NUSU SIKU NDANI YA JENEZA -12-
ILIPOISHIA :
"Alikuwa akikataza na kuruhusu kwa misimu, lakini wakati wote Mungu wenu amekataza binadamu msinywe damu kwa kuwa humo ndimo mwenye nafsi ya mtu."
Aliposema hivyo nilishtuka kidogo kwani ninavyojua mimi kuna kabila nchini mwangu linakula damu ya wanyama. Nilishindwa kuuliza, lakini yule mtu akaendelea kusema:
"Ukikuta mtu anapenda kunywa damu hata ya mnyama, mara nyingi katika maisha atakumbwa na tabia ya kufanya maamuzi ya ajabu yenye vitendo visivyokubalika."
SASA ENDELEA…
"Kama vitendo gani?"
"Vingi tu. Kama vile kuua, kudhuru, kuharibu, kutukana. Mara nyingi kutukana huku kunakuwa hadharani. Pia unaweza kushangaa mtu anakuwa na tabia ya kupenda sana kitu fulani."
"Da! Nimejifunza mengi sana."
"Bado hujajifunza, hapa umeletwa ili ujifunze mbinu inayotumika kuua watu duniani. Hii mbinu tunataka wewe ndiyo uende ukaisambaze kwa dunia ukiwa mwalimu wa mbinu hiyo lakini nguvu yote itatoka kwetu.
"Sasa hivi niliposema kaa lengo langu nianze kukupa hiyo mbinu ili sisi tuweze kuvuna wanadamu wengi katika kipindi hiki ambacho dunia itafikia mwisho wakati wowote ule."
"Kwani hata wewe hujui mwisho wa dunia ni lini?"
"Najua."
"Ni lini?"
"Kha! Mbona hata wewe unajua ni lini!"
"Mimi sijui, kwenye vitabu vyetu tuliambiwa hakuna anayejua siku ya mwisho wa dunia, hata malaika wa mbinguni."
"Ni kweli lakini maandiko hayohayo yameweka wazi ishara ya siku za mwisho na ishara hizo zote zinaonekana sasa au nasema uongo?"
"Ni kweli."
"Kwa hiyo unakubali kwamba hata wewe unajua kuwa dunia imefikia mwisho?"
"Kweli nimejua."
"Sasa tunataka kukutuma duniani, kazi utakayotakiwa kuifanya ni pamoja na kuhakikisha kila siku unaua binadamu zaidi ya mia moja."
"Hee! Niue binadamu wenzangu?" niliuliza kwa mshtuko nikataka kusimama.
"Kijana tulia. Unatakiwa kufuata maagizo yetu."
"Sijawahi kuua na kuua ni dhambi kubwa sana."
"Kwani kuna dhambi ndogo?" aliniuliuza kwa sauti ya ukali.
"Najua hakuna, lakini kuua mtu dhamira inauma sana kuliko nikimwibia mtu."
Aliniangalia kwa karibu dakika moja halafu akageuka pembeni na kumwangalia kiumbe mwenzake mmoja ambaye alikuwa kama msaidizi wake, akasimama na kunisogelea.
Aliponifikia aliweka mkono wake juu ya kichwa changu, palepale nikajikuta niko kwenye kundi la viumbe wengi lakini kuna kiongozi mmoja mkubwa ambaye alikuwa akitoa maagizo fulani.
Alikuwa amesimama akamnyooshea kidole kiumbe mmoja akimwambia:
"Wewe lazima ukamuue kwa ajali leo hii Alia, yule mfanyakazi wa kampuni ya madini, muda huu yupo kazini. Halafu si unajua yule wakati wa kulala au akiamka huwa hasali kwa Mungu wake? Kwa hiyo ni mwepesi sana.
"Unachotakiwa kufanya, nenda nyumbani kwake kampige ugonjwa wa ghafla mkewe na umwangushe chini halafu ashindwe kusema. Yule mtoto wake mkubwa atampigia simu baba yake.
"Sasa baba akiambiwa mkewe kaanguka na hawezi kuongea, itabidi atoke ofisini haraka na ataendesha gari kwa spidi sana.
"Halafu uende pale Kituo cha Mabasi cha Faya, mwamuru dereva mmoja wa daladala aondoe basi kwa kasi ukimpiga upofu asione vizuri mbele, akifika kwenye makutano ya Barabara ya Faya na Morogoro apite bila kuangalia taa, Alia naye atakuwa ameshafika pale na taa zitamruhusu apite, watakutana na ajali itatokea, Alia atakata roho palepale, sawa?"
Kile kiumbe hakikujibu sawa, ila kilisimama wima kikainamia mbele kama ishara ya kumtii kiongozi wake, akafutika mbele yetu. Niliogopa sana kusikia mpangilio ule.
Kumbe ilimaanisha kwamba, ajali inapotokea inakuwa imepangwa na pepo wachafu tena kwa mpangilio wa ajabu, kwamba ajali ianzie wapi na kuishia wapi! Ina maana Alia hakujua kama kule kupigiwa simu kuwa mke wake kashikwa na ugonjwa wa ghafla ndiyo ilikuwa tiketi ya sababu ya kufa kwake.
Kama angejua angetoa amri akimbizwe hospitalini halafu yeye atafuata huko polepole.
Baada ya yule kufutika, yule kiongozi akiwa bado amesimama akamnyooshea kidole kiumbe mwingine, akamwambia:
"Wewe! Kwanza simama."
Yule kiumbe akasimama kwa utii wote huku akimwangalia yule mtoa amri. Mtoa amri akaendelea:
"Nataka ukasababishe ajali mbaya ya lori na basi. Ajali hii nataka itokee Barabara ya Chalinze-Morogoro. Unachotakiwa kufanya, wakati basi linatokea Morogoro kwenda Dar es Salaam, wewe toa malori mawili Chalinze kwenda Morogoro.
"Yale malori yataanza kufukuzana mpaka yanapokaribia kukutana na lile basi, mpige upofu dereva wa lori la nyuma, aamue kumpita mwenzake bila kuangalia mbele na wakati huohuo mfanye dereva wa basi aongeze spidi mpaka kukutana uso kwa uso na ajali itokee.
Utakachotakiwa kukifanya baada ya ajali ni kukusanya damu za watu watakaoumia, lakini usiue maana leo letu ni damu ya binadamu, si mnajua tuna sherehe mwisho wa mwezi huu?
"Basi harakisha ili kitengo cha damu kiwe na akiba ya kutosha, watu waumie sana, wavunjike miguu, mikono, wapasuke vichwa lakini usitoe roho ya hata mmoja wao.
Yule kiumbe naye akainama kwa ishara ya unyenyekevu na kufutika mbele ya macho yangu. Nilianza kujiuliza ina maana katika maelekezo yale itafika zamu yangu?
Kisha yule mkubwa wao akaangalia huku na kule mpaka mimi akanipitia na jicho lake moja tu lililo kwenye paji la uso, akaniambia:
"Wewe, simama kwanza."
Nikasimama huku nikitetemeka moyoni nikijiambia sitakubali kutumwa kwenda kuua wala kusababisha ajali.
Ili kujua zaidi usikose kusoma leo jioni nisiwachoshe sana....