Riwaya - Gereza la Kifo

Riwaya - Gereza la Kifo

Bishop Huruka hii kitu ni balaa sana huenda huko mbele kukatokea mauaji
Gereza la Kifo - 18

Mtunzi - HAMISI KIBARI

ILIPOISHIA

"Yote unayosema ni kweli kabisa, bosi, kwamba mambo hayo yanahitaji ushahidi mkubwa. Lakini mimi naona ushahidi wote ninao kama kuna mtu atapingana na tulichoandika. Kama nilivyokueleza kwa njia ya simu kila kitu kipo," akasema Walari.
Baada ya kusema vile Walari alitoa kile kimtambo cha kunasia sauti na kumfungulia bosi wake ili asikie mazungumzo yake na mahabusu akiwa gerezani.

Tiririka nayo...

"Licha ya mimi mwenyewe kushuhudia baada ya kuingia gerezani na hawa niliyowarekodi, mmoja wa mtu ambaye alikaa mahabusu muda mrefu na ndiye wa kwanza kunipa habari hizi naweza kumpata na ninaamini, hata kama tutafikishwa wapi atasema hali halisi anayoifahamu na ndiyo tutakayokuwa tumeandika. Mchungaji Alex Kabongo ambaye tuliingia naye gerezani pia ni shahidi na yeyé nilimrekodi na utasikia sauti yake. Mkuu, hii ndiyo hali halisi ya gereza la Magamaga. Hali ni mbaya sana," alisema Walari na kuongeza kuwa kuna uwezekano wa kupata hata watu 10 waliofungwa katika gereza hilo na kutoa ushahidi wa hali halisi. Kadhalika alimwonyesha baadhi ya picha alizozipiga kwenye simu, picha ambazo alimtumia pia ingawa hazikuwa na ubora.
Mhariri alisikiliza kanda ile kidogo lakini baada ya sentensi mbili tatu za mfungwa mmoja, akaonekana hana hamu zaidi ya kusikiliza na kumwambia Walari auzime, inatosha.
Walari alitoa kitabu chake kidogo na kumtajia baadhi ya majina ya wafungwa waliokufa katika kipindi cha miezi sita pamoja na namba zao.
"Kama nilivyokwambia kwa njia ya simu, mkuu, nilitaka tutaje idadi tu na ikitokea mtu anapinga ndipo tunachapisha hii orodha ya majina pamoja na namba zao za jela."
Mhariri aliangalia yale majina juu juu kisha akasema kwamba tatizo kubwa la habari yao hiyo linabaki katika kipengele cha kumtuhumu zaidi mkuu wa gereza, hivyo ilitakiwa kumhoji kwa kina zaidi na kumsikiliza namna anavyojibu tuhuma hizo.
"Pia lazima tujue kwamba gereza hili ni dogo sana lakini wanajitahidi kutunza wafungwa wengi kuliko uwezo wa gereza... Lazima tulifikirie na hilo pia, ukiachilia mbali kuwa na ushahidi.”
"Lakini mkuu," akaanza Walari, "Kama umeisoma habari yote nimefanya mahojiano na mkuu wa gereza na kila alichosema nimeandika."
"Sawa, nimeona. Hata mimi nilitaka nimhoji kidogo maswali kwa sababu tuhuma nyingine, kama hili la kuwa na duka la dawa na kwamba dawa za wafungwa pengine anapeleka humo, linahitaji ushahidi zaidi."
"Mimi nilidhani umeshaonana naye, bosi?" Akauliza Walari.
"Bado sijaonana naye. Nimekwenda ofisini kwake sijamkuta. Nimeacha maagizo tuonane jioni hii."
"Yaani tuseme hamjafanya mahojiano tu ama hamjaonana kabisa?" Akauliza tena Walari.
"Hatujaonana kabisa. Toka nimewasili hatujaonana," akajibu mhariri huyo, jibu ambalo lilimshangaza sana Walari, kwani mchana ule pale uwanja wa ndege aliwaona kwa macho yake wakipanda katika gari moja. Tena gari hiyohiyo ya mkuu wa gereza ndiyo ilikuwa tena imemleta mhariri huyo pale ofisini kwake na bila shaka ilikuwa ikimsubiri.
Walari alitamani kumuumbua lakini akasita.
Akamgeukia tena, "Kwa hiyo tuseme bosi ukimaliza uchunguzi wako ndipo habari hii itachapwa, na hii nadhani itakuwa wiki ijayo, siyo?"
"Kwanza lazima niseme ninakupongeza sana kwa hatua uliyofikia. Pili, kama ulivyosema, tutaichapa hii habari tukiona sasa inafaa kuitoa na haitatuletea matatizo yoyote. Na pia lazima niseme, kama tutaona itatuletea matatizo, heri tuachane nayo na kushughulikia habari nyingine."
“Tuachane nayo! Kwa nini bosi?”
“Kwani habari ni ya gereza tu. Zipo habari nyingi za kuandika zihusuzo wananchi. Ni lazima kama chombo cha habari tuangalie pia usalama wa waandishi wetu,” akajibu Mhariri Mtendaji wa Gazeti la Upekuzi, Sam Odoyo.

********************

Kama alivyolala akiwa mnyonge, Walari aliamka asubuhi, siku ya Jumapili akiwa mnyonge pia.
Sentensi ya mhariri wake kwamba, "lazima niseme, kama tutaona (habari hii) itatuletea matatizo heri tuachane nayo...." ilikuwa inamhuzunisha sana kila akiikumbuka.
Yeye bado aliamini kuwa habari ile aliyokuwa ameichunguza kwa kina sana na bado alikuwa akiendelea kuichunguza kuhusu gereza la Magamaga ilikuwa haina matatizo yoyote, na kama isingechapishwa gazetini jamii kubwa pamoja na wakubwa wa serikali huko makao makuu ya nchi wasingefahamu chochote kuhusu namna maisha ya wafungwa na mahabusu yalivyo katika hatari kubwa kwenye gereza hilo.
Pia kitendo cha mhariri kumwambia kwamba alikuwa hajakutana na mkuu wa gereza wakati si kweli, kilimshangaza na asijue nini hasa lengo lake. Kwa kiwango fulani alianza kupata hisia alizokuwa nazo rafiki yake Nurdin kwamba kama habari hii haikutoka wiki iliyopita, pengine mhariri wake alishaahidiwa hongo na mkuu wa gereza.
Lakini kwa jinsi alivyokuwa akimheshimu na kumwamini mhariri, Sam Odoyo, hakutaka aamini kwamba kitu kama hicho kinaweza kutokea.
Kwanza mhariri alikuwa na shida gani? Ingawa naye alikuwa kaajiriwa na taasisi iliyokuwa inamiliki gazeti lao hilo ya Sauti ya Wanyonge Foundation iliyokuwa pia ikiendesha gazeti lingine la uchunguzi kwa lugha ya Kingereza la The Friday Observer, lakini alikuwa amejitosheleza kwa vitu vingi.
Walari alikuwa na habari kwamba mhariri wao, licha ya gari la kampuni alilokuwa anatembelea, yeye mwenyewe anamiliki magari mawili binafsi, alikuwa na ng'ombe kama sita hivi wa kisasa, shamba la mazao mbalimbali nje ya jiji la Bandaria na kubwa alikuwa na nyumba nzuri. Isitoshe mkewe pia alikuwa akimiliki duka zuri la vipodozi na nguo za kike na mara kadhaa akisafiri kwenda China na Dubai kununua bidhaa.
Toka jana yake Zuhura alikuwa ameshagundua mabadiliko ya mumewe na alimuuliza mara mbili kama anaumwa lakini Walari akawa anajibu kwamba hana tatizo lolote.
Hata hivyo, mwanamke huyo alikuwa anahisi sababu ya mumewe kuwa katika hali ile. Ni habari ya gereza kutotoka gazetini. Mara mbili alitaka kumuuliza kwa nini habari haikutoka lakini akasita, akihisi angezidi kumchanganya zaidi mumewe.
Kwa vile ni siku ya Jumapili ambayo huwa anapumzika baada ya mumewe kumaliza kilichokuwa kinampeleka kanisani, ilipofika saa tatu kasorobo ndipo Walari alikuwa anajinyanyua kitandani tayari kwa kuoga.
Alipomaliza kujimwagia maji, alikwenda kwenye sebule yake ndogo kusubiri chai. Hiyo ilikuwa ni siku ambayo mama yake mzazi alikuwa anatarajia kuondoka kurudi kijijini.
Akiwa pale sebuleni akiongea na mama yake, mtu mmoja akapiga hodi. Alikuwa muuza duka ambalo liko jirani na ofisi yake ambamo huwa anapokelea simu.
Alimkaribisha kijana huyo muuza duka ambaye kwa bahati walikuwa wakiishi jirani katika eneo hilo la uswahilini.
Alimkaribisha chai, lakini yule kijana aitwaye Abdul alijibu kwamba asingekaa.
"Nimekuletea taarifa tu halafu ninarudi kazini," akasema huku amesimama karibu na mlango wa kutokea nje.
"Unasemaje Abdul?" akauliza Walari.
"Kuna mtu mmoja anaitwa Sam Odoyo, anahitaji kuongea nawe. Amesema ni muhimu sana na anapiga simu yako ya mkononi hakupati."
"Yeah! Ni bosi wangu toka makao makuu. Na simu ndo nimeamka na kuiweka kwenye chaji... Yuko wapi?"
"Kapiga simu hapo dukani kwangu, akaniambia uwashe simu yako ya mkononi atakupigia kwani ni muhimu sana. Kanikodia usafiri wa pikipiki kukuona"
"Sawa... Ngoja niwashe simu. Kwa vile hii simu ni ya kwangu binafsi na si ya ofisi hawezi kunilaumu kwa kuizima," alisema. Walari aliangalia saa yake. Ilikuwa saa nne kasorobo, asubuhi.
Alinyanyuka ili kumsindikiza yule kijana aliyekataa kunywa chai na kuacha kikombe chake cha chai mezani kikifuka mvuke huku pembeni mwa kikombe hicho kukiwa na vitumbua vitatu vilivyonunuliwa na mkewe asubuhi hiyo kwa jirani yao. Pia kulikuwa na mihogo aliyochemsha mkewe asubuhi hiyo kuongezea kitafunio.
Kabla hajarejea ndani, mara akaja mgeni mwingine ambaye aliegesha pikipiki yake upenuni mwa nyumba hiyo aliyokuwa amepanga Walari, nyumba ya kizamani iliyokuwa na wapangaji wawili. Mwenye nyumba alikuwa akiishi shamba.
Mgeni huyo alikuwa rafiki yake mkubwa, Nurdin. Walari alimkaribisha huku akijiandaa kupambana kwa maneno ya rafiki yake huyo baada ya habari yake kutotoka gazetini.
Wakati Nurdin akishuka kwenye pikipiki huku Walari akiwa bado kasimama mlangoni akimtazama, alimuona akichomoa gazeti alilokuwa amelikunja na kulibana kwa mpira katika kiti cha nyuma cha pikipiki yake, kisha akajongea mlangoni huku akitabasamu.
Walari alimkaribisha ndani na alijua kwamba gazeti alilokuwa ameshikilia ni Upekuzi.
"Tuseme hii habari yako ya gereza la Magamaga imetupwa au kumetokea nini tena?" Akauliza Nurdin akiketi kabla ya salamu. Shemeji yake alimkaribisha chai.
"Shemeji nashukuru," akajibu Nurdin, "Nimeshatoka huko. Kilichonileta hapa ni hili gazeti. Jana nikashangaa nanunua gazeti sioni habari ya mumeo."
Walari alibaki kimya bila kujadili chochote. Nurdin aliuliza tena akitaka kujua ni vipi habari ya gereza haikutoka, na hiyo ni mara ya pili?
"Kama nilivyosema juzi," Walari akalazimika kujibu. "Habari hiyo ni nzito. Bado mhariri anaifanyia kazi."
Hata hivyo, Walari alisita kueleza kwamba mhariri huyo yuko mjini hapo na keshamweleza sababu za kutoichapisha habari hiyo.

Itaendelea...

Sent using Jamii Forums mobile app
 
Gereza la Kifo - 19

Mtunzi - HAMISI KIBARI

ILIPOISHIA

"Tuseme hii habari yako ya gereza la Magamaga imetupwa au kumetokea nini tena?" Akauliza Nurdin akiketi kabla ya salamu. Shemeji yake alimkaribisha chai.
"Shemeji nashukuru," akajibu Nurdin, "Nimeshatoka huko. Kilichonileta hapa ni hili gazeti. Jana nikashangaa nanunua gazeti sioni habari ya mumeo."
Walari alibaki kimya bila kujadili chochote. Nurdin aliuliza tena akitaka kujua ni vipi habari ya gereza haikutoka, na hiyo ni mara ya pili?
"Kama nilivyosema juzi," Walari akalazimika kujibu. "Habari hiyo ni nzito. Bado mhariri anaifanyia kazi."
Hata hivyo, Walari alisita kueleza kwamba mhariri huyo yuko mjini hapo na keshamweleza sababu za kutoichapisha habari hiyo.

Endelea...

Baada ya kusema vile Walari akaharakisha kumjulisha Nurdin kwamba yule kijana aliyekuwa akitoka kumsindikiza kamletea habari kwamba kulikuwa na simu yake ofisini, na hivyo ilikuwa lazima aondoke muda ule kwenda kusubiria simu hiyo.
“Kwani hajui namba ya simu yako ya mkononi?”
“Nilikuwa nimeizima, isitoshe ile ni simu ya mezani ambayo ni rahisi watu wa ofisini kuitumia kulinganisha na hii ya mkononi,” alijibu Walari ambaye hakupenda mkewe, mama wala Nurdin kusikia mazungumzo yake na bosi wake.
"Kama ni hivyo, twende wote kwa sababu hata mimi naelekea hukohuko. Hapa nilipita kuona kama naweza kupata maelezo yoyote kwa nini habari hii haikutoka jana," akasema Nurdin.
"Ni vigumu sana kwa mtu ambaye si mwandishi kama wewe kujua hali halisi inayotokea kwenye chumba cha habari. Watu wengi wakileta habari zenye tuhuma nzito kama hii, kisha zikachelewa kutoka gazetini wakati bado zinashughulikiwa kuona usahihi wake, basi utawasikia wakirukia kusema, 'mmeshahongwa ndiyo maana hamtoi'."
"Ni sawa unavyosema, lakini kwa nini pia usiamini kwamba Masunju ni mtu mwenye pesa na hila nyingi na hivyo anaweza kutumia pesa zake kwa njia yoyote kuhakikisha kwamba habari hiyo haitoki gazetini? Si unajua jinsi nchi yetu ilivyooza kwa rushwa. Wanahongwa mawaziri na kupindisha mambo sembuse mhariri?" Akahoji Nurdin.
"Naona kosa langu ni kuwaeleza kitu ninachoshughulikia, lakini si rahisi pia mkajua mambo yanayotokea chumba cha habari pale habari inapofika mbele ya mhariri. Naye lazima afanye uchunguzi wake au akaamua kuitunza ili aje aitumie siku nyingine, hata baada ya mwezi mzima, kwa sababu zake yeye mwenyewe. Anaweza hata akaamua kuiacha kama akiona itamletea matatizo, lakini kwa nia nzuri tu, si ya rushwa. Jamani, hii ni taaluma ambayo nyiye hamuijui."
Walari alimfahamisha kuwa mhariri ni mtu aliyeridhika na kujaribu kumtajia baadhi ya mali zake.
"Nini kinakufanya usiamini kuwa hizo mali kazipata kwa rushwa?" akauliza Nurdin.
Walari hakutaka kujibu swali hilo bali aliguna tu na kucheka.
Mabishano yao yaliendelea bila kupatikana mshindi hadi Walari alipoaga kwamba ilibidi aondoke haraka kuwahi kwenda kusikiliza simu toka kwa bosi wake.
Nurdin naye aliaga na kuahidi kumsindikiza kwa pikipiki yake. Iliwachukuwa dakika nane wakawa wameshafika eneo la ofisi ya Walari.
Mwandishi huyo aliagana na Nurdin, kisha akaenda ofisini kwake kuwasiliana na bosi wake.
Baada ya kumpigia simu ya mkononi na kukata, Mhariri alipiga simu kwa kutumia simu yake ya mkononi. Alimjulisha kwamba alikuwa hotelini baada ya kukosa nafasi katika ndege iliyokuwa inaondoka mchana huo.
"Sasa nitaondoka kesho saa mbili asubuhi," sauti ya Mhariri ilisikika upande wa pili wa simu.
Kisha Mhariri akamwambia aachane na kufuatilia habari ya gereza kwa kile alichodai kwamba amechunguza na kugundua kwamba, ingawa kuna ukweli kidogo kuhusu habari hiyo, lakini italiletea gazeti lao matatizo mengi na serikali zaidi ya faida.
Walari ambaye alishangazwa na msimamo huo wa bosi wake aling'aka! "Sikuelewi, bosi. Hii habari italiletea gazeti matatizo kivipi?"
Mhariri alidai kwamba tuhuma zilizopo ni nzito, wakati zinahusu suala nyeti la maisha ya wafungwa na uthibitisho ambao Walari anaodai kuwa anao hauwezi kusaidia sana kufanya gazeti lisiingie kwenye msuguano na serikali.
"Unajua baadhi ya mawaziri hawa ni marafiki zetu na wamekuwa wakitusaidia mengi. Sasa ni bora kuachana na habari hii kuliko matatizo tutakayopata kwa kukosana nao," sauti ya mhariri, Sam Odoyo, ikasikika upande wa pili wa simu.
"Mimi nachukulia kwamba kama viongozi wetu wanawapenda binadamu wenzao na wanathamini utu, haki na ustawi wa wafungwa watatupongeza kwa kuwasaidia kuelewa hali halisi ya gereza la Magamaga ili warekebishe mambo," akajibu Walari.
"Sikiliza Walari, nimekuheshimu sana hadi kukueleza haya kwamba uachane na hii habari kwani huenda bado unafuatilia, vinginevyo ningekaa kimya tu. Nataka uelewe kwamba kitu, hata kama ni kizuri, lakini kama kitatuletea matatizo au kukuletea matatizo wewe mwenyewe ni heri kuachana nacho. Tukiiacha hii habari hakuna hasara yoyote tutakayopata. Na sisi katika menejimenti tutaendelea kuthamini mchango na uwezo wako mkubwa katika hii fani."
"Ninajua hakuna hasara tutakayopata kama gazeti, lakini kuna faida kwa jamii. Kwa hiyo itakuwa ni hasara kwa jamii tunayodai kuitumikia, mkuu…"
"Hakuna lolote bwana mdogo," alimkata kauli: "Tunaandika kila siku uoza katika jamii lakini hakuna lolote linalofanyika. Wewe huijui nchi hii? Au kuna watu wameshakununua na wanataka umharibie mkuu wa gereza ndio maana unang'ang'ania sana... Ninajua taabu ya baadhi ya waandishi wetu. Wewe una wasi wasi gani wakati tunataka uhamie makao makuu kuwa mwandishi mkuu wa gazeti utakayefanya kazi chini ya mhariri wa habari na tutarekebisha mshahara wako na kuwa karibu mara mbili ya unaopata sasa?” Alihoiji Mhariri kwa sauti kali inayoonesha madaraka.
Walari na mkuu wake wa kazi waliendelea kubishana lakini mhariri huyo naye aliendelea kubaki kwenye msimamo wake, na alipoona Walari anaendelea kumshawishi achapishe habari hiyo akaamua kukata simu.
Walari, akiwa amechanganyikiwa, alibaki kwa sekunde kadhaa akiangalia simu yake ya mkononi kama asiyeamini kilichotokea punde.
Walari ambaye alikuwa amepanga kurudi nyumbani kushinda na mkewe pamoja na mwanae, baada ya simu hiyo, aliamua kubaki hapo ofisini akitafakari hali ile.
Sasa ilikuwa ni dhahiri kwamba kazi aliyoisumbukia kwa zaidi ya miezi mitatu huku akihamasishwa na mhariri huyohuyo kuishughulikia kwa bidii ilikuwa kumbe haiwezi kuzaa matunda yoyote. Kwamba ni habari hiyo iliyomfanya watu wafikiri kuwa kabadili dini na kumkosanisha kwa kiwango kikubwa na mkewe, ilikuwa haiwezi kuona tena jua.
Kila akikumbuka hali za wafungwa na adha ambazo wanazipata pamoja na adha alizozipata yeye mwenyewe wakati wa kufuatilia habari hiyo ikiwa ni pamoja na kujifanya mwinjilisti, alisikitika sana kuona inaishia kapuni. Alipanga kujaribu tena kumshawishi mhariri hadi achapishe habari kuhusu hali mbaya ya gereza la Magamaga.
Sentensi ya bosi wake kwamba huenda kanununuliwa na watu fulani pale Bulibuli ili kumchafulia jina mkuu wa gereza pia ilimsikitisha sana.
Aliona kuna umuhimu wa kusafiri kwa kutumia gharama zake mwenyewe kwenda makao makuu akiwa na ushahidi wake wote, pengine akafanikiwa kumshawishi mhariri na kukubali kuchapisha habari hiyo ili jamii ijue kilichokuwa kinaendelea katika gereza la Magamaga. Akiwa huko alipanga kumjulisha mhariri kwamba kama angekuwa na nia ya kuitumia habari hiyo kujinufaisha, basi angekubali kupokea hongo nono toka kwa mkuu wa gereza kwani bado ushahidi wa maneno aliyemrekodi mkuu wa gereza alikuwa nao.
"Nilifanya vizuri kuirudufisha ile hati ya nyumba aliyotaka tukabadili jina na bahati nzuri maelezo yote na lengo lake la kutaka kunihonga vitu kibao nimerekodi. Pengine Mhariri atanielewa," akawa anajisemea mwandishi huyo akielekea kwenye ofisi za waandishi wenzake.
Saa saba kasoro robo mchana, Walari alikuwa anaondoka katika ofisi za gazeti alilokuwa akiliandikia zamani, Waraka wa Leo, kuelekea nyumbani kwake kwa mguu baada ya kuona njaa inamuuma na Jumapili hiyo hakuzoea kula kwenye migahawa na mahoteli. Kabla ya kuelekea nyumbani aliingia kwenye msikiti jirani na ofisi hiyo ili kuswali swala ya mchana.
Walari alikuwa kaenda kwenye ofisi za gazeti hilo la kila siku kupiga soga na waandishi wenzake na kusoma barua pepe zake kwenye mtandao wa kompyuta baada ya mhariri wake kumchanganya akili na kujikuta ofisi yake haikaliki, nyumbani hataki kwenda mapema na hana mahala pengine pa kwenda.
Baada ya swala na kujiombea dua, yeye na familia yake, Walari alianza safari ya kuelekea nyumbani kwake huku akijiuliza kama swala yake imepokelewa. Hii ni kutokana na kuswali huku akiwa na mawazo mengi kuhusu hatua ya Mhariri wake kugoma kuchapisha habari kuhusu hali mbaya ya gereza la Magamaga mjini Bulibuli. Kila akijitahidi kutuliza mawazo kwenye swala inashindikana.
Akitembea kwa unyonge na wakati fulani akikaribia kugongwa na magari kutokana na mawazo, ghafla aliona gari la kifahari la mkuu wa gereza likija mbele yake katika barabara kuu aliyokuwa. Alishangaa alipoangalia ndani ya gari hilo wakati limemkaribia zaidi na kumuona mhariri wake, akiwa na mkuu wa gereza, wakiongea na kucheka. Mhariri wake alikaa kiti cha nyuma na mkuu wa gereza aliketi mbele, kushoto kwa dereva.
Watu wale wa kwenye gari walipomuona walionekana kushtuka na kukwepesha macho yao huku wakijifanya kwamba hawajamuona.

Itaendelea...
 
Gereza la Kifo - 20

Mtunzi - HAMISI KIBARI

ILIPOISHIA

Akitembea kwa unyonge na wakati fulani akikaribia kugongwa na magari kutokana na mawazo, ghafla aliona gari la kifahari la mkuu wa gereza likija mbele yake katika barabara kuu aliyokuwa. Alishangaa alipoangalia ndani ya gari hilo wakati limemkaribia zaidi na kumuona mhariri wake, akiwa na mkuu wa gereza, wakiongea na kucheka. Mhariri wake alikaa kiti cha nyuma na mkuu wa gereza aliketi mbele, kushoto kwa dereva.
Watu wale wa kwenye gari walipomuona walionekana kushtuka na kukwepesha macho yao huku wakijifanya kwamba hawajamuona.

Endelea...

Kitendo kile kilimuondolea Walari utando machoni na kuona ukweli wa wasiwasi aliokuwa nao rafiki yake, Nurdin toka mapema.
"Kwa nini pia usiamini kwamba Masunju ni mtu mwenye pesa na hila nyingi, na hivyo anaweza kutumia pesa zake kwa njia yoyote kuhakikisha kwamba habari hiyo haitoki gazetini," Walari alikumbuka sentensi hiyo ya Nurdin aliyomwambia asubuhi hiyo.
Sasa aligundua kwa nini Masunju alikwenda kumpokea bosi wake uwanja wa ndege. Roho ilimuuma sana.
Walari alibaki amesimama, mwili wote akiuhisi kama wa mtu aliyenaswa na umeme.
Alilitazama lile gari la kifahari likitokomea mithili ya mnyama mkubwa huko lilikokuwa likielekea, kama asiyeamini macho yake.
Mwili ulimgomea kabisa kupiga hatua zaidi kuelekea nyumbani kwake ambako alikuwa anawahi chakula ambacho bila shaka mkewe alikuwa amemtunzia.
Ile njaa kali aliyokuwa akiisikia iliyeyuka ghafla baada ya kuzinduka toka kwenye lindi la fikra lililomzonga ghafla na kumfanya aonekane mithili ya mtu aliyepata habari za kufiwa na mzazi wake aliyekuwa akimpenda sana ama kufiwa na mtoto, kaka, mume au mke.
Sasa aliamua kwenda kununua vocha ili kumuumbua mkuu wake wa kazi kupitia simu. Alikuwa amekata tamaa na sasa aliona ni muda mwafaka wa kuachana na ajira katika gazeti la Upekuzi. Ingawa alijijua kuwa na tabia ya kutoa maamuzi ya harakaharaka ambayo siku zingine aliyajutia, lakini katika hilo aliona ni uamuzi wa busara.
"Siwezi kufanya kazi na watu waliooza kwa rushwa. Kumbe mhariri ni mtu dhaifu namna hii. Kwanza Shirika la Utangazaji la Ulaya (EBC) wamekuwa wakinitaka kwa udi na uvumba niwe mwakalishi wao hapa Bulibuli," akajisemea akipiga hatua za harakaharaka kuelekea kwenye duka ambalo angenunua vocha ya simu upande wa pili wa barabara.
Walari aliweka vocha na kuanza kutafuta namba za simu za bosi wake, Sam Odoyo. Haikuwa kawaida yake kumpigia simu kwa namba yake ya mkononi lakini aliona hana jinsi. Namba aliyokuwa kaizoea ni ile ya ofisi.
Odoyo alipopokea simu, Walari hakuona ajizi kumueleza kwamba amegundua kitendo chake cha kukataa habari ya gereza kumbe kilikuwa si kwa lengo jema.
"Walari, mbona sikuelewi?" Sauti ya mhariri upande wa pili ikauliza.
"Sikiliza mkuu, lazima niseme kwamba hamu imeniisha kabisa ya kufanya kazi na kampuni yako. Kuanzia leo najihesabu kama mwandishi wa kujitegemea. Katika hali kama hii lazima nitafute chombo kitakachokuwa kinajali kazi na maadili. Vyombo vya habari viko vingi na kama nilivyokudokeza siku moja, kwa muda mrefu EBC wamekuwa wakinihitaji."
"Lakini Walari mimi sikuelewi. Umehisi nini baada ya kuniona tukiwa gari moja na mkuu wa gereza? Mimi ninaye katika harakati za kufuatilia zaidi habari yako. Wewe unafikiria nini tuseme?"
"Unajua vizuri ninachokifikiria. Naomba tu nikushukuru kwa kufanya kazi kwa muda huu wote kwani ulionyesha ushirikiano na mimi nikakuamini sana. Hata hivyo, lazima nikiri pia kwamba, ingawa ni kwa kipindi kifupi, gazeti lako limenipatia hadhi kubwa zaidi kwa habari za uchunguzi nilizozifanyia kazi nanyi mkazichapisha na ndio maana EBC wananitaka na hata Waraka wa Leo walikuwa wananibembeleza nirudi. Kipindi hiki nitakachokuwa bado sijapata ajira nitakuletea habari kama mwandishi huru. Kwaheri simu yangu inaelekea kukata. Vocha imesha." Walari alikata simu. Bosi wake alimpigia lakini Walari hakupokea.

************************

Saa nne na nusu usiku ilimkuta Walari na mkewe wakiingia chumbani kulala. Usiku huo, Alhamisi, ulikuwa wa giza totoro na joto kiasi, kulinganisha na siku za nyuma. Katika mtaa wao, uswahilini, makelele ya kawaida yaliyozoeleka yalikuwa yamepungua sana kumaanisha kwamba watu wengi walikuwa wameshakwenda kulala.
Kwa mbali kelele zilizokuwa zinasikika ni za muziki kutoka kwenye klabu kimoja cha pombe za kienyeji ama mataputapu kama watu wanavyoita siku hizi. Kilabu hicho ambacho humaliza shughuli zake saa tano na nusu usiku kiko umbali wa mita 300 toka nyumba aliyokuwa akiishi Walari.
Mtoto wao ambaye alikuwa kwenye kitanda chake kidogo chumbani alikuwa ameshaota sana ndoto kutokana na kulala toka saa moja na nusu jioni hiyo.
"Mama Ashraf," aliita Walari.
Mkewe, akiwa amejilaza kando yake aliitika na Walari akaendelea.
"Nilikuwa sijakuelezea. Nimeshaacha kazi katika gazeti la Upekuzi."
"Umeacha kazi! Mbona sikuelewi?" Akauliza Zuhura kwa mshangao huku akinyanyuka na kukaa kitandani.
"Ndiyo, nimeacha. Toka Jumapili ya wiki hii tarehe 8. Karibu wiki mbili sasa zinaisha toka niache. Mimi si mwandishi tena wa gazeti la Upekuzi."
"Imekuaje mwenzangu?" Akauliza Mama Ashraf akichelea kusema labda ni kutokana na habari ya gereza kutochapishwa, hali ambayo alihisi inaweza kumtia ghadhabu mumewe kwa kuwa mwanamke huyo alikuwa mtu wa staha na heshima kubwa kwa mumewe.
"Kwa kifupi ni kama Nurdin alivyotabiri. Akisikia atanicheka sana. Leo nimekutana naye nikasita kumwambia kwamba utabiri wake ulikuwa sahihi."
"Enhe! Imekuwaje tena."
Walari alimsimulia kila kitu. Alianza kumsimulia jinsi alivyopigiwa simu Jumamosi tarehe 7 kwamba mhariri wake alikuwa anakuja Bulibuli na yeye kuamua kwenda kumpokea Uwanja wa Ndege, lakini akashangaa kuona mkuu wa gereza naye akiwa kaenda kumpokea. Akamweleza jinsi alivyowakimbia na baadaye mhariri akaja ofisini mwake na kumwambia mambo ambayo aliyaita utumbo mtupu. Masimulizi ya siku iliyofauta, yaani Jumapili, ndiyo yaliyomwacha hoi mwanamke huyo.
Hata hivyo, Zuhura alionekana kusikitishwa na uamuzi wa ghafla wa mumewe. Akasema alikuwa hamshauri kabisa kuacha kazi kwa ajili hiyo.
“Mimi ndiye mkeo na mshauri wako mkubwa. Tatizo lakio ni kufanya mambo kimya kimya bila kunishirikisha.”
“Kuna mambo ya kazi na mambo ya kijamii. Kweli ni busara mambo ya kazi niwe ninakwambia? Yaani kila kinachotokea ofisini ninakwambia, kila niachotaka kufanya ninakwambia… Kweli?”
“Kuna mambo ya kawaida na yasiyo ya kawaida. Hili lilishaanza kuwa siyo la kawaida. Ulipaswa kunishirikisha. Hata kabla ya kukata shauri la kuacha kazi ambalo ni jambo zito ulipaswa uje kuniambia, tukalijadili pamoja. Ukisikia mfumo dume ndio huo wa kusema yule ni mwanamke tu atanishauri nini.”
“Basi nisamehe kwa hilo, mke wangu. Sasa nitakuwa ninakushirikisha hasa masuala yanayohusu maamuzi. Lakini usije ukaniambia habari ya kupokea rushwa. Heri nife maskini kwani maskini pia Mwenyezi Mungu amewaumba. Kwa nini nisiwe mimi miongoni mwao? Wewe unadhani utajiri wa hongo kama wa Sam Odoyo una hadhi yoyote?”
Zuhura hakujibu hoja ya mumewe. Alibaki kimya kisha akamweleza kwamba yote yanayotokea ni kutokana na kiburi cha kukataa ushauri wake, ushauri wa mama yake na wa rafiki yake, Nurdin.
“Sasa angalia hata kazi yenyewe umeikosa.”
"Lakini usiwe na wasiwasi mke wangu. Nimeshapata kazi nyingine na pengine, japo ni ya mkataba wa miaka miwili tu kwanza, inaweza kuwa yenye manufaa kuliko hata huko nilikokuwa. Ila ninakuomba sana usinishauri kufanya maovu. Hakuna kitu kibaya kwa mwandishi kama kupokea rushwa ambayo hata dini yetu inakataza."
"Umepata wapi kazi?" Akauliza mwanamke yule akiwa bado kaketi kitandani.
"Nimepata EBC. Si niliwahi kukwambia namna hawa watu walivyokuwa wakinitaka. Mwakilishi wao aliwahi kuniambia kama vile masihara. Nimeenda kwa mwakilishi wao huyo hapa Bulibuli akaniambia bado wananihitaji. Unajua yeye anatakiwa kuhamia makao makuu na hivyo walikuwa wanasaka mtu wa kubaki hapa kuchukua nafasi yake na wanasema hawaoni mwandishi mwingine hapa anayefaa zaidi yangu. Yule bwana, Madenge Marare, tuliwahi kufanya naye kazi katika gazeti la Waraka wa Leo, anajua uwezo wangu.
Nilikwenda kumuona Jumatatu, siku hiyohiyo akawasiliana na wakubwa wake London, na leo ndiyo wameleta taarifa. Kesho naanza kazi rasmi na kesho hiyohiyo ninatuma habari yangu ya gereza. Jioni itasikika dunia nzima. Yule mwakilishi wao kaipenda sana hii habari ya gereza. Ingawa miye nilikuwa sipendi kufanya kazi na redio lakini hata hivyo, nashukuru kwamba habari hii itajulisha dunia nzima hali ya gereza la Bulibuli kuliko hata gazeti ambalo linasomwa nchi chache tu, sana sana ni mbili tu, hapa kwetu na majirani zetu wa kaskazini."
Zuhura hakutaka kujadili zaidi kuhusu suala hilo kwa sababu alikuwa anahisi usingizi. Alipanga kuendelea kumhoji mumewe kuhusu uamuzi wa kuacha kazi Upekuzi na kwenda EBC kesho yake.
"Samahani mpenzi, mimi nasikia usingizi sana. Nalala," alisema akijirusha kitandani na kuvuta shuka juu ya nguo yake ya kulalia aliyokuwa kavaa usiku huo.

Itaendelea...
 
Gereza la Kifo - 21

Mtunzi - HAMISI KIBARI

ILIPOISHIA

Nilikwenda kumuona Jumatatu, siku hiyohiyo akawasiliana na wakubwa wake London, na leo ndiyo wameleta taarifa. Kesho naanza kazi rasmi na kesho hiyohiyo ninatuma habari yangu ya gereza. Jioni itasikika dunia nzima. Yule mwakilishi wao kaipenda sana hii habari ya gereza. Ingawa miye nilikuwa sipendi kufanya kazi na redio lakini hata hivyo, nashukuru kwamba habari hii itajulisha dunia nzima hali ya gereza la Bulibuli kuliko hata gazeti ambalo linasomwa nchi chache tu, sana sana ni mbili tu, hapa kwetu na majirani zetu wa kaskazini."
Zuhura hakutaka kujadili zaidi kuhusu suala hilo kwa sababu alikuwa anahisi usingizi. Alipanga kuendelea kumhoji mumewe kuhusu uamuzi wa kuacha kazi Upekuzi na kwenda EBC kesho yake.
"Samahani mpenzi, mimi nasikia usingizi sana. Nalala," alisema akijirusha kitandani na kuvuta shuka juu ya nguo yake ya kulalia aliyokuwa kavaa usiku huo.

Endelea...

"Sawa. Wewe lala. Ngoja miye nisome magazeti. Unajua leo sijapata kabisa muda wa kusoma haya magazeti. Nimesoma juujuu tu vichwa vya habari."
Mwandishi huyo alivuta magazeti matatu yaliyokuwa juu ya meza na kuanza kusoma moja wapo huku akiwa kajilaza kitandani.
Baadaye alisikia mwanae akilia kuashiria kwamba alitaka kujisaidia. Mkewe pia alishtuka kwa kilio hicho, lakini Walari akamtaka aendelee kulala.
Alinyanyuka na kwenda kwenye kitanda cha mtoto. Akamshusha chini na kumsogezea dubwasha la kukojolea. Mtoto alijisaidia kisha Walari akambeba mwanaye huyo na kumlaza kwenye kitanda chake huku akimpiga busu.
Kisha alirudi kuendelea na usomaji wa magazeti. Hata hivyo, baada ya kupitia magazeti mawili alihisi usingizi. Wakati huo mkewe alikuwa anakoroma.
Ilikuwa ni kawaida yake anapopanda kitandani kuchukua kati ya saa moja na mbili akisoma magazeti, hali ambayo mkewe alikuwa ameshaizowea japo ilikuwa inamuudhi, lakini siku hiyo Walari alisikia usingizi mapema kidogo.
Aliangalia saa yake na kugundua kwamba ilikuwa inaelekea saa tano na nusu usiku.
Alinyoosha mkono kupunguza sauti ya redio, kisha akazima taa, akijitupa kitandani pembeni mwa mkewe na kuvuta shuka.
Wakati mwandishi huyo ameshalala usingizi alishituka na kwa sekunde kadhaa hakujua nini kilichomshitua usingizini. Baadaye alisikia kama mchakato au mtu kupita nje ya dirisha la chumba chake.
Alisikiliza kwa makini lakini ule mchakato ukatulia.
Wakati akiwa kaanza tena kusinzia, alisikia kishindo kikubwa ambacho kilimshtua sana. Kishindo hicho kilifuatiwa na kingine na kingine na mara akagundua kwamba mlango wa kuingia kwenye sebule yake ndogo ulikuwa unavunjwa. Mtu akishaingia sebuleni ni rahisi kuvunja mlango wa chumba chake ambao ulikuwa si imara sana.
Mkewe naye alikuwa keshashtuka na kukaa juu ya kitanda. Mara wakasikia mlio wa risasi huko nje. Wakaingiwa uoga zaidi.
"Tupige kelele mume wangu, tumevamiwa," akanong'ona Zuhura karibu na sikio la Walari huku akitetemeka kwa uoga.
Walari alilipuka kwa makelele lakini sekunde ileile mlango wa chumba chao ulikuwa unavunjwa.
Walari na mkewe waliendelea kupiga makelele ya kuomba msaada ambayo inaonekana yalipokelewa vyema kwani kwa mbali walisikia kama milango ya nyumba za majirani nazo zikifunguliwa.
Ghafla mlio wa risasi ukasikika chumbani mwao, na Walari kama umeme akaruka na kulala chini huku akimvuta mkewe.
Mkewe naye alimfuata chini. Risasi ambazo sasa waligundua kwamba zilikuwa zinatokea dirishani zikaanza kumiminika mle chumbani uelekeo wa kitanda chao. Baada ya risasi kusikika, vurugu za kuvunja mlango wao zikakoma lakini bunduki ya dirishani ikaendelea kufyatua risasi mle chumbani kuelekea kwenye kitanda chao ambacho hakikuwa na mtu wakati huo na nyingine zikigonga ukuta.
Mtoto wao alipiga makelele pale kitandani na Zuhura akataka kunyanyuka ili amchukuwe na kulala naye pale chini, lakini Walari akamvuta mkono ili asinyanyuke. Hata hivyo, mwanamke yule akafanya nguvu na kufanikiwa kumponyoka na kunyanyuka.
Sekunde chache baada ya mkewe kunyanyuka, Walari alisikia mlio wa risasi kutoka dirishani na muda huo huo akasikia mkewe anapiga makelele ya kuomba msaada.
Mkewe na mtoto walimwangukia pale chini. Akamsikia mkewe akiugulia kwa maumivu, mwanaye pia, akiwa pale chini alikuwa akiangua kilio kikali.
Risasi ambazo nyingi zilikuwa zikipiga kitandani au kugonga ukuta zilikoma.
Mkewe aliendelea kuugulia kwa maumivu pale chini, pembeni mwa kitanda na yule mtoto sauti ilikuwa imemkauka kwa kulia.
Yeye Walari alikuwa anajiamini kwamba bado yuko salama lakini alikuwa na mashaka na mkewe pamoja na mwanae.
Alipata hali ngumu aliposikia mkewe ananyamaza kimya pamoja na mtoto, muda mfupi baada ya kusikia mlio mwingine wa risasi.
Alihisi mkewe na mwanae wamekufa, akatamani ajitokeze naye auawae.
Aliona hakuna haja ya yeye kusalimika kama mkewe na mtoto watakuwa wameuawa.
Kwa mbali alisikia vishindo vya watu wanaokimbia. Zilipita dakika kama tatu hivi bila kusikia mlio mwingine wa risasi wala kishindo chochote, iwe mle chumbani au nje ya dirisha ambako alihisi majambazi hao walikuweko zaidi ya mmoja.
Alinyanyuka, sasa akiwa tayari kukabiliana na kifo kwani aliamini mkewe na mtoto wameshakufa.
"Niueni nyiye watu. Kwa nini mniulie familia yangu? Kama mngetaka kila changu ningewapa. Si mngechukuwa TV na chochote mnachotaka kuliko kuniulia familia yangu," alisema kwa ukali akinyanyuka na kusimama pembeni mwa mwili wa mke wake katika chumba hicho kilichokuwa giza.
Alisikiliza kidogo na kugundua kwamba hali ilikuwa shwari na bila shaka majambazi hao walikuwa wameshakimbia. Alishangaa kwamba hadi muda huo kulikuwa hakuna jirani yeyote aliyejitokeza.
Walari aliwasha taa ya chumbani baada ya hali ya ukimya kuendelea kutawala. Aligundua kwamba mlango wa chumbani kwake ulikuwa umevunjwa, lakini kulikuwa hakuna dalili kwamba majambazi yale yaliingia chumbani mwake. Akahisi kuwa makelele yao yalisadia wasiingie chumbani na ndipo wakaamua kufyatua risasi kupitia dirishani.
Aliangalia chini na kumuona mkewe akiwa amelala katikati ya dimbwi la damu.
Mwanae mpendwa, Ashraf, naye alikuwa kalala katika dimbwi jingine la damu.
Wakati akijongea kuangalia hali zao, majirani sasa ndipo walikuwa wamepata ujasiri wa kufika nyumbani kwake.
Baadhi walisimama dirishani na wengi wakaingia ndani na kumkuta Walari akiwa kainama pembeni mwa mkewe. Alimgusa na kugundua kwamba alikuwa kazirai lakini bado mzima.
Alimshika pia mwanae kifuani na kugundua kwamba hata yeye alikuwa kapoteza fahamu tu.
Walari aliomba msaada wa haraka. Wale majirani wakafanya haraka kumsaidia na baaada ya dakika chache, gari ikaletwa na majeruhi hao wakakimbizwa hospitali. Gari hiyo ilikuwa ya jirani yao mmoja aliyeonekana kuwa tajiri mkubwa pale mtaani kwao uswahilini.
Walari akiwa na majirani watatu, mmoja akiwa mpangaji mwenzake, ndani ya gari hilo pamoja na dereva, walikumbuka kwamba kule hospitali wasingepata tiba yoyote kama wasingepitia polisi kwanza kuandika maelezo na kupewa hati maalumu ya kwenda nayo hospitali.
"Jamani, mimi ninajua utaratibu ndiyo huo, lakini hamuoni tutawapoteza hawa watu kama tutapoteza muda kwenda huko?" Akashauri Walari akitaka waende hospitali kwanza ambako wangejitahidi kuwashawishi madaktari na wauguzi hadi waelewe hali ilivyo na kutibu majeruhi wao.
"Tiba kwanza, mambo ya polisi baadaye," akawa anasisitiza mwandishi huyo wa habari aliyekuwa na mashaka makubwa juu ya hali ya mkewe na mtoto.
Hata hivyo, majirani wale waling'ang'ania kwamba itakuwa ni kazi bure kwenda hospitali kama hawana hati ya polisi kwani isingelikuwa rahisi wao kupokelewa na kupewa tiba.
Walari hatimaye alisalimu amri baada ya kuona hata dereva aliyekuwa akiendesha gari hilo akisisitiza kwamba, kwa tukio kama hilo, ilikuwa ni kupoteza muda na kuharibu bure mafuta kwenda hospitali bila kupitia polisi kwanza.
Saa nane kasorobo, usiku, Walari na wale wasamaria wema walikuwa wanawasili katika kituo kidogo cha polisi. Kwa eneo hilo, kituo hicho ndicho kilionekana kuwa karibu, japo ilikuwa mbali kidogo kutoka kwa Walari na bila shaka hata milio ya zile risasi ilikuwa ni vigumu kusikia na kama zilisikika basi ni kwa mbali sana.
Pale kituoni walimkuta askari mmoja tu akiandika maelezo ya watu walioaminika kuwa wazururaji ambao baadaye akina Walari waliambiwa kwamba walikamatwa na askari waliokuwa doria, askari ambao baada ya kuwakamata watu hao na kuwaleta kituoni walirudi tena na kumuacha huyo mwenzao mmoja kituoni.
Walishangaa sana kugundua hilo na wakajiuliza kama wale walioko doria hawakusikia milio ya risasi, pengine wangekurupusha majambazi yaliyokuwa yamemvamia Walari. Yule askari wa kituoni naye alijibu kwamba hajasikia mlio wowote wa risasi na akajibu kwamba inaonekana askari waliokuwa doria usiku huo walipita njia tofauti.
Walari na wenzake walimweleza askari yule kuhusu wagonjwa waliokuwa nao mle kwenye gari, lakini askari huyo asiye na cheo, aliyeonakana hana haraka, akawataka wasubiri.
Huku wao wakiwa wamesimama nyuma ya kaunta fupi ya kituo hicho kidogo, askari yule aliendelea kuwahoji wale watuhumiwa wa uzembe na uzururaji taratibu sana huku akiendelea kuandika maelezo ya watuhumiwa hao waliokuwa wameketi sakafuni.
Kila mtu alimshangaa askari huyo kwa kutoonekana kujali taarifa kwamba kikundi kile cha watu kilikuwa na wagonjwa mahututi. Ikabidi tena Walari amjie juu, tena kwa sauti ya hasira.
"Ndugu askari. Tumekwambia tuna wagonjwa mahututi, vipi?"
"Kama mngekuwa na haraka mngekuja jana. First in, first out. Nyiye si mmewakuta hawa, subirini. Kama mgonjwa ni wa kufa atakufa tu."

Itaendelea...
 
Gereza la Kifo - 22

Mtunzi - HAMISI KIBARI

ILIPOISHIA

Walari na wenzake walimweleza askari yule kuhusu wagonjwa waliokuwa nao mle kwenye gari, lakini askari huyo asiye na cheo, aliyeonakana hana haraka, akawataka wasubiri.
Huku wao wakiwa wamesimama nyuma ya kaunta fupi ya kituo hicho kidogo, askari yule aliendelea kuwahoji wale watuhumiwa wa uzembe na uzururaji taratibu sana huku akiendelea kuandika maelezo ya watuhumiwa hao waliokuwa wameketi sakafuni.
Kila mtu alimshangaa askari huyo kwa kutoonekana kujali taarifa kwamba kikundi kile cha watu kilikuwa na wagonjwa mahututi. Ikabidi tena Walari amjie juu, tena kwa sauti ya hasira.
"Ndugu askari. Tumekwambia tuna wagonjwa mahututi, vipi?"
"Kama mngekuwa na haraka mngekuja jana. First in, first out. Nyiye si mmewakuta hawa, subirini. Kama mgonjwa ni wa kufa atakufa tu."

Endelea...

"Jamani tuachane na huyu mtu, twen'zetuni Central (Kituo cha polisi cha kati)" alishauri dereva wa gari walilokuwa nalo.
Walirudi kwenye gari, Mama Ashraf bado alikuwa hajitambui, lakini sasa damu zilikuwa zimekoma kumvuja sehemu ya jeraha baada ya kumpa huduma ya kwanza.
Lakini yule mtoto alikuwa ana fahamu zake, isipokuwa alikuwa analia muda wote kutokana na maumivu.
Walipofika kwenye kituo cha polisi Kati, ambako Walari alienda kwa shingo upande baada ya wenziye kumkatalia tena nia yake ya kwenda moja kwa moja hospitali, walisikilizwa haraka na kupatiwa huduma.
Baadaye wakaondoka kasi kuwahi hospitali ya mkoa. Huko nako, baada ya kuwasili, iliwachukuwa zaidi ya dakika 20 kabla wagonjwa hao hawajaanza kuhudumiwa.
Wakati mkewe anaanza kuhudumiwa wodini ilikuwa ni saa kumi na ushee usiku, zaidi ya masaa mawili toka mwanamke huyo apigwe risasi.
Walari alikuwa na mashaka makubwa kama mkewe atasalimika kifo kwani hata wakati wauguzi wanampokea pale mapokezi walionesha hali ya kukata tamaa. Iligundulika kwamba mkewe alikuwa amepigwa risasi kiunoni na alikuwa ametokwa damu nyingi sana. Kitu kingine kilichomsikitisha Walari ni maelezo kwamba hata kama akipona, kiuno kinaweza kisifanye kazi au miguu kupooza na hivyo akawa ni mtu wa kukaa muda wote mithili ya kiwete.
Daktari aliyewapokea alisema ilitakiwa mwanamke huyo aongezewe damu haraka, lakini benki ya damu ya hospitali hiyo ilikuwa haina hata tone.
Walari na wale majirani wawili pamoja na dereva walijitolea kutoa damu.
"Hata hivyo, itachukuwa muda kumwekea mgonjwa wenu damu. Si mnajua siku hizi damu haziaminiki? Mpaka zichunguzwe sana," akasema daktari huyo baada ya Walari kuona muda unakwenda bila mkewe kuwekewa damu. Wakati huo ilikuwa inaelekea saa 12 alfajiri.
Mtoto Ashraf yeye alikuwa amepata jeraha kwenye bega, kwa kile kilichoonekana kwamba alikwaruzwa na risasi. Tayari mtoto huyo alikuwa ameshashughulikiwa kwa kusafishwa jeraha na kuwekewa dawa na sasa alikuwa kalala chumba cha mapumziko akiwa ametundukiwa dripu ya maji.
Wasiwasi ulizidi kumwandama Walari kuhusu hali ya mkewe. Hata hivyo, daktari aliyekuwa akimhudumia aliwaambia warudi nyumbani na kuja kuangalia hali ya mgonjwa baadaye.
"Mbona kumeshakucha, tuje asubuhi gani tena?" Akauliza Walari akiangalia saa yake.
Lakini jirani mmoja akamkumbusha kwamba walitakiwa kuondoka kwenda polisi kituo cha Kikuu kuwachukua askari kwenda eneo la tukio mapema.
Wakiwa njiani kurudi polisi, pamoja na mtoto Ashraf ambaye alikuwa kalala, jirani mmoja alisema kwamba wakati majambazi yale yanavunja mlango wao walisikia na hadi akina Walari walipokuwa wanapiga makelele wao walikuwa nje na silaha zao duni, lakini waliogopa baada ya kugundua kwamba majambazi hayo yalikuwa mengi pamoja na bunduki zaidi ya moja.
"Sisi tulianza kuja lakini wakafyatua risasi kuelekea upande wetu, ikabidi tukimbie. Walikuwa kama majambazi sita hivi," akasema jirani mmoja, mtu wa makamo, ambaye nyumba yake inapakana na ile aliyopanga Walari.
Mfanyabiashara aliyepanga nyumba moja na Walari yeye alisema kwamba inaonekana majambazi yale yalimpania Walari peke yake, kwani yalipofika yalifunga mlango wa chumba chake na wa sebule yake kwa nje na hilo aliligundua wakati alipojaribu kufungua akidhani labda nyumba iliyokuwa inavunjwa ni ya jirani.
Alisema alipong'amua kwamba majambazi yale yako kwenye nyumba yao, hasa baada ya kusikia milio ya risasi, akalazimika yeye na mkewe kujificha nyuma ya kabati chumbani mwao.
"Hata chumba cha watoto nako walikuwa wamefungiwa kwa nje," alisema mpangaji mwenzake huyo, Ibrahim Nyamsha, ambaye katika nyumba hiyo yenye wapangaji wawili, alikuwa na vyumba viwili na sebule. Akasema baada ya hali kuwa shwari majirani waliofika kwenye tukio ndio waliowafungulia mlango uliokuwa umefungwa kwa nje kwa komeo.
"Kuna haja ya kuweka vitasa vya kisasa ambavyo haviruhusu mtu kukufungia kwa nje," akasema Nyamsha.
Nyamsha ndiye aliyekuwa na sebule kubwa na vitu vingi na mtu yeyote angefikiria kwamba kutokana na kuwa na vitu vingi, angekuwa kivutio kikubwa cha majambazi kumvamia kulinganisha na Walari.
Walifika kituoni na kuondoka na askari wawili hadi nyumbani kwa Walari kufanya uchunguzi wa tukio hilo.
Walipofika nyumbani, majirani kadhaa walikuja asubuhi hiyo, na ndipo mmoja akasema alifanikiwa kumchoma mkuki jambazi mmoja, ingawa ana hakika hakumuua. Hata hivyo akasema nusura na yeye apigwe kwa risasi lakini hawakufanikiwa kumuona na kilichosadia zaidi ni kwamba walikuwa wanakimbia kutoka katika eneo la tukio na mkuki huo ulisaidia kuwakimbiza zaidi kwenye gari lao.
"Mimi nilikuwa nimejibanza mahala na mkuki wangu na wao wakati wanakimbia kurukia kwenye gari aina ya pick-up waliokuwa wameiegesha uchochoroni, mimi nilikuwa nimejificha kwenye banda moja na ndipo nikampiga mkuki mgongoni mmoja wao aliyekuwa mwisho," akasema jirani yule.
Jirani huyo, ambaye alizoeleka kwa jina la Mzee Matata, jina ambalo Walari hajui lilitokana na nini kwani si jina lake halisi, akasema baadaye ule mkuki aliukuta katika eneo la tukio lakini ana hakika ulimpata huyo mtu kwani yeye na watu wengine walishuhudia asubuhi hiyo damu nyingi katika eneo hilo na mkuki wenyewe ulikuwa na damu pia. Akasema inaonyesha mkuki ulimwingia jambazi huyo kiasi cha nchi nne hivi.
"Sijui kaumia kiasi gani na ana bahati mkuki hauna sumu. Ningemuua yule," akasema na kuongeza kuwa ana hakika mtu huyo kama hakumpiga sehemu mbaya inayoweza kusababisha kifo chake basi lazima atapelekwa hospitali kutibiwa na hivyo kuwepo na urahisi wa kumkamata.
"Tatizo nilikuwa mbali kidogo. Kama ningekuwa karibu yule mtu lazima angekwenda chini na asingenyanyuka hata kama mkuki hauna sumu," akasema mzee huyo ambaye zamani alikuwa mwindaji wa kutumia zana za jadi.
Askari waliokuwa wakisikiliza maelezo ya mzee huyo kabla ya kufanya upekuzi ndani ya nyumba ya Walari, waliahidi kufanyia kazi maelezo ya Mzee Matata.
Askari walifanya uchunguzi huku wakimhoji maswali haya na yale Walari pamoja na yule mpangaji mwenziye, wakagundua kwamba hakuna kitu kilichoibiwa mule ndani zaidi ya kamera yake aliyokuwa ameiacha sebuleni juu ya meza wakati anaingia kulala.
Karibu vitu vyote vya maana, kama vile redio kubwa, televisheni na deck vilikuwa mahala pake. Walari pia alishukuru kwamba vifaa vyake vilivyo na habari kuhusu gereza, kama vile mikanda aliyorekodi na kitabu kidogo alichokuwa amenakili majina ya wafungwa waliokufa kwa kipindi cha miezi sita, vilikuwa salama.
Hisia zilianza kujengeka kwamba majambazi yale bila shaka hayakuwa na lengo la wizi, bali kufanya hujuma, na hasa kuua mtu, na bila shaka yalidhamiria kumuua yeye Walari.
Sababu za kutuhumu namna hiyo zilikuwa nyingi kwa polisi waliofanya uchunguzi. Na hata majirani pamoja na Walari mwenyewe alituhumu hivyo.
Moja, ilikuwa hali hiyo ya majambazi yaliyosadikika kuja kwa gari, kuondoka bila kuchukua kitu chochote cha maana zaidi ya ile kamera ambayo ilionekana kwamba pengine watu wale waliichukuwa kama kudanganyia tu au walitaka asitumie tena kifaa hicho, kama siyo kuhisi kwamba kulikuwa na picha wasizopenda zichapishwe gazetini.
Sababu nyingine ni majambazi hayo kulenga zaidi risasi zao kitandani ambako inaonekana yaliamini Walari alikuwapo na kwa vile chumba kilikuwa giza, bila shaka yalikuwa yamefanya utafiti na kugundua mahala kitanda kinapokaa chumbani kwake.
Sababu nyingine ilikuwa ni kumvamia Walari ambaye hakuwa na mali nyingi kulinganisha na mpangaji mwenzake ambaye alikuwa na vitu vingi vya thamani na bila shaka alikuwa hakosi akiba ya kutosha chumbani mwake kulinganisha na Walari.
Akiwa anaelekea kumaliza ujenzi wa nyumba yake si mbali sana na Gereza Kuu la Magamaga mpangaji mwenza huyo wa Walari alikuwa anamiliki duka kubwa la vipodozi stendi na vitu vingi vyenye thamani sebuleni kwake kama redio kubwa na televisheni kubwa bapa ya kisasa.
Mara kadhaa mpangaji huyo alikuwa hafungui muziki kwa sauti kubwa kwa hofu ya kuvutia wezi, hasa kwa kuzingatia kuwa nyumba hiyo ya kizamani waliokuwa wakiishi haikuwa imara sana kwenye milango na madirisha na wala haikuwa na ua.
Pia mpangaji huyo alikuwa na vitu vingi vya kisasa kama vile mafriji, majiko ya gesi, mitambo ya umeme ya kufulia nguo, kompyuta mbili mpakato, yake na ya mkewe na kadhalika.
Walari, katika kusaka mtu anayeweza kuhusika katika tukio hilo, kama si majambazi, moja kwa moja alielekeza tuhuma zake kwa Masunju kwa vile aliahidi kupambana naye.
Alikumbuka maneno aliyoyasema Masunju siku alipomvamia ofisini kwake: "Lakini pamoja na hayo lazima pia nikuonye kitu kimoja. Kama utakataa hii offer yangu na kuendelea na mpango wako utakuwa hutaki urafiki nami, badala yake utakuwa umetangaza vita na mimi. Kwa hali hiyo lazima nami nitajihami na hapo tutalazimika kupimana ubavu. Tafadhali usiseme hivi ni vitisho bali ni ukweli mtupu.... Najua kuna watu wanakutumia ili uniharibie jina kwa malengo yao. Mimi nina maadui wengi sana wasiotaka maendeleo yangu, lakini pia nina marafiki wengi ambao najua watanisaidia kama utaamua kuendelea na vita dhidi yangu."

Itaendelea...
 
Gereza la Kifo - 21

Mtunzi - HAMISI KIBARI

ILIPOISHIA

Nilikwenda kumuona Jumatatu, siku hiyohiyo akawasiliana na wakubwa wake London, na leo ndiyo wameleta taarifa. Kesho naanza kazi rasmi na kesho hiyohiyo ninatuma habari yangu ya gereza. Jioni itasikika dunia nzima. Yule mwakilishi wao kaipenda sana hii habari ya gereza. Ingawa miye nilikuwa sipendi kufanya kazi na redio lakini hata hivyo, nashukuru kwamba habari hii itajulisha dunia nzima hali ya gereza la Bulibuli kuliko hata gazeti ambalo linasomwa nchi chache tu, sana sana ni mbili tu, hapa kwetu na majirani zetu wa kaskazini."
Zuhura hakutaka kujadili zaidi kuhusu suala hilo kwa sababu alikuwa anahisi usingizi. Alipanga kuendelea kumhoji mumewe kuhusu uamuzi wa kuacha kazi Upekuzi na kwenda EBC kesho yake.
"Samahani mpenzi, mimi nasikia usingizi sana. Nalala," alisema akijirusha kitandani na kuvuta shuka juu ya nguo yake ya kulalia aliyokuwa kavaa usiku huo.

Endelea...

"Sawa. Wewe lala. Ngoja miye nisome magazeti. Unajua leo sijapata kabisa muda wa kusoma haya magazeti. Nimesoma juujuu tu vichwa vya habari."
Mwandishi huyo alivuta magazeti matatu yaliyokuwa juu ya meza na kuanza kusoma moja wapo huku akiwa kajilaza kitandani.
Baadaye alisikia mwanae akilia kuashiria kwamba alitaka kujisaidia. Mkewe pia alishtuka kwa kilio hicho, lakini Walari akamtaka aendelee kulala.
Alinyanyuka na kwenda kwenye kitanda cha mtoto. Akamshusha chini na kumsogezea dubwasha la kukojolea. Mtoto alijisaidia kisha Walari akambeba mwanaye huyo na kumlaza kwenye kitanda chake huku akimpiga busu.
Kisha alirudi kuendelea na usomaji wa magazeti. Hata hivyo, baada ya kupitia magazeti mawili alihisi usingizi. Wakati huo mkewe alikuwa anakoroma.
Ilikuwa ni kawaida yake anapopanda kitandani kuchukua kati ya saa moja na mbili akisoma magazeti, hali ambayo mkewe alikuwa ameshaizowea japo ilikuwa inamuudhi, lakini siku hiyo Walari alisikia usingizi mapema kidogo.
Aliangalia saa yake na kugundua kwamba ilikuwa inaelekea saa tano na nusu usiku.
Alinyoosha mkono kupunguza sauti ya redio, kisha akazima taa, akijitupa kitandani pembeni mwa mkewe na kuvuta shuka.
Wakati mwandishi huyo ameshalala usingizi alishituka na kwa sekunde kadhaa hakujua nini kilichomshitua usingizini. Baadaye alisikia kama mchakato au mtu kupita nje ya dirisha la chumba chake.
Alisikiliza kwa makini lakini ule mchakato ukatulia.
Wakati akiwa kaanza tena kusinzia, alisikia kishindo kikubwa ambacho kilimshtua sana. Kishindo hicho kilifuatiwa na kingine na kingine na mara akagundua kwamba mlango wa kuingia kwenye sebule yake ndogo ulikuwa unavunjwa. Mtu akishaingia sebuleni ni rahisi kuvunja mlango wa chumba chake ambao ulikuwa si imara sana.
Mkewe naye alikuwa keshashtuka na kukaa juu ya kitanda. Mara wakasikia mlio wa risasi huko nje. Wakaingiwa uoga zaidi.
"Tupige kelele mume wangu, tumevamiwa," akanong'ona Zuhura karibu na sikio la Walari huku akitetemeka kwa uoga.
Walari alilipuka kwa makelele lakini sekunde ileile mlango wa chumba chao ulikuwa unavunjwa.
Walari na mkewe waliendelea kupiga makelele ya kuomba msaada ambayo inaonekana yalipokelewa vyema kwani kwa mbali walisikia kama milango ya nyumba za majirani nazo zikifunguliwa.
Ghafla mlio wa risasi ukasikika chumbani mwao, na Walari kama umeme akaruka na kulala chini huku akimvuta mkewe.
Mkewe naye alimfuata chini. Risasi ambazo sasa waligundua kwamba zilikuwa zinatokea dirishani zikaanza kumiminika mle chumbani uelekeo wa kitanda chao. Baada ya risasi kusikika, vurugu za kuvunja mlango wao zikakoma lakini bunduki ya dirishani ikaendelea kufyatua risasi mle chumbani kuelekea kwenye kitanda chao ambacho hakikuwa na mtu wakati huo na nyingine zikigonga ukuta.
Mtoto wao alipiga makelele pale kitandani na Zuhura akataka kunyanyuka ili amchukuwe na kulala naye pale chini, lakini Walari akamvuta mkono ili asinyanyuke. Hata hivyo, mwanamke yule akafanya nguvu na kufanikiwa kumponyoka na kunyanyuka.
Sekunde chache baada ya mkewe kunyanyuka, Walari alisikia mlio wa risasi kutoka dirishani na muda huo huo akasikia mkewe anapiga makelele ya kuomba msaada.
Mkewe na mtoto walimwangukia pale chini. Akamsikia mkewe akiugulia kwa maumivu, mwanaye pia, akiwa pale chini alikuwa akiangua kilio kikali.
Risasi ambazo nyingi zilikuwa zikipiga kitandani au kugonga ukuta zilikoma.
Mkewe aliendelea kuugulia kwa maumivu pale chini, pembeni mwa kitanda na yule mtoto sauti ilikuwa imemkauka kwa kulia.
Yeye Walari alikuwa anajiamini kwamba bado yuko salama lakini alikuwa na mashaka na mkewe pamoja na mwanae.
Alipata hali ngumu aliposikia mkewe ananyamaza kimya pamoja na mtoto, muda mfupi baada ya kusikia mlio mwingine wa risasi.
Alihisi mkewe na mwanae wamekufa, akatamani ajitokeze naye auawae.
Aliona hakuna haja ya yeye kusalimika kama mkewe na mtoto watakuwa wameuawa.
Kwa mbali alisikia vishindo vya watu wanaokimbia. Zilipita dakika kama tatu hivi bila kusikia mlio mwingine wa risasi wala kishindo chochote, iwe mle chumbani au nje ya dirisha ambako alihisi majambazi hao walikuweko zaidi ya mmoja.
Alinyanyuka, sasa akiwa tayari kukabiliana na kifo kwani aliamini mkewe na mtoto wameshakufa.
"Niueni nyiye watu. Kwa nini mniulie familia yangu? Kama mngetaka kila changu ningewapa. Si mngechukuwa TV na chochote mnachotaka kuliko kuniulia familia yangu," alisema kwa ukali akinyanyuka na kusimama pembeni mwa mwili wa mke wake katika chumba hicho kilichokuwa giza.
Alisikiliza kidogo na kugundua kwamba hali ilikuwa shwari na bila shaka majambazi hao walikuwa wameshakimbia. Alishangaa kwamba hadi muda huo kulikuwa hakuna jirani yeyote aliyejitokeza.
Walari aliwasha taa ya chumbani baada ya hali ya ukimya kuendelea kutawala. Aligundua kwamba mlango wa chumbani kwake ulikuwa umevunjwa, lakini kulikuwa hakuna dalili kwamba majambazi yale yaliingia chumbani mwake. Akahisi kuwa makelele yao yalisadia wasiingie chumbani na ndipo wakaamua kufyatua risasi kupitia dirishani.
Aliangalia chini na kumuona mkewe akiwa amelala katikati ya dimbwi la damu.
Mwanae mpendwa, Ashraf, naye alikuwa kalala katika dimbwi jingine la damu.
Wakati akijongea kuangalia hali zao, majirani sasa ndipo walikuwa wamepata ujasiri wa kufika nyumbani kwake.
Baadhi walisimama dirishani na wengi wakaingia ndani na kumkuta Walari akiwa kainama pembeni mwa mkewe. Alimgusa na kugundua kwamba alikuwa kazirai lakini bado mzima.
Alimshika pia mwanae kifuani na kugundua kwamba hata yeye alikuwa kapoteza fahamu tu.
Walari aliomba msaada wa haraka. Wale majirani wakafanya haraka kumsaidia na baaada ya dakika chache, gari ikaletwa na majeruhi hao wakakimbizwa hospitali. Gari hiyo ilikuwa ya jirani yao mmoja aliyeonekana kuwa tajiri mkubwa pale mtaani kwao uswahilini.
Walari akiwa na majirani watatu, mmoja akiwa mpangaji mwenzake, ndani ya gari hilo pamoja na dereva, walikumbuka kwamba kule hospitali wasingepata tiba yoyote kama wasingepitia polisi kwanza kuandika maelezo na kupewa hati maalumu ya kwenda nayo hospitali.
"Jamani, mimi ninajua utaratibu ndiyo huo, lakini hamuoni tutawapoteza hawa watu kama tutapoteza muda kwenda huko?" Akashauri Walari akitaka waende hospitali kwanza ambako wangejitahidi kuwashawishi madaktari na wauguzi hadi waelewe hali ilivyo na kutibu majeruhi wao.
"Tiba kwanza, mambo ya polisi baadaye," akawa anasisitiza mwandishi huyo wa habari aliyekuwa na mashaka makubwa juu ya hali ya mkewe na mtoto.
Hata hivyo, majirani wale waling'ang'ania kwamba itakuwa ni kazi bure kwenda hospitali kama hawana hati ya polisi kwani isingelikuwa rahisi wao kupokelewa na kupewa tiba.
Walari hatimaye alisalimu amri baada ya kuona hata dereva aliyekuwa akiendesha gari hilo akisisitiza kwamba, kwa tukio kama hilo, ilikuwa ni kupoteza muda na kuharibu bure mafuta kwenda hospitali bila kupitia polisi kwanza.
Saa nane kasorobo, usiku, Walari na wale wasamaria wema walikuwa wanawasili katika kituo kidogo cha polisi. Kwa eneo hilo, kituo hicho ndicho kilionekana kuwa karibu, japo ilikuwa mbali kidogo kutoka kwa Walari na bila shaka hata milio ya zile risasi ilikuwa ni vigumu kusikia na kama zilisikika basi ni kwa mbali sana.
Pale kituoni walimkuta askari mmoja tu akiandika maelezo ya watu walioaminika kuwa wazururaji ambao baadaye akina Walari waliambiwa kwamba walikamatwa na askari waliokuwa doria, askari ambao baada ya kuwakamata watu hao na kuwaleta kituoni walirudi tena na kumuacha huyo mwenzao mmoja kituoni.
Walishangaa sana kugundua hilo na wakajiuliza kama wale walioko doria hawakusikia milio ya risasi, pengine wangekurupusha majambazi yaliyokuwa yamemvamia Walari. Yule askari wa kituoni naye alijibu kwamba hajasikia mlio wowote wa risasi na akajibu kwamba inaonekana askari waliokuwa doria usiku huo walipita njia tofauti.
Walari na wenzake walimweleza askari yule kuhusu wagonjwa waliokuwa nao mle kwenye gari, lakini askari huyo asiye na cheo, aliyeonakana hana haraka, akawataka wasubiri.
Huku wao wakiwa wamesimama nyuma ya kaunta fupi ya kituo hicho kidogo, askari yule aliendelea kuwahoji wale watuhumiwa wa uzembe na uzururaji taratibu sana huku akiendelea kuandika maelezo ya watuhumiwa hao waliokuwa wameketi sakafuni.
Kila mtu alimshangaa askari huyo kwa kutoonekana kujali taarifa kwamba kikundi kile cha watu kilikuwa na wagonjwa mahututi. Ikabidi tena Walari amjie juu, tena kwa sauti ya hasira.
"Ndugu askari. Tumekwambia tuna wagonjwa mahututi, vipi?"
"Kama mngekuwa na haraka mngekuja jana. First in, first out. Nyiye si mmewakuta hawa, subirini. Kama mgonjwa ni wa kufa atakufa tu."

Itaendelea...
Pole walari na familia yako
 
Dah ni zaidi ya hatari
Gereza la Kifo - 22

Mtunzi - HAMISI KIBARI

ILIPOISHIA

Walari na wenzake walimweleza askari yule kuhusu wagonjwa waliokuwa nao mle kwenye gari, lakini askari huyo asiye na cheo, aliyeonakana hana haraka, akawataka wasubiri.
Huku wao wakiwa wamesimama nyuma ya kaunta fupi ya kituo hicho kidogo, askari yule aliendelea kuwahoji wale watuhumiwa wa uzembe na uzururaji taratibu sana huku akiendelea kuandika maelezo ya watuhumiwa hao waliokuwa wameketi sakafuni.
Kila mtu alimshangaa askari huyo kwa kutoonekana kujali taarifa kwamba kikundi kile cha watu kilikuwa na wagonjwa mahututi. Ikabidi tena Walari amjie juu, tena kwa sauti ya hasira.
"Ndugu askari. Tumekwambia tuna wagonjwa mahututi, vipi?"
"Kama mngekuwa na haraka mngekuja jana. First in, first out. Nyiye si mmewakuta hawa, subirini. Kama mgonjwa ni wa kufa atakufa tu."

Endelea...

"Jamani tuachane na huyu mtu, twen'zetuni Central (Kituo cha polisi cha kati)" alishauri dereva wa gari walilokuwa nalo.
Walirudi kwenye gari, Mama Ashraf bado alikuwa hajitambui, lakini sasa damu zilikuwa zimekoma kumvuja sehemu ya jeraha baada ya kumpa huduma ya kwanza.
Lakini yule mtoto alikuwa ana fahamu zake, isipokuwa alikuwa analia muda wote kutokana na maumivu.
Walipofika kwenye kituo cha polisi Kati, ambako Walari alienda kwa shingo upande baada ya wenziye kumkatalia tena nia yake ya kwenda moja kwa moja hospitali, walisikilizwa haraka na kupatiwa huduma.
Baadaye wakaondoka kasi kuwahi hospitali ya mkoa. Huko nako, baada ya kuwasili, iliwachukuwa zaidi ya dakika 20 kabla wagonjwa hao hawajaanza kuhudumiwa.
Wakati mkewe anaanza kuhudumiwa wodini ilikuwa ni saa kumi na ushee usiku, zaidi ya masaa mawili toka mwanamke huyo apigwe risasi.
Walari alikuwa na mashaka makubwa kama mkewe atasalimika kifo kwani hata wakati wauguzi wanampokea pale mapokezi walionesha hali ya kukata tamaa. Iligundulika kwamba mkewe alikuwa amepigwa risasi kiunoni na alikuwa ametokwa damu nyingi sana. Kitu kingine kilichomsikitisha Walari ni maelezo kwamba hata kama akipona, kiuno kinaweza kisifanye kazi au miguu kupooza na hivyo akawa ni mtu wa kukaa muda wote mithili ya kiwete.
Daktari aliyewapokea alisema ilitakiwa mwanamke huyo aongezewe damu haraka, lakini benki ya damu ya hospitali hiyo ilikuwa haina hata tone.
Walari na wale majirani wawili pamoja na dereva walijitolea kutoa damu.
"Hata hivyo, itachukuwa muda kumwekea mgonjwa wenu damu. Si mnajua siku hizi damu haziaminiki? Mpaka zichunguzwe sana," akasema daktari huyo baada ya Walari kuona muda unakwenda bila mkewe kuwekewa damu. Wakati huo ilikuwa inaelekea saa 12 alfajiri.
Mtoto Ashraf yeye alikuwa amepata jeraha kwenye bega, kwa kile kilichoonekana kwamba alikwaruzwa na risasi. Tayari mtoto huyo alikuwa ameshashughulikiwa kwa kusafishwa jeraha na kuwekewa dawa na sasa alikuwa kalala chumba cha mapumziko akiwa ametundukiwa dripu ya maji.
Wasiwasi ulizidi kumwandama Walari kuhusu hali ya mkewe. Hata hivyo, daktari aliyekuwa akimhudumia aliwaambia warudi nyumbani na kuja kuangalia hali ya mgonjwa baadaye.
"Mbona kumeshakucha, tuje asubuhi gani tena?" Akauliza Walari akiangalia saa yake.
Lakini jirani mmoja akamkumbusha kwamba walitakiwa kuondoka kwenda polisi kituo cha Kikuu kuwachukua askari kwenda eneo la tukio mapema.
Wakiwa njiani kurudi polisi, pamoja na mtoto Ashraf ambaye alikuwa kalala, jirani mmoja alisema kwamba wakati majambazi yale yanavunja mlango wao walisikia na hadi akina Walari walipokuwa wanapiga makelele wao walikuwa nje na silaha zao duni, lakini waliogopa baada ya kugundua kwamba majambazi hayo yalikuwa mengi pamoja na bunduki zaidi ya moja.
"Sisi tulianza kuja lakini wakafyatua risasi kuelekea upande wetu, ikabidi tukimbie. Walikuwa kama majambazi sita hivi," akasema jirani mmoja, mtu wa makamo, ambaye nyumba yake inapakana na ile aliyopanga Walari.
Mfanyabiashara aliyepanga nyumba moja na Walari yeye alisema kwamba inaonekana majambazi yale yalimpania Walari peke yake, kwani yalipofika yalifunga mlango wa chumba chake na wa sebule yake kwa nje na hilo aliligundua wakati alipojaribu kufungua akidhani labda nyumba iliyokuwa inavunjwa ni ya jirani.
Alisema alipong'amua kwamba majambazi yale yako kwenye nyumba yao, hasa baada ya kusikia milio ya risasi, akalazimika yeye na mkewe kujificha nyuma ya kabati chumbani mwao.
"Hata chumba cha watoto nako walikuwa wamefungiwa kwa nje," alisema mpangaji mwenzake huyo, Ibrahim Nyamsha, ambaye katika nyumba hiyo yenye wapangaji wawili, alikuwa na vyumba viwili na sebule. Akasema baada ya hali kuwa shwari majirani waliofika kwenye tukio ndio waliowafungulia mlango uliokuwa umefungwa kwa nje kwa komeo.
"Kuna haja ya kuweka vitasa vya kisasa ambavyo haviruhusu mtu kukufungia kwa nje," akasema Nyamsha.
Nyamsha ndiye aliyekuwa na sebule kubwa na vitu vingi na mtu yeyote angefikiria kwamba kutokana na kuwa na vitu vingi, angekuwa kivutio kikubwa cha majambazi kumvamia kulinganisha na Walari.
Walifika kituoni na kuondoka na askari wawili hadi nyumbani kwa Walari kufanya uchunguzi wa tukio hilo.
Walipofika nyumbani, majirani kadhaa walikuja asubuhi hiyo, na ndipo mmoja akasema alifanikiwa kumchoma mkuki jambazi mmoja, ingawa ana hakika hakumuua. Hata hivyo akasema nusura na yeye apigwe kwa risasi lakini hawakufanikiwa kumuona na kilichosadia zaidi ni kwamba walikuwa wanakimbia kutoka katika eneo la tukio na mkuki huo ulisaidia kuwakimbiza zaidi kwenye gari lao.
"Mimi nilikuwa nimejibanza mahala na mkuki wangu na wao wakati wanakimbia kurukia kwenye gari aina ya pick-up waliokuwa wameiegesha uchochoroni, mimi nilikuwa nimejificha kwenye banda moja na ndipo nikampiga mkuki mgongoni mmoja wao aliyekuwa mwisho," akasema jirani yule.
Jirani huyo, ambaye alizoeleka kwa jina la Mzee Matata, jina ambalo Walari hajui lilitokana na nini kwani si jina lake halisi, akasema baadaye ule mkuki aliukuta katika eneo la tukio lakini ana hakika ulimpata huyo mtu kwani yeye na watu wengine walishuhudia asubuhi hiyo damu nyingi katika eneo hilo na mkuki wenyewe ulikuwa na damu pia. Akasema inaonyesha mkuki ulimwingia jambazi huyo kiasi cha nchi nne hivi.
"Sijui kaumia kiasi gani na ana bahati mkuki hauna sumu. Ningemuua yule," akasema na kuongeza kuwa ana hakika mtu huyo kama hakumpiga sehemu mbaya inayoweza kusababisha kifo chake basi lazima atapelekwa hospitali kutibiwa na hivyo kuwepo na urahisi wa kumkamata.
"Tatizo nilikuwa mbali kidogo. Kama ningekuwa karibu yule mtu lazima angekwenda chini na asingenyanyuka hata kama mkuki hauna sumu," akasema mzee huyo ambaye zamani alikuwa mwindaji wa kutumia zana za jadi.
Askari waliokuwa wakisikiliza maelezo ya mzee huyo kabla ya kufanya upekuzi ndani ya nyumba ya Walari, waliahidi kufanyia kazi maelezo ya Mzee Matata.
Askari walifanya uchunguzi huku wakimhoji maswali haya na yale Walari pamoja na yule mpangaji mwenziye, wakagundua kwamba hakuna kitu kilichoibiwa mule ndani zaidi ya kamera yake aliyokuwa ameiacha sebuleni juu ya meza wakati anaingia kulala.
Karibu vitu vyote vya maana, kama vile redio kubwa, televisheni na deck vilikuwa mahala pake. Walari pia alishukuru kwamba vifaa vyake vilivyo na habari kuhusu gereza, kama vile mikanda aliyorekodi na kitabu kidogo alichokuwa amenakili majina ya wafungwa waliokufa kwa kipindi cha miezi sita, vilikuwa salama.
Hisia zilianza kujengeka kwamba majambazi yale bila shaka hayakuwa na lengo la wizi, bali kufanya hujuma, na hasa kuua mtu, na bila shaka yalidhamiria kumuua yeye Walari.
Sababu za kutuhumu namna hiyo zilikuwa nyingi kwa polisi waliofanya uchunguzi. Na hata majirani pamoja na Walari mwenyewe alituhumu hivyo.
Moja, ilikuwa hali hiyo ya majambazi yaliyosadikika kuja kwa gari, kuondoka bila kuchukua kitu chochote cha maana zaidi ya ile kamera ambayo ilionekana kwamba pengine watu wale waliichukuwa kama kudanganyia tu au walitaka asitumie tena kifaa hicho, kama siyo kuhisi kwamba kulikuwa na picha wasizopenda zichapishwe gazetini.
Sababu nyingine ni majambazi hayo kulenga zaidi risasi zao kitandani ambako inaonekana yaliamini Walari alikuwapo na kwa vile chumba kilikuwa giza, bila shaka yalikuwa yamefanya utafiti na kugundua mahala kitanda kinapokaa chumbani kwake.
Sababu nyingine ilikuwa ni kumvamia Walari ambaye hakuwa na mali nyingi kulinganisha na mpangaji mwenzake ambaye alikuwa na vitu vingi vya thamani na bila shaka alikuwa hakosi akiba ya kutosha chumbani mwake kulinganisha na Walari.
Akiwa anaelekea kumaliza ujenzi wa nyumba yake si mbali sana na Gereza Kuu la Magamaga mpangaji mwenza huyo wa Walari alikuwa anamiliki duka kubwa la vipodozi stendi na vitu vingi vyenye thamani sebuleni kwake kama redio kubwa na televisheni kubwa bapa ya kisasa.
Mara kadhaa mpangaji huyo alikuwa hafungui muziki kwa sauti kubwa kwa hofu ya kuvutia wezi, hasa kwa kuzingatia kuwa nyumba hiyo ya kizamani waliokuwa wakiishi haikuwa imara sana kwenye milango na madirisha na wala haikuwa na ua.
Pia mpangaji huyo alikuwa na vitu vingi vya kisasa kama vile mafriji, majiko ya gesi, mitambo ya umeme ya kufulia nguo, kompyuta mbili mpakato, yake na ya mkewe na kadhalika.
Walari, katika kusaka mtu anayeweza kuhusika katika tukio hilo, kama si majambazi, moja kwa moja alielekeza tuhuma zake kwa Masunju kwa vile aliahidi kupambana naye.
Alikumbuka maneno aliyoyasema Masunju siku alipomvamia ofisini kwake: "Lakini pamoja na hayo lazima pia nikuonye kitu kimoja. Kama utakataa hii offer yangu na kuendelea na mpango wako utakuwa hutaki urafiki nami, badala yake utakuwa umetangaza vita na mimi. Kwa hali hiyo lazima nami nitajihami na hapo tutalazimika kupimana ubavu. Tafadhali usiseme hivi ni vitisho bali ni ukweli mtupu.... Najua kuna watu wanakutumia ili uniharibie jina kwa malengo yao. Mimi nina maadui wengi sana wasiotaka maendeleo yangu, lakini pia nina marafiki wengi ambao najua watanisaidia kama utaamua kuendelea na vita dhidi yangu."

Itaendelea...

Sent using Jamii Forums mobile app
 
Gereza la Kifo - 23

Mtunzi - HAMISI KIBARI

ILIPOISHIA

Walari, katika kusaka mtu anayeweza kuhusika katika tukio hilo, kama si majambazi, moja kwa moja alielekeza tuhuma zake kwa Masunju kwa vile aliahidi kupambana naye.
Alikumbuka maneno aliyoyasema Masunju siku alipomvamia ofisini kwake: "Lakini pamoja na hayo lazima pia nikuonye kitu kimoja. Kama utakataa hii offer yangu na kuendelea na mpango wako utakuwa hutaki urafiki nami, badala yake utakuwa umetangaza vita na mimi. Kwa hali hiyo lazima nami nitajihami na hapo tutalazimika kupimana ubavu. Tafadhali usiseme hivi ni vitisho bali ni ukweli mtupu.... Najua kuna watu wanakutumia ili uniharibie jina kwa malengo yao. Mimi nina maadui wengi sana wasiotaka maendeleo yangu, lakini pia nina marafiki wengi ambao najua watanisaidia kama utaamua kuendelea na vita dhidi yangu."

Endelea...

Walari sasa aliona ile ni vita aliyoahidi Masunju na bila shaka alikuwa amedhamiria kumuua yeye baada ya kusikia kwamba amehamia kikazi katika Shirika la Utangazi la Uingereza, EBC.
Kwa mujibu wa maelezo ya Masunju alipomtembelea ofisini kwake, kuna waandishi wa habari ambao hakumtajia majina waliokuwa wakimpa habari zake kama vile kwamba alikuwa bado akiishi kwenye nyumba ya kupanga, ana mtoto mmoja na kadhalika ambao sasa Walari alihisi watakuwa ndio wamemwambia kwamba ameajiriwa na EBC kwani ni jambo ambalo halikuwa siri miongoni mwa waandishi wa mji wa Bulibuli.
Mwandishi huyo sasa akahisi kwamba watu waliomvamia usiku, walikuwa wamekodishwa na mkuu huyo wa gereza ili wamuue, alipona kwa kudra za Mwenyezi Mungu.
Wale polisi waliokuja kufanya uchunguzi wa tukio hilo la kijambazi kabla hawajaondoka na Walari kwenda tena kituoni kuandika maelezo zaidi walimuuliza kama kuna watu kawadhulumu au kuwa na uhasama nao.
"Tuna matukio mengi ya aina hii ambayo watu hufanya tukio la ujambazi lakini lengo ni kuua mtu. Mara nyingi sababu huwa ni kudhulumiana," akatoa ufafanuzi askari mmoja.
Walari akamgeukia askari huyo: "Sijadhulumu mtu yeyote na sina uhasama na mtu yeyote zaidi ya mmoja tu."
"Wewe si umesema ni mwandishi wa habari, siyo?" Akauliza askari mwingine, "Hebu kumbuka watu wote ambao umeshawaandika katika habari ambazo zimewaudhi kwa kiasi kikubwa."
"Sina uhasama na mtu yeyote isipokuwa mmoja tu ambaye muda wote nahisi ndiye kanifanyia kitendo hiki kiovu," akasema Walari na kumtaja Masunju kwamba ndiye mtuhumiwa wake namba moja.
"Huyu mtu ni kwamba aliahidi kabisa kunifanyia kitendo kibaya kama nisingeacha kufanya uchunguzi wa hali mbaya za wafungwa katika gereza lake."
Walari aliendelea kueleza kuhusu vitisho vya ofisa huyo wa magereza ambavyo alivirekodi. Akasema kwa bahati mkanda aliyotumia kumrekodi Masunju akimtolea vitisho uko salama.
"Aliwahi kunishikia bastola ofisini kwake... Naamini huyu ni Masunju na alidhamiria kuniua mimi," akadai Walari.
Wale askari walimwambia atunze vizuri vielelezo alivyo navyo kama ushahidi na kisha wakasema wangeishughulikia ipasavyo kesi hiyo baadaye.
Pia waliahidi kuanza kumsaka mtu ambaye anaweza kuwa kaenda hospitali baada ya kupigwa mkuki kwani ingeweza kuwa chanzo cha kuwafahamu wahusika.
Asubuhi, baada ya saa chache toka aachane na askari, Walari alikwenda tena hospitalini kuona maendeleo ya mkewe na kumwacha mwanae Ashraf, kwa mpangaji mwenziye.
Alipowasili hospitalini asubuhi hiyo, pale nje alikutana na yule mtu wa chumba cha maiti, Nyamagwila na kuanza kumsemesha.
"Rafiki yangu, toka umepata majina yako ya wafungwa (wanaokufa gerezani) hutaki hata kupita na kujulia hali... Siku wakikuleta mortuary ukiwa umenuna (utakapokufa) nami nitakununia," akasema mtu huyo mwenye kupenda utani.
Baadaye, Walari ambaye alikuwa anaona kama rafiki yake huyo anamchuria bure, alijilazimisha kumchangamkia kisha akaagana naye na kwenda wodini.
Huko mwandishi huyo alijulishwa kwamba mkewe alikuwa na ahueni kidogo lakini alikuwa na tatizo jingine kubwa zaidi ambalo lingeweza kuhatarisha maisha yake.
Daktari alimjulisha kwamba, ingawa mkewe alikuwa na mimba ya miezi saba na ushee tu, lakini, pengine kutokana na tukio la kupigwa risasi alikuwa amefikwa na uchungu wa kuzaa.
Ataingia theatre (chumba cha upasuaji) saa tatu asubuhi hii na damu zaidi itatakiwa. Kwa hiyo unatakiwa kutafuta watu haraka wa kuchangia damu," akasema yule daktari na kuongeza kwamba muda huo alikuwa ametolewa kwenye chumba cha kipimo kiitwacho ultra sound.
"Sawa, dokta, nitakwenda sasa hivi kusaka watu. Lakini kama sikukusikia vibaya umesema mgonjwa sasa hivi angalau hali yake ni nzuri, anaongea?"
"Anajitahidi kuongea, lakini anajisikia vibaya. Ana jeraha la risasi ambayo mpaka sasa haijatolewa mwilini na anasikia uchungu wa kuzaa. Hata hivyo, nimemuona ni mwanamke mvumilivu sana."
"Dokta, naweza kuzungumza naye kidogo kabla sijaenda kutafuta watu wa damu?"
"Ruksa kuongea naye," akajibu yule Daktari. Walari aliingia wodini na kujongea kitanda alichokuwa kalazwa mkewe huku akiwa katundukiwa drip. Alikuwa akigugumia kwa maumivu makali pale kitandani.
Walari alisimama pembeni mwa kitanda akimwangalia mkewe kwa huruma huku machozi yakimlenga lenga. Zuhura, labda kutokana na maumivu, alikuwa hajamtambua Walari licha ya kufumbua macho mara mbili kumwangalia na kuyafumba tena.
Walari aliinama kwenye kitanda chake na kumuuliza hali yake.
"Baba Ashraf," aliita kwa sauti ya mbali," hali yangu ni mbaya. Sijui kama nitapona."
"Usiondoe matumaini mke wangu, Mungu atakujaalia."
"Nashukuru uko hai mpenzi, nilidhani umekufa baada ya zile risasi. Madaktari ndiyo wameniambia kwamba mlinileta usiku. Mwanangu anaendeleaje?"
"Yeye anaendelea vizuri tu."
"Haya majambazi yameiba nini?"
"Wamechukuwa kamera tu."
"Mume wangu, kweli haya ni majambazi au ni watu aliowatuma mkuu wa gereza. Mbona napata hizo hisia?" Akauliza yule mwanamke.
Walari alibaki kimya kwa sekunde kadhaa kisha akamjibu mkewe kwamba hata yeye anahisi kwamba shambulio lile linaweza kuwa limeandaliwa na Masunju.
"Nahisi Masunju alikodi majambazi au hata yeye mwenyewe alikuwepo. Dhamira yao nadhani ilikuwa kuniua mimi. Hisia zinanituma hivyo."
"Unaona mume wangu, kila siku tulikwambia ukubaliane na matakwa ya huyu mtu. Ni mtu mbaya. Unaona sasa. Ubishi wako utatuletea maafa."
"Usiseme hivyo mke wangu. Huyu mtu lazima nitamfikisha kwenye vyombo vya sheria. Atakuwa ni yeye tu."
"Mume wangu, chonde nakusihi, achana naye na acha kabisa kumfuatilia. Humuwezi. Atatumaliza. Huyu ni mtu mbaya sana. Hata mimi nikifa, chukua ushauri wangu huu, baba Ashraf," akasema mwanamke huyo kwa sauti inayoonyesha kwamba alikuwa anajikakamua tu lakini alikuwa katika maumivu makali.
Walari aligeuka nyuma na kumwona daktari akiwa kasimama pembeni mwake.
"Bwana mzee. Ungefanya haraka kusaka watu wa kumuongezea huyu mkeo damu. Nadhani hilo ndilo jambo la msingi zaidi," akasema yule daktari.
Aliinama na kumpiga busu mkewe ambaye alikuwa bado akigalagala kwa maumivu pamoja na uchungu wa kujifungua pale kitandani.
Mwandishi huyo wa habari alimwangalia tena kwa huruma mkewe akawa anasikia uchungu na hasira nyingi huku machozi yakilowanisha shati lake. Aligeuka na kutoka nje ya wodi hiyo ya wazazi alikokuwa kahamishiwa mkewe huku akifuta machozi kwa kitambaa alichokichomoa toka kwenye mfuko wa suruali.
Pale nje ya wodi, Walari alikutana na rafiki yake, Nurdin, ambaye baada ya kuambiwa kwamba rafiki yake kavamiwa na majambazi alikwenda nyumbani kwa mwandishi huyo ambako alisimuliwa mengi kuhusu tukio hilo na yule mpangaji mwenzie na ndipo akaja haraka hospitalini hapo.
Marafiki hao wawili walisimama pembeni, Walari akamsimulia tena namna alivyovamiwa na hadi kinachotakiwa sasa, yaani damu zaidi na tena haraka ili mkewe afanyiwe operesheni.
"Mimi nilivyosimuliwa nikapata hisia kwamba hivi vita ni vya Masunju. Kwa asilimia 90 ninaamini ni yeye," akasema Nurdin.
"Hata mimi ninamtuhumu yeye kwa asilimia nyingi na n'najua alidhamiria kuniua mimi. Niko tayari aniue tu lakini sirudi nyuma. Mimi nikiogopa kwa kweli nitakuwa ninaikosea sana taaluma hii muhimu (ya uandishi wa habari)," akasema Walari akionesha ana haraka ya kuondoka. Pia alimjulisha kwamba kuna mtu mmoja alipigwa mkuki na jirani yake kwa hiyo anataka kumsaka katika hospitali hiyo ili kufahamu kama mtu huyo atakuwa kalazwa.
"Sasa unaelekea wapi, mbona unaonekana una haraka?" Akauliza Nurdin.
"Wewe ninakuomba unisubiri hapa kwa sababu damu yako inahitajika sana. Mimi ninakwenda kutoa taarifa hii kwa waandishi wa habari wenzangu na kuwaomba waje wamchangie damu shemeji yao. Wao pamoja na wewe ninawategemea sana. Huyo mtuhumiwa nitamsaka baadaye, lakini nahisi hata polisi wanamsaka," akajibu Walari.
"Ninapenda sana kutoa damu hata dakika hii, lakini si unajua tena siku hizi damu zetu haziaminiki? Na kusema kweli naogopa sana kupima. Majibu yakionyesha kwamba ninao (Ukimwi), si nitakufa kihoro?"
"Kwanza ninakusahihisha. Kwa vile ninakuona una afya njema, ukipima, kinachoweza kuonekana ni virusi na sio Ukimwi. Ukimwi ni ugonjwa ambao humpata mtu aliyeambukizwa virusi baada ya kupita muda. Lakini ninachojua mimi ukitoa damu, kama itakuwa chafu, ni siri ya hao waliokupima, nawe au mtu mwingine hatojua chochote, labda kama wewe mwenyewe utataka uambiwe. Na hata kukwambia, kama utapenda kujua, kama mambo si mazuri, hawakurupuki tu, mpaka wakuandae kisaikolojia kupokea majibu hayo. Hilo litafuatiwa na kukupa ushauri nasaha. Nurdin kupima afya yako ni jambo jema sana rafiki yangu."

Itaendelea...
 
Gereza la Kifo - 24

Mtunzi - HAMISI KIBARI

ILIPOISHIA

"Ninapenda sana kutoa damu hata dakika hii, lakini si unajua tena siku hizi damu zetu haziaminiki? Na kusema kweli naogopa sana kupima. Majibu yakionyesha kwamba ninao (Ukimwi), si nitakufa kihoro?"
"Kwanza ninakusahihisha. Kwa vile ninakuona una afya njema, ukipima, kinachoweza kuonekana ni virusi na sio Ukimwi. Ukimwi ni ugonjwa ambao humpata mtu aliyeambukizwa virusi baada ya kupita muda. Lakini ninachojua mimi ukitoa damu, kama itakuwa chafu, ni siri ya hao waliokupima, nawe au mtu mwingine hatojua chochote, labda kama wewe mwenyewe utataka uambiwe. Na hata kukwambia, kama utapenda kujua, kama mambo si mazuri, hawakurupuki tu, mpaka wakuandae kisaikolojia kupokea majibu hayo. Hilo litafuatiwa na kukupa ushauri nasaha. Nurdin kupima afya yako ni jambo jema sana rafiki yangu."

Endelea...

"Wewe ulishapima? Mbona wayajua haya!"
"Ninapima kila mara. Hata hivi mimi na mke wangu kwa sababu ya ujauzito tulishajipanga tena kupima. Inshallah, akipona janga hili tutapima, ingawa itakuwa kama ushahidi tu kwani wote tunajiamini tuko fiti. Ninamwamini mke wangu kwa kuheshimu ndoa na mimi ninajiamini pia."
Walari aliondoka akimwacha Nurdin akienda kutoa damu.
Ilikuwa asubuhi hiyo atume habari ya gereza EBC lakini badala yake alipofika kwenye ofisi yake mpya, mwandishi mwenziye ambaye ilikuwa ahamie makao makuu ya nchi muda wowote, alilazimika kumhoji na kutuma habari kuhusu kuvamiwa na majambazi. Hata hivyo, Walari katika mahojiano na mwandishi huyo wa EBC aliepuka kumtaja Masunju kama mtuhumiwa namba moja kwa sababu bado hakuwa na ushahidi wowote, na isitoshe alikuwa bado anafuatilia vipengele fulani katika habari yake kuhusu gereza.

******************************

Saa tisa na nusu mchana, madaktari waliokuwa wakimfanyia upasuaji Zuhura walitoka chumba cha upasuaji, huku Walari, Nurdin na waandishi wenziye watatu pamoja na mpangaji mwenzake wakiwa pale nje ya chumba hicho.
Madaktari hao wakiwa na nyuso za huzuni hawakusema chochote, isipokuwa dakika ileile Walari akaona wauguzi wakipita haraka wakimsukuma mkewe kwenye kitanda cha matairi kuelekea chumba cha wagonjwa mahututi.
Hali ile ilimshtua sana Walari na wenzake aliokuwa nao. Alimfuata daktari mmoja na kutaka kujua maendeleo ya mkewe.
"Bado tunamtibu lakini tumeshamfanyia operesheni na tayari mtoto, kwa vile hajatimiza miezi yake, keshapelekwa kwenye chumba maalumu. Lakini mkeo hali yake ni mbaya sana na ndio hivi unaona tuko katika kujaribu kuokoa maisha yake. Mapigo yake ya moyo hayaendi vizuri."
"Kajifungua mtoto gani?"
"Ni mtoto wa kike. Mtoto anaonekana hana matatizo yoyote," alijibu daktari yule.
Baadaye Walari alielekea kwenye chumba cha mapokezi kuulizia kama kuna mtu alikuwa kalazwa katika hospitali hiyo baada ya kutobolewa na kitu chenye ncha kali kama vile mkuki.
Huko aliambiwa kwamba kulikuwa hakuna mtu kama huyo, na kisha akaonyeshwa kitabu cha orodha ya watu waliolazwa katika siku hizo.
Yule mtu wa mapokezi pia alimwambia kwamba kulikuwa na askari wawili ambao pia walikuja kuulizia mtu wa aina hiyo lakini hawakumpata.
"Nimesikia wanasema kuwa wanaelekea kwenye hospitali za watu binafsi labda akawa kalazwa huko," akajibu mtu yule wa mapokezi.

****************************

Saa 12:15 Asubuhi, Walari akiwa amembeba mwanaye, Ashraf, alikuwa anawasili katika hospitali ya Bulibuli.
Kwa siku tatu mfululizo hali ya mkewe ilikuwa bado mbaya. Licha ya jeraha la risasi na jeraha la mshono, matatizo ya moyo yalikuwa yakimsumbua sana na mara kadhaa alikuwa akipoteza fahamu.
Kutokana na hali hiyo, Walari alikuwa ameshindwa kufanya kazi na karibu muda wote alikuwa anashinda hospitali au polisi.
Baada ya kuomba ulinzi polisi akidai kwamba anahofia maisha yake, polisi walikuwa wamempuuza na hivyo Nurdin akawa amemshauri ahamie kwake kwa njia ya kificho, isijulikane analala wapi, kwani walihisi kwamba kama shambulio lile lilikuwa la 'kigaidi' na si ujambazi, basi wahusika wangeweza kuwa wanatafakari kumvamia tena Walari kwa lengo la kumuua. Hata safari zake za kwenda hospitali alikuwa akizifanya kwa uangalifu mkubwa. Alikuwa akivaa miwani ya jua na kofia pana.
Katika siku hizo tatu, Walari alianza kugundua kitu kingine. Polisi walionekana hawafuatilii chochote na wala walikuwa hawataki kumhoji Masunju ambaye Walari alimtaja kama mtuhumiwa namba moja.
Polisi sasa walibadili msimamo. Wakawa wanadai kwamba tukio lile wanaliona kama la ujambazi tu, na hivyo kulikuwa hakuna maelezo yoyote ya maana ya kuwafanya polisi wafikie hatua ya kumhoji ofisa wa juu wa serikali, kama Mkuu wa Gereza kwa tuhuma za eti kumfanyia ujambazi mwandishi huyo wa habari.
Polisi walimwambia kwamba kama angekuwa ana uthibitisho wowote, kama vile Masunju kudondosha kitambulisho chake cha kazi katika eneo la tukio, pengine wangefikiria kumhoji lakini hakuwa na ushahidi wa aina hiyo.
Wakamweleza kuwa hawawezi kufanya kazi kwa hisia ama kuridhisha tu matakwa yake.
Alipowaambia kuwa ana ushahidi wa maneno aliyomrekodi ofisa huyo wa magereza, polisi wale wakacheka wakasema huo hautoshi kuthibitisha kwamba yeye Masunju atakuwa kamkodia majambazi na kwamba anaweza kuiga sauti yake na kuirekodi.
Pia walimjibu kwamba hawajasikia mtu yeyote aliyelazwa hospitalini kwa kupigwa mkuki. Lakini Walari aligundua kuwa polisi walikuwa hawajazungukia mahospitali ya binafsi kama walivyoahidi siku walipokwenda hospital ya mkoa.
Wauguzi wawili walimkaribisha mwandishi huyo ambaye asubuhi hiyo hakuwa ameandamana na rafiki yake Nurdin isipokuwa shemejiye, yaani mke wa Nurdin, ambaye alikuwa kabeba kifungua kinywa kwa ajili ya mgonjwa wao.
"Leo mgonjwa wako kalala na hali mbaya zaidi," akasema muuguzi mmoja baada ya Walari kuwasili pale wodini.
"Usiku wa leo kwa kweli hakulala na pengine asubuhi hii tutamrudisha kule kwenye wodi ya wagonjwa mahututi ambako ataungwa kwenye vifaa vya kumsaidia kupumua."
Taarifa hizo za muuguzi alizisikia kama zinachoma maini yake kama upanga. Jana yake alikuwa ameona matumaini ya mkewe kupona yanarejea baada ya kuonekana ana hali njema na akiongea kidogo, tofauti na siku za nyuma, hali iliyosababisha atolewe kwenye wodi ya wagonjwa mahututi na kuletwa ile ya kawaida.
Walari alikwenda kwenye kitanda cha mkewe na kumkuta akigugumia kwa maumivu. "Nakufa. Nakufa... Nakufa bila kumbeba mwanangu mchanga," akawa analalamika mwanamke huyo Walari akiwa kainama pale kitandani.
Mwandishi huyo wa habari, akiwa na mwanae Ashraf pembeni, alimshika mkewe kifuani kisha akamwita kwa sauti ya chini.
Mkewe ambaye alikuwa akionekana mwenye maumivu makali alifumbua macho na kumtazama mumewe.
"Mume wangu, sidhani kama nitapona... Nasikia vibaya sana. Ninakuomba uwaangalie watoto. Naomba sana uchague mwanamke mwingine wa kuoa ambaye atajali watoto wetu. Usikurupuke kuoa mwanamke atakayetesa watoto. Usiache ibada. Usiache kuniombea kila unaposwali," akasema mwanamke yule kwa taabu.
"Usiseme hivyo, Zuhura, Inshallah Mwenyezi Mungu atakunusuru na kifo," alisema Walari akiwa bado kamwinamia mkewe na kuomba dua pamoja na kumsomea mkewe Qur’an ili Mwenyezi Mungu Mlezi amfanyie wepesi. Pembeni mwake akiwa kasimama mke wa Nurdin, maarufu kama mama Hadija, sasa akiwa ametua chini ule mzigo wake wa kifungua kinywa aliokuja nao kwa ajili ya mgonjwa huyo.
Zuhura alitaka kuongea kitu lakini akashindwa. Jasho likawa linamtoka kwa wingi kwenye paji la uso.
Alinyoosha mkono kwa taabu na hatimaye akafanikiwa kusema, "mwanangu Ashraf, sogea nikuage...."
Alimshika kichwani mtoto huyo ambaye alikuwa amesogea karibu na kitanda cha mama yake. Akataka kuongea maneno mengine lakini akashindwa. Akafanikiwa kusema maneno ya Kiarabu Laa ila ha-illallah (hakuna apaswaye kuabudiwa kwa haki ila Mwenyezi Mungu mmoja) Akashtuka kidogo na mara mkono wake ukalegea ukiwa bado juu ya kichwa cha mwanae.
Walari alimshika kifuani. Moyo ulikuwa umesimama kusukuma damu kuashiria kwamba uhai ulikuwa umemtoka mwanamke huyo mswalihina. Tena kifo hicho kilikuwa kimempata siku chache kabla hajaanza kufunga mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhani.
Walari hakutaka aamini kwamba Zuhura alikuwa ameshindwa kupambana na kifo. Aliamini kwamba muda wowote Mwenyezi Mungu anaweza kufanya maajabu yake mkewe akarudishiwa uhai wake.
Mwandishi huyo alibaki ameduwaa akitazama mwili wa mkewe pale juu ya kitanda huku mkono wake ukiwa bado umenyooka juu ya kichwa cha mtoto wao Ashraf.
Alijaribu kumwita. Mwanamke yule hakuitika. Akamwita huku akimtikisa lakini mwanamke yule hakuitika.
"Mpenzi Zuhura, usife tafadhali... Zuhura usife," akawa anasema Walari akiutingisha mwili wa mkewe pale kitandani. Lakini Zuhura, akiwa kama aliyelala usingizi hakuitika wala kutikisika.
Walari akaanza kulia kwa sauti. Yule mke wa Nurdin (Mama Hadija) alishajua kwamba Zuhura amekata roho. Alijua pia kwamba shemeji yake keshachanganyikiwa na haamini tukio lile lililotokea mbele yake.

Itaendelea...
 
Back
Top Bottom