Riwaya: Kikosi cha Kisasi

Riwaya: Kikosi cha Kisasi

Tatizo riwaya zenu huwa haziishi,mnakoziiba huko sijui huwa wanawashtukia?
 
SURA YA TANO
MWANZO WA MAPAMBANO
Yule kijana alipoangalia usoni mwa Willy mara moja alijua huyu mtu hakuwa na mzaha. Hivi akiwa mikono yake ikiwa imeshika kwenye usukani wa gari na mwili wake mzima akiwa amekauka kama mti uliopigwa radi alimjibu Willy, "Tafadhali niache, mimi ni Robert Sikawa."
"Nitajuaje kama wewe ni Robert Sikawa?" Aliuliza Willy hali uso wake ukiwa bado mzito.
"Maana wewe ni Willy Gamba, kiongozi wa 'Kikosi cha Kisasi' kwa kifupi KK, ambacho makao yake makuu yako Lusaka..."
"Oke, siku nyingine ujiangalie unaweza kupatwa na matatizo bure. Vile vile unapofuata mtu, inabidi ufunye vizuri kuliko ulivyofanya hasa unapofuata mtu mwenye ujuzi katika mchezo wetu huu," Willy alimweleza Robert huku akiwa ameisharudisha bastola yake na tayari uso wake ukiwa unaonyesha urafiki, na vile vile akiwa amempa nafasi Robert kutoka ndani ya gari na kusimama wote nje ya gari la Robert.
"Ama kweli ndiyo sababu umechaguliwa kuongoza 'KK'", alieleza Sikawa. "Mimi nilishangaa nilipoambiwa inabidi nichukue amri toka kwako tangu wakati utakapofika, maana mimi mwenyewe najiamini sana. Hivi sikuona kwanini tena aje mtu nichukue amri kutoka kwake badala yake yeye kuchukua amri kwangu. Hivi nilikuwa uwanja wa ndege kukupokea na vile vile kukujaribu una ujuzi kiasi gani. Jaribio langu dogo hili linanidhihirishia kuwa kweli wewe ni mjuzi katika mchezo wetu huu, maana mimi ninapomfuata mtu huwa ni vigumu sana kunigundua. Kule kwetu Lusaka katika idara yetu huwa wananiita 'Nyoka wa kijani' sababu hii hii. Hivyo bosi wangu ninakukaribisha mjini Kinshasa," alieleza Robert.
"Ulijuaje kama ninakuja?".
"Chifu wako alinitumia habari jana pamoja na picha yako ambayo ingeweza kunifanya nikutambue".
"Picha, bado unayo?"
"Ndiyo".
"Tafadhali itatue sasa hivi. Si vizuri kiusalama mpelelezi kutembea na picha ya mpelelezi mwenziwe, kitu anachobidi kufanya ni kuhakikisha kuwa anaangalia picha mara moja na kuiweka sura yake ndani ya kichwa chake kisha anaitatua hiyo picha hapo hapo", Willy alimshauri.
"Vizuri", alijibu Robert huku akitoa picha ya Willy ndani ya mfuko wa koti lake na kuwasha kibiriti na kuichoma hiyo picha pale pale.
"Utafikia hoteli gani?", aliuliza Robert.
"Nafikiri Memling Hoteli itanifaa".
"Yaa, hoteli hiyo ni tulivu itakufaa. Sijui tuonane muda gani ili niweze kukupa habari nilizonazo kikamilifu?"
"Tuonane jioni saa mbili hivi na kuendelea, maana sasa hivi itabidi nipumzike kidogo".
"Sawa basi tuonane Vatcan Klabu huko Matonge saa hizo.
"Sijui unaifahamu?".
"Hamna taabu, naifahamu." Alijibu Willy.
"Oke basi tuonane huko saa hizi".
"Oke Robert, asante sana, tutaonana", alijibu Willy huku akiondoka na kuelekea kwenye gari lake. Robert alibaki amesimama pale penye gari lake akimwangalia Willy kwa shauku.
Willy alipanda gari lake akalitia moto na kuondoka kuelekea Memling Hoteli. Alipofika Memling Hoteli alikuta kuna nafasi.
"Karibu," alikaribishwa na mfanyakazi mmoja msichana aliyemkuta hapo kwenye mapokezi ya hoteli hii.
"Naweza kupata chumba?", aliuliza Willy.
"Bila shaka, unakaribishwa kwa dhati. Una mzigo?".
"Nina mkoba mmoja uko ndani ya gari".
Yule msichana alimwita mchukuzi ili akachukue ule mzigo.
"Acha tu nitakwenda kuuchukua mwenyewe", Willy alieleza huku akienda kwenye gari.
"Tunavyo vyumba wazi kwenye ghorofa ya pili, tatu na tano, sijui ungependelea ghorofa ipi?", yule msichana alimuuliza Willy, aliporudi na mkoba wake.
"Wewe unafikiri ghorofa ipi ni nzuri?".
"Hii inategemea na uchaguzi wa kila mtu binafsi".
"Uchaguzi wako ndiyo utakuwa wangu", Willy alimwambia yule msichana huku akimtolea bonge la tabasamu.
"Chumba nambari 240 kwenye ghorofa ya pili kitakufaa," yule msichana alimjibu Willy naye akitoa tabasamu.
"Asante sana, hicho hicho chumba kitanifaa." Willy alijaza fomu kama ilivyo desturi, kisha akapelekwa na askari wa hoteli mpaka chumbani kwake. Chumba alichokuwa amepewa kilikuwa kwenye sehemu nzuri sana na chumba chenyewe kilikuwa kimepangwa na kuwekwa vyombo vizuri saana. Askari alipokuwa amekwishaondoka, Willy alianza kukipekua kile chumba, na kukikuta salama. Alipokwisha kufanya hivyo alifungua mkoba wake na kuanza kupanga vitu vyake. Alipomaliza alienda akaoga kisha akatelemka chini kwenda kupata chakula cha mchana. Alipomaliza kula alipita pale kwa yule msichana wa mapokezi.
"Haya kisura bado unaendelea na kazi!"
"Ndiyo, heri nyinyi wenye bahati ya kutembea nchi mbali mbali na kustarehe. Sijui lini mimi nitapata nafasi kama hii!", alijibu yule msichana kwa masikitiko.
"Siku ipo itafika usiwe na shaka, ya Mungu mengi sana. Fanya kazi yako kwa bidii, tumia mapato yako kwa mpango, huku ukiweka akiba kwa ajili ya safari kama hii, ukifanya hivi nina imani siku moja ndoto zako za kutembea nchi mbali mbali zitakuja kweli," alimshauri Willy.
"Ndivyo wewe ulivyofanya?" Yule msichana alimuuliza.
"Lazima, hamna dawa nyingine," alijibu Willy huku akitoa pesa ili kubadilisha kutoka kwenye dola ili apate Zaire. Msichana yule alipombadilishia pesa zake, Willy alitoa Zaire kumi akampatia yule msichana.
"Za nini?" Yule msichana alimuuliza.
"Asante yako kwa kunipokea vizuri. Wewe unaitwa nani?"
"Naitwa Mwadi," yule msichana alisema huku akionekana kuwa na mshangao.
"Jina zuri 'Mwadi', haya asnate Mwadi tutaonana jioni".
"Jioni nitakuwa nimeishamaliza kazi, namaliza saa tisa mchana, hivi nitakuwa nyumbani."
"Basi tutaonana kesho,"
"Haya asante," alijibu Mwadi, huku akimwangalia Willy kwa macho malegevu. Willy alipoondoka alimwacha yule msichana moyo wake unapiga haraka haraka. Maishani mwake alikuwa ameishaona wavulana wengi sana, hasa ukitilia maanani kazi yake hii, lakini alikuwa hajaonana na mvulana mwenye kusisimua kama huyu. Pale pale alijawa na moyo wa kimapenzi juu ya Willy.
Willy naye alienda chumbani kwake na kupumzika.
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA TANO
MWANZO WA MAPAMBANO
II
Baada ya kuondoka nyumbani kwa Pierre, Jean aliendesha gari lake moja kwa moja mpaka kwake 'G.A.D'. Alikuta kazi ya kutengeneza magari inaendelea kama kawaida. Alikaguakagua kazi kisha akawaita faraghani wafanyakazi wake wawili ambao walikuwa wakisimamia kazi. Mmoja aliitwa Kabeya Mwabila na mwingine Charles Besaleti, mwenye asili ya Kibeligiji. "Jamani kuna kazi muhimu", aliwaeleza. "Tunatakiwa tuchunge kiwanja cha ndege na mahoteli yote kuhakikisha kuwa hakuna mgeni ambaye anaingia mjini hapa bila sisi kuwa na maelekezo yake. Mnaweza kuweka watu wengi mnavyoweza na kutumia kiasi chochote ili mradi jambo hili lishughulikiwe kikamilifu. Kufanyika lifanyike kwa siri kama kawaida kiasi cha kwamba Polisi au CND* haiwezi kututuhumu. Tumeelewana?". alimaliza Jean.
"Tumeelewa, hilo hamna taabu, litafanyika kwa makini kabisa maana kila hoteli tunaye mtu kwenye orodha yetu ya mshahara ambaye kazi yake ni hiyo kila tuhitajipo maelezo," alijibu Charles.
"Sitaki kusikia makosa, Kazi hii ifanyike kikamilifu kabisa, watu mnao, pesa zipo, ninachohitaji ni utekelezaji." Jean aliwatilia mkazo.
"Usitie shaka, kazi itakwenda kama siku zote," Kabeya alimhakikishia na wote wawili wakatoka ndani ya ofisi ya Pierre tayati kufanya kazi.
*CND* Idara ya Upelelezi ya Zaire.
"Wewe shughulikia mahoteli na mimi nitashughulikia njia zote za kuingia Kinshasa, hasa uwanja wa ndege na kwenye kivuko cha kwenda Braville." Charles alimshauri mwenziwe.
"Vizuri, mahoteli yote nitayashughulikia mimi na pale patakapokuwa lazima nitapashughulikia mwenyewe".
"Oke, basi tulishughulikie mara moja".
Kila mmoja aliondoka na kupita kwa vijana waliokuwa wanashughulikia magari, wakiitwa mmoja mmoja hapa na pale tayari kwenda kwenye shughuli hii maalumu ambayo kimsingi ndiyo ilikuwa kazi waliyoajiriwa. Haya mambo ya kutengeneza magari ilikuwa geresha tu, ili kuivuruga serikali isijue maovu yao.
Ilikuwa yapata saa tisa kasoro robo wakati Kabeya ambaye alikuwa ofisini mwake huku akipiga simu mahotelini kwa wadukuzi wake alipofika Memling Hoteli kwenye orodha yake.
"Hapo ni Memling Hoteli?" aliuliza.
"Ndiyo".
"Mwadi yupo?" Mwandi ndiye alikuwa kwenye orodha ya mshahara ya 'WP' hapa Memling Hoteli kutokana na habari alizokuwa akizitoa kuhusu wageni. Kwa vile alikuwa akilipwa vizuri kwa kutoa habari ambazo alifikiria hazina madhara, alikuwa anaona kama ni bahati kwa upande wake alipoambiwa na Kabeya kufanya hivyo kwa malipo hayo.
"Ndiyo, yupo subiri", alijibiwa. Baada ya muda kidogo aliweza kuunganishwa na Mwadi.
"Halo Mwadi hapa".
"Ohoo Mwadi, Kabeya hapa habari yako?" Moyo wa Mwadi ulistuka kidogo kumsikia ni Kabeya, ingawaje alikuwa anajua habari alizokuwa anazitoa kwa Kabeya hazikuwa mbaya, lakini wakati mwingine alikuwa akiingiwa na wasiwasi hasa kwa vile sura ya Kabeya ilikuwa ikionyesha uovu mwingi sana. Kwa hivi alipopata simu mchana huu kutoka kwa Kabeya moyo wake ulishtuka sana, bila kuwa na sababu kamili.
"Mzuri, habari yako na wewe?".
"Mzuri tu".
"Unasemaje, maana mimi namaliza kazi nataka kwenda kupumzika".
"Nina kazi kidogo tu Mwadi, ile ya kila siku. Naomba unipe majina na maelezo ya wageni walioingia hotelini kwako toka jana hadi leo na vile vile endelea kunipa kwa siku hizi zitakazofuata. Malipo yako yatakuwa mara tatu ya kawaida. Tafadhali maelezo hayo yanahitaji kabla ya saa kumi leo. Yatakuja kuchukuliwa mahali pa kawaida. Sawa Mwadi?" Mwadi ambaye mara moja mawazo yake yalikwenda kwa kijana yule ambaye alikuwa amewasili mchana ule alisita kidogo kisha akasema.
"Sawa Kabeya nitashughulikia".
"Asante", alijibu Kabeya na kukata simu.
Mwadi alibaki huku akiwa na wasiwasi, na alikuwa hajui kwa nini roho yake ilikuwa haipendi kufikiria juu ya kutoa maelezo ya huyu kijana Willy Chitalu kwa Kabeya.
"Sijui ni kwa sababu nimempenda?" alijiuliza. Mawazo mengine yalimjia yakiwa yanamshauri kuwa maelezo haya yalikuwa yakitakiwa kwa ubaya ndiyo sababu walikuwa wako tayari kumlipa mara tatu ya kawaida. Hata hivyo moyo wake nao ulikuwa na wasiwasi na Willy maana kijana huyu alimsisimua sana. Mwishoni aliamua kuwa afadhali atengeneze orodha na kumpelekea Kabeya bila ya kina la Willy, kusudi kama maelezo haya yatakuwa kwa ubaya, ubaya huu usije ukamdhuru kijana huyu ambaye moyo wake ulikuwa umempenda bila kijana mwenyewe kujua. "Afadhali mimi nipate matatizo kuliko yule kijana," alijisemea.
ITAENDELEA
 
Mkuu kuna watu wamezaliwa na bahati zao,hasa huyu gamba
 

Tag me please iddy eba

Sitaki kuikosa story hii maana inanikumbusha miaka ya nyuma kidogo enzi za O-level tulipokuwa tukikaa mduara darasani kumzunguka msomaji pale itokeapo mwalimu wa somo fulani hajatokea...[/QUOTE]
 
Iddy eba unanikumbusha mbali sana na hizi riwaya za Elvis Musiba. Please nahitaji kupata vitabu hivi vya willy gamba na joram kiango ntavipata wapi?
 
Tukumbushie enzi zetu miaka ya 80...Musiba Elius Musiba alikuwa na kipaji kikubwa sana katika utunzi wa vitabu vya riwaya, mungu amlaze mahali pema peponi.
 
Back
Top Bottom