Penzi bila maumivu

Penzi bila maumivu

SEHEMU YA 11...
Mwanamke yule akaanza kutembea kwa mwendo wa harakaharaka kuelekea kule alipokuwa Sangiwa na wanaume wengine, alikuwa na taarifa nzuri ya kumpa Sangiwa juu ya kile kilichokuwa kimeendelea mule ndani.
“Kuna nini?” aliuliza Sangiwa.
“Hongera sana.”
“Mtoto gani?”
“Wa kike.”
“Unasema kweli?” “Ndiyo! Ni mzuri kama mama yake,” alisema mwanamke yule.
Sangiwa hakutaka kubaki hapo, alichokifanya ni kusimama na kuanza kuelekea kule ilipokuwa nyumba yake. Kwa kumwangalia tu, wala isingekupa wakati mgumu kugundua kwamba alikuwa na furaha mno.

Alipoifikia nyumba ile, akaufungua mlango na kuingia ndani. Alichokiona ndicho alichoambiwa, mke wake, Frida alikuwa hoi, wanawake waliochukua nafasi za manesi, wakunga walikuwa pembeni yake huku mmoja wao akiwa amembeba mtoto huyo aliyekuwa akilia mfululizo.
Akaanza kupiga hatua mpaka pale aliokuwepo mke wake na kisha kuushika mkono wake. Frida alipomuona mume wake tu, akaachia tabasamu pana.
“Hongera sana me wangu,” alisema Sangiwa.”
“Nashukuru sana.”
“Unamkumbuka Tatiana?”
“Ndiyo!”
“Naomba tumpe jina hilo kama ukumbusho wa Mzungu yule,” alisema Sangiwa.
“Hakuna tatizo.”

*****

Tatiana alikuwa msichana mzuri, uzuri aliourithi kutoka kwa mama yake. Alivutia kwa kila mwanaume aliyekuwa akimwangalia kiasi cha wengi kusema kwamba angeweza kuwa miongoni mwa wasichana ambao wangekuja kutikisa sana katika Kijiji cha Chibe na vijiji vingine pia.
Alichukua kila kitu kutoka kwa mama yake, kwa kumwangalia, kwa mbali Tatiana alionekana kuwa na mchanganyiko wa rangi, alipendwa na kila mtu huku watu wengine wakitaka kumbeba, mikono yao kuwa na mtoto kama Tatiana ilikuwa ni faraja kubwa.
Frida alimlea mtoto wake kwa mapenzi ya dhati, alikuwa akimbembeleza kila alipokuwa akilia huku kila siku akimnyonyesha kitu kilichomfanya kuwa na afya njema kabisa.

Wakati mwezi wa sita unakatika, Frida akahisi kwamba mtoto wake alikuwa na tatizo kwani kila alipokuwa akiuchezesha mkono wake mbele ya uso wa Tatiana kwenda huku na kule, mboni za Tatiana wala hazikucheza.
“Mmmh!” aliguna Frida.
 
Shunie kweli umeamua kutulaza na penzi bila maumivu.

Hongera sana, nami sibanduki hapa hadi umalize
 
SEHEMU YA 12...
Hali hiyo ilimshangaza, haikuwa kawaida kwani alikuwa na watoto, tangu walipokuwa na muda huo, kila alipokuwa akiuchezesha mkono wake, zile mboni nyeusi zilikuwa zikihama kwenda huku na kule kuufuata mkono ule.
“Huyu mtoto ana nini?” aliuliza Frida.
“Kwa nini?”
“Mboni zake hazichezi kabisa.”
“Unasemaje?”
“Ndiyo hivyo! Hebu jaribu kuchezesha vidole vyako mbele yake,” alisema Frida, alikuwa akimwambia mumewe, Sangiwa ambaye akafanya hivyo, kweli mboni hazikuwa zikicheza.

Hilo likaonekana tatizo kubwa, wazazi hao wakachanganyikiwa, wakajua kwamba kulikuwa na kitu hakikuwa sawa kabisa, walichokifanya ni kusafiri mpaka Shinyanga mjini ambapo huko wakampeleka katika Hospitali ya mkoa ambapo madaktari wakaanza kumpima na kugundua tatizo.
“Poleni sana,” alisema daktari kwa sauti ya taratibu.
“Kuna nini? Mbona pole tena?”
“Mtoto wenu ni mzuri ila ni kipofu.”
“Unasemaje?”

“Tatiana ni kipovu, ana upofu wa kuzaliwa,” alijibu daktari yule.
Frida akashindwa kujizuia, majibu ya daktari yule yalimfanya kuhuzunika na baada ya sekunde chache tu, akaanza kulia kama mtoto huku akimlaumu Mungu kwa kile kilichotokea.
Mume wake, Sangiwa akashindwa kumfariji kwani hata na yeye alikuwa akibubujikwa na machozi tu, moyo wake ulimuuma pia mpaka kufikia kipindi akahisi hasira zake zikipanda dhidi ya Mungu.

Moyo wake ulikuwa kwenye maumivu makali, hakuamini kama mtoto wake wa mwisho ambapo baada ya hapo angejizuia kuzaa tena alikuwa kipofu, kila alipokuwa akimwangalia, moyo wake uliendelea kumuuma mno.
Hawakuwa na jinsi, wakarudi kijijini huku wakiwa na huzuni tele. Hawakutaka kuficha chochote kile, wakawaambia wanakijiji wengine ambao walizipokea taarifa hizo wakiwa na majonzi tele.
“Poleni sana.”
“Asanteni, haina jinsi, kila kitu ni mipango ya Mungu,” alisema Frida huku akiendelea kububujikwa na machozi.
Huo ndiyo uliuwa mwanzo wa kila kitu. Mtoto Tatiana akaanza kukua, alipofikisha mwaka mmoja, akaanza kujifunza kutembea. Hapo ndipo Frida alipoumia zaidi, kila alipomwangalia mtoto wake, alikuwa akipapasa kila alipokwenda, hakuona, aliishi kwa hisia, kuna wakati alikuwa akijikwaa na kudondoka, alisimama na kuendelea tena.
 
SEHEMU YA 13
Si Frida tu aliyemuonea huruma Tatiana bali hata wanakijiji wengine. Miaka ikakatika zaidi, uzuri wake ukaanza kujidhihirisha mbele ya watu wengine, baada ya miaka kumi, Tatiana akawa msichana mrembo, alikuwa akisoma lakini vitabu vyake vyote vikiwa na alama za nukta tu.

Hakuona kitu chochote kile, alinyimwa uwezo wa kuona lakini darasani, Tatiana alikuwa mwanafunzi mwingine kabisa. Uwezo wake mkubwa ukamshangaza kila mtu. Wengi walisema kwamba alikuwa genius kwani hata kama hakuwepo shuleni, kile walichokuwa wakifundishwa wanafunzi wengine kilipotoka katika mitihani, alifanya vizuri na kuongoza.
Baada ya kufikisha miaka kumi na tano, Tatiana akamaliza kidato cha nne. Urembo wake, ukaendelea kuwapagawisha wavulana wengi kijijini pale. Alikuwa mkimya, kila alipokaa, pembeni kulikuwa na fimbo yake ambayo ilimuongoza kutembea kila alipotaka kwenda.

“Mama...” aliita Tatiana.
“Unasemaje binti yangu?”
“Hivi kuna siku nitaweza kuona?”
“Mmmh! Kwa kweli sifahamu.”
“Natamani nione, najiona kutokukamilika pasipo kukuona mama yangu kipenzi, ninapenda nione kama wengine mama,” alisema Tatiana huku machozi yakianza kumbubujika.
Frida akashindwa kujizuia, maneno aliyoyazungumza binti yake yaliuchoma moyo wake vilivyo. Ni kweli alijua kwamba binti yake alikuwa na kiu ya kutaka kuona tena lakini hakuwa na jinsi, alizaliwa akiwa hivyo, walimpeleka katika hospitali nyingi lakini huko kote walisema kwamba kama alizaliwa hivyo, asingeweza kuona tena.

Mbali na kuwa kipofu, Mungu alimpa uzuri wa sura na umbo, wanaume wengi waliokuwa wakimwangalia, walimmezea mate lakini msichana huyo hakutaka kukubaliana na mtu yeyote, hakuamini kama hapa duniani kungekuwa na mwanaume ambaye angependa kuwa na mke kipofu.

Uzuri wake wa sura aliokuwa amepewa, haukuwa peke yake bali Tatiana alipewa na uwezo mkubwa wa kuimba. Alikuwa na sauti nzuri, kanisani, alikuwa mwanakwaya, tena yule aliyewaongoza wote.
 
SEHEMU YA 14...
Alipokuwa akiimba, kila aliyeisikia sauti yake, alikiri kwamba hawakuwahi kumuona msichana aliyekuwa akiimba kwa sauti nzuri kama Tatiana. Kanisa lilipokuwa likiandaa mikutano kijijijini hapo au hata kwenye vijiji vya jirani, Tatiana ndiye alikuwa muimbaji kiongozi, sauti yake, ilizitetemesha ngoma za masikio ya watu wengi.
*
*

“Daah! Huyu msichana ana sauti nzuri mno, aiseee, anaimba kama Celine Dion,” alisema kijana mmoja, alikuwa miongoni mwa watu waliokuwa wamehudhuria mkutano wa Injili uliokuwa ukiendelea.
“Kweli, hebu isikie inavyojichuja masikioni, aiseeee, hii sauti ya kumtoa nyoka pangoni kaka,” alisema kijana mwingine.

Msichana Tatiana alikuwa akiimba jukwaani, ulikuwa mkutano maalum ulioandaliwa na mhubiri kutoka jijini Mwanza aliyeitwa kwa jina la Christopher Lazaro, mkutano huu uliitwa Deliverence (Ukombozi)
Sauti yake kali na yenye mvuto ndiyo iliyowavuta watu waliokuwa mbali mpaka katika mkutano ule. Hawakuamini kama mtu aliyekuwa akiimba alikuwa binadamu wa kawaida, walipofika hapo na kuangalia jukwaani, msichana Tatiana alikuwa akiendelea kumsifu Mungu tu.
Hakukuwa na mtu aliyegundua kama msichana yule alikuwa kipofu, pale jukwaani, alikuwa akitembea huku na kule lakini waimbaji wenzake walikuwa makini kumwangalia, kama angekosea hatua, wangemuwahi na kumdaka.

Baada ya kipindi cha kusifu na kuabudu, mchungaji Lazaro akakaribishwa na kuanza kuhubiri mkutanoni hapo, mahubiri yaliyochukua dakika arobaini tu kisha mkutano kufungwa.
“Unaimba vizuri sana mpendwa,” alisema kijana mmoja, sauti yake ilisikika vizuri masikioni mwa Tatiana.
“Utukufu kwa Mungu!” alisema msichana huyo huku akiachia tabasamu pana.
“Hivi unaitwa nani?”
“Naitwa Tatiana, wewe?”
“Naitwa Peter Lazaro, mtoto wa huyu mchungaji aliyetoka kuhubiri,” alijibu kijana huyo.

“Nashukuru kukufahamu.”
“Usijali. Unaishi hapahapa kijijini?”
“Ndiyo! Nipo hapahapa.”
“Nimefurahi kukufahamu,” alisema Peter.
“Asante. Karibu tena,” alisema Tatiana.
Uzuri wa msichana huyo ukaichanganya akili ya Peter, hakuamini kama duniani kulikuwa na msichana mrembo kama alivyokuwa Tatiana, alimwangalia vizuri, sura yake ‘iliita’
 
SEHEMU YA 15...
Peter hakuwa na raha tena, muda mwingi alionekana kuwa na mawazo huku akitumia wakati dakika kumwangalia Tatiana ambaye alikuwa akifuatwa na watu wengi kisha kupewa pongezi kutokana na huduma aliyoitoa, na kila aliposifiwa, alijibu ‘Utukufu kwa Mungu’.
Mpaka watu wanatawanyika mkutanoni hapo, bado Peter alikuwa akimfikiria msichana huyo kipofu. Kesho ilipofika na mkutano kuanza tena, kitu cha kwanza kabisa mara baada ya kufika uwanjani hapo, Peter akaanza kumtafuta Tatiana, alitaka kuzungumza naye hata kabla mkutano haujaanza.

“Nataka nimuone Tatiana,” alisema Peter, alikuwa akiwaambia baadhi ya wanakwaya.
“Yupo kule ndani, chini ya jukwaa anasali,” alijibu mwanakwaya mmoja.
Peter hakutaka kubaki mahali hapo, alichokifanya ni kuelekea kule alipoambiwa kwamba Tatiana alikuwa akisali, alipofika, akalifunua turubai lililoziba jukwaa lile kwa chini na kuchungulia, macho yake yakamuona Tatiana akiwa amepiga magoti huku mikono yake akiwa ameikutanisha.
Peter akaachia tabasamu pana, moyo wake uliokuwa na mawazo lukuki juu ya msichana huyo, ukafarijika kupita kawaida, akakenua na kuanza kumfuata msichana huyo, alipomfikia, akasimama pembeni yake.

“Wewe nani?” aliuliza Tatiana mara baada ya kumaliza kusali.
“Peter.”
“Umekuja kufanya nini?”
“Kusali pamoja nawe Tatiana,” alijibu Peter.
Tatiana alikuwa akiogopa mno, mapigo yake ya moyo yakaanza kudunda kwa nguvu. Pale walipokuwa, haikuwa sehemu salama hata kidogo, sehemu nzima ilikuwa imefunikwa kwa turubai na walikuwa wawili tu sehemu hiyo. Alichokifanya Tatiana ni kuchukua fimbo yake na kuanza kujiongoza mpaka nje ya jukwaa lile.

Peter alikuwa akimfuata kwa nyuma, moyo wake uliumia sana kwani pamoja na msichana huyo kuwa mzuri vile, alikuwa kipofu kitu kilichomfanya kuwa na hamu ya kufanya muujiza ili msichana huyo aweze kuona.
Huo ndiyo ukawa mwanzo wa kila kitu. Peter akafa na kuoza kwa msichana huyo ambaye hakuwa na hisia zozote zile za kimapenzi kwake. Katika siku saba za mkutano huo wa injili, bado Peter alikuwa akijitahidi sana kuwa karibu na Tatiana.
“Unaishi wapi?”
“Hapahapa.”
 
SEHEMU YA 16...
“Nyumba gani?”
“Kwa mzee Sangiwa.”
“Wala simfahamu huyo.”
“Ukiuliza utapafahamu tu.”
“Sawa. Ningependa tuwe marafiki Tatiana.”
“Marafiki?”
“Ndiyo! Tuwe tunapeana Neno la Uzima,” alisema Peter.
“Mmmh!”
“Nini tena?”
“Kuna urafiki kati ya mwanaume na mwanamke kweli?”

“Hata kama haupo, acha sisi ndiyo tuuanzishe, unaonaje?”
“Sawa, ila shetani asije akaingia kati.”
“Hakuna kitu kama hicho, nakuahidi, tena nitafunga na kuomba asiingie,” alisema Peter.
Huo ndiyo ulikuwa mwanzo wa urafiki wao. Japokuwa kwa Tatiana aliona kuwa urafiki wa kawaida lakini kwa Peter hali ilikuwa tofauti kabisa, kitu alichokifikiria ni msichana huyo kuwa mpenzi wake tu.
Siku hiyohiyo akaamua kufika mpaka kwa kina Tatiana ambapo akakutana na ndugu zake, wazazi wake na kuzungumza nao huku akitambulishwa kama rafiki, mtoto wa mchungaji Lazaro.
“Unaishi wapi?”
“Kwa kawaida ni Mwanza, ila kwa sasa nipo likizo, nasoma hapo Buluba Secondary hapo Shinyanga,” alijibu Peter.
“Kidato cha ngapi?”
“Cha tano.”

“Sawa. Nimefurahi kukufahamu zaidi.”
“Asante.”
Kesho yake, mchungaji Lazaro, timu yake ya wanakwaya na watu wengine wakaanza safari ya kurudi jijini Mwanza. Kwa Peter, yalikuwa ni maumivu makali ya moyo, alimpenda sana Tatiana kiasi kwamba kila siku alitamani sana akae naye karibu na kufanya mambo mengine.
Alikuwa mzuri wa sura, na hata kwenye mambo ya dini, msichana huyo hakuwa nyuma kitu kilichompelekea kuona kwamba endapo angewaambia wazazi wake kuhusu Tatiana wangefurahi pia.
Walipofika Mwanza, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kutafuta njia ya kuwasliana na Tatiana, hakujua ni kwa namna gani angeweza kuwasiliana na msichana ambaye alikuwa ndoto ya maisha yake.

“Nitamuandikia barua,” alisema Peter. Alichokifanya ni kuzungumza na baba yake ili apate anuani ya lile kanisa walilokuwa wameitwa kijijini kule kwa ajili ya mkutano, akapewa, hivyo kazi ikabakia kwake kumwandikia barua msichana huyo.
 
SEHEMU YA 17...
Peter alikuwa amedhamiria kumwandikia barua msichana huyo pasipo kukumbuka kwamba alikuwa kipofu. Siku iliyofuata, akaandika barua ndefu iliyojaza maneno matamu ambapo moja kwa moja akaelekea mjini ambapo huko akaituma kwa njia ya posta tena huku akiwa ameinyunyizia na manukato yaliyokuwa yakinukia vizuri.

Hakutaka kupoteza muda mjini, alichokifanya ni kurudi nyumbani huku akionekana kuwa na furaha tele. Katika kila alilokuwa akilifanya, bado kichwa chake kilimkumbuka msichana huyo ambaye alionekana kuwa kila kitu.
Usiku, usingizi wake ulikuwa wa mang’amung’amu, hakulala hata mara moja kutokana na mawazo mazito aliyokuwa nayo juu ya msichana huyo mrembo.
“Mmmh!” Peter alitoa mguno.
Hapo ndipo alipokumbuka kwamba msichana aliyekuwa amemtumia barua ile, Tatiana hakuwa mzima wa macho, alikuwa kipofu kwa asilimia mia moja, akaanza kujiuliza ni kwa namna gani ujumbe ule ungeweza kumfikia na kuusoma.

Barua ilijaza maneno mengi ya kimapenzi, alifahamu kwamba Tatiana aliheshimika sana kijijini kwa kuwa alikuwa mtu wa dini sana, lakini kitendo cha kumwandikia barua ile kilimaanisha kwamba ni lazima barua ile apewe mtu fulani na kumsomea, je hilo lisingekuwa tatizo kwake?
Tayari akaanza kupata mawazo mengine, hayakuwa mawazo mazuri bali yalikuwa mabaya ambayo aliona kwa namna moja au nyingine ingeweza kumuharibia msichana huyo aliyeaminika sana katika suala zima la dini.

Hakutaka kujali sana, kama kosa alikwishafanya hivyo alichokuwa akikisubiri kwa wakati huo ni kuona kitu gani kingetokea, kama lingekuwa tatizo kwake, basi alikuwa tayari kukabiliana nalo.
****
Tatiana aliendelea kumtumikia Mungu kupitia uimbaji wake kanisani. Moyo wake ulikuwa ukifarijika mno kila alipokuwa akikumbuka kwamba pamoja na kuwa msichana kipofu lakini bado Mungu alikuwa na mipango mingi na maisha yake.

Hali aliyokuwa nayo ilikuwa imekwishazoeleka maishani mwake. Tangu azaliwe, hakuwahi kumuona mtu yeyote zaidi ya kusikia sauti zao huku akiwa na hisia kali kwamba mtu aliyesimama mbele yake alikuwa nani na katika umati wa watu uliokuwa mbele yake, kulikuwa na watu wangapi.

Itaendelea.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom