Riwaya - Balaa

Riwaya - Balaa

SIMULIZI; BALAA
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA AROBAINI NA NANE

Dokta Yusha alichoka, alikaa chini ili kusubiri kukiona kifo cha njaa jinsi kinavyokuwa.

Saa kumi kamili alfajiri ilimkuta Dokta Yusha akiwa macho. Alikuwa hajasinzia hata kidogo, muda wote alikuwa anafikiria namna ya kutoka katika chumba kile lakini hakupata namna ya kutoka.
Mara, alisikia tena kelele za mlango kwa nje, ishara kama ya mwanzo kuwa mlango ulikuwa unafunguliwa.

'Ama zake, ama zangu!'

Aliingia tena Sita, akiwa kashika bunduki aina ya SMG mkononi. Alisimama pale mlangoni na kumwangalia Dokta Yusha. Sita wa Six killers alikuwa ameenda kuhakikisha tu kama Dokta Yusha hajafanya ujanja wowote wa kujaribu kutaka kutoroka. Sita alimshuhudia Dokta Yusha akiwa amekaa palepale alipomwacha awali. Akadanganyika kwamba Dokta Yusha hajafanya kitu chochote kile cha kujaribu kutoroka.
Alijidanganya. Dokta Yusha alitafuta sana njia ya kutoka mle ndani lakini hakuipata.
Sita aligeuka nyuma ili arudi nje kuendelea na lindo lake.
Kwa kasi ya haraka Dokta Yusha alinyanyuka pale chini na kupiga hatua mbili kubwa sana, hatua zilizomfikisha mpaka pale mlangoni. Alipokuwa Sita wa Six killers.
Wakati Sita anataka kugeuka nyuma kujua sababu ya vishindo viwili alivyovisikia, alichelewa sana!
Alikuwa kakabwa vizuri sana na Dokta Yusha. Kabali maridadi iliyomtetemesha Sita na kuidondosha bunduki chini.
Dokta Yusha hakujari, alimvuta Sita kwa nyuma kwa nguvu. Mwanzoni Sita alijikomaza lakini baadae Ilibidi ajilegeze, maana kukomaa ilimaanisha kuumizwa zaidi na ile kabali.
Kujilegeza nako lilikuwa kosa kubwa sana alilolifanya Sita. Kosa ambalo atalijutia mpaka kesho, kama kuna maisha baada ya kilichomtokea pale. Dokta Yusha alimvuta Sita kwa nguvu na kujikuta akimsukumia pale katika kiti cha kifo!
Balaa!
Sita alibadirika naye, mwili ulibadirika sambamba na kiti, Ilikuwa ni rangi nyekundu mithili ya tanuru la moto!

ITAENDELEA KESHO MUNGU AKIPENDA.
 
SIMULIZI; BALAA
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA AROBAINI NA TISA

'Auae kwa upanga siku zote huuwawa kwa upanga'

Iko hivyo, na wahenga walishasema zamani sana. Sita wa Six killers alikufa aina ya kifo sawa na aliyokufa yule askari. Na watu wengine wengi waliouwawa na kiti kile cha kifo!

Sasa Dokta Yusha alikuwa huru tena lakini katika jumba hatari sana. Jumba ambalo hakuwa anajua linalindwa na walinzi wangapi, jumba ambalo hakujua ni aina gani ya ulinzi wanaoutimia. Ni mbwa ama binadamu?

'Bora nife kwa bastola, bora nife kishujaa, kuliko kufa kwa njaa!"

Dokta Yusha aliiokota ile bunduki iliyokuwa inatumiwa na Sita, SMG ambayo dokta Yusha alikuwa anajua kuitumia. Alifunzwa Kiwira Mbeya, katika Chuo cha Magereza, na alishawahi kuitumia mara kadhaa huko Mtwara, alikoajiriwa.

Dokta Yusha alipiga hatua za taratibu kuelekea nje ya chumba kile. Chumba alichoambiwa ndio kaburi lake. Kwa maana hiyo Dokta Yusha sasa alikuwa anatoka katika kaburi lake!

Nje kulikuwa na giza, ingawa si kubwa sana kama la mle ndani. Nje angalau kulikuwa na mbalamwezi, mbalamwezi ambayo ilimuwezesha kuona Dokta Yusha. Kwa mwendo wa kunyata Dokta Yusha alikuwa anatambaa na ukuta wa kile chumba kuelekea upande wa mashariki, upande ambao lilikuwepo geti kubwa jeusi la nyumba ile. Aliishika imara ile bunduki iliyomdondoka Sita, tayari kupiga endapo atasikia ukelele wowote ule utakaotokea mbele yake. Dokta Yusha alikuwa tayari kwa lolote.
Tayari kuuwa!
Tayari kuuwawa!

Aliambaa na ule ukuta wa bluu hadi akaumaliza, sasa ilimbidi apite sehemu ya wazi ili kulifikia geti. Sehemu hatari zaidi, sehemu ambayo ni rahisi sana kudunguliwa na risasi! Maana hakukuwa na kizuizi chochote. Alikwenda kwa haraka, kwa kusaidiwa na giza, au tunaweza sema kwa kudra za Mwenyezi Mungu, alilifikia geti. Dokta Yusha aliangalia pembeni ya geti, alimwona mlinzi, mlinzi ambaye alikuwa amelala huku akitoa sauti mbaya ya kukoroma. Mlinzi mzembe sana akiyelinda nyumba hatari sana! Dokta Yusha alimsogelea yule mlinzi taratibu akijua kwa vyovyote funguo ya geti atakuwa nayo yeye.

Alimfikia.

Kwa kutumia mkono wake wa kulia alimpiga karate moja ya nguvu katika chembe, mlinzi hakuweza kustahamili uzito wa karate ile, alikufa usingizini. Alimpekua haraka haraka yule mlinzi, alikipata alichokitaka...funguo. Dokta Yusha sasa alikuwa anafungua geti la kutoka nje ya nyumba ile hatari, nyumba ambayo hakuna mateka aliyewahi kutoka hai baada ya kuingia mle.....


ITAENDELEA KESHO MUNGU AKIPENDA
 
SIMULIZI; BALAA
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA HAMSINI

Dokta yusha alifungua geti na kutokomea msituni akiwa na bunduki yake.
Wakati Dokta Yusha, akitoroka kule kambini msituni. Kundi la Six killers walikuwa njiani wakirejea kambini kwao. Walikuwa wanatoka Kilwa Masoko mjini, walikoenda kufanya starehe zao. Wote walikuwa wamelewa ndani ya gari huku wanaimba nyimbo zisizoeleweka. Walikuwa na furaha sana baada ya kuona mipango yao inaenda kama ilivyopangwa, pia waliweza kumkamata mtu ambaye alikuwa anawasumbua sana, Dokta Yusha.

'Laiti wangejua'

*****

Katika hospitali ya wilaya Kilwa Kivinje hali ya wagonjwa ilikuwa mbaya sana. Kulikuwa hakuna huduma kabisa kwa wagonjwa wa hospitali hiyo. Madaktari waliokuwa wanaaminiwa sana kwa kutoa huduma nzuri sasa walikuwa wamebadirika. Walidharau sana wagonjwa, hawakuwajari kabisa. Malalamiko mengi yalipelekwa katika uongozi wa wilaya, lakini malalamiko hayo hayakubadirisha kitu. Madaktari hawa sasa walikuwa na pesa nyingi sana, pesa za kumuhonga mtu yeyote yule atakayeonesha kutaka kuwaingilia au kukwamisha mipango yao.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Kilwa alikuwa kimya, mkuu wa wilaya ya Kilwa alikuwa kimya, na mbunge pia alikuwa kimya, ingawa walipelekewa malalamiko mara kwa mara huku hali za wagonjwa waliolazwa hospitali zikiendelea kuwa mbaya!

Upande wa hali za Nasra, Hasina nazo zilikuwa taabani. Nasra alikuwa anapumulia mashine katika hospitali ile iliyokuwa na huduma dhaifu sana kwa sasa, Nasra alikuwa amehamishwa wodi na kupelekwa katika chumba cha wagonjwa mahututi, ICU, hali yake ilikuwa mbaya sana. Huku Hasina na Mzee Mpaukha wakiwa bado wanapigania maisha katika wodi ileile aliowaacha Dokta Yusha.

Mwili wa marehemu dereva Musa ulikuwa ushatolewa katika ile wodi na kupelekwa machinjioni. Katika chumba cha kuhifadhia maiti ambako ndipo kundi la Six killers walikuwa wanafanyia shughuli zao...

ITAENDELEA KESHO MUNGU AKIPENDA
 
SIMULIZI; BALAA
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA HAMSINI NA MOJA

Kutoonekana kwa Dokta Yusha siku nzima, ilizua hofu kwa ndugu zake. Dokta Yusha alitafutwa ule usiku hakupatikana, na kwa bahati mbaya zaidi alikuwa hapatikani kwa simu yake.

Hali ilikuwa ngumu sana kwa familia zote mbili. Familia ya Mzee Mpaukha na familia ya Mzee Yusuph, baba yake na Dokta Yusha. Dokta Yusha alikuwa anahitajika sana wakati ule, alikuwa mtu muhimu sana, licha ya kutaka kujua usalama wake mwenyewe, lakini pia alihitajika sana kuwahudumia wagonjwa wa pale hospitali, hasa kumuhudumia mkewe Nasra na rafiki wa mkewe Hasina. Ambao walikuwa na hali mbaya kupita kiasi.
Walitafuta sana.
Lakini Hawakumuona!

*****

Usiku huo Kundi la Six killers nd'o walikuwa wanarudi kambini kwao, huko porini Ngome. Walishuka katika gari yao huku wakiwa na furaha kubwa sana. Furaha iliyotokana na pombe, furaha iliyotokana na mipango yao kwenda sawa.
Taa za gari yao zilipomulika geti wote walipigwa na butwaa!
Geti lilikuwa wazi, walipoingia ndani moja kwa moja bila kusemeshana walienda katika chumba cha mateka wao. Walimsahau hata mlinzi pale mlangoni.
Mateka hakuwepo!
Cha kushangaza hata Sita waliyemuacha kwa ajili ya kumlinda Dokta Yusha nae hakuwepo. Walirudi tena getini, walimkuta mlinzi amelala, walipomgusa ili kumuamsha, mlinzi alidondoka chini moja kwa moja...

ITAENDELEA JIONI MUNGU AKIPENDA
 
Umesuuza moyo wangu haswaaa Leo sina kinyongo nina furaha tele hadi pale utakapobandika muendelezo tena. Ubarikiwe sanaa
 
SIMULIZI; BALAA
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA HAMSINI NA MBILI

Macho yaliwatoka vibaya sana!
Dokta Yusha alikuwa kawaweza sana, ilikuwa haijawahi tokea hata siku moja kutoka mtu salama katika nyumba ile. Ilikuwa ni mwiko, ilikuwa ni dhambi kubwa sana kutoka katika nyumba ile ukiwa hai! Ile nyumba ilikuwa ni zaidi ya kaburi, kile kiti kilikuwa ni mithili ya Israel mtoa roho. Nyumba ile ilikuwa imeondoka na roho za watu wengi sana. Roho za watu mbalimbali wasio na hatia, roho za askari wengi, roho za wapelelezi wengi, roho za viongozi na watu wa kawaida. Kile kiti kilikuwa kimewageuza rangi watu wengi sana. Kutoka rangi yao halisi, kuwapeleka rangi nyekundu kisha nyeusi tii, kisha kutoa harufu kali sana. Kile kiti hakikuwahi kukosea.

"Natoa nusu saa, Dokta Yusha awe mbele yangu hapa, hapana siyo Dokta Yusha, natoa nusu saa ninaitaka maiti ya Dokta Yusha. Akija mzima hapa nitamfanya kitu kibaya sana, naona bora mniletee maiti tu" Don Genge aliunguruma kwa hasira. Dokta Yusha sasa aligeuka mwiba. Mwiba mkali sana!
Vijana wa Six killers, ambao sasa walibaki wanne tu. Tano alikuwa anauguza goti lake, na Sita alikuwa hajulikani alipo mpaka sasa. Moyo wa Don Genge ulikuwa unafukuta moto, alikuwa na hasira isiyomithilika katika moyo wake. Ni kweli, Dokta Yusha angepelekwa hai pale, ingekuwa balaa!

Walipotoka nje kundi la Six killers walijigawa. Wakati Moja na Nne wakielekea upande wa mashariki wa pori lile, Moja na Tatu walielekea upande wa magharibi. Kumsaka Dokta Yusha.
Ilikuwa ni msake mpaka umpate!

ITAENDELEA MUNGU AKIPENDA
 
Tupe ingine leo hatutoki kwetu kuna mvua nyingi
 
SIMULIZI; BALAA
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA HAMSINI NA TATU

Wakati kundi la Six killers likijigawa kumsaka Dokta Yusha kwa kwenda upande wa mashariki na magharibi. Dokta Yusha alikuwa mbali kidogo na ile kambi ya wale makatiri. Ilikuwa ni porini sana, Dokta Yusha alikuwa anasonga mbele akiwa hajui anaelekea wapi. Hadi sasa alikuwa hajui msitu ule upo sehemu gani nchini Tanzania. Alikuwa anaenda mbele tu ili kukiepuka kifo. Na bunduki yake mikononi.

Saa kumi na mbili asubuhi ilimkuta Dokta Yusha akiwa katika ufukwe mwanana wa bahari ya hindi. Ufukwe ambao hakuwahi kufika wala kuuona hapo kabla.

Moja na Nne, waliokuwa wanakuja huu upande wa mashariki, upande sahihi alioelekea Dokta Yusha. Huu upande kulikuwa na ufukwe wa bahari ya hindi ambao watu wengi ndani ya Kilwa walikuwa hawaufahamu.
Moja na Nne nao walifika katika ule ufukwe. Ingawa ilikuwa mbali na pale alipotokea Dokta Yusha. Jamaa wakaanza kutembea ufukweni kumsaka Dokta Yusha.
Dokta Yusha alikuwa amechoka sana, alikuwa anatembea taratibu ufukweni huku akiangalia nyuma mara kwa mara. Ufukwe ulikuwa mrefu sana, kiasi kwamba ni ngumu kumuona mtu aliye mbele yako.

Kundi la six killers walipewa nusu saa kupeleka maiti ya Dokta Yusha, sasa ni masaa mawili hawakuwa na maiti ya Dokta Yusha wala Dokta Yusha mwenyewe.
Mara kwa mara Don Genge alikuwa anawapigia simu watu wake, lakini jibu lilikuwa lilelile, hawakumuona Dokta Yusha. Mwishowe Don Genge aliwaambia watu wake warudi kambini, ili waende kujipanga upya. Hiyo ndio ilikuwa nusra ya Dokta Yusha kukamatwa kule ufukweni...

ITAENDELEA MUNGU AKIPENDA
 
SIMULIZI; BALAA
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA HAMSINI NA NNE

Dokta Yusha aliendelea kuufata ule ufukwe. Bila kujua ufukwe ule utamfikisha wapi?
Lakini aliufata.

Kambini kundi la Six killers walikutana. Kilikuwa ni kikao tofauti na vikao vyote walivyowahi kufanya. Kikao hiki kilitawaliwa na hasira, hofu na chuki!

Wote walikuwa na hasira sawa kwenda kwa Dokta Yusha, wote walikuwa na hofu ya kukamatwa na Polisi, maana yake walikuwa wanaamini Dokta Yusha alishaijua mahali ilipokuwa kambi yao, wote walikuwa na chuki, walikuwa wanamchukia sana Dokta Yusha, ni yeye ndiye aliyeingilia kati mipango yao ambayo ingewawezesha kupata hela nyingi sana. Hela ambazo zingewawezesha kuwa matajiri milele.

"Mambo yamebadirika haraka sana, sisi tulipanga hivi lakini mambo yanaenda vile. Sasa tumefikia katika hali mbaya sana, mipango yetu inaenda mramba, ndio...mipango yetu inaenda songombingo. Kidudu kidogo sana kinawasumbua. Kumbukeni nyinyi ni nusu makomando, mnashindwaje kumkamata mtu ambaye hajapita kozi yoyote. Tano, Sita nimewapoteza ilhali yule nyang'au hana hata jeraha letu. Yaani Tano anapambana na kale jamaa na kukishindwa, hizo ni dharau, dharau kubwa sana. Natoa oda mpya sasa, ukimuona Dokta Yusha popote pale muuwe kwanza kisha nd'o umuhoji. Hatutakiwi kufanya mchezo kabisa! Kumtafuta Dokta Yusha kwende sambamba na kutoa mioyo kule hospitali. Leo usiku tumepanga na Dokta Sharifa tuwatoe mioyo wale majaamaa zake, ili imuumize, tukimuuwa mkewe na kumtoa moyo lazima atajitokeza, hapo ndipo tutamuuwa kirahisi" Don Genge alitoa hotuba ndefu huku kila mtu alikubali kwa kutingisha kichwa. Six killers walikuwa wanataka kupiga pigo la mwisho!

ITAENDELEA MUNGU AKIPENDA
 
SIMULIZI; BALAA
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA HAMSINI NA TANO

Baada ya maelezo hayo kila mmoja aliingia ndani kupumzika. Six killers walikuwa wamechoka sana. Wote pombe zilikuwa zimewaisha kichwani mwao. Ama hakika Six killers walikuwa wamepatikana, na kupata pigo kubwa sana, baada ya wapiganaji wao wawili kukutana na mkono wa Dokta Yusha!

Wakati vijana wanne wa Six killers wakiwa wameenda kupumzika, Don Genge yeye hakwenda kupumzika kabisa. Yeye ndiye alikuwa mkuu wa misheni hii. Na ilimpasa kupeleka ripoti kwa wakuu wake, na sio ripoti tu, wakuu walikuwa wanataka ripoti nzuri ya kueleweka toka kwa Don Genge. Don Genge atapumzika vipi wakati hakuwa na ripoti ya kueleweka hadi sasa? Pamoja na kupata idadi ya mioyo waliyoagizwa lakini Tano alikuwa mgonjwa, Sita alikuwa kapotea, adui yao namba moja duniani, Dokta Yusha alifanikiwa kuwatoroka. Ni ripoti mbaya zaidi tangu Don Genge apewe kazi hii.
Hakika hakupaswa kupumzika, na hakupumzika kweli!

Don Genge alienda sebuleni, aliwasha kompyuta yake na kuanza kuikagua, kila kitu kilikuwa sawa. Alifungua kabati kubwa lililopo pale sebuleni, namo kila kitu kilikuwa sawa. Don Genge akajua kwamba Dokta Yusha hakuwa ameingia mle ndani. Alirudi kwenye sofa kubwa lililopo pale sebuleni, alikaa kwa mtindo wa kujitupia sofani. Alianza kuwaza mustakabali wa kisanga kile kilichokuwa kinawaendea mrama sasa.

*****

Dokta Yusha aliendelea kuufuata ule ufukwe, cha ajabu ule ufukwe uliomfikisha katika kijiji cha Mpara, kijiji ambacho kipo ndani ya Kilwa. Alipofika hapo kijijini ndipo aligundua kumbe bado yupo ndani ya Kilwa. Porini Mpara Dokta Yusha alichimba shimo refu na kuifukia ile bunduki, huku akiweka alama kwa juu asiisahau sehemu ile. Alivyomaliza akaendelea kutembea na pori. Hakutaka kabisa kupita barabarani akiuhofia usalama wake. Lakini alitoka kule porini na kuikaribia vipori vidogo vilivyokuwa karibu na barabara kuu ya lami. Alivyogundua kama yupo Mpara, nia na madhumuni yake ni kwenda hospitali ya Kilwa Kivinje kwa miguu!
Ilikuwa ni safari ngumu lakini na ndefu lakini ilikuwa ni lazima aende Kilwa Kivinje, alihisi hatari kubwa sana kumuacha mke wake na ndugu zake wengine katika hospitali ya wilaya Kilwa...

ITAENDELEA MUNGU AKIPENDA
 
SIMULIZI; BALAA
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA HAMSINI NA SITA

Kweli Dokta Yusha alitembea kwa miguu, ilikuwa safari ngumu sana, lakini hakukuwa na namna nyingine. Ilikuwa ni lazima atembee.
Alipofika hospitali ya Kivinje breki yake ya kwanza ilikuwa ni wodi aliyowaacha kina Nasra. Alipofika mlangoni tu na kuangalia katika kitanda alipokuwa amelazwa mkewe, Nasra.
Alipingwa na butwaa!
Kitanda cha Nasra kilikuwa tupu. Hakukuwa na mtu. Akiwa kasimama palepale mlangoni chozi la uchungu liligusa sakafu ya hospitali. Dokta Yusha alikuwa analia. Kutumuona Nasra pale kitandani alijua kuna mawili, kama mkewe kipenzi hajafariki na kuhamishiwa katika chumba cha kuhifadhia maiti basi kundi lile la wanaharamu itakuwa wamemteka. Lakini Dokta Yusha yote hayo mawili hakutaka kabisa yatokee. Alikuwa anampenda sana Nasra, na alikuwa anatamani sana kumuona Nasra anakuwa na siha njema kama zamani.

Dokta Yusha alipiga hatua za taratibu kuingia ndani ya hospitali, huku akifuta machozi kwa kutumia kiganja chake, alikipita kitanda cha mkewe, Nasra akiwa anakiangalia sana, alifika katika kitanda alicholala Hasina, alipofika tu pale kitandani kilitokea kitu cha ajabu sana! Hasina alifungua macho!
Dokta Yusha hakuamini alichokuwa anakitazama, ulikuwa ni ukweli ambao hakukubaliana nao.

"Umeamka Hasina, niambie mke wangu Nasra yuko wapi, naomba uniambie hata kama wamemchukua wale washenzi, wewe nambie tu"
Dokta Yusha alikuwa anaongea na Hasina lakini ilikuwa ni kama anaongea na sanamu, Hasina alimwangalia tu, bila kusema chochote.
Maneno yale ya Dokta Yusha yalimuamsha Mzee Mpaukha toka usingizini. Naye alishangaa sana kumuona Dokta Yusha pale. Kwa sauti dhaifu aliongea.

"Ulikuwa wapi Dokta, umeacha watu wanateseka sana hapa, hii sio hospitali kabisa, hapa ni wakala wa kifo!"

Dokta Yusha alimwacha Hasina, alisogea taratibu kuelekea katika kitanda alicholala Mzee Mpaukha huku akiyasikiliza kwa umakini sana maneno akiyoyaongea Mzee yule. Yalimuingia kabisa akilini.

"Nimekuelewa Mzee wangu"

Dokta Yusha aliongea kwa huzuni alipofika pale kitandani. Huku akijificha ili asijulikane kama alikuwa analia.

"Katafute gari sasahivi Dokta, katafute gari kama unatujari, utuhamishe katika hospitali hii"
"Nasra yupo wapi baba?"
"Nasra yupo ICU"
"Tutaondoka vipi sasa baba na mke wangu yupo ICU?"
"Ni kwa kudra ya Mwenyezi Mungu, hata huko ICU unafikiri anapewa huduma gani, amelazwa tu kama alivyolazwa hapa! Tuhamishe Dokta hii siyo hospitali!"

******

Don Genge alikaa pale sofani muda mrefu kidogo. Baada ya kutafakari sana akapata wazo kichwani kwake, na akalifanyia kazi wazo lake muda huo huo. Aliitoa simu yake katika mfuko wa suruali yake, akatafuta mamba fulani na kuzipiga.

"Hallo Dokta Zaidi Kilumba"
"Nambie Don"
"Huyu jamaa katoroka huku, lakini kwa vyovyote vile lazima aje hospitali kuviangalia hivyo vikaragosi vyake, weka mtu makini wodini atuambie pindi tu atakapotia mguu wake hapo hospitali"
"Sawa Don, natekeleza hilo sasahivi"

ITAENDELEA KESHO MUNGU AKIPENDA
 
SIMULIZI; PENZI CHUNGU
MWANDISHI; HALFANI SUDY


Cha ajabu na kushangaza wote watatu walikuwa wanakoroma. Mikoromo mikali sana. Kila mmoja alikuwa anakoroma huku anatabasamu. Alikuwa anajua kuwa anamdanganya mwenzake. Nani wa kumdanganya mwenzie kati ya watu wale watatu. Wote walikuwa mashujaa katika nyanja yake.

Mikoromo bandia ya watu wale ilivuka mipaka. Sauti za mkoromo zilipita mlangoni na kutokea jikoni. Pale alikolala Suto Sutani awali. Sauti hazikukomea hapo, zilisafiri na kutoka nje ya kibanda kile. Kule nje sauti ilisafiri kwa kasi zaidi ikisaidiwa na upepo na kufika katika sikio la mnyama mkali zaidi porini, Simba!
Simba yule jike nae hakuidharau sauti ile ya mkoromo, alianza kuifuata.
Ndio! Sauti ilimfikisha mpaka nje ya kibanda walicholala kina Mzee Mapengo.

Alipofika pale nje Simba alitulia, ghafla hakuisikia tena ile mikoromo, ilikata ghafla. Simba alikaa pale nje kama dakika mbili, hali ilikuwa shwari. Simba alikizunguka kile kibanda mara tatu, alivyomaliza akatulia katikati ya mlango. Akatoa muungurumo mdogo na kuamua kuingia ndani. Mlango ulikuwa mkubwa na uko wazi, hakukuwa na zuio lolote, aliingia ndani kwa madaha makubwa sana. Alipofika pale jikoni alisita kidogo, akabadiri mtindo, sasa alikaa kitayaritayari kupambana na chochote mbele yake. Aliunguruma muungurumo mkali, akiwa katikati ya mlango wa chumba walicholala Daniel Mwaseba, Suto Sutani na Mzee Mapengo.
Alipofika pale mlangoni, macho ya Simba yaliangalia haraka haraka na kuwaona maadui zake watatu..

JIPATIE KITABU CHA PENZI CHUNGU KWA SH 8000 TU...PIGA SIMU NO 0687028898 KAMA UNAKIHITAJI.
 
Back
Top Bottom