Kujiheshimu na kuwaheshimu wengine
Katika Uislamu kila mtu anayo haki ya kuheshimiwa. Heshima
ni haki ya mwanaadamu aliyozaliwa nayo. Miongoni mwa mambo ya
msingi aliyousia Mtume (s.a.w) katika khutuba yake ya kuaga aliyoitoa
katika uwanja wa Arafa 9 Dhul-Hijjah 10A.H, ni kulinda heshima ya kila
mtu. Aliusia:
Enyi watu hakika damu yenu (yaani uhai wenu), mali zetu na
heshima yenu ni vitu vitakatifu kamwe visiharibiwe hadi
mtakaposimamishwa mbele ya Mola wenu, kwa utukufu wa vitu hivyo ni
kama ulivyo Utukufu wa siku hii, na mwezi huu na mji huu. Kwa
hakika mtakutana na Mola wenu na atakuulizeni juu ya vitendo vyema.
Je, nimefikisha ujumbe? Ee! Allah shuhudia.
Kuwaheshimu watu wa dini nyingine kwa kutowabughudhi,
kutowadharau au kutowadhalilisha kwa namna yoyote ile:
Wala msiwatukane ambao wanaabudu kinyume cha Allah, wasije
wakamtukana Allah kwa jeuri zao bila kujua.... (6:108).
Waite (watu) katika njia ya Mola wako kwa hekima na mawaidha mema,
na ujadiliane nao kwa namna iliyo bora. Hakika Mola wako ndiye
anayemjua aliyepotea katika njia yake.. (16:125).