PENZI LENYE MAUMIVU-10
Mtunzi:Juma Hiza
Simu:0712988278
Sikutaka kupoteza muda tena, nilichokuwa nikitaka kuona ni Lydia akiuwawa kama alivyouwawa Christopher. Niliamini kwa kufanya hivyo siri isingeweza kufichuka.
Kama ilivyokuwa kawaida nikampa dili hilo Maxwell huku nikimuahidi kumlipa kiasi kikubwa cha pesa mara mbili ya aliyokuwa akitaka nimlipe.
“Hii kazi sio ngumu hata kidogo mkuu,” aliniambia Maxwell huku akionekana kujiamini kupita kawaida. Hilo lilizidi kunipa matumaini na kuamini kwa asilimia mia moja kuwa ni lazima Lydia angeuwawa na ushahidi wote kupotea.
Ili kuifanikisha kazi hiyo Maxwell alihitaji taarifa za kina kuhusu msichana huyo, hilo halikuwa tatizo, nilimueleza kila kitu.
Lydia alikuwa akiishi Sinza, maisha yake yalitawaliwa na starehe kwa asilimia kubwa, kila wikiendi alikuwa ni mtu wa kwenda klabu. Huko alijichanganya na kutembea na wanaume tofauti tofauti ambao ndiyo walikuwa wakimpa pesa.
Alikuwa ni msichana mzuri mwenye shepu iliyojaa mvuto alikuwa nayo. Mwili wake ulikuwa mwembamba huku kwa mbali hipsi zake zikiwa zinaonekana. Pamoja na shepu yake lakini aliutumia uzuri wake kama rasilimali kwa kutembea na wanaume ambao walikuwa wakimpa pesa kwa maana nyingine tunasema alikuwa ni danga hapa mjini.
Mpaka kufikia muda huo Maxwell alishafahamu ni kitu gani ambacho alitakiwa kukifanya kwa msichana huyo. Akatabasamu kidogo kisha akaniahidi kuifanikisha kazi hiyo kama nilivyotaka.
Nilifanya mambo yote haya huku lengo langu likiwa ni kumpa maumivu Getrude moyoni mwake, kifo cha Christopher ambaye ndiye alikuwa mpenzi wake niliamini kilikwenda kumpa maumivu makali mno. Maumivu hayakuishi kwa mpenzi wake tu, baada ya kupita siku kadhaa mwili wa rafiki yake Lydia nao ulikutwa ukiwa tayari maiti ndani ya chumba cha hoteli moja ya kifahari iliyokuwepo hapa jijini Daresalaam. Mwili wake ulijeruhiwa sehemu kubwa huku macho yakiwa yametolewa.
Mpaka kufikia muda huo niliamini mpango wangu ulifanikiwa kwa asilimia mia moja, Getrude alikuwa katika kipindi kigumu cha kuondokewa na mpenzi wake pamoja na rafiki yake kipenzi. Hilo ndilo nililokuwa nikihitaji kuliona kwa wakati huo.
Baada ya jeshi la polisi kufanya uchunguzi wake wa kina ilibidi wamuhoji Getrude kwani tayari mauaji hayo yalionekana kuwa na utata ndani yake. Watu waliyokuwa wakiuwawa walikuwa ni watu wake wa karibu tu.
Baada ya mahojiano hayo kufanyika mtu ambaye alimtaja kama anayemuhisi kuhusika na mauaji hayo alikuwa ni mimi.
Nakumbuka nilikuwa nyumbani kwangu, siku hiyo nilionekana kuwa mwenye furaha mno kushinda siku zote nilizowahi kuwa na furaha katika maisha yangu mpaka mke wangu akawa ananishangaa, siku hiyo nilizidisha mapenzi mpaka kuna muda nikaonekana kuwa wa tofauti maana sikuzoeleka kuwa katika hali kama hiyo.
Huku mke wangu akiwa hajui hili wala lile mara Polisi wawili waliyovalia mavazi ya kiraia waliingia ndani, wakajitambulisha kuwa wao ni Polisi kwa kuonyesha vitambulisho vyao, walipofahamu kuwa mimi ndiye Kelvin wakaniambia kuwa nilikuwa nikihitajika kituoni.
Mke wangu alishangaa, hakujua ni nini kilichokuwa kimetokea kwa wakati huo, kitendo cha kuwaona Polisi wakiwa ndani ya nyumba yetu huku wakinitaka niongozane nao hadi kituoni kilimshtua mno, kama ilivyokuwa kawaida yake machozi yakaanza kumdondoka mashavuni mwake.
“Jamani amefanya kosa gani mume wangu?” aliwauliza huku machozi yakiendela kumdondoka.
“Usijali ataenda kujulia kituoni, kwasasa tunaomba tufanye kazi yetu iliyotuleta hapa,” alisema Polisi mmoja kwa msisitizo.
Hakukuwa kuna muda wa kupoteza, walichokuwa wakikihitaji Polisi kwa wakati huo ni kuondoka na mimi mpaka kituoni, hilo sikutaka kupinga, kwa kuwa nilijiamini, nilifuata vile walivyotaka, nikaondoka nao mpaka kituoni.
Mke wangu alikuwa kama mtu aliyechanganyikiwa, hakujua ni nini ambacho alitakiwa kukifanya.
“Unatuhumiwa kwa kesi ya mauaji ya watu wawili,” aliniambia Polisi mmoja mara baada ya kufika kituoni, nikaingizwa kwenye chumba maalum halafu nikaanza kuhojiwa.
“Mauaji?” nilimuuliza huku nikionekana kushangaa, nilionekana kama mtu ambaye nilikuwa sifahamu lolote lililokuwa limetokea.
“Ndiyo,” alinijibu huku akionyesha msisitizo.
“Hapana afande sihusiki katika hilo,” nilimwambia huku nikimuaminisha.
Kwa muonekano ambao niliuonyesha ilikuwa sio rahisi kuamini kwamba mimi ndiye niliyehusika kumtuma mtu akafanye mauaji hayo, kila swali ambalo niliulizwa nililikanusha, sikuwa tayari kukubali kirahisi kesi hiyo ya mauaji.
Kipindi kesi hiyo ikiendelea mke wangu alikuwa ni mtu wa kusali na kuomba Mungu usiku na mchana, hakutaka kuona nikifungwa.
“Naamini tutashinda kesi hii mume wangu, Mungu anatupitisha katika kipindi hiki cha majaribu ili azipime imani zetu, tumuamini yeye ndiye atakayetusaidia,” aliniambia Lillian.
“Sawa nimekuelewa,” nilimwambia huku nikionyesha sura ya huruma.
Kitu ambacho alikuwa akikifahamu ni kwamba kesi hiyo nilisingiziwa na mtu aliyenisingizia alikuwa na lengo la kunichafua. Hilo aliliamini na ndiyo sababu iliyomfanya akawa ananiombea usiku na mchana huku akimlaani mtu huyo vikali, hakujua upande wa pili kama kweli nilihusika.
Siku ziliendelea kukatika, Polisi nao wakaendelea kufanya uchunguzi wao juu ya kesi hiyo ambayo ilikuwa ikinikabili. Nilitumia pesa kuwahonga Polisi pamoja na wanasheria na mwisho wa siku kesi hiyo iliweza kufutwa hapa ni baada ya kuonekana sina hatia yoyote.
Kilikuwa ni kipindi ambacho Getrude hakutaka kuamini kile kilichotokea, japokuwa aliamini mimi ndiye niliyehusika na mauaji hayo lakini hakukuwa kuna mkono wa sheria tena, kila kitu kilikuwa ndani ya uwezo wangu.
“Haya ndiyo maumivu ambayo nilitamani uyasikie na wewe, nilitaka uyaonje maumivu ambayo ulinipa,” nilimwambia Getrude huku nikiamini hakuwa na sehemu nyingine ya kukimbilia.
“Umenifungulia kesi ya mauaji, nimeshinda, hii yote inaonyesha ni jinsi gani nilivyokuwa nina nguvu na uwezo, kwangu hakuna kitu kinachoshindikana,” nilimwambia huku nikijisifia, nilijiona kuwa mshindi.
Maumivu aliyoyapata Getrude niliyafurahia kwasababu nilitaka na yeye aumie kama alivyoniumiza, kitendo cha kutumia pesa zangu na mwanaume mwingine kiliniudhi na ndiyo sababu iliyosababisha mpaka nikafanya mauaji.
Kweli mapenzi yana nguvu na wala usishangae mimi kufanya haya yote, nilifanya kwasababu ya mapenzi. Usaliti ambao alinifanyia Getrude uliniumiza kiasi kwamba naweza kusema nilisahau kabisa kwamba na mimi nilikuwa nikimsaliti mke wangu kwa kutembea naye.
Naamini nitachukiwa na kila mtu ila ukweli ni kwamba moyo wangu ulikuwa katika maumivu katika kipindi hicho, sijui niseme nini ila baada ya kufanikiwa kumtuma Maxwell kufanya mauaji moyo wangu ulikuwa na furaha, maumivu ambayo ulikuwa umeyaonja yalipungua, hapa ni baada ya kumuona Getrude na yeye akiumia mara mbili yangu.
****
Baada ya kupita sekeseke la kesi hiyo ya mauaji iliyokuwa ikinikabili, maisha yaliendelea huku furaha ikionekana kushika hatamu kwa upande wa familia yangu.
Niliishi maisha ya furaha lakini kila nilipokuwa nikimuona Brighton nilikuwa nikijisikia vibaya moyoni mwangu. Kuna kipindi hata kuwaita matajiri wenzangu waje kumuona niliona aibu maana alionekana kuwa kama kituko.
Kwa jinsi alivyokuwa akionekana Brighton hakufanania kabisa kuwa na baba kama mimi ambaye nilikuwa na muonekano mzuri, sijui hata alirithi sura na ulemavu kutoka kwa nani?
NENO LANGU;
Napenda kuwapa pole wale wote waliowahi kuumizwa mapenzini mwaka huu, waliowahi kunyanyasika kwa kuwa hawakuwa na kitu fulani, wanachuo na wanafunzi ambao walikaa nyumbani kwa kuwa walikosa ada huku masomo yakiendelea, wale ambao waliwaamini wapenzi wao japokuwa walikuwa wakisalitiwa, wale ambao walijua thamani ya mapenzi ingawa wao kamwe hawakuonyeshewa thamani hiyo. Pia nawapa pole wale wote ambao mwaka mzima walikosa furaha na amani, waliotengwa kwa kuwa walikuwa na udhaifu fulani au ulemavu miilini mwao, wale ambao walidiriki kupenda pale ambapo kamwe hawakupendwa. Poleni sana, amini kwamba Mungu Yu pamoja nanyi.