Gereza la Kifo - 13
Mtunzi - HAMISI KIBARI
ILIPOISHIA
"Kwa hiyo, mimi mke wangu sijabadili dini. Nilijaribu kuchunguza utaratibu wa viongozi wetu wa Kiislamu nikagundua kwamba utaratibu wao usingeniwezesha kukutana na hadi kuongea na wafungwa ana kwa ana."
Akamwambia mkewe kwamba kwa vile shule ya sekondari aliyosoma ilikuwa inamilikiwa na kanisa, ilimsaidia kufahamu mambo mengi kuhusu dini ya Kikristu na ndiyo maana hakupata taabu alipoingia kanisani na kwenda sambamba na waumini wengine.
"Shuleni kwetu, japo kila mtu alikuwa na dini yake na anaruhusiwa kuabudu siku yake ikifika, lakini ilikuwa lazima pia kuingia kanisani. Nilipoamua kwenda kanisani nilijifunza harakaharaka sana na kwa bidii. Nikamvutia sana Mchungaji Kabongo na ndiyo maana amekuwa akinitafuta akitaka nirudi kanisani, lakini hataniona tena. Kilichonipeleka huko kimeisha," akasema.
Endelea...
Zuhura alifurahi sana kusikia habari zile, lakini akamlaumu mumewe kwa kumficha ukweli.
"Umeniweka roho juu sana katika kipindi chote hiki. Ulipaswa kuniambia. Kwa kweli sasa nilikuwa napania niende kwenye baraza la dini kujadili hatma ya ndoa yetu baada ya kuona wazazi wako ambao niliwaandikia barua toka majuzi wakiwa hawatokei."
Walari alimjulisha mkewe kwamba sehemu ya kwanza ya habari hiyo alikuwa aitume siku hiyo lakini mkuu wa gereza alikuja ofisini kwake na kumchanganya.
"Sasa nitaituma kesho na itakuwa bado imewahi," akasema.
Alimsimulia kuhusu ahadi za mkuu wa gereza na namna anavyomshangaa kwa kujaribu kumhonga ili aachane na habari hiyo.
"Huyo ofisa wa magereza mjinga sana. Yaani anaamini kuwa atatumia umaskini wangu kuniziba mdomo nisiueleze umma maovu yake. Kesho nitakwenda kumbwagia ofisini kwake hati yake ya kiwanja ambayo nimeshairudufisha, halafu nitatuma habari yangu kama kawaida. Jumamosi gazeti litakapotoka hataamini macho yake," akasema Walari na kumsimulia mkewe ahadi zote za Masunju ikiwa ni pamoja na kumpeleka mtoto wao kusoma nje ya nchi, kuanzia masomo ya chekechea na kuendelea.
Muda wote mkewe alikaa kimya akimsikiliza na Walari akaendelea: "Tena huyu ofisa atajiona mjinga sana kwa sababu mazungumzo yote tuliyofanya naye, pale aliponitisha kule ofisini kwake na ofisini kwangu wakati anabembeleza kunipa rushwa yote nimerekodi. Hana ujanja hata siku moja na hakuwa anajua kabisa kwamba nimemrekodi," akasema na kutoa kimtambo chake kidogo cha kunasia sauti mfukoni na kumfungulia sehemu kidogo mkewe, mahala anakosikika ofisa huyo akimwahidi kumjengea nyumba na kusomesha mtoto wao.
"Japo ushahidi wa kurekodi sauti wakati mwingine unakataliwa, lakini kulingana na mazingira ya tukio lenyewe ninaamini utanisaidia baadaye kumkomesha huyu mshenzi."
Baadaye, mwanamke huyo aliyekuwa kimya muda wote akisikiliza, alimgeukia mumewe na kumwambia kwamba maneno yake yanazidi kumshangaza na kumuumiza roho badala ya kumfurahisha kama pale mwanzo alipomwambia kuwa hajabadili dini.
"Mume wangu, kwanza nashukuru kwamba kumbe hajabadili dini na ninakupongeza kwa hatua uliofikia katika kufuatilia suala hili la wafungwa, lakini msimamo wako sikubaliani nao kabisa, na tena ninakushangaa sana."
"Msimamo gani huo na unanishangaa kwa kitu gani?"
"Yaani unaona hali zetu wenyewe zilivyo. Nyumba wala kiwanja hapa mjini hatuna, leo unapata bahati, mtu anakupa hati ya kiwanja kilichopimwa na serikali halafu unataka kupoteza bahati hii! Labda kama umechomwa sindano ya ujinga."
"Mimi nilidhani ninavyokuona ukisali dini imekuingia, kumbe sivyo? Unasema hatuna kiwanja na kile cha kijijini kwetu ni kitu gani?"
"Kiwanja cha kijijini utalinganisha na cha hapa mjini wewe?" Akahoji na kumgeukia tena. "Hivi una maana gani kusema ninasali lakini dini haijaniingia?"
"Kwani hujui kwamba suala hili la kupewa kiwanja, kujengewa nyumba pamoja na ahadi zingine za huyu dhalimu ni rushwa? Licha ya ukweli kwamba rushwa si kitu kizuri kabisa, lakini hata wewe unajua kwamba dini yetu inakataza kabisa kupokea na kutoa rushwa!"
"Sikiliza mume wangu, Mwenyezi Mungu anaweza kukushushia kipato kwa njia ambayo hukutegemea na ukiikataa akakususa hadi ukafa hivyohivyo. Mimi naona Mungu kakushushia kipato kupitia kwa huyu ofisa wa magereza na wale watu waliokuja kukwambia ufuatilie suala hili waliongozwa na Mungu kukuonyesha kitu cha kufanya ili kikusaidie katika maisha yako."
"Bado sikuelewi kabisa, mke wangu. Yaani unamsingizia Mwenyezi Mungu katika kutenda uovu?"
"Mimi naona ulichofanya mpaka sasa kinatosha. Huyo mkuu wa gereza sasa ataogopa kuendelea na maovu kwa sababu waandishi wapo wengi ambao watafuatilia suala hili. Halafu, nchi hii rushwa imekita mizizi kila mahala. Wewe mtu mdogo utaweza kuikomesha?” alisema huku Walari akimtazama kwa mshangao.
Akaendelea: “Usilaze damu mume wangu. Chukua kiwanja tujengewe nyumba, tutakaa nyumba za kupanga, tena za kizamani kama hii hadi lini? Ona tunaanza kuwa na watoto," akasema mwanamke huyo ambaye alikuwa na ujauzito wa pili.
"Hivi itakuwa na maana gani kweli, sisi kufaidika na hii rushwa wakati jamii inateketea kwa ufisadi unaofanywa na mkuu wa gereza? Utalala kwenye nyumba inayopatikana kwa rushwa huku ukijua fika kwamba binadamu wenzako wanakufa kila siku gerezani? Ina raha gani nyumba hiyo?”
Walari akaendelea kusema: “Hivi kweli mke wangu unashindwa kujua kwamba kama ni utajiri atatupa Mwenyezi Mungu na umaskini ni makadirio yake pia. Mke wangu unashindwa kukumbuka kwamba hapa dunia tunaishi muda mfupi sana na muda mwingi tutakuwa kaburini na kisha kufufuliwa kwa maisha ya milele? Huko tutamwambia nini Mwenyezi Mungu mlezi?"
Walari aliendelea kumkatalia mkewe na kusisitiza kwamba kulikuwa hakuna cha kumzuia kuendelea na mpango wake wa kufichua hali mbaya ya gereza la Magamaga kupitia vyombo vya habari.
Mwanamke huyo naye hakuonekana kuchoka kumshawishi mumewe: "Wewe mwenyewe huwa unasema jamii nzima imeoza. Sasa hiyo habari yako si utaishia kuandika tu na watu kusoma lakini hakuna kitachofanyika! Namaanisha watu wataiacha kama ilivyo. Utakuwa umefaidika nini?"
"Lakini unasahau kwamba mimi ni mwandishi wa habari. Kazi ya mwandishi ni kuripoti tu. Suala la kufuatilia au habari hiyo kusaidia marekebisho muhimu katika jamii ni jingine. Nikishafichua kinachoendelea gerezani, kazi yangu, kama mwandishi, itakuwa imekamilika."
"Halafu utapata nini, sifa? Kwanza nina wasiwasi utajitumbukiza katika majanga na matatizo tu. Kama mkuu wa gereza anaweza kuahidi kukupa vitu vikubwa namna hiyo, anajua ni habari mbaya kwake, kwa hiyo ukiitoa utakuwa hasimu wake mkubwa."
"Sasa hayo mke wangu ni matusi. Lini uliona nafanya kazi kwa kutaka sifa? Mimi naheshimika sana, pengine kuliko mwandishi yeyote hapa Bulibuli kutokana tu na kuheshimu kazi yangu.
Huwezi mtu kuuza utu na heshima yako kirahisi namna hii. Nimeshasema, Mwenyezi Mungu Mlezi akikupangia kupata nyumba utapata na akikupangia kukosa hupati ng'o, hata kama utapokea rushwa na rushwa."
"Hiyo heshima unayopata mbona haijakuletea nyumba?" Zuhura akazidi kuhoji.
Walari akamjibu kwamba watu wenye tabia kama ya mkuu wa gereza, akishakupa rushwa nawe ukaipokea, anaanza kukuendesha anavyotaka.
"Atakudharau, kisha atakuendesha kadri anavyotaka. Leo atakwambia andika wafungwa wa gereza la Bulibuli wamefurahia huduma muhimu wanazopata kutoka kwa maofisa wao wakati hakuna kitu kama hicho na kesho atakwambia kitu kingine. Mfano hai ni mwandishi mwenzetu hapa Bulibuli jinsi anavyowashangaza wafanyakazi wa kiwanda cha Matunda.
Amekuwa akiandika mambo ya uongo kutukuza uongozi wa kiwanda hicho wakati ukweli ni kinyume chake. Majuzi wafanyakazi wamegoma kwenda kazini ili kuulazimisha uongozi wao dhalimu kuweka mazingira bora zaidi ya kazi lakini yeye anaandika kwamba wafanyakazi wote wamesusia mgomo ulioitishwa na chama cha wafanyakazi cha tawi, na eti shughuli ziliendelea kiwandani hapo kama kawaida.
Majuzi nusura wafanyakazi wampige kwa kuandika uongo. Kila anakopita anazomewa. Unataka kunifikisha huko?" Akauliza Walari.
Wanandoa hao waliendelea kubishana hadi usiku wa manane.
Katika ubishi huo, Zuhura aliendelea kumtaka mumewe kuacha msimamo wake huo ili apate vitu alivyoviita vyenye manufaa kutoka kwa mkuu wa gereza pamoja na mtoto wao kuwa na uhakika wa kusoma shule yenye ubora wa kimataifa. Lakini Walari akasema hata mbingu zikipasuka na jua kwenda kinyume hawezi kuacha kufichua uoza katika gereza kuu la Bulibuli.
Licha ya pale mwanzo mwanamke huyo kufarijika kusikia mumewe hajabadili dini, sasa alinuna, tena hasira zilimjaa kooni akimshangaa mumewe kukataa kitu ambacho aliamini kingerahisisha maisha kwa kile alichoamini ni tabia ya mumewe kutaka sifa kwamba yeye ni mwandishi mahiri.
Hata pale Walari alipomweleza mkewe kwamba kinachofanywa na mkuu wa gereza ni unyama mkubwa sawa na unaofanya na wale watu wa Manispaa wenye jukumu la kuzika maiti wasio na ndugu, mkewe aliendelea kutomuunga mkono.
Waliamua kulala huku kila mmoja akiwa kanuna kutokana na kushangaa msimamo wa mwenziye. Walari usingizi haukuja, akaamka na kuandika hili shari ambalo alipania pia kulichapisha kwenye gazeti.
Aliniambia babu, binadamu sawa duma
Ni kitu ustaarabu, kinachompa huruma
Kinamtenga na dubu, akawa mwenye heshima
Binadamu ni mnyama, akiniambia babu.
Anapokivua hima, atatisha kwa unyama
Hutokwa chembe ya wema, kwa wanziye wanadama
Hovyo atawasukuma, bila roho kumuuma
Binadamu ni mnyama, akiniambia babu.
Binadanamu kwa asili, ni mchoyo heri kima
Anapoiona mali, inamtoka hekima
Atamuua Jamali, ili apate neema
Binadamu ni mnyama, akiniambia babu.
Babu akanisaili, niihofu jahanama
Niishi kwa maadili, nimpendeze Karima
Sikuelewa kauli, utoto ulinizama
Binadamu ni mnyama, akiniambia babu.
Mwanadamu ni hatari, leo nami ninasema
Anapenda ufahari, wenzake awale nyama
Ni chanzo cha kukuthiri, maafa katika umma
Binadamu ni mnyama, akiniambia babu.
Wasio hofu na Mungu, viongozi wenye dhima
Husababisha machungu, jamii kwenda mrama
Kila mali kwake yangu, hawakihofu Kiama
Binadamu ni mnyama, akiniambia babu.
Pesa ndio iko mbele, utu sasa umekoma
Mwenye haki tupa kule, muovu huitwa mwema
Mimi napiga kelele, sintokubali dhuluma
Binadamu ni mnyama, akiniambia babu.
Walari alirudia kusoma shauri aliloandika akilighani kwa sauti ya chini na kujisikia faraja kidogo. Akapanda kitandani na sasa alipata usingizi.
Itaendelea...