Penzi bila maumivu

Penzi bila maumivu

SEHEMU YA 42...
Ili kuonyesha ni jinsi gani alikuwa amedata kwa penzi la msichana huyo, kila siku alikuwa akielekea sehemu ya mazoezi, alipofika huko, alikuwa kimya pembeni akiwaangalia wanamuziki hao waliokuwa wakifanya mazoezi kwa nguvu zote.

Ukaribu wa Tatiana na Nathan ukamtia mashaka, ukamfanya kuanza kuona wivu kupita kawaida, kila alipokuwa akiwaangalia, ukaribu ule ukaanza kumuumiza mno. Hakujua kama watu hao walikuwa wapenzi au marafiki kama walivyokuwa wengine, alichokifanya ni kuanza kufuatilia.

Kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kumfuatilia Nathan. Akagundua kwamba mvulana huyo alikuwa ametoka nchini Liberia katika Jiji la Monrovia hivyo hakuwa na haki ya kuwa na msichana huyo kwani yeye ndiye alikuwa mtu wa kwanza kumuona nchini Tanzania.
Hakutaka kuendelea kuumia zaidi, alichokifanya ni kuanza mishemishe za kuonana na Tatiana. Siku ambayo walichukuliwa na kupelekwa katika Jimbo la Nevada ndani ya Jiji la Las vegas, hapo ndipo alipoamua kumfuata hotelini ili japo apate nafasi ya kumwambia kile kilichokuwa kikiendelea moyoni mwake.
Alipokwenda hotelini na kuitiwa msichana huyo, mapigo yake ya moyo yakaanza kumdunda mno, akahisi akizidi kumpenda msichana huyo zaidi ya kipindi kilichopita. Kila alipokuwa akimwangalia, uso wake ulijawa na tabasamu pana kiasi kwamba akajiona kushindwa kuvumilia kwa mapenzi yake.

“Niambie kuna nini,” alisema Tatiana huku akinywa maziwa aliyoletewa.
“Tatiana...”
“Abeeee.”
“Kuna kitu ninataka kukwambia, nimeshindwa kuvumilia, naomba nijiweke wazi kwamba nina....” alisema Smith na kukaa kimya.
“Una nini?”

“Ninakupenda mno, ninataka uwe mke wangu wa ndoa,” alisema Smith.
Moyo wa Tatiana ukashtuka, hakutegemea kusikia kile alichokuwa amekisikia mahali hapo, alihisi kama masikio yake yalizembea kusikiliza kile alichokizungumza Smith mbele yake, akauliza tena na tena lakini jibu la Smith lilikuwa lilelile kwamba alikuwa akimpenda kwa mapenzi ya dhati.
“Smith....”
 
SEHEMU YA 43...
“Naomba usiniambie neno la kuniumiza Tatiana, nimetokea kukupenda tangu nilipokuona kwa mara ya kwanza nchini Tanzania, umekuwa msichana mwenye uzuri wa ajabu ambaye siwezi kumuacha akapita, Tatiana, umeuteka moyo wangu, sitaki kuona ukiolewa na mtu mwingine tofauti na mimi, ninakupenda Tatiana,” alisema Smith huku akimshika Tatiana mkono wake uliokuwa juu ya meza.
“Hapan Smith...” alisema Tatiana huku akianza kububujikwa na machozi.
“Kwa nini hapana? Kwa nini unataka kuniumiza hivi?”
“Smith....nina mpenzi...”

“Hapana Tatiana, siwezi kuamini hilo, nimekuwa nikikufuatilia kwa kipindi kirefu, ni bora kama unanikataa unikatae kwa sababu nyingine lakini si kunidanganya kwamba una mpenzi. Tatiana, ninataka kukufanya kuwa mke bora, naomba uwe mpenzi wangu na mwisho wa siku nikuoe,” alisema Smith huku naye akianza kububujikwa na machozi.
Hicho kilikuwa kipindi kigumu katika maisha yake, hakuamini kile kilichokuwa kikiendelea, iweje wanaume wawili watokee ghafla katika maisha yake na kumwambia kwamba walikuwa wakimpenda?

Hapo ndipo alipoanza kumkumbuka Peter, mwanaume wa kwanza kumwambia kwamba alikuwa akimpenda kwa mapenzi ya dhati, huyo ndiye aliyekuwa na moyo wake, huyo ndiye aliyekuwa amemteka vilivyo, hakujua sababu ya wanaume hao kuibuka ghafla namna hiyo.
“Naomba nikupe muda wa kujifikiria, na hongera sana kwa sauti nzuri uliyobarikiwa,” alisema Smith na kisha kumuinua msichana huyo kumrudisha ndani ya hoteli.
 
SEHEMU YA 44...
“Wewe ni mpenzi wangu Tatiana, haiwezekani kuona ukiolewa na mtu mwingine, siwezi kuona harusi hii ikitokea,” ilisikika sauti ya mwanaume mmoja akiongea kwa hasira sana huku mkononi akiwa ameshika chupa ya pombe kali aina ya John Walker.

Mwanaume huyo alisimama katika mlango wa kanisa, alionekana kuwa mlevi, nywele zake zilikuwa timutimu. Kanisani hapo kulikuwa na watu wengi waliokuwa wamekuja kuhudhuria harusi iliyokuwa imetangazwa sana kati ya Tatiana na mwanaume wa Kizungu. Msichana Tatiana alisimama mbele ya kanisa hilo huku akiwa na mwanaume wa Kizungu aliyevalia suti nyeupe.

Ilikuwa ni siku ya harusi yake, mwanaume huyo wa Kizungu alikuwa Smith aliyekuwa kwenye mshangao mkubwa mara baada ya kumuona mwanaume huyo mlevi akiingia kanisani na kutaka mchungaji asifungishe ndoa, alikuwa Peter.
Kichwani akawa na mawazo, mwanaume yule alikuwa nani na alikuwa na uwezo gani wa kusimamisha ndoa ile isifanyike? Kila alipojiuliza, alikosa jibu kabisa.
Tatiana hakuzungumza kitu, alikuwa akimwangalia mwanaume yule huku akiwa kimya kabisa, kilio cha kwikwi kikaanza kusikika kutoka kwake, alikuwa kwenye kipindi kingine kigumu kuliko vipindi vyote maishani mwake.

Wazazi wake ambao walikuwa kwenye viti vya mbele kabisa walibaki wakimwangalia mwanaume yule aliyeonekana kuwa chakari kutokana na pombe kali alizokuwa akinywa.
Huku kanisa likiwa limetaharuki, mara mtu mwingine akaingia kanisani humo akiwa hoi, mwili wake ulijeruhiwa na alikuwa na bandeji kubwa mwilini mwake. Alipomuona, alimkumbuka vilivyo kwamba mwanaume huyo alikuwa Nathan, alisimama kule mlangoni na kuanza kuzungumza kwa sauti kubwa,
“Tatiana....” alianza kusema Nathan na kuendelea:

“Hata kama umenifanyia hivi, kuniua ili uolewe na huyu Mzungu wako, kumbuka ni jinsi gani ninakupenda, kumbuka ni jinsi gani tulivyokuwa pamoja,” alisema Nathan, watu wote waliokuwa kanisani wakabaki kimya.

Smith alionekana kuwa na hasira mno, kila alipokuwa akiwaangalia watu hao alishikwa na hasira zaidi hali iliyompelekea kuchomoa bunduki yake iliyokuwa kiunoni na kisha kuanza kuwasogelea watu wale.
 
SEHEMU YA 45...
Kila mmoja akagundua kile kilichokuwa kikitaka kutokea, kwa kasi ya ajabu, Tatiana akaanza kumfuata Smith, alipomfikia, akamshika mkono ili asifanye kile alichotaka kufanya. Hiyo haikuweza kuzuia, alichokifanya Smith ni kuwanyooshea bunduki na kisha kuwafyatulia risasi.

“Noooooooooo......” alipiga kelele Tatiana.
Ilikuwa ni moja ya ndoto mbaya na iliyomsisimua kupita kawaida. Alikuwa akipiga kelele zilizomfanya Angelina kushtuka kutoka usingizini na kumwangalia rafiki yake huyo. alichokifanya ni kumuuliza nini kilikuwa kimetokea lakini Tatiana hakujibu kitu chochote zaidi ya kulia tu.
“Tell me what’s wrong with you,” (Niambie una nini?)
“It was a nightmare,” (Ilikuwa ndoto mbaya)
“Oooh! It was just a nighmare, don’t cry Tattie,” (Oooh! Ilikuwa ndoto mbaya tu, usilie Tattie) alisema Angelina huku akimkumbatia.
Tatiana hakuwa na raha tena, moyo wake ulikuwa kwenye mawazo mazito juu ya ile ndoto mbaya aliyokuwa ameiota, moyo wake ulimuuma sana kwani hakutegemea kitu kama kile kutokea katika maisha yake.

Aliichukulia ndoto ile kuwa miongoni mwa ndoto mbaya na hakika isingeweza kuwa kweli kwani piga ua alijiahidi kutokuolewa na mwanaume yeyote yule zaidi ya Peter aliyemuacha nchini Tanzania.
Siku ziliendelea kukatika kama kawaida. Shindano lile liliendelea kwenda mbele kama kawaida na walipobaki watu hamsini wa mwisho, kwa bahati mbaya kwake, Nathan akawa amechujwa katika shindano hilo na kutakiwa kurudi nchini kwake huku akikabidhiwa kitita cha dola elfu kumi (zaidi ya milioni ishirini) kama kifuta jasho.

Fedha halikuwa tatizo katika maisha yake, alitoka familia ya mzee aliyekuwa na fedha nyingi nchini Liberia. Baba yake alikuwa miongoni mwa watu waliokuwa na fedha nyingi kwa kujishughulisha na biashara ya madini huku akimiliki migodi mbalimbali ya almasi nchini humo.
“Tatiana, siwezi kuondoka, bado ninahitaji kuwa karibu nawe,” alisema Nathan.
 
SEHEMU YA 46...
Hilo halikuwa tatizo kwa Tatiana lakini suala la kuendelea kubaki ndani ya hoteli hiyo ilikuwa kinyume ya kile kilichokuwa kikiendelea na kilikuwa nje ya uwezo wa Tatiana. Kuwa karibu na msichana huyo hakuzuiliwa lakini hakutakiwa kuwepo ndani ya hoteli hiyo kwa kuwa hakuwa mshiriki tena.

Kila kitu kikaonekana kuwa kigumu kwa Nathan, kile kilichokuwa kikiendelea kilimuumiza mno kwani ilikuwa ni lazima arudi nyumbani na amuache msichana huyo nchini Marekani.
Kitu kilichomuumiza mno kichwa ni kwamba mpaka kipindi hicho msichana huyo hakuwa amekubaliana naye kama alikuwa tayari kuwa naye kimapenzi au la, alitakiwa kuondoka kurudi Liberia.
Hiyo ikawa nafasi kubwa kwa Smith, kitendo cha Nathan kuondolewa nchini hapo, moja kwa moja akamfuata Tatiana na kumwambia kwamba alitaka kumleta mtu maalumu kwa ajili ya kumsaidia katika kila kitu likiwemo suala la kumuongoza kila atakapotaka kwenda na gharama zote zingekuwa chini yake.
Tatiana akakubaliana naye na kazi kuanza mara moja. Kila siku wawili hao wakawa wakikutana, Smith alijitahidi kumuonyeshea Tatiana kwamba alikuwa akimpenda kwa kumaanisha na hakuwa akimtamani hata mara moja.

Mapenzi yalimlevya hivyo akataka Tatiana naye awe katika hali hiyo jambo lililohitaji kazi kubwa tena ya kujitoa mpaka aingie katika ulimwengu wa mapenzi kama alivyokuwa yeye.
Baada ya siku wiki chache, tayari watu walioingia kwenye tano bora wakajulikana, kulikuwa na Waafrika wawili tu, yaani Tatiana na msichana Febby Grace kutoka nchini Ghana. Shindano lilikuwa kubwa na lilileta sana msisimko.

Katika hatua hiyo, walichukua mwezi mzima kujiandaa huku wakitembezwa sehemu mbalimbali na kukutanishwa na walimu wengi wa muziki ambao wote hao waliushangaa uwezo mkubwa aliokuwa nao Tatiana.

Alikuwa na sauti nzuri mno, kila alipokuwa akiimba wimbo wowote ule, sauti ilipangiliwa kiasi cha walimu kukiri kwamba hawakuwahi kukutana na mtu aliyekuwa na sauti nzuri kama Tatiana.
“Sitochoka kukwambia kwamba nakupenda Tatiana,” alisema Smith, hayo yalikuwa maneno yake ya kila siku alipokuwa akikutana na Tatiana.
 
SEHEMU YA 47...
“Najua.”
“Unanipenda?”
“Swali gumu sana Smith.”
“Lakini linaweza kujibika, si ndiyo?”
“Naomba uniache kwa kipindi hiki, si unajua siyo kizuri sana?”
“Najua, lakini hebu niambie japo niridhike,” alisema Smith.
“Nitakujibu.”
Hilo halikuwa tatizo, Smith hakutaka kuwa na haraka, aliamini kwamba ilikuwa ni lazima Tatiana akubali kuwa naye na hatimae amuoe na kuwa mke wake. Hakujali kama msichana huyo alikuwa na mpenzi wake au la, alichokuwa akikijua yeye ni kwamba kuna siku msichana huyo angekuwa mpenzi wake tu.

Siku ziliendelea kukatika na hatimaye siku ambayo fainali ilitakiwa kufanyika ikatangazwa, watu wote duniani wakaanza kuisubiria kwa hamu. Tatiana alionekana kuwa na wasiwasi moyoni mwake lakini kila siku Smith alikuwa na jukumu kubwa la kumtia moyo kwamba angeshinda shindano hilo.

“Niamini Tatiana, unajua sana, wewe ni bora zaidi ya hawa wote,” alisema Smith huku akimwangalia Tatiana usoni.
“Kweli?”
“Ndiyo! Wewe ni bora zaidi ya mtu yeyote yule,” alisema Smith.
Maneno yale yakamtia moyo Tatiana, hakuamini kama angeweza kupata mtu ambaye angemtia moyo namna ile katika kipindi kigumu kama kile ambacho alihitaji faraja kubwa kutoka kwa mtu wake wa karibu.

Pasipo kupenda, pasipo kulazimishwa, Tatiana akajikuta akimbusu Smith shavuni na kuhama kisha kuanzakubadilishana mate. Moyo wake ukabadilika, hakumkumbuka tena Peter, mtu ambaye alikuwa naye kwa karibu kipindi hicho alikuwa Smith tu na ndiyo maana alikuwa radhi kumpa ladha ya mate yake kwa mara ya kwanza kabla ya mwanaume yeyote yule, naye, mapenzi yakaanza kumchanganya huku Peter akisahaulika kwa kasi.
 
SEHEMU 48....
Japokuwa shule zilikuwa zimefunguliwa lakini Peter hakutaka kurudi shuleni, moyo wake ulikuwa na hamu ya kujua juu ya lile shindano ambalo kila wiki lilikuwa likionyeshwa katika televisheni.
Moyo wake ulifurahi mno, kitendo cha kuona Tatiana akiendelea kuwa juu kutokana na umahiri wake kilimpa moyo sana kwa kuona kwamba msichana huyo angefanikiwa na kuchukua ushindi katika shindano lile.

Kura za awali zilionyesha kwamba Tatiana alikuwa akiongoza kwa asilimia 70 tofauti na wengine ambao waligawana hizo thelathini zilizobakia. Tatiana alipendwa na kila mtu, si kwa hali yake tu aliyokuwa nayo bali hata uzuri wake katika uimbaji uliwafanya watu wengi kuamini kwamba msichana huyo alizaliwa akiwa na kipaji cha kuimba.
Peter alikuwa makini, alipenda kufuatilia kila kitu kuhusu msichana huyo. Wazazi wake walijua kila kitu kilichokuwa kikiendelea, walifahamu ni kwa namna gani Peter alikuwa akimpenda msichana Tatiana hivyo hata alipokuwa bize na televisheni badala ya kwenda shule alipokuwa akisoma, hawakutaka kumghasi sana.

Siku iliyokuwa ikisubiriwa kwa hamu ikawadia, siku hiyo peter alijiweka vizuri kochini huku moyo wake ukiwa na furaha kubwa kwamba hatimaye siku hiyo ndiyo mpenzi wake angetangazwa na kuwa mshindi wa shindano hilo. Kwa Tanzania, shindano hilo lilikuwa likionyeshwa saa mbili asubuhi huku Marekani, hasa katika Jiji la New York ikiwa ni saa nnembili usiku wa jana yake.
Dola milioni tano zilikuwa fedha nyingi mno ambazo kila mtu alizitolea macho, shindano lile liliendelea kupata watazamaji hasa katika kipindi kile cha mwishomwisho akiwemo Peter ambaye hakutaka kubanduka mbele ya televisheni yake.

“Mungu! Naomba Tatiana ashinde,” alisema Peter huku akiikutanisha mikono yake.
Ilikuwa ni siku ya Jumapili lakini Peter hakwenda kanisani, siku hiyo alishinda nyumbani kwani alitaka kufahamu kile kilichokuwa kikiendelea, kama mpenzi wake atachukua ushindi au la.

Baada ya wanamuziki waalikwa kuitwa na kutumbiza, washindani wakaanza kuimba nyimbo zao na walipoaliza, wakaambiwa wajipange kwa ajili ya mshindi kutangazwa, kila mtu aliyekuwa akifuatilia shindano lile, moyo wake ukaanza kumdunda kwa nguvu.
 
SEHEMU 49...
“Nathan, speak out, I want to hear what you are about to tell me,” (Natha zungumza, ninataka kusikia hicho unachotaka kuniambia) ilisikika sauti ya msichana mrembo, alikuwa akizungumza simuni na Nathan.
“We are not going to get married,” (Hatutoona)
“Why?” (Kwa nini?)

Nathan hakutaka kujibu swali hilo, alibaki kimya na baada ya sekunde tatu akakata simu. Moyo wake ulikuwa kwenye maumivu makubwa, alijua ni kwa jinsi gani msichana huyo alikuwa akimpenda na kumthamini, alikumbuka mapenzi makubwa aliyokuwa nayo kabla ya kwenda nchini Marekani ambapo huko alikutana na Tatiana ambaye aliamini alikuwa akimpenda kama alivyokuwa akimpenda.

Hakutaka kusikia lolote lile kutoka kwa msichana wake wa kipindi kirefu, Dassy, moyo wake ulikuwa umezama kwa msichana Tatiana kwa asilimia mia moja na hakukuwa na nafasi nyingine ya kumuingiza msichana yeyote akiwemo huyo aliyekuwa ameongea naye, Dassy.
Dassy alikuwa msichana mrembo ambaye alifanikiwa kunyakua taji la urembo la Liberia miaka miwili iliyopita. Mara baada ya kuchukua taji hilo, wanaume wengi wakaanza kumtolea macho akiwemo Nathan ambaye alikuwa hali, hanywi kwa ajili ya msichana huyo.

Alimsumbua sana lakini baada ya mieizi mitatu ya kumfuatilia, Nathan akawa mwanaume mwenye bahati kubwa baada ya kuuteka moyo wa Dassy. Mahusiano ya kimapenzi yakaanza rasmi, wawili hao wakawa pamoja kila sehemu waliyokwenda huku kila mmoja akimuonyesha mwenzake ni kwa namna gani alikuwa akimpenda.

Baada ya uhusiano huo kudumu kwa kipindi kirefu, hapo ndipo walipoamua kupanga mikakati ya kutaka kufunga ndoa, ila kwa kuwa kulikuwa na shindano la kuimba nchini Marekani na Nathan alibahatika kupata nafasi, akazungumza na wazazi wake kwa kuwaambia kwamba atakaporudi nchini Liberia basi angeweza kumuoa msichana huyo, wazazi wa pande zote mbili wakakubaliana naye.

Nathan alirudi, wazazi wote walifurahi lakini alionekana kubadilika mno. Hakuwa Nathan yule aliyemthamini Dassy, huyu alikuwa Nathan mwingine ambaye hakutaka kusikia kitu chochote kile kuhusu msichana huyo.
 
50...
Hilo liliwashtua mno wazazi, wakaamua kumuita na kumuweka kikao ili awaambie ni kitu gani kilikuwa kikiendelea, Nathan hakuficha, akawaambia ukweli kwamba alipokwenda nchini Marekani, alikutana na msichana wa Kitanzania ambaye alitokea kumpenda kwa dhati.
“Whaaaaaaaaat?” (Niniiiiiiii?) aliuliza mama yake huku akionekana kutokuamini.
“This is my decision mom, I will never get married with Dassy,” (Huu ni uamuzi wangu mama, kamwe siwezi kumuona Dassy) alisema Nathan.

Japokuwa wazazi hawakuamini kile kilichokuwa kimezungumziwa lakini ule ndiyo ulikuwa uamuzi wake alioamua kuuchukua kwa wakati huo. Hakutaka kuwa na msichana Dassy ambaye alimsifia sana kutokana na uzuri wake, msichana pekee aliyekuwa akimpenda kwa wakati huo alikuwa Tatiana tu.
Dassy alilia na kulia, hakuamini kile kilichokuwa kimetokea kwamba hatimaye mpenzi wake, Nathan hakutaka kuwa naye tena. Hakuridhika na ile simu, aliamini kwamba Nathan aliamua kufanya vile kwa kuwa tu walikuwa wakizungumza simuni, hivyo akaanza kumtafuta. Alipompata, akaanza kuzungumza naye.

“Kile ndicho nilichokimaanisha Dassy! Siwezi kuwa nawe, nimempata msichana mwingine,” alisema Nathan huku akionekana kumaanisha alichokizungumza.
“Nathan, naomba usinitanie, niambie ukweli.”
“Naonekana kama natania?”
“Niambie ukweli.”
“Ndiyo huo! Siwezi kuwa nawe.”
Alivyokuwa akiongea, Dassy alifikiri kwamba Nathan alikuwa akitania lakini ukweli ni kwamba alimaanisha kile alichokuwa akikizungumza mbele yake. Dassy aliumia zaidi moyoni mwake lakini hakuwa na jinsi, huo ndiyo ukawa mwisho wa uhusiano wake na Nathan.

Akili ya Nathan ikatulia kwa Tatiana, kila siku alikuwa akilifuatilia shindano lile lililoonekana kushika kasi kadiri siku zilivyozidi kwenda mbele. Moyo wake uliendelea kumpenda Tatiana, kila alipokuwa akimwangalia, alijipongeza kwa kufanya uamuzi ulio sahihi wa kumuacha Dassy kwa ajili ya Tatiana.

Siku zikaendelea kukatika mpaka siku ya fainali ya shindano lile ilipowadia. Kama kawaida yake, Nathan akakaa sebuleni kwa ajili ya kuona ni nani angechukua ubingwa ule. Japokuwa matokeo ya awali yalisema kwamba Tatiana alikuwa akiongoza lakini hakutaka kujifariji kwani alijua kwamba hata Marekani napo fitina zilikuwepo pia.
 
ahsante sana,huku hakuna arosto hadi raha,ila tumosa simuoni jaman
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom