MAGNUM22
Sehemu 17
SEHEMU FULANI HUKO SOMALIA
KIKOSI cha vijana kama elfu moja waliovalia nguo za kijeshi na kujifunga vitambaa vichwani mwao na wengine wakiwa wamevaa soksi usoni, kila mmoja alikuwa na bunduki kubwa ya kisasa yenye nguvu mkononi mwake, walikuwa wamesimama kimya katika vikosi vya watu mia moja mia moja huku kila kikosi kikiwa na bendera nyeusi. Licha ya kuwa na silaha hizo nzito, kila mmoja alikuwa na sime kiunoni mwake.
“TUNAUTAKA UMOJA WA NCHI ZA AFRIKA KUIGAWA JAMHURI YA SOMALIA NA KUWA NCHI MBILI HURU!” alisikika mtu mmoja aliyekuwa amesimama mbele yao juu ya kijukwaa kidogo, akiwa na kipaaza sauti mkononi mwake.
“MAZUNGUMZO YA MWISHO YATAFANYIKA WIKI MOJA IJAYO, HIVYO WAKIKUBALI, ARDHI HII TULIYOSIMAMA ITAKUWA NCHI YETU, WAKIKATAA TUTAANZISHA VITA ISIYO NA MWISHO!” akawaambia na wao kwa kutii agizo hilo, wakainua bunduiki zao na kupiga risasi juu mara tatu.
Baada ya taarifa hiyo wanajeshi hawa wakatawanyika na kuingia katika maficho yao ya kila siku. Fadicky Al – Habib aliteremka kwenye kile kijukwaa na kuvuta hatua huku akifuatwa na vijana wengine wanne ambao nao walivalia kijeshi kama wale wanajeshi.
“Unafikiri watakubaliana na matakwa yetu?” mmoja wa wale vijana akamuuliza.
“Wasipokubali ndipo watakuwa wamefungulia bomba la damu katika ardhi hii,” akasimama na kumwambia yule kijana, “Jaffer anahitaji kitu kimoja tu, ardhi ya mama zetu, hivyo wasipoitoa kidiplomasia wataitoa kwa mtutu wa bunduki,” kisha akaendelea kutembea na kuingia ndani ya hema ndogo yenye ulinzi mkali kwa nje. Wakaketi katika zuria kubwa na la kisasa, wanadada wawili warembo wakapiga magoti huku na huku wakimkandakanda mabega.
“Yusra, jiandae, weka watu wako vizuri, siku isiyojulikana tutaondoka hapa kuelekea Addis!” akamwambia yule kijana.
* * *
DAR ES SALAAM
OFISI YA MUDA YA BARAZA LA USALAMA LA A.U
Kikao cha wajumbe wale wale kilikutana tena katika afisi hii iliyoteuliwa kuhifadhi nyaraka zote za kiusalama kwa kipindi hiki. Usiku huu kama walivyoitwa na Mwenyekiti wa baraza hilo walifika na akidi ilitimia. Madam S alikuwa ameketi katika kiti chake kile kile na wajumbe wengine nao vivyo hivyo.
“Kama tulivyoelekezana kuwa kwa kazi hii tutaitana muda wowte hata kama ni usiku wa manane kama leo hii … nimekuitena kwa sababu kuna jambo ambalo limejitokeza na lazima lifanyiwe kazi. Kikao cha dharula cha wadau wa AU baada ya kukutana jana pale Addis, kimeamua kwamba ufanyike mkutano wa mazungumzo kati ya AU na huyu Bwana Jaffery Bakhary ili kufikisha mwisho mgogoro huu…” akalieleza jopo hilo ambalo lilikuwa kimya kabisa likifuatilia nini mkuu huyo anataka kusema.
“Hivyo basi siku saba zijazo kutafanyika kikao hicho ndani ya ukumbi mdogo wa mikutano katika jingo letu la AU Headquaters. Dhumuni la kikao hiki sasa ni kwamba sisi kama baraza la usalama la jumuia hii tunatakiwa tuandae ullinzi wa kutosha kuwalinda viongozi wetu siku hiyo. Sasa nakaribisha mawazo yenu ni jinsi gani tutaweka ulinzi eneo hilo,” akamaliza na kuzima kifaa chake cha kuzungumzia.
“Tupo kwenye harakati za kuwasaka hawa jamaa wanaofanya mauaji ya viongozi … sasa na tena tunaandaa kikao cha viongozi hao hao, Mwenyekiti huoni kama tunaweza kuwa tunarahisisha kazi kwa wauaji kutekeleza mpango wao?” mjumbe mmoja akauliza.
“Lakini je, huoni kuwa inawezekana kuwapata wauaji kirahisi kama watakuja mahalia hapo, na najua kwa vyovyote watakuja kwa sababu ni wafuasi wa mtu huyu, nsiyo maana nataka tujadiliane jinsi ya kuweka ulinzi huu na kuhakikisha tunamtazama kila mtu,” yule mwenyekiti akasema. Ukimya ukajidai kwa nukta chache kisha mjumbe mwingine akakohoa.
“Kwa hiyo tunafanyaje? Vijana tuliowasambaza tunawarudisha na kuwapeleka Addis au tunaunda kikosi kazi kingine?” mwingine akauliza.
“Ndiyo nataka tuone pamoja kama tunawapa kazi hawahawa au hawa tuwaache na misheni yao kule waende wengine…. Tuweke mawazo pamoja!” mwenyekiti akaeleza.
“Mjue mnapambana na nani!” Madam S akawaambia, “wale au yule kama ni wauaji au muuaji mwenye profesheno yake katika kazi msifikiroi atajileta kirahisi hivyo au atatumia mbinu ile ile. Tazameni alivyoua Angola sivyo alivyoua Ivory Coast … alipojaribu kutumia mbinu ileile hapa Tanzania tukampa ambush ya nguvu hata silaha yake akaicha hapa, sasa unafikiri kama atakuja Addis atatumia mbinu hiyo hiyo?” akawaacha kwa swali.
“Sure! Anachosema Madam pale ni sahihi kabisa, inabidi tutanuke na tunuse katika kila kitu ikiwezekana tupenyeshe watu wetu kwenye kona zote muhimu, ili waangalie kila kitu kwa ukaribi zaidi…” mjumbe mwingine akasema.
Kikao kikaendelea na mipango mingi ikasukwa kwa ajili ya siku hiyo, wakatakiwa kukusanya wana intelijensia kutoka sehemu tafauti za Afrika ili kuwapenyeza kwa siri katika Jiji hilo kuweka usalama. Lakini katika uteuzi wote huo haikuguswa idara nyeti ya TSA, kwa kuwa ilisemwa kuwa Tanzania imeshindwa kuongoza operesheni hiyo tangu awali, hata Madam S alipotaka kutetea hilo hakusikilizwa,”
“Kwa kuwa hawa washenzi walitaka kutekeleza mauaji ndani ya nchi hii, vijana wangu wataendelea kuwasaka popote walipo katika dunia hii bila kujihusisha na kikosi cha AU…” Madam S akazungumza kwa hasira.
“Sasa mjumbe kutoka Tanzania, kumbuka kijana wako unayemtegemea sana mpaka sasa hajulikani alipo, utampelekea nani tena huko, hili swala liache, tutalifanyia kazi kama kamati…” mwenyekiti akasema.
“Sina kijana mmoja, ninao zaidi ya mia tano wazuri kuliko yule. Ninachotaka nikwambie ni kwamba, siridhiki na mwenendo wa kamati hii, kuna ulakini hapa, leo sintosema lakini nitakuja kuwaambia bado nafanya uchunguzi wangu… si ajabu kuna watu au mtu anajua kila kinachoendelea lakini anajifanya msafi…” Madam akazungumza huku tayari anataka kuondoka.
“Mjumbe, naomba utangue kauli yako… ina maana humu ndani kuna msaliti, unamaanisha hivyo? Yaani sisi wenyewe ndiyo tufanya mauaji ya viongozi wetu?” akaongea kwa ukalia.
“Mi sijasema hivyo, ila hayo umesema wewe…”
“Wewe lazima ushughulikiwe, we mwanamke wewe lazima ushughulikiwe na kamati ya nidhamu,” Mwenyekiti akaongea huku kijasho kikiwa kinamtoka, akaketi na kushuhudia mwanamke huyo akiishia nje ya jengo.
“Aaaaaaggghhhh!!!! Ameniuzi kabisa bullshit!” akang’aka na kuinuka kitini, akaingia katika mlango mwingine na kujifungia maliwato kwa dakika kadhaa, kisha akarudi kuungana na wengine na kikao kikaendelea.
* * *
USIKU HUO HUO
Katika makutano ya Barabara ya Morogoro na Bibi Titi, Madam S alikuwa akikatisha usiku huo kuelekea ofisi ndogo. Mara kutoka barabara ya upande wa pili alisikia sauti kali ya gari, akageuka na kuona Land Rover nyeusi ikiwa mita mbili kutoka kwake, kabla hajafanya lolote, kishindo kikubwa kikasikika. Lile Land Rover likaipamia gari la Madam S na kulisukumia pembeni, likatupwa na kubingirita upande mwingine, lile Land Rover likakaa barabarani vizuri na kuendelea na safari kwa kasi kuelekea upande wa Mahakama ya Kisutu.
Usiku huo kulikuwa na watu wachache sana barabarani, hawakuzidi hata kumi, wakawahi kufika katika lile gari na kushuhudia uharibifu mbaya. Madam S alikuwa amebanwa na mkanda wa kiti alichokaa, hakuweza kutoka, damu zilikuwa zikimwagika kichwani. Kazi kubwa ilikuwa ni kumnasua mama huyo ili angalau wamweke pembeni apate upepo. Vibaka nao hawakuwa mbali aliyechukua simu akafanya hivyo aliyenyofoa redio haya.
Dakika kama thelathini baadae, gari la polisi likawasili eneo hilo, itifaki za kusalama zikaendelea na kumkimbiza mwanamama huyo Muhimbili, mpanga dakika hiyo hakuna mtu aliyemgundua majeruhi huyo.
Na huko Shamba TSA members walikuwa wakiendelea na shughuili zao, kila mmoja akiwa katika jukumu lake analopaswa kufanya. Simu ya mezani ikaanza kuita kwa fujo, haikuwa mbali sana na pale ambapo Chiba alikuwa ameketi.
Nani anayepiga hii simu? Akajiuliza huku akisukuma kiti chake kidogo ili kuifikia. Kila mmoja alishangaa kwa mwito huo maana simu hiyo inaweza ikakaa hata miezi miwili isitumike nah ii ni kwa sababu ni ya siri sana, njia zake zimefungwa kitaalamu kiasi kwamba haziingiliani na simu za kawaida. Ikiita ama inatokea Ikulu, Makao makuu ya Usalama wa Taifa na watu wachache wenye namba hiyo wasiozidi wane Tanzania nzima. Wote wakaikaribia wakati Chiba akiinyakuwa na kuiweka sikioni huku tayari kitufe cha kurekodi kikiwa kinafanya kazi.
“… umesema? … nheee…. Usiku huu au?” Chiba alionekana kuhamanika kwa simu aliyokuwa ameipokea. Baada ya hapo akakata na kuiweka mahala pake, akageuka na kukutana na macho nane yakimtazama.
“Vipi?” Amata akwa wa kwnza kuuliza.
Chiba hakujibu zaidi ya kuwatazama tu.
“Chiba nini?” Gina akadakia kuuliza.
“Madam S amepata ajali usiku huu kama saa moja au dakika arobaini na tatno zilizopita,” Chiba akawaeleza.
“What?”
Amata akang’aka na kuwaacha wenzake, dakika chache baadae akarudi akiwa keshavaa koti lake, “Simu imepigwa na nani?” akauliza.
“Inspekta Simbeye!”
“Smbeye?” akauliza na kuchukua simu yake, akapiga namba za inspekta huyo na kuzungumza naye machache kisha akaitua na kuitia mfukoni.
“Ok! Dkt. Jasmine, Scoba na Chiba nendeni Muhimbili haraka sana mkaweke mambo sawa, Mimi na Gina tunaenda eneo la tukio. Dakika ya tisini tuwasiliane,” Amata aatoa maagizo na kila mmoja akatawanyika tayari kwa kazi aliyopewa.
ENEO LA TUKIO
Gina aliegesha gari kando kando ya wigo wa Chuo Cha Ufundi Dar es salaam (Dar Tech) na wote wakateremka na kuelekea eneo hilo ambalo lilizungukwa na askari wa usalama barabarani na wale wa kawaida ambao walikuwa na silaha mikononi mwao. Amata na Gina wakawasabahi askari hao na kusogea pale lilipokuwa gari lile. Askari wenye silaha wakawazuia kwa kuwa tayari breakdown lilikuwa kwenye mchakato wa kuinua na kuivuta mpaka kituo cha polisi. Mazungumzo ya sekunde chache yakafanyika na Amata akaruhusiwa kusogea eneo lile, moja kwa moja akazunguka upande wa mlango wa dereva na kupenyeza mkono kwa upande wa chini, alipoutoa alikuwa na vitu viwili mkononi mwake; bastola ndogo ambayo haraka aliipachika kiunoni na kitu kingine kama pakiti la sigara lakini hiki kilikuwa cheusi, akakitia mfukoni na kutoka eneo hilo. Kando akakutana na askari mmoja mwenye sare nyeupe aliyekuwa na faili mkononi mwake na kuonekana akiandikaandika vitu fulani.
“Mmefanikiwa kuona gari lililosababisha ajali?” akamuuliza.
“Hapana! Inaonekana hawakusimama, kwani sisi tumefika kwa kuchelewa kidogo,” akajibu. Amata akatulia kidogo.
“Una undugu na huyu mama?” yule askari akamuuliza.
“Ndiyo, ni mama yangu…”
“Oh pole sana, wahi Muhimbili, hali yake sijui kama atapona,” sentesnsi hii ya mwisho iliufanya moyo wa Amata kupaa kwa hofu, haraka akarudi garini na kuketi kitini, akashusha pumzi ndefu.
“Vipi?” Gina akamtupia swali.
“Hali ya mama ni mbaya,” akajibu huku akichukua simu yake na kabla hajabofya namba yoyote ikaita, akaichukua na uiweka sikioni.
“Chiba!” akaita.
“Mama yupo mahututi,” Chiba akamwambia Amata.
“Nipo njiani kaka!”
Gina akawasha gari na safari ya Muhimbili ikachukua nafasi, “Ni ajalia au?” Gina akauliza.
“Siwezi kujua kwa sasa, lakini nitachekecha vizuri akili tutajua tu, hata gari iliyofanaya ajali itapatikana tu,” Amata akajibu wakati gari likiiacha Barabara ya Umoja wa Mataifa na kuchukua Mtaa wa Mindu kuelekea katika hospitali hiyo.
Hatua za harakaharaka zikawafikisha katika jengo la wagonjwa mahututi, wakaingia kadiri ya utaratibu wa wodi hiyo. Ndani ya chumba cha pekee Madam S alikuwa amelala kimya huku mashine ya oksijeni ikiwa puani mwake na ile ya kufuatilia mwenendo wa moyo nayo ilikuwa ikionesha mapigo hafifu. Daktari Jasmini alikuwa hima hima na madaktari wengine wakijaribu kufuatilia kila kinachoendelea kwa mgonjwa wao.
“Tunafanyaje?” Chiba akamuuliza Amata wakati tayari wakiwa nje ya jingo hilo, saa ya mkononi mwa Amata ilionesha saa nane usiku.
“Tutulie tu na tufuatilie kila kitu kwa ukaribu, ila kwa sasa tuzuie kila baya kama lipo, tutafanya hivi; Gina tunakuacha hapa na Scoba, muangalie usalama wa Mama kama mnahisi au mnamhisi yeyote kutaka kufanya baya, hakikisheni mnashughulikia. Madam S asiguswe na mtu yeyote kitandani iwe kuchomwa sindano au kufanyiwa tiba yoyote zaidi ya Dkt Jasmine, muwe macho. Mimi na Chiba kuna mambo tunayaweka sawa kisha tutawasiliana…” akatoa maagizo.
“Sawa, umesomeka mkuu…” Gina akajibu.
Chiba na Amata wakaingia garini na kutokomea zao. Breki ya kwanza ilikuwa katika kituo polisi kati, hapo wakakutana na Inspekta Simbeye ndani ya afisi yake chakavu ambayo hata haina mpangilio vizuri.
Mzee huyo aliyebwaga moyo wake kitini huku miguu yake mifupi ikiwa juu ya meza, aliwakaribisha wageni wake na kisha akaketi vizuri kwa mazungumzo.
“Tumekuvamia!” Amata akamwambia.
“Na nilijua mtakuja,” Simbeye akawajibu, “kwanza poleni sana kwa yaliyotokea…”
“Asante sana, tunasikitika sana na tunamhitaji huyo aliyefanya hivi, kwa akili yangu mbaya najua wazi kuwa si ajali ya kawaida,” Amata akamwambia Simbeye.
“Ndiyo, upo sawa, Kamanda … mnazungukwa! Naanza kung’amua kitu…” Simbeye akasema.
“Utu uzima dawa, nambie baba labda utaifungua akili yangu iliyolala,” Amata akamwambia simbeye huku akijiweka sawa kitini. Inspekta Simbeye, hakuzungumza kitu, akachukua simu yake na kumpatia Amata, naye akatupia jicho juu ya kioo na kuusoma ujumbe uliyoandikwa.
‘Usiku huu nitafanya msilolitegemea, free Somali Land’
Baada ya kuusoma ujumbe huo akatazama saa ngapi ulitumwa, akagundua kuwa haikupita hata saa tatu ni saa mbili na dakika kadhaa. Tofauti kati ya muda wa ajali na muda was ms ile ni dakika kama ishirini na nne hivi.
“Nini hiki?” akauliza huku akimpa Chiba simu ile.
“Utashangaa kwa kuwa hujui hili, huu si ujumbe wa kwanza ni wa tatu sasa, na namba ndiyo hii, ‘unknown’, Chiba pale anajua na imemtesa sana kuifuatilia,” Simbeye akasema. Amata akamtazama Chiba kana kwamba anamuuliza, ‘ni kweli?’
Namba zake zimefungwa kwa code ngumu sana, nimejaribu mara kadhaa lakini nimeshindwa kumpata mtumaji…”
“Na umeamua kuacha?” Amata akauliza.
“Si kuacha ninamsaka bado, nitamtia nguvuni tu, na asije kujaribu siku akapiga simu ndiyo utakuwa mwisho wake,” Chiba akazungumza kwa uchungu.
“Simbeye, mimi naweza kuichukua ajali hii kama hujuma katika sakati ambalo tunadili nalo kwa sasa, kwa mbali ninaanza kuona nini kinajiri, nakuhakikishi, huyu mpumbavu nitamleta hapa umle nyama,” akasema na tayari akawa wima kwa safari.
“Unaenda wapi?” Simbeye akamuuliza.
“Nataka niwe karibu na Madam S, ili akiamka tu anambie nini kimemsibu,” akajibu.
“Good! Hata mimi nipo kwenye kumtafuta juha huyu, nikipata fununu nitakwambieni, ila kwa sasa tuondokeni wote kwenda Muhimbili,” akawaambia kisha wote watatu wakatoka na kuingia garini. Safari ya kuelekea Muhimbili ikaanza, wakapita barabara ya Bibi Titi ili makusudi kufika eneo la tukio, wakati huu kulikuwa kimya hakuna mtu.
“Walizamilia kumuua,” Chiba akasema.
“Na hawatampata!” Chiba akajibu huku tayari wakiingia katika uwanja wa hospitali hiyo, haraka haraka wakateremka na kuliende jengo la wagonjwa mahututi. Wakiwa hatua chache kabla ya kulifikia lango kuu wakakutana na watu kama wane hivi waliokuwa wakizungumza kwa lugha ya Kifaransa, Amata akasimama na kuwatazama, kisha akamtazama Chiba.
“Vipi unawajua?” akamuuliza.
“Hapana, isipokuwa mmoja wao kama nimewahi kukutana naye vile,”
“Wapi?”
“Sikumbuki, ila nimewahi kukutana naye,” akajibu kisha wakaingia ndani na kumkuta Scoba na Gina wakiwa katika ulinzi madhubuti. Gina akaamka mara moja na kumuendea Amata.
“Vipi Kamanda… tetesi yoyote?”
“Hakuna kitu, mbingu bado nyeusi!”Amata akajibu huku akimshika mkono na kumvutia pembeni, kisha kwa sauti ndogo ya kuwatosha wao akamnong’oneza.
“Kuna watu wamekuja hapa kumwona mama?”
“Ndiyo wamekuja, lakini tumewakatalia kuingia, kwani hamjapishana na watu fulani hapo nje?”
“Ndiyo maana nimekuuliza…” Amata akamwambia. Wakati wao wakijifanya kuongea peke yao kumbe Inspekta Simbeye amewasiki vyema kabisa, na Amata alipachana na Gina na kurudi kuungana na wengine, Simbeye akamwambia.
“Ina maana we wale huwajui?”
“Hapana, ila mmoja nimeshawahi kukutana sehemu…”
“Wajumbe wa Baraza la Usalama la AU ambao wameweka kambi hapa Dar kwa ajili ya kuendesha oparesheni ile ya kumsaka muuaji shetani,” akamwambia.
Muda huo huo, Dkt. Jasmin akaungana nao, haraka, Simbeye na Amata wakamdaka juu kwa juu na kumvutia pembeni kwa mazungumzo.
“Vipi, mmegundua nini huko?” Amata akawa wa kwanza.
“Madam hajaumia yaani kupata majeraha, ila inaonekana amejipiga kichwani ndo maana amepoteza fahamu..”
“Ndani ya kichwa hakuna tatizo kubwa?” Simbeye akauliza.
“Hapana, hajapata tatizo lolote baya, na ataamka tu, tunaamini atakuwa na kumbukumbu zake sahihi kabisa,” Jasmine akawajibu na kila mtu moyo wake ukatua.