MAGNUM 22
Sehemu 22
Hoteli ya Blue Moon
Kamanda Amata alijibwaga kitini, akakitoa kile kitabu alichopewa na yule mwanamke, akakiweka mezani kisha akijimiminia pombe katika bilauri yake na kupiga mafunda mawili tu, ikaisha, akjimiminia tena na kupiga funda moja kisha akitua mezani. Baada ya ukimya wa sekunde kadhaa akiwa katika kutafakari jambo, akapeleka mkono na kutaka kuchukua kile kitabu. Mbisho wa hodi ukamshtua, akachomoa bastola yake na kuiweka tayari. Hodi ile ikarudiwa tena.
Jinsi ilivyokuwa ikigongwa, haikuwa ngeni masikioni mwake kwani kati idara ya TSA kila mmoja alikuwa na jinsi ya kugonga hodi au kengele ya mlangoni. Ijapokuwa alijua kuwa hiyo ni code ya Gina, Amata hakutaka kukubaliana na moyo wake.
Trust no one! Akajisemea moyoni huku akiinuka taratibu na bastola yake mkononi, akauendea mlango na kukinyonga kitasa taratibu. Akaufungua mlango huku yeye akibaki nyuma yake.
“TSA 5!” Gina akatamka kabla ya kuingia ndani. Kamanda Amata akajitokeza baada ya kusikia sauti tamu ya msichana ampendaye. Wakakumbatiana kwa nguvu na kupeana mabusu motomoto, hata sekunde kumi hazikupita wakaangushiana kitandani na kupeana mahaba mazito waliyoyamisi kwa siku nyingi. Saa nzima ya pilika pilika za kitandani ilipokwisha, wakasindikizana maliwatoni na kujiweka sawa, kisha wakarudi tena chumbani.
“Mmefika lini?” Amata akamuuliza. Hili ndilo lilikuwa swali la kwanza la Amata kwa Gina tangu wakutane saa moja iliyopita.
“Leo hii mida kama ya saa nne au tano hivi,” akajibu.
“Umejuaje kama niko hapa?”
“Nipo na Chiba…”
“Aaaa basi hapo lazima mnipate. Sasa inabidi tutafute pa kuweka kambi maana mambo tayari yameiva, mi nimeshaliamsha dude,” Amata akamwambia Gina.
“Kinachotakiwa ni wewe kufunga kilicho chako hapa na kunifuata, tayari tumepata kambi ambayo Madam S alikwishaiandaa kwa siri…”
“Iko wapi?” Amata akauliza.
“Just do kile nimekwambia!”
“Sawa Kiongozi,” Amata akajibu na kuanza kuweka vizuri vikorokoro vyake, dakika kumi baadae alikuwa tayari kwa safari. Katika meza ya mapokezi akahakikisha ameipia kila kitu na hakujibu hata swali moja la mhudumu. Wakaingia garini na Gina akashika njia na kutokomea mjini.
“Vipi, hatuna msindikizaji?” Gina akauliza.
“Tupo peke yetu tu,” Amata akajibu huku akirudisha macho yake kutoka nyuma kuja mbele. Mwendo nusu saa uliwafikisha katika jingo lile lile upande wa maegesho. Gina akaegesha gari na kuteremka akifuatiwa na Amata, wakachukua mizigo na kupita katika njia ile aliyoelekezwa na Archimedeus.
“Karibu sana Kamanda!” Chiba akamkaribisha katika sebule ile waliyokabidhiwa.
“Asante sana, nashukuru kwa kuwa mmekuja, vipi bibi anaendeleaje?” Amata akauliza.
“Nimewasiliana naye si muda mrefu, yuko poa na ameruhusiwa kurudi nyumbani,” Chiba akaeleza huku akiweka kando mkoba wa Amata alioutwaa toka mabegani pake pindi tu alipompokea.
“Hatuna budi kuanza kazi mara moja kwani muda unakimbia,” Chiba akasema na Amata akaafiki kwa kichwa, “mpaka sasa duru zote zinaonekana zikiamini kuwa Gupter hayupo nchini hapa…”
“Ni hatari sana kwa sababu watalegeza ulinzi wakati mshenzi huyu na timu yake wamejaa tele ndani ya Addis!” Amata akamkatisha na kumjibu. Gina na Chiba wakashtuka kidogo.
“Yupo?” Chiba akauliza.
“Kabla ya yote mmekagua hiki kiapartment, kusije kuwa kuna watotot wanatusikiliza tu!” Amata akawaambia akimaanisha kama kuna vinasa sauti vya siri.
“Aaaaa Kamanda, hilo ni jukumu la kwanza, unaona kifaa hiki hapa…?”
“Yap!”
“Hiki ni kifaa kipya kabisa, hapa kilipo kikigundua tu kuwa tunasikilizwa kitapiga kelele; kwa ukimya wake ujue mambo shwari,” Chiba akamwambia.
“Ok! Gupter na washenzi wake wameingia hapa masaa ishirini na nne hivi au arobaini na nane labda…”
“Una uhakika?” Gina akauliza.
“Huwa sibahatishi mama! Mi nimefika hapa nikitokea Sierra, pale nilipata namba ya mtu wa huku ambaye nahisi Gupter alikuwa akiwasiliana naye…”
“Yupo wapi tumtaiti mapema?” Chiba akawahi kuuliza.
“Umechelewa Chiba, ndiyo maana kuna TSA 1 na TSA2, wewe ni 2, kwa maana hiyo 1 alishafanya kazi na huyu mshenzi tayari anahemea kuzimu,” Amata akaeleza.
“Umemuua?” Gina akauliza.
“Hakukuwa na jinsi kwa maana ningemwacha hai angeweza kuwapa taarifa ‘kina Guter kuwa nawasaka, hivyo mpaka sasa hata wao hawajui kuwa nipo, ukizingatia wanaamini kuwa mimi ni mfu na ninaoza tu kwenye kaburi la pamoja…” Amata akaeleza.
“Nakuamini Kamanda, lazima uoneshe heshima ya cheo chako,” Chiba akamsifia.
“Sasa ipo hivi, yule Mtaliano ni tajiri wa kukodisha majumba ya kuishi na ana nyumba zake huko mashambani, na kati ya nyumba hizi moja wapo kwapangisha kina Gupter…”
“Wapi huko?” Gina akadakiza swali.
“Aleltu!”
“Aleltu, Aleltu, Aleltu!!!”
“Huwezi kupajua bwana,” Amata akamwambia Gina huku akiweka mezani kile kitabu cha ramani, akakifungua na wote kwa pamoja wakaanza kuisoma ramani hiyo ya Jiji la Addis na viunga vyake. Wakati Gina na Amata wakisoma, Chiba alikuwa akitafuta katika mtandao, eneo lilipo, namba za nyumba na wamiliki.
“Batlomino Augusto!” akatamka baada ya kupata tafutishi za kutosha, “Hapa kuna nyumba namba na mtaa,” akaeleza Chiba.
“Twendeni tukavamie tumalize mchezo!” Gina akapendekeza.
“Mmmmmh Gina kila mara namkwambia, ‘don’t put your best foot forward’. Adui kama huyu si bwege kama waliokula pesa za EPA, wakati mwingine mwache adui hata anywe chain a wewe ukiwa unamwangalia tu kwa sababu huo si wakati mzuri wa kufanya uvamizi,” Amata akamwambia Gina.
“Unamaanisha nini, tumwache mpaka afanye mauaji mengine hapo kesho?” Gina akaongea kwa uchungu.
“Si hivyo, ili kumtia mbaroni muuaji mwenye taaluma kama huyu inabidi kwanza umsome aina yake ya kuua; anavizia? Anadhamiria? Au anafanyaje… Gupter lazima tumstadi kwa muda mrefu…”
“Hatuna muda Amata, time is now!” Gina akang’aka.
“Sikiliza Gina, wenzako tulishaanza kumstadi huyu mjinga miezi miwili ilopita, na tumegundua kwamba, mauaji aliyotaka kuyafanya Dar es salaama ndiyo atakayoyafanya hapa, nikiwa na maana kuwa, atatekeleza mauaji baada ya kikao, huo ndiyo mpango,” Amata akasema.
“Sasa tufanyaje, tuwasake tuwatait usiku huu au tufanyeje?” Chiba akauliza.
“Hawa lazima watembelewe usiku huu huu, na kukiwakuta hatakiwi kuachwa mtu, ni kuwatia tunduni tu!” Amata akasisitiza. Akaitazama saa yake, tayari ilikuwa ni saa nane inaenda tisa za alasiri.
* * *
Hoteli ya Golden Tulip – Addis Ababa
Kama ni ulinzi basi hapa ulikuwa umeimarishwa, kila aliyekuwa akiingia ndani ya hoteli hii alikuwa akipekuliwa vilivyo. Mitambo ya kisasa ilifungwa pande tafauti za hoteli hiyo kuanzia juu mpaka chini na kuhakikisha hata akipita mende anaonekana. Alasiri hiyo Martin Gupter aliegesha gari katika eneo la kuegeshea la hoteli hiyo. Ndani ya gari lake alikuwa yeye na Fredy huku wakimwacha Amanda akiwasili na gari lingine.
“Lazima tuujaribu ulinzi!” Guter akasema.
“Huo ni mchezo wa hatari sana kaka,” Fredy akamwambia.
“Sikiliza, mimi kwangu ni mchezo wa kawaida sana kwa sababu nimeshafanya kazi hiyo kwa miaka mingi, najua nini na nini cha kufanya na nijikute ndani ya hoteli…” akasema.
“Ok! Jaribu…. Unataka kuingia?”
“Yeah! Nataka kuingia na kunya bia moja, we nisubiri hapa,” Gupter akamwambia Fredy na kushuka, moja kwa moja akauendea mlango wa hoteli hiyo ambao mbele yake kulikuwa na askari kama wane hivi wakiwajibika huku na huko, kumkagua huyu na yule.
Sasa hii ni hoteli tu kwa ajili ya chakula cha jioni, huko wanakolala kuna ulinzi gani! Guter akawaza wakati akipandisha ngazi za kuingia ndani.
“Hey man! Stop for inspection please!” askari mmoja alimuomba asimame kwa ukaguzi, Gupter akafanya hivyo. Akapekuliwa kila kona ya mwili wake, na upande mmoja wa koti akakutwa na bastola, ikachomolewa.
“We ni mgeni wa hoteli hii?” akaulizwa.
“No, ila mara kadhaa hupenda kuja kupata kinywaji kidogo au kucheza poker,” Gupter akajibu.
“Sawa, sasa hutoruhusiwa kuingia na hii silaha, ni hatari kwa sasa, utaiacha hapa, na kuichukua ukitoka,” yule askari akamwambia. Wakati Gupter akimsikiliza, kulikuwa na askari mwingine akimtolea macho kijana huyu wa kizungu mwenye mustachi wa wastani na ndevu za kuote kwa mbali na sura yake ni kama iliwahi kuungua miaka mingi nyuma. Gupter alimwona askari huyu akahisi labda amemgundua, akapiga moyo konde.
“Ok, waweza kuendelea na safari yako,” akaruhusiwa. Hatua kama kumi mbele akasikia sauti ikimwita.
“Hey man!!!” askari yule yule wa kwanza akamwita tena.
Ohoooo huku kuitana mara mbili kuna jambo! Gupter akawaza na kugeuka kiuvivu kidogo.
“Wallet yako hii,” akaambiwa. Kumbe wakati anasachiwa alikuwa ameweka waleti mezani na kuisahau hapo.
“Asante sana!” akashukuru na kuichukua kisha akaingia zake ndani.
Kutoka katika maegesho, Amanda akashusha darubini yake na kushusha pumzi ndefu, akaiweka kando na kutulia kwa sekunde kadhaa. Akafungua mlango na kushuka, akaufunga kwa mguu nyuma yake na kuvuta hatua kuelekea kwenye vibanda vya kuuza mambo ya utamaduni, huko akapoteza kama saa nzima hivi akinunua hiki na kuangalia kile, lakini yote hayo yalikuwa geresha tu, lengo kuu lilikuwa ni kupata habari mbili tatu kutoka kwa wananchi hao.
Baada ya saa moja kupita, Martin Gupter akatoka kwenye mlango ule ule na kuchukua bastola yake, kisha akavuta hatua na kulielekea gari la Amanda akaingia na kuketi.
“Vipi?” Amanda akauliza.
“Ulinzi mwepesi sana kwa mtu kama mimi, nitaingia na kufanya yangu pindi ikibidi na nikitakiwa kufanya hivyo. Twende sasa tukaonane na Fadick,” akamwambia Amanda.
“Unapajua alipo?”
“Ndiyo maana nikakwambia twende,” Gupter akajibu na mwanamke huyo akaliondoa gari na mita chache nyuma akafuatwa na Fredy.
Drunken Hamidou
Mara alipotoka uwanja wa ndege, kijana huyu mpelelezi machachri wa jumuia ya ECOWAS akafika katika chumba cha siri ambacho yeye na wenzake wawili walioteuliwa kuunda timu ya kipelelezi ya kumsaka muuaji wa viongozi wa Afrika hukutana na kuweka mezani tafutishi zao. Kama ilivyo ada kwao, muda huo kila mmoja alfika kwa njia yake na kukutana ndani ya chumba hiki cha siri katika moja ya ofisi za jingo kubwa la mikutano na ofisi la Umoja wa Afrika.
“Kazi ni ngumu, viongozi wote wamefika salama, sasa sihida ni kuhakikisha huyu jamaa kweli hajaingia nchini?” mmoj wao kutoka jumuia ya SADC akawaambia wenzake.
“Tunapiga ngumi kichakani, kumbukeni mshenzi huyu naye ni kachero kama sisi hivyo anajua mbinu zote tunazotumia, nimehakikisha ulinzi mkali upo katika hoteli ambayo Mwenyekiti wa atafikia…” mwingine akasema.
“Nimemwona Amata Ric!” Drunken Hamidou akawaambia swahiba zake. Kila mmoja akashtuka na kumtazama kijana huyo, “Amata!? Wa TISS” akauliza yulle wa SADC.
“Ndiyo, alikuja uwanja wa ndege, akaenda mapokezi na baada ya dakika chache akatoka kwa mwendo wa kasi kidogo akaingia kwenye gari aina ya Range Rover na kuondoka,” akawaambia.
“Umemfananisha! Inasemekana Amata ametoweka na habari ambazo ninazo ni kuwa Idara ya usalama wa Taifa ya Tanzania, inaficha habari hii kwa aibu kwa kuwa walijinasibu kuwa wataimaliza kazi hii kwa siku chache,” mwingine akaongea kwa kujiamini kabisa.
“Narudia, nimemwona Amata Ric, na kama yeye yuko hapa basi Gupter yupo hapa, tuwe makini… Amata si mtu wa kutoweka ovyo, kama kweli alitoweka basi alitoweka kikazi, na sasa ameibukia Addis… pendekezo langu mimi tutumie dakika chache kumsaka kwa njia zote, na tukimpata tufanye kazi pamoja, kwa vyovyote yuko mbele kuliko sisi, si ajabu anamjua hata demu wa Gupter anaishi wapi…” Drunken akawaambia wenzake, ukimya ukajidai kati yao, hakuwa aliyeongea lolote.
“Hapana, hata kamati yenyewe itatushangaa, tunaacha kutegua kitendawili na kumtafuta Amata…”
Baada ya kikao hicho kifupi kukamilika, wakatawanyika, lakini kama kazi yao ili, siri hufanyika kwa siri na siri huwa siri ya siri. Kila mmoja alifika kwa mkuu wake kwa siri na kumpa taarifa aliyokuwa nayo kutokana na kazi yake ya siku hiyo.
Ni huyu Drunken Hamidou ndiye aliyetoa taarifa kwa mkuu wake na ikasambaa katika kamati ya usalama ya umoja huo kuwa Amata yupo Addis. Haikuwa rahisi kueleweka kwa wadau wa kamati hiyo, habari hii iliwachanganya kiasi na swali likawa, je TSA wapo Addis? Mwenyekiti wa baraza hilo, hakufurahishwa hata kidogo na habari hiyo, akauliza mara kadhaa kama ni kweli wana uhakika aliyeonekana ni huyo au kivuli chake, akahakikishiwa kuwa ni yeye.
Katika kikao cha jioni hiyo, wadau wa baraza la usalama walikuwa na mjadala mzito sana kuhusu jambo hilo.
“Mimi, nikiongea kama mwenyekiti, mwenye mamlaka, nasema hivi, haitakiwi kwa idara yoyote ya usalama, kutoka popote pale, kuingilia mchakato huu wa kumnasa Gupter bila kibali chetu. Na kwa kanuni hii natoa amri na itekelezwe mara moja, huyu kijana wa TSA, nani sijui…”
“…Amata!”
“Yes! Amata, akamatwe na kuwekwa ndani ili kupisha kazi yetu ifanyike kwa umakini,” akamaliza kusema na ukimya ukatawala. Hakuna mjumbe yeyote aliyejibu au kuweka neno lolote. Hoja chache zikaendelea na baadae kikao hicho kikavunjwa ikiwa bado mwenyekiti wa baraza hilo la usalama la muda akitaka Amata akamatwe. Mara baada ya kumaliza kikao, mwenyekiti yule akatoka na kuwaacha wajumbe wake, akaingia gari ni kuelekea katikati ya mji, ndani ya jengo fulani ambalo kwalo alikutana na watu wengine watatu.
“Nahitaji mnifanyie kazi moja tu,” akawaambia.
“Ipi mkuu?”
“Kuna huyu mpelelezi wa Tanzania, inasemekana yupo hapa Addis, huyu anaweza kutuharibia kazi yetu, hivyo akamatwe awekwe ndani haraka kabla ya giza hili alijaisha,” akawaambia. Wale vijana wakatazamana kwa sekunde kadhaa kisha mmoja wao akahoji.
“Mkuu, kwa nini tusimjumuishe huyo mtu katika timu yetu? Maana mpaka sasa huyu Gupter anatuumiza vichwa, sisi hapa tuna tetesi tu kuwa anaweza kuwa nchini…”
“Mmejuaje?” akahoji.
“Mpaka sasa tunafuatilia ndege ya jana ambayo ilipata hitilafu, tunahisi hawa jamaa wameingia nchini kwa kutumia njia hiyo, yaani kushuka kwa miamvuli,” mmoja wa wale vijana akaeleza. Maelezo haya yakamfanya huyu mzee kuduwaa, hakuwahi kufikiri kitu kama hicho kichwani mwake.
“Any way, vyovyote vile, nataka huyu bwana akamatwe, mkishamkamata, tutamhoji kama ana habari yoyote juu ya mtu au watu hawa,”mwenyekiti akawaambia na kuwaaga pasi na kuruhusu swali lolote.
* * *
Ujumbe kutoka Oman, uliotumwa na Jaffer Bakhari uliwasili Addis Ababa ukiongozwa na Fadicky Al Habib. Ingawa baraza la usalama la muda lilikwishamtuhumu mtu huyu kama kiongozi wa mauaji haya, bado hawakuweza kumkamata kama wengi walivyotaka. Walijua amefika na watu wengine kama kumi hivi lakini kwa sheria za kimataifa hawakuweza kuwagusa watu hao.
“Kesho ni mwisho, wakikubali, itakuwa sherehe kwetu kuikomboa nchi yetu, wakikataa basi wataendeea kushuhudia mauaji na vita visivyokwisha,” wengine wakaitika na kuunga mkono.
Watu hawa walijipanga kwa hoja nzito dhidi ya Umoja wa Afrika, wakidhamiria kuipata ardhi ya mama zao.
“Na huyu mwenyekiti ndiye anayatunyima ardhi ile, hastahili kuishi, na kesho aongozwe na dhamira yake akubali ombi letu,” akawaambia.
Akiwa katika kuongea huko, simu yake ikaita, akaitazama na kuona namba ambayo alikwishapewa kuwa itampigia. Akainuka na kuingia katika chumba maalumu ambacho hakiruhusu sauti kutoka nje.
“Yes Shooter!” akaitikia simu hiyo.
“Tupo!” sauti ya pili ikasema.
“Mpango ni kama ulivyoambiwa, haujabadilika, ikiwa positive, utafanya ulivyoambiwa na ikiwa negative utajua wewe unamalizaje mchezo,” Fadicky akamwambia mtu wa upande wa pili.
“Unafikiri kuna kikwazo? Mbegu zetu tumezipanda kila mahali na zinamea vyema, over and out!” Fadick akasema.
“Hakuna kikwazo, kila tundu linapenyeka, over and out!” sauti ya upande wa pili ikajibu.
“Uno trabajo!”
Simu ikakatika.
* * *
Martin Gupter, akashusha simu sikioni na kubaki kimya huku akitafuna bubble gum kinywani mwake. Kwa taratibu sana, akafungua mlango na kukanyaga ardhi yenye vumbi, ya kijiji hiko cha Alertu. Akavuta hatua na kuingia ndani ya nyumba hiyo, giza lilikuwa limetawala ndani mwote. Fredy na Amanda walikuwa wamebaki mjini wakiendelea kupanga hiki na kile kwa kificho kikubwa ili wasijulikane. Ni Martin Gupter pekee alikuwa amerudi muda huo akiwategemea wenzi wake usiku wa baadae wa siku hiyo. Hatua zake chache zikamfikisha chumbani, na hapa ndipo moyo wake ulipolipuka kama kombora. Juu ya kitanda chake alikuta vitu viwili ambavyo hakutegemea; bunduki kubwa ‘Magnum 22’ na ua waridi.
Nani kaweka vitu hivi? Akajiuliza, hakupata jibu. Moyowe ukadunda kwa nguvu na hofu, akavuta hatua na kukikaribia kabisa kitanda kile, macho yake yakatua vyema katika bunduki ile, kilichomshangaza zaidi ni kuwa ilikuwa ile ile ya kwake. Bunduki aina ya Magnum 22 Riffle, na juu yake imefungwa hadubini ile ile. Martin Gupter, mikono ikamtetemeka, kijasho chembamba kikamtiririka, hakuelewa kama anaota au yu macho. Akatzama huku na huko, huku akichomoa bastola yake kutoka kiunoni na kuikamata barabara kabisa. Kutoka hapo akaanza kupita chumba kimoja kimoja kuangalia kama adui yake yupo ndani ya nyumba yake hiyo, la. Martin Gupter, kila alipojaribu kufikiria juu ya hilo, alijikuta yupo njia panda, akajitupa kitini na kuinua simu yake, na kuwataka Amanda na Fredy kurudi.
Robo saa baadae, wawili hawa wakaingia katika nyumba hiyo, tayari ilikuwa usiku wa saa tatu na nusu hivi kadiri ya saa iliyoning’inizwa ukutani.
“Martin!!” Amanda akaita na kumfanya kijana huyo kugutuka kama aliyepigwa shoti ya umeme, “Vipi, mbona umetutaka kurudi mapema ilhali bado tulikuwa kazini?” Amanda akasema.
“Kila kitu kimerudi, ndugu zangu hapa kazi ni ngumu!” akamjibu.
“Kivipi? Sikuelewi!” Fredy akadakiza.
Martin akainuka kitiki na kuwapa ishara ya kuwa wamfuate, nao wakafanya hivyo, wakafika chumbani kwa Martin na kujikuta wakipigwa butwaa. Fredy akamgeukia Martin na kumwambia, “They are here!” (wapo hapa).
“Yes! Na hii sasa ni hatari, jamani uamuzi wangu ni huu, hatuna budi kuhama hili eneo haraka, maana adui yetu keshajua wapi tulipo,” Martin akasema.
Amanda akatulia kimya bila kujibu neno lolote, akili yake ilikuwa bado ikijaribu kuyapanga mambo.
“Ina maana TSA wapo hapa?” akarudia swali ambalo alishaliuliza kwanza.
“Kwani ni nani alikuwa nabunduki hii? Si ilitoka mikononi mwangu tukiwa Tanzania, kwa mara ya kwanza katika maisha yangu!” Martin akasema.
“Sawa, tuhame na tuhamie tusipopajua lakini kama tumefanikiwa kumuua namba moja wao, hawa wengine hawatatusumbua kabisa,” Amanda akasema na Fredy akatikisa kichwa huku akitoa mkoba wake kabatini.
“Jamani, sikilizeni, kule Free Town tulipomkamata yule bwege, kumbuka tulimwekea nini kitandani… si ua waridi?” Fredy akawakumbusha kwa maneno hayo. Ukimya wa sekunde kadhaa ukapita katikati yao, Amanda akamtazama kijana huyo kwa macho ya kidadisi, “Unataka kusemaje?” akauliza.
“Yule mjinga hajafa! Kwa sababu nani awape ujumbe kama huu wenzake? Hamuoni kwamba kataka kujitambulisha kuwa yupo hapa, yaani mzima wa afya…” Fredy akasema.
“Katokaje mle ndani, mle hatoki mtu labda kama hana mwili,” Martin akamjibu.
“Hajafa, na yupo hapa, kwanza Battlomino ameuawa leo, vipi kama ni yeye kampa ramani ya tulipo,” Fredy akazidi kudadavu mambo.
“Tuondokeni!” Martin akazidi kusisitiza, akaichukua ile bunduki na kulitia lile ua katika kopo la takataka, “Tukapige kambi Etonto,” akasema akiwa tayari mkoba begani.
“Etonto?” Amanda akauliza.
“Ndiyo, Etonto… kesho tutakuja mjini kwa tukio moja tu, kuua au kunywa soda!” Gupter akamjibu na kutoka nje, dakika tano baadae wawili hao nao wakatoka na kuingia garini, wakaondoka zao na kuiacha nyumba hiyo kama walivyoikuta.
“Simwelewi huyu jamaa, kama ni yeye kweli, basi si mtu wa kawaida,” Fredy akasema huku akiendesha gari kwa kasi.
“Huyu ni shetani! Tena shetani asiye na mkia,” Amanda akajibu.
“Sasa awe shetani asiwe shetani, kesho nikimtia machoni tu, nitamuua kwa bunduki hii hii, mtoto wa kahaba yule!” Martin akaongea kwa hasira.
“Nimekumbuka!” Amanda akasema na kumpa ishara Fredy asimame, “Ni vipi kama hiyo bunduki imewekwa GPS na inmfanya adui atufuatilie kirahisi?” akasema. Martin akaitazama ile bunduki na kuigeuzageuza, akafungua mlango wa gari na kutoka nje, akaitupa kwenye vichaka na kurudi garini.
“Umeitupa?”
“Nimeificha!”
Fredy akarudisha gari barabarani na kuendelea na safari.
* * *
Chiba akaegesha gari jirani kabisa na kichaka kile kile ambacho Martin aliitupa ile bunduki muda mchache uliopita. Gina akashuka na kufuatiwa na Kamanda Amata, wakaingia kichakani na kuichukua ile bunduki kisha wakarudi garini.
“Wana bahati sana, wameshtukia njama,” Amata akasema.
“Kwa hiyo!!” Chiba akauliza.
“Turudi mjini, tukajipange upya, kesho lazima tuwatie nguvuni kabla hawajaleta madhara,” Amata akajibu huku gari likigeuzwa na kurudi mjini.
Baada ya kama nusu saa hivi, wakawasili mjini na Chiba aliendesha gari kwa mwendo wa wastani huku mazungumzo ya hapa na pale yakiendelea.
“Chiba!” Amata akaita.
“Sema!” Chiba akaitikia.
“Nahisi tuna kampani nyuma yetu, nimeangalia kwa muda mrefu sana, kuna magari mawili yanatufuatilia, kila mmoja ajiweke tayari maana hatujui kama ni marafiki au maadui,” Amata akawaambia huku akiiweka bastola yake vyema, tayari kwa lolote litakalotokea, Amanda naye akafanya hivyo hivyo na kumkabidhi Chiba bastola huku yeye akiweka yake wake tayari.
“Tayari?” Chiba akauliza.
“Ndiyo, weka gari pembeni na asishuke mtu tuone!” amata akatoa maelekezo na Chiba akafuata. Akaegesha gari kando ya barabara. Amata alikuwa sahihi kabisa kwani mara baada ya kusimama, yale magari nayo yakasimama moja nyuma na jingine mbele huku wao wakiwa katikati. Vijana kama sita hivi wakateremka, kati yao, wawili wakasogelea gari walilokuwamo TSA na kugonga kioo cha mbele. Chiba akashusha kioo robo tu ili kusikiliza nini kitazungumzwa.
Wale mabwana wakatoa vitambulisho na kujitambulisha kuwa wametoka ofisi maalumu ya usalama ya AU. Chiba naye akato kitambulisho chake halisi kabisa cha TSA na kuwaonesha na Gina akafanya vivyo hivyo na Amata pia baada ya kushusha kioo mpaka chini.
“Tuna shida na Amata Ric, shida ya kikazi, tumepata taarifa kuwa yuko hapa na tumefurahi kwa kuwa tumemuona!” mmoja wao akasema. Gina na Chiba wakatazamana kisha wakamtazama Amata.
“Ngoja niwasikilize,” Amata akasema na wenzake wakamruhusu, akateremka garini na kuitia bastola yake katika kikoba chake, wakasimama pembeni kama mita nne hivi kutoka walipoegesha magari yao.
“TSA! Tumepata taarifa kuwa u hapa, na kwa sababu wewe ni mwanausalama kama sisi, mkurugenzi wetu wa idara ya AU anahitaji kukuona kwa mazungumzo ya kikazi,” mmoja wa wale vijana akamwambia Amata kwa kiingereza chenye lafudhi ya kihabeshi. Kamanda Amata akatulia kimya kama sekunde kumi hivi kisha akavuta hatua kurudi katika gari, akawaambia wenzake jambo hilo.
“No! tunaenda wote, sisi tutaamini vipi juu ya hilo? Vipi kama ni njama, je?” Gina akauliza.
“Mchezo wetu ni ule ule…” Amata akasema.
“Aaaakh! Ok, code gani?” Gina akauliza.
“300.1R” akamjibu na kuondoka. Wale vijana wakaongozana nae na kuingia kwenye gari lao kisha yote mawili yakaingia barabarani na kuondoka kwa kasi, si kwa mwendo waliokuja nao. Chiba naye akaingiza gari barabarani na kutokomea mjini, Gina akajiegemeza kitini huku mkono mmoja ukiwa umeegemezwa kwenye dirisha na kiganja kichwani.
“Code 300.1R” Gina akarudia kodi hiyo aliyopewa na Amata ambayo ni moja kati ya kodi nyingi wanazotumia kwa ajili ya kazi zao, ikiwa na manaa kwamba 300 ni masaa matatu kamili, .1 ni sekunde ya kwanza baada ya masaa hayo matatu na R ni Rescue, yaani ikifika masaa matatu bila taarifa yoyote kutoka kwa Amata basi sekunde ya kwanza ikigonga waanze mikakati ya kumuokoa, tayari atakuwa matatizoni.
* * *
Ndani ya gari lile, Amata aliketi kiti cha nyuma katikati kushoto na kulia kukiwa na wale vijana. Dereva amaye alificha macho yake kwa miwani ya giza japokuwa ni usiku alikuwa ametingwa na kazi yake wala hakujali jambo jingine lolote.
“Lini umefika Addis?” kijana wa upande wa kushoto akauliza.
“Miezi mitatu ilopita!” Amata akajibu.
“Miezi mitatu!?” yule jamaa akajiuliza na kushangaa.
“Ee, miezi mitatu…” akajibu na kubaki kimya. Lile gari likapenya mitaa kadhaa na kuibukia upande mwingine mji. Baada ya mwendo wa takribani dakika hamsini hivi wakaingia kwenye jingo moja kubwa na lile gari likateremka chini jingo hilo. Ndani tu ya jingo hilo, lile gari lilitembea kama dakika kumi na tano hivi na mwisho likaegeshwa sehemu fulani ambapo palikuwa kama stoo ka jinsi makorokoro yalivyozagaa huku na huko.
“Tumefika!” yule kijana akamwambia Amata.
“Mkurugenzi yuko wapi?” Amata akauliza.
“We teremka atakuja tu,” akajibiwa.
Kengele za hatari kichwani mwa Amata zikagonga, “Sishuki mpaka mkurugenzi afike maana ndiye anayenihitaji si ninyi,” akawajibu kijeuri.
“Asee, usitake tutumie njia za kisovieti…” kijana mwingine mwenye mwili mkubwa uliojaa nyama akasema huku akisogelea gari lile.
“Kwa hiyo si mkurugenzi anayenihitaji, mmeniteka sivyo, yaani wanausalama mnamteka mwanausalama! Haya tumieni njia mnayotaka kunishusha…” akajibu kijeuri huku akiwa bado kaketi kitini na mkanda ukiwa umezunguka kiunoni mwake. Yule bwana akasogea mpaka pale na kuwahi kuufyatua mkanda wa kiti, Amata akasogea pembeni na kumpa wakati mgumu jamaa yule, mara akaona mlango wa upande huo nao ukifunguliwa na mtu mwingine. Akafanya kama anatoka na yule bwana akampokea kwa konde moja zito tumboni, Amata akajikunja kwa maumivu na kurudi ndani ya gari. Jamaa aliyempiga ngumi akaingia mkono kumshika, Amata akakamkata mlango na kuubamiza kwa nguvu, akambana vidole na yule jamaa akapiga yowe la uchungu. Upande wa pili yule bonge alimdaka Amata na kumvuata nje, akambaga chini lakini Amata akawahi kusimama, kabla hajajiandaa akajikuta akipokea mapigo mazito kutoka kwa bonge huyo kisha na virungu kadhaa vikatua mwilini mwake na kumbakisha akiwa hoi sakafuni.
“Unajifanya mjanja kwenye ardhi ya watu!” yule bonge akamwambia Amata.
Haikupita hata dakika ishirini, Marcedec Benzi moja jeusi likaingia na kufuatiwa na Nissan Patrol short Chassis nalo jeusi pia, yakasimama na taa zake zikiwa full zikimmulika Amata usoni.
“Hah! Hah! Hah! Hah! Aaaaaah, umefufuka siyo?” sauti nzito ya mtu ambaye hakuweza kumwona vizuri ilisikika, “sikiliza kijana, hizi kazi si za kufanya kama ufanyavyo wewe, kukuepushia haya, ulishauawa wewe kule Waterloo, kwa nini hukutulia ufe?” akamuuliza. Kamanda Amata akainua uso wake kwa taabu kidogo na kumtazama huyo asemaye, hakumwona sura ila kitambulisho alichokuwa amekivaa kilimtambulisha kwa kusomeka MARILEKC FikrMARYAM. Jina tu tayari lilimpa habari kamili Amata, alilijua kwa sababu ni huyu ndiye aliyeteuliwa kuongoza kamati ya dharula ya usalama ya AU iliyokuwa na jukumu la kumsaka muuaji wa viongozi wa Afrika ambayo iliweka makao yake katika Jiji la Dar es salaam. Ni huyu, mtu wa ngazi ya juu sana katika idara ya usalama ya Umoja wan chi za Afrika, raia wa Elitrea mwenye unasaba wa karibu na Uethiopia.
“Marilekc FikrMaryam! Kumbe ni wewe… unyeihujumu Afrika na watu wake…” Amata akasema. Mzee huyo akahisi ganzi mwili mzima kwa maana jina lake daima huwa halitambuliki, akajipapasa kifuani na kukuta kitambulisho kikiwa kinaning’inia. Kwa sekunde chache, sura ikaonesha uzee mara mbili ya ule aliyokuwa nao. Marilekc akamtazama Amata pale chini na kujikuta mate yakimkauka, akameza funda kubwa na kusimama wima, kwa mkono wake wa kulia akakivua kile kitambulisho na kukitia mfukoni.
“Make him uncomfortable…” akawaamuru wale vijana nao wakaanza kumsulubu Kamanda kwa zamu. Walipiga kila mmoja kwa jinsi yake, aliyetumia mateke sawa, aliyechukua fimbo sawa, mwenye gongo twende. Dakika tano za kipigo zilimwacha Amata akiwa hoi pasi na kujitetea.
“Mwacheni!” akaamuru, na wale vijana wakamwacha na kusimama kando. Marilekc akachutama na kumtazama Amata, “unajua nini kuhusu muuaji wa viongozi wa Afrika?” akamuuliza.
“Ni-ni-ni-ttta-ju-a ni-ni, wa-ka-ti mi-mi si-hu-si-ki?” Amata akajibu kwa taabu kidogo.
“Wewe unajua, na hapa Addis umekuja kufanya nini?”
“Ni-me-ku-ja kumlinda –ra-i-s wa-ngu!” akajibu na kujinyoosha kidogo. Marilekc akawatazama vijana wake, akawaona wapo ngangari wakisubiri amri ya mkubwa wao, akarudisha macho kwa Amata.
“Nataka unipe tafutishi zote za sakata hili…” akamwambia.
“Sina!” Amata akajibu kwa neno moja tu.
“Huna!? Na zile ulizochukua Angola…”
“Anhaaa wewe ni mmoja wa-o,” Amata akasema, mara akajikuta akipokea teke moja zito usoni lililomtupia upande wa pili, damu zikamtiririka puani, akakohoa na kujaribu kujiinua, mara yule bonge akampiga teke jingine la tumboni na kumbwaga kando.
“Ni-ninyi ni wa-na-u-sssa-la-ma au ma-ja-mbazi?” akauliza.
Marilekc akasogea na kuchutama kwa mara nyingine, “Nakuuliza kwa mara ya tatu, zi wapi tafutishi za mpango huu wa mauaji ya viongozi?”
“Zipo Tanzania, wasiliana na Madam Sellina, atakupatia mpaka nilipoishia…” Amata akajibu, mara hii kwa ukakamavu kidogo.
“Sikiliza we bwege, mimi nina akili, mimi ni mwenyekiti wa kamati ya usalama, kukukamata na kukuweka hapa ni moja ya mbinu za kutaka kusaidia uchunguzi dhidi ya mauaji haya, najua wewe unajua, lakini tulipoiondoa idara yenu katika hili, tulimaanisha kuwa mnatakiwa kuwasilisha tafutishi zote mikononi mwetu…”
“…ndiyo maana mkamtengenezea ajali Madam Sellina, mlidhani mtamuua? Hajafa, hajafa, yupo hai na hivi tunavyoongea, usiku huu anatua Addis…”
“SHUT UP!!!! SON OF BITCH!” Malirekc akang’aka na kumrukia Amata, hapo ndipo alipofanya kosa ambalo alilijutia. Kamanda Amata akaviringika upande wa pili na kumshuhudia mtu mzima huyo akitua sakafuni kwenye makolokolo na uchafu, akachomoa bastola na kuifyatua, Amata akapiga sarakasi na risasi ile ikaingia moja kwa moja kwenye tenki la mafuta katika gari iliyoegeshwa jirani. Mlipuko mzito ukatokea, lile gari likabiringishwa hewani na kujipigiza juu kisha likarudi chini, mara gari lingine nalo likadaka moto.
“Ita fayaaaa!!!” kelele zikasikika, huku vijana wa Marilekc wakitawanyika kumsaka Amata asiwapotete.
“Hakikisheni hatoroki,” Malirekc akawaambia huku akijiondoa eneo lile na ving’ora vya polisi vikisikika nje.
Kamanda Amata baada ya kuruka sarakasi ile akaangukia upande wa pili lakini kutokana na maumivu aliyokuwa nayo akajikuta anashindwa hata kujisogeza. Akiwa katika kuhangaika akasikia bunduki zinazoondolewa usalama, akatulia tuli na kuweka mikono yake kisogoni huku akiwa kalala kifudifudi. Vijana wa Marilekc kutoka idara nyeti ya usalama ya AU wakamzunguka wakiwa na shot gun na wengine bastola.
“Arrest him!” (mkamateni) Malireck akatoa amri na Amata akatiwa pingu na kusombwa mpaka kwenye gari moja jeusi, akasukumiwa ndani na kufungiwa. Ving’ora vya magari ya polisi vikatulia na kubaki vimulimuli vikipendezesha eneo lile kwa taa zake za rangirangi na magari ya faya yalikwishawasili na kuanza kazi yao mara moja. Malireck akaonesha kitambulisho chake na kupigiwa saluti za heshima, kisha kwa ishara ya mkono akawaamuru vijana wake wamtoe Amata na kumkabidhi kwa wale polisi.
“Make naye huyu, asihojiwe na wala asichanganywe na mtuhumiwa yeyote, tutakuja wenyewe kumhoji, ni mmoja wa watu tunawatafuta kwa kuhatarisha usalama wa Afrika!,” akawaambia wale askari, nao wakamchukua na kumtia garini kisha wakaondoka naye kwenda kumhifadhi.