SEHEMU YA 35...
Huo ndiyo ulikuwa mwanzo wa ukaribu wao. Wasichana wengi walionekana kuumizwa na ukaribu wa Tatiana na Nathan kwa kuwa kila mmoja alitaka kuwa karibu na mvulana huyo aliyekuwa na sura nzuri.
Kwa Maria ndiye aliyeonekana kukasirika zaidi, wivu mkali ukamkamata moyoni mwake, alimpenda mno Nathan na hakutaka mvulana huyo awe na msichana yeyote zaidi yake.
Kitendo cha Tatiana kuanzisha ukaribu na Nathan tayari kwake kukawa na maumivu makali ya moyo kiasi kwamba kila alipokuwa akiwaona, alisikia kitu chenye ncha kali kikiuchoma moyo wake.
Taratibu chuki ikaanza kujengeka dhidi ya Tatiana, hakutaka kumshikia fimbo yake na kumuongoza tena kama ilivyokuwa zamani, alichokifanya ni kumsusa hivyo Nathan kuchukua jukumu hilo ambalo likamfanya kuwa karibu zaidi na msichana huyo.
Siku zikaendelea kukatika, japokuwa kila mmoja alikuwa muimbaji lakini waliikubali sauti ya Tatiana ambayo iliwasisimua wote waliokuwa wakiisikia. Sauti ile ikawavunja moyo na kuona kwamba ilikuwa ni lazima wao kuwa wasindikizaji na msichana huo kuchukua ushindi katika shindano hilo.
“Unajua kuimba,” alisema Nathan.
“Nashukuru! Hata wewe unajua.”
“Najua ila si kama wewe. Unanifurahisha sana, unautetemesha mtima wa moyo wangu kila nikusikiapo,” alisema Nathan huku akimshika mkono Tatiana pale walipokaa, Tatiana akashtuka.
“Nathan! Kuna nini?”
“Sikiliza Tatiana!”
“Kuna nini?”
“Nimeshindwa kuvumilia.”
“Kuvumilia nini?”
“Nataka nikwambie ukweli wa moyo wangu,” alisema Nathan.
“Ukweli upi?”
“Kwamba ninakupenda.”
“Unanipenda?”
“Ndiyo! Ninataka nikuoe kama ikiwezekana,” alisema Nathan, moyo wa Tatiana ukapiga paaaaaaa! “Unataka......”
“Nikuoe! Usiwe na wasiwasi, ninataka niwe nawe, haijalishi tutaishi wapi, ukitaka Tanzania, sawa, Liberia, sawa pia ila ukweli, popote pale lakini mwisho wa siku nataka kuwa na wewe, uwe mama wa watoto wangu,” alisema Nathan, hapohapo Tatiana akaanza kububujikwa na machozi, maneno aliyoongea Nathan, yaliugusa moyo wake.