesalia kwa sababu milango yetu siyo imara kiasi cha kumzuia asiivunje. Ni heri tufe tukipigana naye kuliko tujifungie ndani naye aje atukamate kama mwewe akamatavyo vifaranga. Je mnavyakula vya kutosha siku ngapi? Sasa hamuoni mnawindwa na njaa pamoja na simba? Aliyetayari kupambana ajitokeze sasa.”

Zilipita dakika tisa tangu azungumze maneno hayo. Hakuna mwanamume aliyetoka ndani kuja nje kuungana naye, Bwana Mako akaamua kuingia msituni peke yake kumsaka Simba mzee. Akiwa anatembea alirushiwa mkuki.

“Chukua mkuki huo utakusaidia kupambana na simba huyo,” ilisema sauti kutoka nyumba moja, kisha ikasikika sauti ya kufunga mlango, pakawa kimya.

“Ni uonevu kumuua simba mzee kwa mkuki, simba mzee anauliwa kwa viganja vitupu!” alijibu Bwana Mako kisha akapotelea msituni.

Wanakijiji walichungulia katika madirisha yao kama wanaoangalia sinema. Ukimya ukatanda tena kwa dakika ishirini.

Ukimya ulivunjwa na miungurumo ya simba, wanakijiji walitazama lakini hawakumuona simba waliishia kusikia ile miungurumo yake tu. Baadaye ikasikika sauti ya Bwana Mako akilia kisha pakawa kimya. Kimya kuliko muda wote.

Baadaye vilianza kusikia vishindo vikija katika kijiji. Hofu ikawajaa, wakasali kila mtu kwa imani yake wasijetafunwa na yule simba.

Vishindo viliendelea kusikika mpaka walipoona kitu ambacho hawakuamini. Bwana Mako alibeba mwili wa Simba yule mzee katika mabega yake. Naye alitembea kwa vishindo vya shujaa.

Furaha ilirejea tena kijijini, wanakijiji walifungua milango yao wakampokea Bwana Mako na kumshukuru kwa msaada wake. Baada ya kumaliza maombolezo ya ndugu zao waliotafunwa na Simba yule, walifanya sherehe kubwa kufurahia ushindi wa Bwana Mako.”

Dada wa kazi alimaliza kusimulia mkasa wa Mako. Hata akina dada wengine nao wakavutiwa na Mako lakini waliogopa kuonesha waziwazi kwa sababu walitambua kuwa malkia alikwisha mpenda.

***​

Ilikuwa usiku wa manane katika jumba la kifalme. Malkia alilala na alizama katika usingizi. Mfalme wa Kanakantale yeye hakulala. Suala la utawala ni gumu na kuna mambo ambayo yamekuwa yakimnyima usingizi, basi akiwa kimya, alisikia malkia akiota kwa sauti.

“Mako nakupenda, naahidi kuwa wako daima, njoo unikumbatie Mako wangu.”

Mfalme aliyasikia maneno hayo, pia alibaini ilikuwa ndoto tu, hata hivyo Mako alimfahamu, alimfahamu kwa sababu ya mikasa yake ya kila siku. Kilichomtesa mfalme ni hilo jina Mako limeingiaje katika ndoto ya Malkia.

Mfalme aliamua kumuamsha Malkia na kumuuliza juu ya ndoto yake. Malkia hakuonekana kukumbuka kitu. Mfalme alisimulia ilivyokuwa, pia alimueleza Malkia kuwa, ndoto ni matokeo ya mawazo yako ya siku nzima.

Malkia alijitetea kwa kueleza tukio lake la kukutana na Mako, alisema alikutana na mtu huyo mchana wa siku hiyo na hakuna kingine kilichoendelea.

Japo Mfalme hakuendelea kujibishana na Malkia, hakulizishwa na utetezi. Asubuhi aliamuru askari wamtafute popote alipokuwa Mako, wampeleke kwake tayari kujibu mashtaka.

Inaendelea Jumatatu...
 
Mfalme Anataka Kuniua | Sehemu ya Nne

Haikupita muda, Mako aliletwa kwa mfalme akiwa chini ya ulinzi mkali wa askari wapandao punda. Alishushwa, naye kwa heshima akapiga mguu wa kuume mara tatu kumsalimu mfalme. Mfalme hakujibu salamu hiyo. alimtazama kwa ghadhabu Mako.

Baraza lilikaa ili kusikiliza mashtaka. Mako alivalia shati kubwa la bluu, suruali pana kiasi na viatu imara vya ngozi. Jamii ya Kanakantale, haikuwa nyuma katika teknolojia ya mavazi, watu wake walivaa mavazi ya kisasa!

Mfalme alianza kusoma mashtaka, “Mako, mkulima, mfugaji na muwindaji, unatuhumiwa kwa kosa la kujihusisha na mahusiano na mke wa mfalme, yaani Malkia wa nchi ya Kanakantale. Usiku tukiwa tumelala, nilisikia kwa masikio yangu Malkia akitamka kuwa anakupenda na anaahidi kuwa wako daima. Japo Malkia alikuwa ndotoni, haimaanishi kuwa huna mahusiano naye. Kinachotokea ndotoni ni matokeo ya kilichotendeka mchana. Una chochote cha kujitetea?”

“Mfalme wangu,” alijibu Mako, “nimekosa nini hata niwe na mahusiano na Malkia wa nchi yangu? Naruhusiwa kuoa wanawake wengi kadri ya uwezo wangu vipi niwe na Malkia. Tazama nchi hii ilivyojaa wanawake, wote hawa sijawaona hata nikaja kwa Malkia wangu mwenyewe? Mfalme tuhuma hizi siyo za kweli. Siwezi kufanya hivyo.”

Baada ya utetezi wa Mako, mfalme alikaa na baraza lake, wakajadili kwa muda. Wazee wale wenye ndevu nyeupe, walikubaliana jambo, mfalme akasoma hukumu.

“Tumekubaliana kuwa, Mako una hatia ya kuwa na mahusiano na Malkia. Ushahidi upo katika ndoto ya Malkia. Jambo hili ni kosa baya kabisa tena lisilokubalika. Hivyo, unahukumiwa adhabu ya kifo. Utakaa gerezani kwa muda wa mvua mbili, kisha utanyongwa hadharani iwe fundisho kwa wengine. Kwa kipindi chote hicho, hakuna anayeruhusiwa kuja kukuona ila kwa idhini ya mfalme.”

Mako hakuamini maneno yale. Aliinamisha kichwa chake hata mikono ikagusa zile nywele za kipilipili. Alishangazwa na hukumu ile ambayo haikutenda haki. Kukaa gerezani kwa muda wa mvua mbili maana yake ni kwamba, angekaa gerezani mpaka pale mvua ingenyesha kwa mara ya kwanza, kisha kwa mara ya pili, baada ya hapo angenyongwa.

Habari ya hukumu ya kifo cha Mako ilisambaa kama mchanga jangwani. Habari hii iliwaumiza sana wananchi wa kawaida. Mako alikuwa msaada mkubwa kwao. Hukumu hii iliumiza familia ya Mako na wote waliompenda kwa ule moyo wake wa kusaidia. Pengine habari hii ilimfurahisha mfalme peke yake kwa maana hakuna mwingine aliyefurahishwa na hukumu hii ya ajabu.

Wananchi walionekana kutoridhishwa na hukumu hii, waliwaza, kama kweli Mako ana mahusiano na Malkia, iweje basi ahukumiwe Mako peke yake naye Malkia aachwe?

Mchana wa siku hiyo Mako alitupwa gerezani akiwa kavikwa mavazi meupe. Gereza lilikuwa kubwa lililojengwa kwa miti ya mkonge. Liligawanywa katika vyumba vya watu wanne. Wafungwa hawakuruhusiwa kutoka katika vyumba isipokuwa mara moja kwa siku pale walipotakiwa kwenda kufanya usafi wa miili yao.

Mako aliwekwa chumba kimoja na wenzake watatu, yeye akawa wa nne. Wote hao walisubiri hukumu ya kifo kwa makosa mbalimbali waliyofanya.

Inaendelea Kesho...
 
Mfalme Anataka Kuniua | Sehemu ya Tano

Aliweza kuwatambua watu hao. Mmoja aliitwa Sasi, kosa lake Wizi. Wala hakusingiziwa. Sasi alikuwa mwizi aliyechukiwa na watu wote. Wa pili alikuwa Athu, yeye alifungwa kwa kosa la uharifu kama Sasi. Naye hakusingiziwa, alikuwa mwizi wa mifugo aliyechukiwa na wafugaji wote. Wa tatu aliitwa Sipe, alifungwa kwa hofu ya mfalme. Mfalme alimuogopa Sipe kuwa ipo siku angempindua. Sipe alikuwa mtu mwenye maneno ya busara. Mara chache alitabiri mambo yakatokea, hii ilimpa hofu mfalme kwa kuona Sipe atapendwa na watu kuliko yeye na kuleta mapinduzi. Sipe alionewa!

“Hamjambo ndugu zangu?” Alisalimia Mako.

“Hatujambo,” walijibu. Sipe akaendelea. “Hakuna aliyesalama, hata wewe Mako umeletwa humu? Umefanya kosa gani hasa?”

“Ni uonevu tu,” alijibu Mako, akikaa katika kitanda cha majani, “nina mvua mbili za kunifanya niendelee kuwa hai. Nimehukumiwa kunyongwa kwa kosa la kuonekana katika ndoto ya malkia. Malkia kaota kwa sauti akisema ananipenda na hawezi kuniacha milele!”

Wote walicheka, lakini kicheko cha huruma. Hawakuwahi kusikia hukumu ya kustaajabisha kama hii.

Katika hali isiyotarajiwa, mvua kubwa ilinyesha, simanzi ikawakumba wafungwa wale wanne. Ilibaki mvua moja tu, Mako anyongwe!

Japo Mako ni jasiri, kunyesha kwa mvua kulimtetemesha na kumkata maini. Alikiweka kichwa chake katikati ya magoti, asiyeamini hukumu hiyo ya aina yake.

Hata usingizi ulipotaka kumchukua, ulishindwa na hata ulipomchukua, aliota ndoto mbaya akaamka haraka. Baridi ilikuwa kali, lakini kijasho kilimtoka.

Kwa mbali kupitia dirishani, malkia wa nchi ya Kanakantale alionekana akibishana na mfalme. Malkia alivaa vazi refu, pana, jeupe aliloliburuza atembeapo. Mfalme alivaa suruali nyeusi na shati jeupe.

“Umemhukumu kumfunga mtu asiye na hatia, mbaya zaidi anatakiwa kunyongwa… haki iko wapi?” alilalamika Malkia.

“Mimi ndiyo mfalme, wewe ni mwanamke tu. Huna haki ya kuhoji maamuzi haya yametoka wapi? Nchi nzima haithubutu kunihoji utaweza wewe?”

“Hata kama. Hukutakiwa kutoa hukumu ya kifo kwa mtu asiye na hatia. Kumbuka mtu huyu ana familia inayomtegemea. Ana ndugu na jamaa wanaompenda, pia, hukumu hii inawafikirisha watu kama wana mfalme anayejielewa sawasawa…”

Mfalme aliyechoka kubishana, akamchapa kofi kali malkia na kuacha alama ya vidole vitano vionekane katika mashavu laini ya mke huyu wa mfalme. Malkia akalia kwa uchungu lakini walinzi hawakuweza kumsaidia kwa sababu aliyempiga kofi ni mfalme!

Kuona hivyo, akatoka na kuelekea katika chumba cha wale dada wa kazi wanne, dada hawa wamekuwa wasaidizi wake wa muda mrefu nao hukaa chumba kimoja kikubwa katika kona ya kulia ya Kasri la mfalme wa Kanakantale.

Malkia aliingia humo akibubujikwa na machozi, wasaidizi wakampokea na kumkarisha katika kitanda kikubwa cha manyoya.

Inaendelea Kesho...
 
Kwa mwendo huu tutaacha kusoma mpaka iwe na vipande vingi maana unatupia kidogo Sana mkuu angalia kiu ya wasomaji wako please!!
 
Mfalme Anataka Kuniua | Sehemu ya Sita

“Nini kinakuliza Malkia wangu, ni hii habari ya Mako kuhukumiwa kunyongwa!” aliuliza dada yule aliyemsimulia malkia mkasa wa Mako na Simba mzee.

“Ndiyo, mtu asiye na hatia atakufa baada ya mvua mbili kwa sababu yangu.”

“Maskini Mako, ni aheri angebaki katika nchi ya majitu kuliko kurudi tena huku!” alijibu Dada.

“Una mkasa mwingine wa Mako nisimulie tafadhali,” alisema Malkia akifuta machozi. Dada akakaa sawa kusimulia, nao wenzake wote wakakusanyika na kutengeneza kikao cha watu watano.

“Kwa muda mrefu Bwana Mako alitamani kuitembelea Dunia aione yote akiwa juu. Ndipo alipopata wazo la kutengeneza ndege ambayo ingemsaidia kutimiza malengo yake. Umbo la ndege lilitengenezwa kwa mbao za mninga, ndani aliweka furushi kubwa la nyasi ambalo lingetumika kama kiti cha rubani, nyuma ya kiti cha rubani aliweka godoro nene, hili lingetumika kulala pale anapokuwa amechoka na muda huo ndege ingekuwa katika ‘autopilot.’ injini za ndege hii na namna ilivyofanya kazi, ilikuwa siri yake Bwana Mako.

Aliamka asubuhi kabla mkewe na mtoto wake mdogo hawajaamka. Aliandika ujumbe katika kikaratasi, “Nakwenda ziara, nitarudi baada ya siku tatu.” kisha akaelekea mpaka mahali alipoegesha ndege, akaingia humo, alipokaa vyema, akavuta kigingi cha kwanza, ndege ikaunguruma kwa sauti kubwa na kuanza kuserereka taratibu kama maharusi. Baadaye iliongeza kasi, ikaserereka kwa sekunde chache, kisha akavuta kigingi cha pili, ndege ikaanza kunyanyuka juu, hapo akatazama chini kukiona kijiji chake, loooh! Kumbe wanakijiji waliamshwa na yale makelele ya ile ndege, wote walikuwa nje ya nyumba zao, kuona hivyo, akafungua mlango haraka, akawapungia mkono na kuwafanyia ishara ya kwamba angerejea baada ya siku tatu, akimaliza kufanya hivyo, akaufunga mlango.

Ndege ilikuwa imepaa juu kiasi alichokitaka, akagusa kigingi cha tatu, ikawa sawia huku ikisonga mbele, aliweza kuiona Dunia kwa namna alivyotamani. Aliliona bara la Afrika kama alionavyo katika ramani, akaongeza mwendo zaidi, ndege ikawa inatembea mwendo wa kunguru kumi na tisa kwa saa! Alipoiona Afrika ya Kusini, alitamani atue, awacharaze bakora vijana wahuni wa pale, lakini akapanga kurejea siku nyingine.

Mpaka giza linaingia, alikuwa ameliona bara la Afrika, Amerika ya kusini na sehemu kubwa ya bara la Amerika ya kaskazini. Kwa sababu giza lilimzuia kuona, aliamua kutua Marekani ili kukikucha, apae tena na aweze kuendelea na safari yake ya udadisi. Basi akapapasa mkono wake ili akishike kigingi cha nne, masikini! Kigingi hakikuwepo, alisahau kukiweka kwa sababu ya ile haraka yake ya kutaka kuizunguka Dunia.

Ndege iliendelea kupaa, naye akawa anawaza namna ya kutua, akiendelea kuwaza, ghafla aliona kitu kama kilele cha mlima, akashika haraka kigingi cha pili, ndege ikapaa juu zaidi. Lakini kwa sababu ya kule kupaa juu kwa ghafla na kasi iliyokuwepo, Bwana Mako akateleza na kudondokea upande wa nyuma kulikokuwa na kitanda. Alijaribu kurejea katika kiti chake cha rubani lakini hakuweza, basi akabaki kuangalia jinsi ndege ilivyokuwa ikielekea juu asiyejua hatma yake.

Ndege ilikwenda juu kwa kasi kubwa kwa muda wa saa kumi na nne. Muda wote kulikuwa giza. Lakini baadae mwanga ulionekana ghafla na kumshitua Bwana Mako aliyekuwa amekata tamaa. Akiendelea kutazama vizuri ili atambue eneo hilo, ndege ilianguka chini, ikapasuka vipande viwili, bahati njema kumbe alijua angeanguka muda wowote, hivyo alikuwa tayari kajifunga katikati ya godoro na hivyo akanusurika, pengine na yeye angepasuka vipande kama ile ndege yake.

Alisimama haraka na kuanza kuchunguza mahali pale ili abaini alikuwa wapi, japo alitazama kwa jicho la udadisi hakuweza kutambua wala kufananisha. Ilikuwa sehemu ya tofauti, tambalale yenye nyasi fupi ngumu ajabu!

Inaendelea Kesho...
 
Mfalme Anataka Kuniua

Sehemu ya Saba

Akiendelea kushangaa, alishtushwa na sauti ya vishindo, alipotazama mbele, aliona Jitu kubwa refu lipatalo futi hamsini na unene wake ni kama mibuyu miwili. Bwana Mako mwenye futi tano nukta nane, alionekana kiumbe mdogo ilhali Duniani alikotoka yeye ni miongoni mwa watu warefu. Basi kwa kuhofia, alikimbia akajificha nyuma ya mbao mojawapo ya ndege.

“Usijifiche,” jitu lilisema kwa upole, “nimekuona tangu unadondoka na chombo chako. Siwezi kukudhuru kiumbe mdogo.”

Bwana Mako alisogea karibu na Jitu akizungumza, lakini kwa sababu ya ule urefu wake, Jitu halikuweza kumsikia, hivyo lilimbeba likamweka juu ya bega lake mahali palipo karibu na sikio mazungumzo yakaendelea.

“Asante kwa msaada, hapa nipo wapi?” aliuliza Bwana Mako.

“Hapa ni Mailanda, nchi ya mfalme Solupa, katika bara la pili kati ya matatu yaliyopo katika sayari yetu isiyo na jina.” Jitu lilijibu. Bwana Mako akagundua kuwa, ndege yake ilimshusha katika sayari nyingine ya watu hao wakubwa.

Waliendelea kuzungumza, Bwana Mako alisimulia alivyotengeneza ndege yake na jinsi alivyosafiri, alisimulia yote bila kuacha kitu. Mwisho jitu liliahidi kumsaidia kurudi nyumbani, lakini lilimtaka limpeleke nyumbani kwake ili apumzike. Wakati wanaondoka, lilimuweka Bwana Mako katika mfuko wa shati, kisha likayabeba mabaki yote ya ndege kwa mkono mmoja na kuanza kutembea kuelekea uliko mji.

Jitu lilifika nyumbani kwake likiwa limemuweka Bwana Mako mfukoni. Mke wa Jitu pamoja na watoto wake wawili, walikaa sebuleni. Jitu lilipoingia tu, watoto walilikimbilia wakifurahi kurejea kwa baba yao. Hata hivyo, Jitu halikuwa na furaha kwa sababu siku hiyo halikurudi na chochote cha kulisha familia. Kumbe Jitu lilikuwa masikini!

Jitu lilisogea mpaka alipokaa mkewe, likamshika mkono wa utosi kuashiria kwamba halikufanikiwa kupata chochote. Mke wa Jitu asiye na maneno mengi, aliwaamuru watoto waingie vyumbani kulala kuisubiri kesho.

Bwana Mako aliyaona yote haya akichungulia kutoka mfukoni mwa shati alimokuwa. Nalo jitu lilikwenda mpaka katika kitanda kikubwa likakaa na kumtoa.

Bwana Mako asiye na hofu tena, aliliamuru Jitu limuweke sikioni apate kuliambia jambo.

“Rafiki mwema,” Bwana Mako alianza kusema, “nimeona wewe ni masikini, kiasi kwamba huna chochote cha kulisha wanao. Lakini rafiki, nakuahidi kukufanya tajiri mkubwa katika jamii yako.”

“Ha! Ha! Ha!” Jitu lilicheka, “kwa umbo lako, huwezi kufanya kazi yoyote wala jambo ukaondoa umasikini wangu, nadhani utakuwa umechanganyikiwa kwa sababu ya ile ajali kiumbe mdogo.”

“Ni nani huyo unayezungumza naye?” mke wa Jitu aliuliza, kumbe muda wote alikuwa akimtazama mumewe akiwa katika maongezi.

“Kabla sijakuambia, niitie watoto ili niwaeleze kwa pamoja habari za huyu kiumbe mdogo.”

Watoto walifika na Jitu lilisimulia namna lilivyompata Bwana Mako. Mwisho Bwana Mako alikwenda kulala na watoto. Walimbeba na kurushiana kwa zamu, isingekuwa uhodari wao wa kudaka, Bwana Mako angeanguka na kuvunjika mbavu.

Siku mpya ilifika, Bwana Mako na watoto wa Jitu walikuwa wa kwanza kuamka, na tazama akishirikiana na watoto wa Jitu, alikuwa ametengeneza meza kubwa ambayo ilikuwa na kimo sawa na tumbo la majitu. Baada ya kukamilika kwa meza, akashirikiana na watoto kuipeleka nyuma ya nyumba ambako kulikuwa na ukumbi mkubwa, kisha akawaamuru watoto wakamuite baba yao.

“Niliahidi kukufanya tajiri.” alisema Bwana Mako baada ya Jitu kufika.

“Na hii meza ndiyo utajiri wenyewe?” Jitu liliuliza.

Inaendelea Kesho...
 
Mh! Nliacha kusoma siku nne nzima! Leo nimefungua nimekasoma kwa dakika 5 tu! Pamoja na kwamba tunasoma hii stori bure! Na tunashukuru sana! Ila tuna suffer na psychology tortures! Vi scene vifupi mno
 
Mfalme Anataka Kuniua

Sehemu ya Saba

Akiendelea kushangaa, alishtushwa na sauti ya vishindo, alipotazama mbele, aliona Jitu kubwa refu lipatalo futi hamsini na unene wake ni kama mibuyu miwili. Bwana Mako mwenye futi tano nukta nane, alionekana kiumbe mdogo ilhali Duniani alikotoka yeye ni miongoni mwa watu warefu. Basi kwa kuhofia, alikimbia akajificha nyuma ya mbao mojawapo ya ndege.

“Usijifiche,” jitu lilisema kwa upole, “nimekuona tangu unadondoka na chombo chako. Siwezi kukudhuru kiumbe mdogo.”

Bwana Mako alisogea karibu na Jitu akizungumza, lakini kwa sababu ya ule urefu wake, Jitu halikuweza kumsikia, hivyo lilimbeba likamweka juu ya bega lake mahali palipo karibu na sikio mazungumzo yakaendelea.

“Asante kwa msaada, hapa nipo wapi?” aliuliza Bwana Mako.

“Hapa ni Mailanda, nchi ya mfalme Solupa, katika bara la pili kati ya matatu yaliyopo katika sayari yetu isiyo na jina.” Jitu lilijibu. Bwana Mako akagundua kuwa, ndege yake ilimshusha katika sayari nyingine ya watu hao wakubwa.

Waliendelea kuzungumza, Bwana Mako alisimulia alivyotengeneza ndege yake na jinsi alivyosafiri, alisimulia yote bila kuacha kitu. Mwisho jitu liliahidi kumsaidia kurudi nyumbani, lakini lilimtaka limpeleke nyumbani kwake ili apumzike. Wakati wanaondoka, lilimuweka Bwana Mako katika mfuko wa shati, kisha likayabeba mabaki yote ya ndege kwa mkono mmoja na kuanza kutembea kuelekea uliko mji.

Jitu lilifika nyumbani kwake likiwa limemuweka Bwana Mako mfukoni. Mke wa Jitu pamoja na watoto wake wawili, walikaa sebuleni. Jitu lilipoingia tu, watoto walilikimbilia wakifurahi kurejea kwa baba yao. Hata hivyo, Jitu halikuwa na furaha kwa sababu siku hiyo halikurudi na chochote cha kulisha familia. Kumbe Jitu lilikuwa masikini!

Jitu lilisogea mpaka alipokaa mkewe, likamshika mkono wa utosi kuashiria kwamba halikufanikiwa kupata chochote. Mke wa Jitu asiye na maneno mengi, aliwaamuru watoto waingie vyumbani kulala kuisubiri kesho.

Bwana Mako aliyaona yote haya akichungulia kutoka mfukoni mwa shati alimokuwa. Nalo jitu lilikwenda mpaka katika kitanda kikubwa likakaa na kumtoa.

Bwana Mako asiye na hofu tena, aliliamuru Jitu limuweke sikioni apate kuliambia jambo.

“Rafiki mwema,” Bwana Mako alianza kusema, “nimeona wewe ni masikini, kiasi kwamba huna chochote cha kulisha wanao. Lakini rafiki, nakuahidi kukufanya tajiri mkubwa katika jamii yako.”

“Ha! Ha! Ha!” Jitu lilicheka, “kwa umbo lako, huwezi kufanya kazi yoyote wala jambo ukaondoa umasikini wangu, nadhani utakuwa umechanganyikiwa kwa sababu ya ile ajali kiumbe mdogo.”

“Ni nani huyo unayezungumza naye?” mke wa Jitu aliuliza, kumbe muda wote alikuwa akimtazama mumewe akiwa katika maongezi.

“Kabla sijakuambia, niitie watoto ili niwaeleze kwa pamoja habari za huyu kiumbe mdogo.”

Watoto walifika na Jitu lilisimulia namna lilivyompata Bwana Mako. Mwisho Bwana Mako alikwenda kulala na watoto. Walimbeba na kurushiana kwa zamu, isingekuwa uhodari wao wa kudaka, Bwana Mako angeanguka na kuvunjika mbavu.

Siku mpya ilifika, Bwana Mako na watoto wa Jitu walikuwa wa kwanza kuamka, na tazama akishirikiana na watoto wa Jitu, alikuwa ametengeneza meza kubwa ambayo ilikuwa na kimo sawa na tumbo la majitu. Baada ya kukamilika kwa meza, akashirikiana na watoto kuipeleka nyuma ya nyumba ambako kulikuwa na ukumbi mkubwa, kisha akawaamuru watoto wakamuite baba yao.

“Niliahidi kukufanya tajiri.” alisema Bwana Mako baada ya Jitu kufika.

“Na hii meza ndiyo utajiri wenyewe?” Jitu liliuliza.

Inaendelea Kesho...
Duh
 
Mfalme Anataka Kuniua

Sehemu ya Nane

“Ndiyo, meza hii ndiyo utajiri wenyewe, lakini haiwezi kuwa utajiri bila mimi niliyekaa juu yake.”

“Sikuelewi unanichanganya!” lililalamika Jitu.

“Sikiliza rafiki mwema,” alisisitiza Bwana Mako, “watume wanao waende mjini, wawatangazie watu maneno haya: Nyumbani kwa baba yetu, kuna maonyesho hayajawahi kutokea. Mtu mkubwa kutoka sayari iitwayo Dunia, amemtembelea baba yetu, ajabu ni kwamba, pamoja na ukubwa wake huko Duniani, huku anaonekana kiumbe mdogo. Ama kweli kila mkubwa na mkubwa wake. Njoo ujionee kiumbe huyu wa ajabu kwa kiingilio cha pesa mbili tu.”

Jitu lilimwelewa Bwana Mako na liliona ubora wa wazo hilo hata likastaajabu sana uwezo wa akili ya mwanadamu kutoka Duniani.

Basi watoto wa jitu walitembea mjini wakitangaza, “Nyumbani kwa baba yetu, kuna maonyesho hayajawahi kutokea. Mtu mkubwa kutoka sayari iitwayo Dunia, amemtembelea baba yetu, ajabu ni kwamba, pamoja na ukubwa wake huko Duniani, huku anaonekana kiumbe mdogo. Ama kweli kila mkubwa na mkubwa wake. Njoo ujionee kiumbe huyu wa ajabu kwa kiingilio cha pesa mbili tu.”

Kufumba na kufumbua, majitu mengi yalijaa nyumbani kwa Jitu, yote yalitaka kumuona kiumbe kutoka duniani na yalilipa kiingilio cha pesa mbili. Yalipelekwa mpaka katika meza aliyosimama Bwana Mako. Kwa sababu yalikuwa mengi, basi yaligawanywa katika makundi ili yaweze kumuona kwa zamu.

Bwana Mako alifanya michezo ya kufurahisha, kwanza alianza kwa kupiga danadana mpira, majitu yakashangaa. Kisha akacheza mziki, halafu akaruka sarakasi, sarakasi zenyewe hazikuwa sarakasi bali zilikuwa zile za upande upande, ni ushamba tu wa majitu kushangaa sarakasi hizo. Ama naweza kusema, burudani haswaa ilikuwa ni ule udogo wa Bwana Mako katika macho ya majitu. Alitaka kufanya mchezo wa ngumi, lakini alihofia labda majitu yanaweza kuiga na kusababisha vita vya mikono mahali pale, basi badala ya ngumi, akaweka vichekesho.

“Ujinga wa ndoto ni huu, utaota umeokota pesa ukiamka hakuna. Utaota umeokota dhahabu ukiamka kitandani patupu. Ila ukiota umekojoa, unakuta imooo!”

“Ha! Ha! Ha!” majitu yalicheka yakishika mbavu.

Kuna Jitu moja lilisikika likimwambia mkewe, “pesa yangu imekwenda kihalali, pesa mbili, vicheko lukuki.”

Hayo ndiyo yakawa maisha ya Bwana Mako na Jitu. Kazi hiyo iliwapatia pesa elfu mbili kila siku. Pesa hizo ni sawa na shilingi milioni nne za Kitanzania. Jitu likawa tajiri kama lilivyoahidiwa. Halikulala tena njaa, maisha yakabadilika.

Bwana Mako hakusahau kuhusu kurejea nyumbani. Ila, alitaka ashirikiane kwanza na majitu yale ili aweze kuyafahamu zaidi. Pia, aliendelea kuikarabati ndege yake, safari hii, hakusahau kuweka kigingi cha nne, pia alifurahishwa na miti ya kule, ilikuwa migumu kama chuma.

Aliendelea kufanya maonyesho na kushangiliwa na majitu kila siku mpaka taarifa zilipomfikia mfalme wa majitu. Ujumbe ukafika haraka, kiumbe kutoka Duniani, anatakiwa barazani kwa mfalme kabla tonge la kwanza la chakula cha mchana halijaguswa…”

Wakati dada anasimulia, Mfalme aligonga katika chumba kile na kumtaka Malkia aongozane naye haraka. Basi Malkia akasimama asiyetaka huku akiuliza, “Ikawaje sasa, niambie haraka niende…”

“Mako alienda Kwa mfalme…” alijibu dada akiongea haraka, “alipofika kwa mfalme wa majitu akafanya maonyesho kadhaa yaliyokusanya majitu mengi ajabu. Lile jitu lililompokea nalo likapewa cheo nyumbani kwa mfalme hata likasahau habari za umasikini wa awali. Baada ya kuwa amekaa kwa muda wa miaka miwili, Mako akamuomba mfalme huyo amsaidie kurejea Duniani kwa lengo la kuwatoa hofu ndugu na jamaa zake ambao wanaweza kudhani kuwa amekufa. Basi Mfalme wa Majitu alimsaidia Mako kurejea na tangu arejee hajarudi tena huko japo njia anaifahamu.

Alimaliza dada kusimulia. Wakati huo mfalme alikwisha fungua mlango na kumkamata mkono Malkia aliyekuwa amesimama kisha akatembea naye haraka kuelekea alikojua yeye.

Inaendelea Kesho...

Msisitizo:
Niliahidi hapo juu kwamba, hadithi hii itakwenda mpaka mwisho bure bila janjajanja yoyote. Nimefurahi kuona maoni ya wasomaji hapa, lakini nimeshtushwa na malalamiko yanayosema natuma vipande vifupi. Inawezekana ni utamu wa simulizi ndiyo unafanya vipande vionekane vifupi, au labda vipande ni vifupi kweli. Binafsi sitegemei hadithi kuendesha maisha, nafanya kazi zingine na muda kidogo niupatao, ndiyo nautumia kuwaletea hivyo vipande kila siku. Tujadiliane wote kwa pamoja, niache kazi, niwekeze muda mwingi katika kutuma vipande virefu vya simulizi, wanangu watakula hadithi?

Mjadala upo wazi.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom