Riwaya: ANGAMIZO

Riwaya: ANGAMIZO

SEHEMU YA KUMI
Daniel alikuwa amelala vya kutosha pale hotelini.
Aliamka, alioga na kuagiza chakula palepale
hotelini. Baada ya kula alipiga simu kwa rafiki
yake mmoja wa wafanyakazi katika uwanja wa
ndege wa Zanzibar, akajibiwa kuna ndege ya saa
kumi inayoenda Dar es salaam. Akamuomba
amkatie tiketi moja.
Daniel aliamua kurejea Dar es salaam tena !
*****************
Ndege ya saa kumi jioni kwenda Dar es salaam
ilijikuta imepandwa na maadui wawili. Daniel
Mwaseba na Kerspersky . Hakuna aliyekuwa
kamuona mwenzie.
Daniel ndiye alikuwa wa kwanza kuingia kwenye
ndege. Alikwenda uwanja wa ndege mapema
zaidi. Alikosa cha kufanya kule hotelini. Aliona
bora awahi kwenda uwanjani. Saa nane kamili
ilimkuta ndani ya uwanja wa ndege wa Zanzibar.
Akisubiri muda wa kuondoka ndege ufike.
Arudi Dar es salaam.
Kerspersky yeye alifika baadae pale uwanjani.
Alifika Zanzibar saa tisa na nusu akitokea Mbeya.
Baada ya kumaliza utaratibu wa pale uwanjani,
Kerspersky aliingia ndani ya ndege.
Daniel alikuwa amekaa katika siti ya nyuma
kabisa ya ndege ile. Akiwa amezongwa na
mawazo tele. Hakutegemea kama kazi ya
kuwafichua wauaji wale ingekuwa ngumu kiasi
kile. Sasa aliona siku tatu ni chache sana.
Kutokana na kuelemewa na mawazo mengi
aliamua kuyapunguza kwa kusoma riwaya.
Alifungua kibegi chake kidogo na kutoa kitabu
cha riwaya ya Mdunguaji, riwaya iliyotungwa na
Gwiji wa riwaya Tanzania, Hussein I Tuwa.
Alikifunua taratibu na kuanza kukisoma. Mambo
ya Badi katika riwaya ile yalimsahaulisha kidogo
Daniel adha za Dunia.
Alielea katika dunia nyingine kabisa.
Wakati Daniel anasoma kitabu ndipo Kerspersky
aliingia ndani ya ndege ile. Alikaa siti za mbele
kabisa. Kerspersky hakuwa makini kuwachunguza
watu waliokuwepo katika ndege ile. Alitulia
shwari katika siti yake. Akiiwazia kwa kina kazi
iliyopo mbele yake.
Kerspersky alipanga kwenda katika chuo cha
usimamizi wa fedha IFM kutekeleza adhma yake.
Chuo alichokuwa anasoma mtoto wa waziri wa
kilimo na chakula, Mheshimiwa Nyongo Daudi.
Alidhamiria kwenda kumuua Janeth Nyongo.
Mtoto wa waziri wa kilimo na chakula.
Saa kumi kamili ndege ile iliiacha ardhi ya kisiwa
cha Zanzibar, kuelekea Dar es salaam.
Baada ya muda mchache ndege iliwasiri katika
uwanja wa Mwalimu Julius Nyerere, Jijini la Dar
es salaam.
Abiria mmojammoja walianza kushuka kwenye
ndege ile. Daniel alikuwa abiria wa mwisho
kushuka katika ndege ile. Akitanguliwa
Kerspersky na abiria wengine.
Daniel alikuwa makini sana. Alikuwa anaifata kila
hatua akiyopiga Kerspersky . Jamaa hakujua
kabisa kama anafuatwa.
Alichukua teksi pale nje ya uwanja wa ndege wa
Mwalimu Julius Nyerere, na kuelekea Posta,
maeneo kilipo chuo cha IFM.
Daniel nae alifata kwa kutumia teksi. Ulikuwa
mfuatano wa kimya kimya.
Kerspersky hakuwa makini kabisa. Hakuwa na
wasiwasi kabisa. Alifika posta, akashuka.
Sasa akawa anaelekea IFM kwa miguu, Daniel
akiwa nyuma yake !
Kerspersky alifika chuoni IFM. Kerspersky
akapita katika geti la chuo bila wasiwasi wowote.
Hakuwa na hofu yoyote, na wala hakuna
aliyemtilia shaka.
Alianza kuwauliza wanafunzi. Mwanafunzi wa
kwanza hakuwa anajua Janeth anakaa chumba
gani, mwanafunzi wa pili bila kujua dhamira ya
jamaa yule alimuelekeza Kerspersky chumba
alichokuwa anakaa mtoto wa waziri wa kilimo na
chakula, Janeth.
Taratibu Kerspersky akawa anaelekea huko
alikoelekezwa.
Kerspesky alikuwa anaelekea hosteli huku
akigeuka nyuma mara kwa mara. Lakini
hakumwona mtu wa kumtilia shaka.
Alipanda ngazi za kuelekea hosteli kwa mwendo
wa haraka sana.
Sasa damu ilikuwa inamchemka mwilini mwake,
alikuwa amedhamiria kuuwa !
Akafika chumba namba 33. Chumba
alichoelekezwa kuwa ndicho anachokaa Janeth.
Aligonga hodi kwa kutumia mpini wa kisu chake
kirefu, lakini mlango haukufunguliwa.
Akarudia kugonga tena.
Sasa taratibu mlango ulikuwa unafunguliwa .
Aliangaliana na bastola !
Alikuwa Daniel Mwaseba!
Kumbe Kerspersky alivyokuwa anamuuliza
mwanafunzi wa kwanza na kumfata wa pili.
Daniel alimfata yule wa mwanafunzi wa kwanza.
Baada ya kumuuliza alimwambia yule jamaa
alikuwa anamuulizia Janeth, Daniel alipiga hatua
moja mbele. Kwa haraka akaenda kumuuliza
mwanafunzi mwengine.
Alielekezwa chumba cha alichokuwa anakaa
Janeth. Alitangulia yeye chumba namba 33. Kwa
bahati nzuri kilikuwa kimefungwa. Alifungua kwa
kutumia funguo wake malaya, alifanikiwa.
Alitulia kitandani akimsubiri mgeni wake.
Kerspersky alipigwa na butwaa. Hakutegemea
kumkuta Daniel pale. Pia hakutegemea
kukaribishwa kwa mtindo ule.
"Karibu sana"
Kerspersky hakujibu.
Daniel alitabasamu.
"Najua hukutegemea kukaribishwa na mimi.Ila
imekukuta bahati mbaya "
Jamaa kimya.
"Natakaa uongee ukimya haukusaidii ! " Daniel
alisema kwa ukali.
Hakujibu.
Daniel alikasirika. Alimpiga kwa kutumia kiwiko
cha mkono kwenye mdomo. Kerspersky alianza
kutokwa na damu.
"Utaongea huongei?"
Jamaa aligeuka bubu.
Alimchukua na kwenda kumhifadhi kituo cha
Polisi Posta.
Daniel alitoka nje ya kituo kile akiwa hajui
anaelekea wapi ? Alikuwa na mawazo mengi
sana. Hajui aelekee wapi ? Hajui afanye nini?
Baada ya masaa mawili kuzunguka mtaani alirudi
tena kituo cha Polisi Posta.
"Naomba unitolee yule Mhalifu"
Kerspersky akaitwa.
Akakaa mbele ya Daniel.
"Utaongea sasa hivi" Daniel akasema kwa upole.
Kerspersky akawa anamwangalia tu.
"Usinilazimishe kufanya ninachotaka kukufanya"
"Nifanye chochote sikwambii chochote "
Daniel akaisikia sauti ya Kerspersky kwa mara ya
kwanza.
Daniel alinyanyuka. Akaenda pale kwenye kabati
la pale kaunta . Akafungua droo moja ya kabati.
Akachukua mkanda mdogo, ulikuwa kama saa ya
mkononi ndogo.
Akamvesha ule mkanda mkononi kwa Kerspersky.
Ulimkaa vizuri sana.
Akamfunga mkono mwengine kwa pingu
akiunganisha na kile kiti cha chuma alichokalia
Kerspersky .
Baada ya muda mfupi ule mkanda ukaanza
kumbana Kerspersky. Ulianza kumbana taratibu,
baadae kasi ya kubana ule mkono iliongezeka.
Ukazidi kubana ule mkanda !
Kerspersky alianza kusikia maumivu yakizidi.
Maumivu yakazidi sasa.
Ule mkanda ukaanza kupita kwenye nyama za
mkono wa Kerspersky.
Machozi yalianza kumdondoka
Damu zikaanza kumwagika Kerspersky !.
Kerspersky alianza kulia kwa sauti. Maumivu
hayakuwa na mfano sasa !.
"Nitasemaa.. ! "
Daniel alijifanya kama hamsikii.
Hali ilikuwa ngumu sana kwa Kerspersky.
Mkono wa Kerspersky ulikuwa unaelekea
kukatika. Sasa ule mkanda ulifika kwenye mfupa
wa mkono !
Daniel alikuwa mtu katili sana. Hakumuonea
huruma. Alikuwa anamwangalia tu Jamaa.
Sasa Daniel alitosheka. Akamfungua ule mkanda
Kerspersky.
"Utaongea" Alimuuliza huku anaangalia pembeni.
"Ndio kaka" Alijibu kwa sauti ya huruma.
"Unaitwa Nani?"
" Abednego "
"Nani anayekutuma kuua ?"
"Salehe"
"Yuko wapi sasa hivi ?"
"Mbeya"
"Amefata nini Mbeya"
Kerspersky huku analia alieleza kila kitu kuhusu
Mpango wao wa Angamizo.
Alieleza pia kuhusu watu waliotuma Kigoma na
Mara.
Daniel aliwapigia simu wakuu wa Polisi wa
Kigoma na Mara. Kuhakikisha wale watu
wamakamatwa.
Na mwenyewe alijiandaa kwenda Iringa
kusimamisha Mpango huo haramu.
Aliwachukua askari kumi pale kituo cha Polisi
Posta. Kwa ajili ya kwenda kuuangamiza Mpango
wa Angamizo.
***Ahsante, Daniel!!
ITAENDELEA
 
Huyu Jamaa IDD Eba yuko mahiri anakwenda na wakati tofauti na Bold ,ana mapose sana!
 
duuh noma sana nausibir mzgo mwingne tena!! usisahau kun mention mkuu
 
SEHEMU YA 11
Aliwachukua askari kumi pale kituo cha Polisi
Posta. Kwa ajili ya kwenda kuuangamiza Mpango
wa Angamizo.
***************
Saa mbili usiku waliwasiri jijini Iringa Kwa ndege.
Kuhakikisha silaha zote zilizopo katika ghala kuu
la silaha la Taifa haziibiwi.
Zinabaki salama !
Kwa ruhusa ya Raisi, Daniel na askari wale kumi
waliingia kwenye ghala la silaha. Huku askari
wengine wakibaki nje kufanya doria. Wakatulia
tuli kusubiri chochote kitakachotokea.
Huko Jijini Mbeya Salehe alikuwa anasubiri
taarifa za angamizo kwa watu aliowatuma.
Salehe alipanga usiku ule wafanikishe mauaji
makubwa . Kabla jioni hawajaenda Makete
Kuhitimisha angamizo, Salehe aliamua kuacha
Angamizo kubwa Tanzania.
Salehe alienda sokoni Mwanjelwa. Mkononi
akiwa kajipaka sumu ya Proxine. Kutokana na
wingi wa watu Mwanjelwa, Salehe aligusana na
watu wengi sana. Alihakikisha kila baada ya
dakika tatu anapaka dawa ya kuondoa madhara
ya Proxine. Ndani ya dakika kumi, watu ishirini
walikufa kifo cha kinyama sana pale sokoni.
Polisi walipata taarifa, wakati Polisi wanaenda
Mwanjelwa kwa kasi kwa gari yao. Salehe
alikuwa kashatoka, alikuwa stendi kuu ya mabasi
Mbeya. Nako aliacha Angamizo.
Polisi walipata taarifa za mauaji mapya ya
kinyama stendi kuu ya mabasi Mbeya. Polisi
walichanganyikiwa sasa. Gari za Polisi ziliwasha
moto kwenda stendi. Walienda kwa kasi kubwa
sana, ndani ya dakika tano stendi ilijaa Polisi.
Saa kumi na mbili jioni ilimkuta Salehe ndani ya
uwanja wa mpira wa Sokoine. Daniel aliteketeza
mashabiki wengi sana wa mpira kwa sumu ya
Proxine.
Salehe aliangamiza !
Kamanda mkuu wa Polisi mkoa wa Mbeya alipiga
simu kwa Mkuu wa Polisi nchini.
Aliomba msaada.
Aliomba Daniel aende Mbeya kusaidia.
IJP Rondo alivyomaliza kuongea kwa simu ya
Kamanda wa Polisi wa Mbeya, kamanda wa
Polisi wa mkoa wa Mara nae Alipiga, watu ishirini
walikuwa wameteketea kwa sumu ya Proxine,
sokoni Musoma.
Naye aliomba msaada, alikuwa anamhitaji Daniel.
Ghafla simu ya kamanda wa Polisi mkoa wa
Kigoma nayo iliingia , wavuvi sita walikuwa
wameuwawa kwa sumu ya Proxine, ufukweni
mwa ziwa Tanganyika.
Naye aliomba Daniel aende Kigoma.
Sasa nchi ilitingishika !
Mkuu wa Polisi Tanzania, IJP Rondo jasho
lilikuwa linamtiririka !
Akapiga simu kwa Daniel, Daniel alikuwa
hapatikani !
IGP Rondo alizidi kuchanganyikiwa ! Mara,
Kamanda wa Polisi mkoa wa Kigoma akawa
anapiga tena simu.
IGP Rondo aliiangalia tu simu ile. Hakutamani
kabisa kuipokea. Simu iliita hadi ikakata.
Ilivyokata, simu yake ilikuwa inaita tena, alikuwa
kamanda wa Polisi mkoa wa Mara naye alipiga
tena.
IGP Rondo macho yalimtoka pima !
Aliichukua ile simu na kuitoa betri kabisa. Alikaa
kwenye sofa akiwa kajishika tama !
Alielekea kuwehuka !
Zwangendaba alitumwa kupeleka Angamizo
Kigoma wakati Nduli alitumwa kupeleka
Angamizo Mara. Salehe alibakisha Angamizo jijini
Mbeya. Kila mmoja alikuwa na chupa za Proxine
kumi. Walidhamiria kuleta kweli vita vya tatu vya
dunia.
Walikuwa wanaua bila huruma !
Huko Kigoma, baada ya Zwangendaba kutoka
katika ufukwe wa ziwa Tanganyika, sasa alikuwa
anaingia katika uwanja wa lake Tanganyika.
Kulikuwa na onyesho la mziki. Alidhamiria
kwenda kuuwa humo. Alifanikiwa, watu zaidi ya
ishirini waliuwawa kinyama kwa sumu ya Proxine.
Baada ya kupata habari za vifo vya watu hawa
tena, Kamanda wa Polisi alimpigia simu IJP
Rondo. Simu haikupokelewa. Alijaribu kupiga
tena, simu haikupatikana. Kamanda wa mkoa wa
Kigoma alichanganyikiwa sana.
Huko Mara nako hali Ilikuwa tete. Nduli alipeleka
madhara makubwa katika mkoa huo. Nduli
aliingia baa moja , ndani ya dakika tano
alihakikisha amewagusa watu wote mule baa.
Baada ya muda mfupi baa nzima ikibaki mifupa
na mafuvu.
Walevi kumi na sita walienda kuzimu bila ngozi !
Saa mbili usiku ilimkuta Salehe akiwa Mbeya
carnival. Disko lilikuwa limeshaanza muda huo.
Alipanda kule juu kwa DJ na kufungua vichupa
vitatu vya Proxine. Alirusha hewani sehemu
ambayo kulikuwa na watu wanacheza disco.
Baada ya dakika kumi kulitokea picha mbaya
ndani ya Mbeya carnival.
Watu wengi waliuwawa kwa sumu ile !
Saa nne usiku iliwakuta wakina Salehe wakiwa
ndani ya chumba kilekile, ndani ya Green view
hoteli. Zwangendaba na Nduli washarejea,
walikuwa wanamsubiri Kerspersky ili safari yao
ya kwenda Makete ianze. Kerspersky hakuwa
anapatikana !
Walimsubiri mpaka walichoka !
Waliamua kwenda Makete bila Kerspersky, ndege
ya kukodi ilitua Iringa saa tano na robo usiku.
Walikuwa watu kumi na mbili hatari !.
Walikuwa tayari kwa mapambano. Walikuwa
wanajiamini, kwa maangamizo waliyoyapeleka
Mara, Mbeya na Kigoma waliamini ulinzi
hautokiwa mkubwa sana Makete.
Walijipanga vizuri. Walikuwa na vifaa na zana
zote muhimu. Walikuwa wana silaha za kutosha.
Waliandaa maroli saba kwa ajili ya kubebea
silaha. Waliyapaki porini.
Sasa wenyewe walikuwa wananyemelea katika
ghala kuu la silaha.
Wanajeshi wanne. Meja Badi Bwino, meja Fuga
Tindo, Meja Kurasa Allen na Meja Swalo
Mbombwe, Zwangendaba. Nduli. Kulikuwa na
Salehe pamoja na madada watano hodari katika
mapigano ya ana kwa ana, walikuwa wanajiita,
Dadaz killers .Walikuwa na sifa moja kuu,
shabaha ya kutisha unapowakabidhi bastola.
Ghala kuu la silaha lilikuwa kijijini Makete. Ni
watu wachache sana ndio walikuwa wanajua
uwepo wa ghala lile kijijini hapo. Wanajeshi hawa
wanne ndio walifichua uwepo wa ghala hilo.
Taarifa zikapenya kwa Salehe. Naye akazivujisha
kwa Mzee Makame.
Mzee Makame alikuwa mtu mjanja sana. Alikuwa
Mtoto wa mjini. Taarifa za kuwepo ghala kuu la
silaha Iringa ilikuwa ni taarifa muhimu sana
kwake. Aliiona ni kama fursa na aliamua
kuitumia.
Ni yeye ndiye aliyeongea na wanamgambo wa
kikundi cha kigaidi cha huko Somalia. Na
kumuahidi fedha nyingi sana endapo
wangezipeleka silaha hizo.
Mpango pia ulihusisha na mawaziri. Waliokuwa
wanakitumia kivuli cha Mzee Makame.
Kundi la watu kumi na mbili sasa walikuwa
wanalikaribia ghala kuu la silaha. Sehemu
muhimu sana kwa Taifa.
Daniel Mwaseba alikuwa kashawapanga vizuri
askari wake kumi, wametulia tuli ghalani, na
askari wakiolilinda ghala lile kwa nje, walikuwa
ishirini. Jumla walikuwa askari thelathini imara.
Wakiwa tayari kulitetea Taifa lao juu ya udhalimu
huu mkubwa.
Sasa kundi lile hatari lilibakisha mita mia moja tu
kulifikia ghala.!
Kule ndani ya ghala askari walikuwa wametulia
tuli, wakiongozwa na Daniel Mwaseba.
Lilikuwa ghala kubwa, lenye kila aina ya silaha.
Daniel Mwaseba alikuwa amekaa karibu kabisa
na mlango wa ghala lile.
Alikuwa mtulivu sana.
Akiwa tayari kwa lolote !
Ghafla, taa zilizimika. Eneo lote kuzunguka ghala
kulikuwa na giza !
Kuzimika kwa taa ilimaanisha muda wakiosubiria
wakina Daniel Mwaseba umefika.
Muda wa kupambana!
Historia ya ghala lile ilikuwa halijawahi kuwa giza
vile tangu lianzishwe.
Kulikuwa hakujawahi kuzimika umeme kabisa.
Walikuwa wanatumia umeme maalumu
ukiozalishwa kwa nishati ya jua.
Kwahiyo watu wote walitambua kwamba, umeme
ulikuwa haujakatika,
Ila umeme ulikuwa umekatwa! Hali ya tahadhari
iliongezeka kwa askari wale.
Sasa kila mtu alikuwa imara, kaishikilia bunduki
yake.
Tayari kwa lolote.
Daniel Mwaseba, aliona ule sasa haukuwa wakati
wa kukaa ndani, kusubiri maadui waje. Aliona ule
ni wakati wa kutoka nje, kupambana na adui.
Ulikuwa muda wa kufa,
ama kupona !
Daniel aliwapa ishara wale askari kumi, wote
wakawa wanatoka nje.
Kumtafuta adui !
Nje kulikuwa na giza totoro. Ghala la silaha
lilikuwa msituni. Msitu nao uliozidisha hali ile ya
giza.
Sasa ilikuwa hatari!
Hatari ya kupigana risasi wenyewe askari,
endapo hawatokuwa makini.
Daniel Mwaseba aliwaamrisha askari wote kurudi
ghalani.
Ili wajipange upya.
Kule nje, Meja Badi Bwino, ndiye alikuwa
anaongoza operesheni hii kwa upande wa
maadui.
Meja Badi Bwino aligawa kikosi chake katika
makundi manne, yenye watu watatu watatu.
Kundi la kwanza liliongozwa na Meja Kurasa
Allen, kundi hilo alikuwemo pia Nduli na
mwanadada mmoja, walielekea upande wa
mashariki wa ghala lile.
Kundi la pili liliongozwa na Meja Fuga Tindo,
katika kundi hili walikuwemo pia Zwangendaba na
mwanadada mmoja, kundi hili lilienda upande wa
magharibi wa ghala lile.
Kundi la tatu liliongozwa na Meja Swalo
Mbombwe, Salehe na mwanadada mmoja. Wao
walibaki palepale ili kutoa msaada upande
wowote watakaohitaji msaada, iwe magharibi au
mashariki.
Wao ndio walikuwa walinzi wa wenzao.
Na kundi la mwisho liliongozwa na mwenyewe
Meja Badi Bwino, aliongozana wadada wawili.
Walikuwa wanaenda mahali geti lilipo. Kijana
mmoja shushushu alifanya kazi nzuri.
Ni yeye aliyeharibu mfumo wa umeme kule
ndani.
Hakika walijipanga vizuri sana watu hawa !
Kule ndani kulikuwa na mvurugano. Askari
waliingiwa na woga !
Woga wa kuuliwa!
Woga wa kuuwawa!
Hawakuwa wanajua kuna maadui wangapi huko
nje ?
Woga pia ulichangiwa na lile giza.
Askari waliingiwa na taharuki hofu kubwa ! Daniel
akajua bila kuwa imara yeye, watafeli katika
operesheni ile.
Ulikuwa wakati mgumu sana kwa Daniel,
ukiohitaji hekima, busara na akili za Daniel
Mwaseba.
Woga ni kitu kibaya sana katika operesheni za
hatari kama hizi !
Daniel alishauri askari wote thelathini wabaki
kulinda silaha mle ghalani, yeye pekee aende
kupambana gizani, na wauaji asiowajua idadi yao.
Wale askari wengine walikubaliana na Daniel.
Daniel Mwaseba alitoka nje peke yake, akiacha
kuwafungua askari wale kwa nje.
USIKOSE SEHEMU YA MWISHO
 
SEHEMU YA MWISHO
Kule nje, kundi lililoelekea magharibi mwa ghala
lile. Walifika ukutani. Kundi lilikuwa linaongozwa
na mwanajeshi hatari sana, Meja Fuga Tindo.
Ghala lilizungukwa na ukuta mrefu sana, ambao
haukuwa rahisi kupandwa na binadamu wa
kawaida. Lakini Fuga Tindo hakuwa binadamu
wa kawaida kama wewe. Aliuparamia ukuta ule
mithili ya paka, kimya kimya. Zwangendaba na
yule dada walishangaa sana uwezo wa Fuga
Tindo. Giza lilikuwa upande wake Fuga. Na
kutetereka kwa wale askari mle ndani lilikuwa
kosa kubwa sana. Maana hakukuwa na askari
yeyote akiyeulinda ukuta ule. Fuga Tindo, sasa
alikuwa ndani ya uwanja mpana wa ghala lile.
Alikuwa ananyata taratibu.
Bila kutoa sauti yoyote ile.
Kwa upande wa Daniel Mwaseba aliamua
kupambana, sasa alichukulia kama yuko peke
yake katika operesheni ile.
Aliapa kimoyomoyo, lazima ashinde,
ndio !
Lazima auangamize mpango wa Angamizo !
Kuzimika kwa umeme ghafla kulimjurisha kitu
Daniel, alijua kwa vyovyote aliyekorofisha umeme
ule alikuwa ndani ya ghala mlemle.
Daniel Mwaseba sasa alizidisha umakini,
hakumuamini mtu yeyote .
Alinyata taratibu gizani na kujibanza katika kona
moja, kona ambayo ilimuezesha kuona japo kwa
shida ukuta ule wote kwa mbele.
Kule upande wa mashariki, Meja Kurasa Allen na
watu wake, nao waliufikia ukuta . Kama Meja
Fuga Tindo, Meja kurasa nae aliparamia ukuta
ule.
Meja Kurasa sasa alikuwa juu ya ukuta ule.
Akijiandaa kuteremka kwa ndani.
Alichelewa !
Risasi moja ilitua kichwani kwa Meja Kurasa.
Alirudi kwa kasi kule nje alikotoka.
Bastola ya Daniel Mwaseba ilifanya alichoituma !
Nduli alienda kwa kasi pale alipoanguka Meja
Kurasa. Walimkuta na jeraha baya sana kichwani,
damu zinabubujika ! Alikuwa kashakata roho !
Taharuki !
Daniel Mwaseba aliachana kabisa na kivuli kile
alichokitungua. Sasa alikuwa anatambaa kukifata
kivuli kikichonyata kimya kimya, kilikuwa kivuli
cha Meja Fuga Tindo.
Wakati Meja Fuga akinyata kwa kutembea, Daniel
Mwaseba alikuwa anamnyatia huku amelala !
Lilikuwa giza hasa mule ndani, Zilikuwa
zinatumika hisia zaidi ya macho.
Akiwa pale chini, Daniel Mwaseba alitoa bastola
yake yenye kiwambo cha kuzuia sauti. Alikilenga
mgongoni kile kivuli cha Meja Fuga Tindo. Risasi
ya moto isiyotoa sauti hata kidogo ilitua katika ya
uti wa mgongo wa Meja Fuga. Daniel
alikishuhudia kivuli kile kikidondoka chini kama
mzigo!
Daniel alifanikiwa kumuuwa mtu wa pili hatari
usiku ule.
Kule nje, Badi Bwino, mkuu wa operesheni hii,
akiwa na wadada wawili walikuwa wanalikaribia
geti kuu la ghala lile. Walishangazwa sana na
ukimya wa mahali pale.
Ndani ya ghala kulikuwa kimya, kama hakukuwa
na watu.
Meja Badi Bwino aliingiwa na wasiwasi sana.
Kilikuwa kimya cha kuogofya !
Walizidi kusogea, kila mmoja akiwaza lake
kichwani.
Ghafla wote walipigwa na butwaa !
Geti la ghala kuu lilikuwa wazi !
Mtego!
Sasa Meja Badi Bwino na wale madada wawili
walizidisha umakini. Walisogea taratibu, kwa
tahadhari kubwa. Haikuwa kawaida geti lile kuwa
wazi, tena usiku wa manane !
Kule ndani, Daniel Mwaseba alirejea katika lindo
lake. Alikuwa kabana palepale konani, huku
macho yake yote yakiwa pale getini. Alifungua
geti makusudi, ili akilenge Kivuli chochote
kitakachojitokeza.
Na kweli.
Kivuli kilitokea !
Ilihitaji mtu makini kuweza kukilenga kivuli kile,
kukiwa na giza namna ile, na umbali na umbali
namna ile.
Mtu wa aina hiyo alikuwepo, Daniel Mwaseba.
Daniel Mwaseba alikuwa na uwezo huo.
Aliitoa bastola yake kiunoni taratibu.
Alikilenga vizuri kile kivuli. Akafyatua !
Risasi ile ilitua katikati ya shingo ya Dada mmoja
aliyefatana na Meja Badi Bwino.
Yule Dada alitoa mguno hafifu.
Akaiaga dunia !
Kule nje ilibaki taharuki. Meja Badi Bwino
hakuelewa risasi ile ilitokea upande gani, shingo
yote ya yule dada ilitapakaa damu !
Meja Badi Bwino na yule Dada walirudi nyuma.
Kusonga mbele, iliashiria kukisogelea kifo zaidi .
Kule upande wa mashariki. Baada ya Meja
Kurasa kuuwawa kwa risasi ya kichwa, Nduli na
yule Dada, sasa walikuwa wanarudi usawa wa
getini. Wao hawakuwa na uwezo kabisa wa
kuupanda ule ukuta.
Sasa walifika getini. Giza lilikuwa limetanda lakini
halikuwazuia kujua kama lile geti lilikuwa wazi, si
Nduli wala yule Dada aliweza kuiona maiti ya
yule Dada pale chini.
Wote mioyo yao iliingiwa na furaha. Kuona geti
lilikuwa wazi. Sasa kwa mwendo wa kunyata
Nduli na yule dada walikuwa wanaingia ndani,
kupitia getini.
Kule upande wa magharibi nako hali ilikuwa tete.
Zwangendaba na yule dada mwengine walisubiri
ishara yoyote wakiwa kule chini kwa nje toka
kwa Meja Fuga Tindo ambaye alikuwa
kauparamia ukuta ule. Hawakujua yaliyomkuta,
na wangejua vipi ?
Walisubiri bila mafanikio.
Sasa wakahisi kutakuwa na hatari !
Lakini waliendelea kusubiri palepale, wakijua
muda wowote labda Meja Fuga Tindo angerejea.
Kule getini yule dada alitangulia. Akimuacha
Nduli hatua kama tatu nyuma yake. Dada
alilisogelea geti kwa mwendo wa taratibu sana,
akiwa kashika bastola kwa mkono wake wa
kuume. Nyuma yake akifatwa kwa ukaribu na
Nduli.
Kule ndani Daniel Mwaseba kwa kutambaa
akitumia tumbo alikuwa amesogea kidogo pale
konani. Sasa alikuwa nyuma ya pipa la maji.
Akiwa mtulivu kupita kiasi. Akisubiria kusikia
mtikisiko wowote autungue!
Akisubiri kitokee kivuli chochote akipoteze!
Sasa alikiona kivuli kinaingia kupitia pale getini.
Alikiona kwa hisia zaidi ya macho.
Ukweli kutokana na giza ilikuwa ngumu sana
kuona kivuli kwa uhakika. Ulikuwa mchezo wa
hisia ambao Daniel Mwaseba alikuwa ndio
mwalimu wake.
Sasa Daniel Mwaseba alinyanyua mkono wake
wa kuume wenye bastola, alikilenga kile kivuli
alichokuwa anakiona kwa hisia .
Alifyatua risasi iliyopenya kifuani kwa yule Dada.
Yule dada alienda chini mzimamzima kama gunia
la mchanga.
Nduli alirudi nyuma kwa haraka. Nduli alikuwa
anakimbia sasa, kurudi kule walikokuwa kina
Meja Swalo Mbombwe.
Aliona kwenda mbele ni kukifata kifo chake.
Daniel Mwaseba sasa alitoka pale nyuma ya
pipa. Alikuwa anatambaa kuelekea getini. Kwa
tahadhari kubwa sana.
Kule kwa kina Zwangendaba waliamini kuna
jambo baya lililomkuta Meja Fuga.
Maana walikaa muda mrefu sana bila taarifa
yoyote.
Nao waliamua kurudi nyuma. Kwenda kujipanga
upya. Wakati kina Zwangendaba wakirudi, Daniel
Mwaseba alikuwa anaenda, sasa aliamua
kuwafata nje maadui zake.
Kule ndani ya ghala kulikuwa kimya. Askari
thelathini walikuwa kimya, kila mmoja akiomba
dua yake. Akimuombea Daniel Mwaseba ashinde
ili nao waokoke.
Walikuwa askari imara, lakini waogopa kifo
hodari !
Kule nje , gizani kulikuwa na mtafutano.
Daniel Mwaseba akiwa na bastola moja kila
mkono alikuwa anaambaa upande wa magharibi
wa ghala.
Alikuwa makini kwa kila hatua anayoipiga.
Wakati Daniel anaenda upande ule wa magharibi
ya ghala, Zwangendaba na yule Dada walikuwa
wanakuja mashariki mwa ghala lile.
Wote walikuwa wananyata!
Wote walikuwa makini sana!
Kule walikobaki wakina Meja Swalo Mbombwe,
kulikuwa na mfadhaiko mkubwa sana.
Meja Badi Bwino na yule Dada walirudi wakiwa
wametaharuki, huku wakidai wamempoteza Dada
mwengine.
Na sasa Nduli alikuwa anarejea mbio huku akidai
Meja Kurasa Allen na yule Dada mwengine
wameuwawa!
Taarifa zile ziliwaacha midomo wazi kina Salehe.
Hawakuamini !
Wala, hawakutegemea kinachotokea!
Mpaka sasa hawakujua Meja Fuga Tindo na
wakina Zwangendaba wako wapi ? Angamizo
sasa lilielekea kuwaangamiza wenyewe !
Sasa walipanga upya operesheni yao.
Ikiongozwa na yuleyule, Meja Badi Bwino.
"Sasa naona " Plan A" imefeli. Sasa lazima
tutumie 'Plan B'. Sasa ni kwenda kwa pamoja.
Kila mmoja akiwa mlinzi kwa mwenzake.
Huyo Mdunguaji mwoga,
Ama zake !
Wote walisimama nusu duara 'Cow horn' Wakawa
wanaenda kwa pamoja, kwa nguvu mpya sasa.
Sasa walibaki sita, wanne walikuwa wameuwawa
na bastola ya Daniel, na wawili walikuwa
hawajarudi mpaka sasa, wakina Zwangendaba.
Kule upande wa magharibi, Daniel na kina
Zwangendaba walikaribiana sasa.
Daniel aliwaona wakija, kama kawaida, hisia ndio
alizozitumia, alijibanza nyuma ya mti.
Zwangendaba na yule dada walikuwa bado
hawajamwona Daniel.
Zwangendaba na yule Dada walipita karibu
kabisa na ule mti aliojificha Daniel. Daniel alitulia
kimya kabisa.
Kina Zwangendaba walipita mita chache sana
karibu na ule mti aliojibanza Daniel. Sehemu ile
ilikuwa kimya, kama hamna kiumbe hai chochote
kile.
Kulikuwa kimya !
Ubaridi wa Iringa ulikuwa umeshamiri.
Kina Zwangendaba walitembea bila kutoa ishara
yoyote.
Ilikuwa ni kimyakimya .
Kwa mwendo wa kimyakimya kina Zwangendaba
waliukaribia ule mti aliojificha Daniel. Sasa
walikuwa kama hatua tatu kuufikia mti ule.
Wakinyata taratibu, wakiangaza mbele kwa
umakini mkubwa sana, wakaupita bila kujua kuwa
adui yao alikuwa nyuma yao hatua chache sana.
Taratibu Daniel alijigeuza pale kwenye mti, sasa
akawa anaviona japo kwa shida vivuli vile
kutokana na giza.
Alinyanyua mikono yake yote miwili iliyoshika
bastola. Akailenga kuelekea kwenye vile vivuli
viwili.
Daniel Mwaseba, alifyatua risasi mbili, kwa wakati
mmoja, zilizoenda sambamba na kutua sehemu
tofauti za mwili, kwa watu wale wawili.
Wakati risasi moja ikitua na kukifumua vibaya
kisogo cha Zwangendaba, risasi nyingine ilisafiri
kwa kasi na kwenda kutua katika mgongo laini
wa yule Dada. Nguvu ya risasi ile ilimsukuma
yule dada na kumuangusha mbele kama hatua
sita. Wakati mwili wa yule dada unadondoka
chini, roho yake iliruka juu na kuelekea mbinguni!
Daniel Mwaseba kwa mara nyingine tena
alifanikiwa kuwaonesha wale maadui wabaya
yeye ni nani katika dunia ya wababe !
******
Lile kundi la watu sita, wenye hasira na kuamua
kuungana pamoja, lilikuwa linakaribia getini. Sasa
walikuwa makini, walijua kuingia kwa papara ni
kukata tiketi ya kifo!
Walilikaribia kabisa geti. Meja Badi Bwino alitoa
wazo kwa sauti ndogo lakini iliyosikika vyema
kwa kila mmoja.
"Geti lile limefunguliwa kama mtego, tusipite
pale. Tutafute njia nyingine, kupita getini ni
kukikimbilia kifo"
"Sasa tutapita wapi Meja?" Salehe aliuliza kwa
sauti ndogo pia.
"Hapa inabidi tujigawe, watatu waende Magharibi
ya ghala, na watatu waende upande wa
mashariki ya ghala. Kila kundi litafute pa kupita
huko" Meja Badi Bwino alieleza.
"Sawa" waliitikia wote.
Sasa walijigawa tena, Meja Badi Bwino, Salehe
na dada mmoja walienda mashariki wa ghala.
Meja Swalo Mbombwe, Nduli na Dada mmoja
walielekea upande wa maghari wa ghala.
Wote walitawanyika !
Wale waliokuwa wameelekea upande wa
magharibi ndio walikuwa wanaenda kukutana na
balaa, Daniel Mwaseba alikuwa upande huo.
Meja Mbombwe, Nduli na Dada mmoja ndio
walikuwa wanaelekea upande huo.
Baada ya kuwauwa wakina Zwangendaba, Daniel
alipanda juu ya ule mti, sasa aliweza kuoona hadi
ndani ya ghala. Alitulia kimya, akisubiri waje,
awaue !
Kina Meja Mbombwe walifika usawa uleule
wenye mti alioupanda Daniel Mwaseba.
"Sasa tunafanyaje hapa?" Meja Mbombwe
aliuliza.
"Inabidi tupande ukuta" Nduli alijibu.
"Kupanda hapo juu ni kujianika kwa walinzi" Meja
Mbombwe alijibu.
" Sasa tunafanyaje?" Yule dada aliuliza.
"Nduli hebu panda juu ya huu mti uangalie hali
ilivyo humo ndani"
"Sawa"
Nduli alipanda katika mti, ili kuangalia ndani. Mti
uleule aliopanda Daniel Mwaseba!
Bila kufikiria Nduli alianza kuupanda ule mti.
Akiwa kule juu ya mti, Daniel aliviona vivuli vitatu
pale chini.
Aliviona vikijadiriana, lakini hakusikia
wanajadiliana nini. Alikuwa katulia tuli kule juu.
Kashika bastola yake mkononi. Na ile bastola
nyingine kaiweka kiunoni.
Mara alikiona kivuli kimoja kikipanda juu.
Daniel alitabasamu !
Aliona kama kile kivuli kilikuwa kinafata kifo
chake !
Kile kivuli kiliendelea kupanda.
Sasa kilifika katikati ya ule mti.
Kule juu, Daniel aliishika imara bastola yake
mkononi.
Alilenga katika utosi wa kile Kivuli. Alivuta pumzi
kwa ndani. Alifyatua ile bastola. Risasi ilimpata
Nduli katika utosi wake ! Alianguka chini mithili
ya embe bivu. Meja Mbombwe na yule dada
walienda pale alipoanguka Nduli. Akatoa tochi
ndogo na kummulika, walishuhudia picha mbaya
sana!
Ubongo wa Nduli ulitapakaa pale chini. Ilikuwa ni
kichefuchefu kuangalia ubongo ule mbichi wa
ukiwa umetapakaa pale chini !
Meja Mbombwe nae alifanya kosa. Kuwasha
tochi mahali pale lilikuwa kosa kubwa sana. Yeye
alidhani Nduli ameanguka tu kule juu ya mti.
Hakuhisi kama atakuwa kapigwa risasi.
Alizima tochi yake haraka!
Lakini Kuwasha tochi ni kosa kubwa sana
alilolifanya Meja Mbomwe, na Daniel alilitumia
vizuri sana kosa lile. Sasa Daniel Mwaseba
hakutumia hisia, alishawaona kabisa maadui
zake.
Bastola yake ilikohoa harakaharaka mara mbili.
Kikohozi kilichomsafirisha izrael toka alipokuwa
mpaka Makete. Kuja kuwatoa roho watu wawili
kwa mpigo. Meja Swalo Mbombwe na yule Dada.
Walikufa wakiwa wanashangaa, wakiushangaa
ubongo mbichi ulioambatana na damu wa Nduli.
Kule upande wa mashariki, Meja Badi Bwino,
Salehe na yule Dada, walikuwa wanahangaika
kupanda ukuta.
Baada ya robo saa walifanikiwa, ingawa kwa
shida sana.
Sasa walikuwa ndani ya uwanja mpana
wakielekea kwenye ghala.
Walinyata taratibu, sasa walifika mlangoni,
kwenye mlango wa ghala la silaha. Salehe
alikuwa anahangaika kufungua mlango, kwa
kutumia funguo waliyokuja nayo. Mlango ulikuwa
unaelekea kufunguka.....
Daniel Mwaseba alirudi ndani kwa mwendo uleule
wa kunyata. Alienda moja kwa moja katika
chumba kikichohusika na kuzalisha umeme.
Alimkuta askari akiongea na simu.
Alimsogelea taratibu bila kutoa sauti yoyote,
alimpiga karate moja ya nguvu ya shingo askari
yule, karate iliyompeleka askari yule chini. Askari
yule hakuweza kabisa kuistahamili karate ya
Daniel Mwaseba.
Askari alizimia !
Kule kwa kina Salehe.
Ghafla, umeme uliwaka!
Meja Badi Bwino, Salehe na yule Dada walipigwa
na butwaa, waliishiwa nguvu kabisa.
Walikuwa wanatetemeka!
Hawakuelewa kitu gani kimetokea. Sasa
walikuwa wapo kwenye mwanga mkali huku
wakiwa hawajui adui yupo wapi?
Bastola zao sasa zilikuwa kama midoli tu
mkononi.
Hazikuwa na kazi.
Ghafla! Umeme ulizimika tena!
Wote watatu walipumua kwa nguvu.
Ilikuwa kama miujiza !
Ilikuwa kama ndoto !
Ilikuwa giza!
Ikaja nuru!
Limerudi giza!
Kurejea kwa giza ilikuwa kama ruhusa kwa
Salehe aendelee kufungua tena ule mlango.
Alifungua huku akitetemeka vibaya sana!
Geti lilifunguka!
Ndani kulikuwa na giza totoro!
Ghafla nuru ilirejea tena!
Daniel Mwaseba alikuwa anawachezea mchezo
watu wale.
Mara ya pili ulivyowaka ilikuwa picha mbaya sana
kwa Salehe, Meja Swalo Mbombwe na yule Dada.
Walikuwa mbele ya askari thelathini walioshika
bunduki imara mikononi mwao.
Bunduki thelathini ziliwaelekea Meja Badi Bwino,
Salehe na yule Dada vifuani kwao.
Kina Salehe walikamatwa kirahisi sana !
Daniel alikuja kwa nyuma yao. Kina Salehe
hawakuamini macho yao kumuona Daniel
Mwaseba pale.
Sasa walijua, aliyekuwa anawadungua mmoja
baada ya mwengine alikuwa Daniel Mwaseba.
Wote Walikiri,
Daniel Mwaseba alikuwa mtu hatari sana!
Kwa mara nyingine tena, Daniel alifanikiwa
kuliokoa Taifa la Tanzania kwenye hila mbaya za
watu wabaya sana!
Salehe na kundi lake walikamatwa, walisafirishwa
kwa helkopta kuelekea Dar es salaam usiku
uleule.
Huko Dar es salaam, Ispekta Jenerali wa Polisi,
IJP John Rondo alikuwa kalala fofofo. Baada ya
kupigiwa simu za makamanda wa mikoa ya Mara,
Kigoma na Mbeya, na kupewa taarifa mbaya za
mauaji ya raia wema, alichanganyikiwa sana.
Hakuamua kuzima simu tu, alitoa kabisa na betri
yenyewe toka katika simu yake.
IJP Rondo aliamua kwenda Baa kunywa bia ili
kupunguza mawazo.
Hakunywa bia chache.
Alimimina kwa pupa kwenye tumbo lake pana bia
ishirini na mbili.
Alilewa sana!
Alijikongoja hadi nyumbani kwake na kukaa
sofani. Aliwasha televisheni, hakuwahi kuangalia
chochote, alipitiwa na usingizi palepale sebuleni,
huku televisheni ikiongea kwa sauti kubwa. Lakini
yeye hakuisikia.
Wakati Daniel Mwaseba akipambana na wauaji
kule msituni, IJP Rondo alikuwa kalala usingizi
mzito sana nyumbani kwake !
Simu iliyopigwa asubuhi ndiyo iliyomuamsha IJP
Rondo.
"Halloo mkuu"
"Hallo inspekta"
"Njoo kituo cha Polisi cha kati afande kuna
habari kubwa" IJP alipata mstuko mkubwa sana,
akihisi wale wauaji wamefanya tukio kubwa
lengine.
"Kuna nini Inspekta?"
"Daniel Mwaseb.." Inspekta hakumalizia kusema.
"Amekufaaa ?"
"Hajafa afande, Daniel Mwaseba amefanikiwa
kuwakamata wahalifu"
"Wahalifu gani hao?"
"Wale wakiotumia sumu ya Proxine kuuwa !"
"Whaaaaaaaaat?, nakuja sahivi."
Pombe zilimtoka IJP John Rondo.
Alienda kituoni.
***************
Wakati IJP Rondo akiwa kituo cha Polisi cha kati
kuwahoji wauaji wale. Daniel Mwaseba alikuwa
angani kuelekea jijini Arusha, kwa Abdul.
Daniel alikuwa na furaha sana kumuokoa kijana
yule dhaifu kwenye mdomo wa kifo cha watu
hatari.
Alimkuta Abdul, na Abdul alimshukuru sana
Daniel.
"Pongezi hizi zinakuhusu pia Abdul, wewe,
Mayasa na Raiya mnastahili pongezi hizi.
Mmefanikisha kugundulika kwa njama hatari
sana. Angamizo lingetuangamiza kweli! Fikiria
nchi ingejilindaje toka kwa maadui zake bila
silaha. Tungekuwa watumwa, tungepata hasara
kubwa sana. Abdul, wewe ni shujaa !
Mayasa, na Raiya ni mashujaa. Mungu awalaze
mahali pema mashujaa wale wa kike!"
*************
Abdul aliamua kuahirisha mwaka wa masomo
pale chuoni, na kuamua kurudi nyumbani
Bagamoyo, kupumzika kwa wazazi wake.
Aliongozana na Daniel kuelekea Bagamoyo.
Njiani Daniel alikumbuka kuwa alikuwa na deni
Bagamoyo. Deni la kumlipa Mzee Washiro na
mkewe kwa wema waliomfanyia. Alipanga baada
ya kumpeleka Daniel nyumbani kwao, lazima
aende kwa Mzee Washiro kutimiza ahadi yake.
Ingawa hakujua atampa zawadi gani Mzee
Washiro na mkewe. Lakini aliamua kwenda.
Waliwasiri Bagamoyo jioni. Daniel na Abdul
walichukua teksi kuelekea nyumbani kwa Abdul.
Njiani Daniel hakuwa na wasiwasi wowote na
uelekeo wakioufuata.
Hakuwa anaijua njia ya kuelekea kwa Mzee
Washiro. Aliletwa akiwa mfu, na alirudi kwa
ndege ya jeshi.
Walipoikaribia ile nyumba Daniel alipakumbuka.
"Hivi unaitwa Abdul nani?"
"Naitwa Abdul Washiro"
Daniel alipigwa na butwaa.
"Vipi kaka Daniel?"
"Wazazi wako ni watu wema sana, na wana
mchango mkubwa katika kufanikisha operesheni
hii"
"Wamefanyaje kwani?"
"Utajua tukifika"
Baada ya kufika nyumbani kwa Washiro pande
zote mbili zilikuwa na furaha sana.
Hawakutegemea kabisa.
Daniel alimsaidia Abdul bila kumjua, na
Mzee Washiro alimsaidia Daniel bila kujua.
Mzee Washiro alimsimulia Daniel juu ya dhiki
iliyoota mizizi katika familia yake.
Daniel aliahidi kuwasaidia.
Baada ya mwezi mmoja kulikuwa na tafrija
ndogo Bagamoyo, Daniel alikuwa anamkabidhi
mzee Washiro nyumba bora ya kisasa.
Aliyoinunua kama kulipa fadhila kwa wema
waliomfanyia familia ile.
Mbele ya nyumba ile kulikuwa na fremu kubwa
ambayo Daniel alipanga kuwafungulia duka
kubwa la vifaa vya magari.
Tafrija ilifana sana pale sebule kwenye sebule ya
kisasa. Mzee Washiro na familia yote kwa ujumla
walimshukuru sana Daniel.
Saa mbili kasoro. Daniel alipigiwa simu. Simu
ilitoka kwa IJP Rondo ikimsisitiza asikose
kuangalia taarifa ya habari.
Saa mbili kamili, Ilipoanza taarifa ya habari
iliwanyamazisha watu wote pale sebuleni.
"....mawaziri watatu, na watu wengine watano
wamehukumiwa hukumu ya kunyongwa hadi
kufa !. Mawaziri hao wakishirikiana na watu
wengine watano...."
Hawakusubiri taarifa ile iishe. Watu wote
waliripuka kwa shangwe na kumkumbatia Daniel
Mwaseba !
"Wewe ni shujaa pia Daniel!" Abdul Washiro
alisema huku chozi zito likimdondoka.
Mawaziri watatu, Salehe, Meja Badi Bwino,
Kerspersky, yule Dada, na askari mzima umeme
ghalani, walihukumiwa kunyongwa hadi kufa!
MWISHO
 
Back
Top Bottom