NUSU SIKU NDANI YA JENEZA - 5-
ILIPOISHIA :
Wapo waliokuwa na mapembe mawili kwenye pande mbili za vichwa, pia kuna wengine walikuwa na pembe moja tu juu ya mapaji ya uso, hivyo kuonekana kama yule mnyama aitwaye faru.
Kusema ule ukweli walitisha sana, kama mmoja wao ningebahatika kukutana naye barabarani tena tukiwa wawili lazima hali ya hewa ingebadilika, kama si mimi kuanguka na kufa basi ningekimbia nikipiga kelele sana.
Una swali? yule kiumbe wangu aliniuliza.
Mengi sana.
Uliza sasa.
SASA ENDELEA
Sasa hawa ni akina nani?
Hawa ndiyo wale ambao nyinyi duniani mnawaita mashetani na kuwachora vibaya.
Sasa uhakika ni upi? Nyinyi ni wabaya au si wabaya?
Kwanza kabla sijakujibu naomba nikwambie kwamba muda umekwenda sana, kule duniani wameanza kushughulikia jeneza lako mapema sana.
Nilishtuka sana kusikia habari hizo, kwamba jeneza langu limeshaandaliwa kabisa.
Ndani kuna maiti?
Hakuna, maiti wewe upo hospitali.
Ni hospitali gani wamenipeleka?
Mwananyamala.
Halafu huku niliko?
Huku hakuhusiani na kule.
Ina maana kule wanaendelea na kuomboleza?
Tena wanalia sana kama ulivyokwishaona muda ule.
Nilisikia uchungu sana.
Sasa nikujibu, watoto waliozaliwa na uzao wa binadamu na malaika ndiyo hawa wenye maumbo ya kutisha.
Kwani kuna malaika na binadamu walizaa?
Hujawahi kusoma?
Popote pale?
Sijawahi.
Ni hivi, kuna wakati ulimwengu wenu ulikuwa na wanawake warembo sana, siku moja malaika walishuka wakawaona, wakawaingilia wale wanawake nao wakapata mimba na kuzaa.
Wale watoto kwa wakati ule walikuwa na maumbo tofauti, wengi walikuwa warefu, wakubwa sana, wana maumbo ya kutisha.
Wakati wa gharika la Nuhu, wale malaika walitaka kurudi kwa Mungu lakini walishindwa wakaishia kusikojulikana ndiyo hao vizazi vyao sasa.
Na malaika wanawake waliondoka na watoto wao waliowazaa na wanaume wa duniani?
Hakuna malaika wanawake.
Aliposema hakuna malaika wanawake nikasimama vizuri, nikamwangalia kwa kumkazia macho na kugundua kuwa, yule kiumbe hakuwa anajua mambo kwa undani, asingeweza kusema vile. Nikamuuliza:
Kwa nini hakuna malaika wanawake wakati sisi kule duniani mpaka matangazo, nyimbo za wanamuziki, maboksi ya sabuni yanaonesha kuna malaika wanawake?
Jiulizeni nyinyi binadamu, mmepata wapi hizo habari kwamba kuna malaika wanawake.
Nilijikanyaga mwenyewe, nikashindwa kuthibitisha kwamba kuna malaika wanawake, lakini nikakumbuka wimbo wa Nakupenda Malaika ulioimbwa na wanamuziki mbalimbali wakiwemo Bony M.
Labda nikwambie kwamba malaika wote ni wanaume. Kwenye vitabu vyenu mliandika kuna Malaika Gabriel, huyu kazi yake ilikuwa kupeleka habari kutoka kwa Mungu kwenda sehemu nyingine.
Kuna Malaika Michael, huyu ni jemedari wa vita, alikuwa akipigana na maadui wa Mungu. Si ndiyo?
Ndiyo, nilimjibu, akaendelea.
Kama unakumbuka wakati wa Lutu, Sodoma na Gomora, malaika wa Mungu walipotumwa kwenda kwake, wale wakazi wa pale walimwambia wanataka kuwaingilia kimwili.
Hapohapo nilipata cha kumuuliza.
Sasa kama hakuna malaika wanawake hao wakazi wa Sodoma na Gomora walitaka kuwaingilia akina nani?
Hujasoma sifa mbaya ya Miji ya Sodoma na Gomora ilikuwa ya ulawiti?
Nilitingisha kichwa kukubaliana naye kwani ni kweli nilisikia dhambi kubwa ya miji ile ilikuwa ni wanaume kuingiliana wenyewe kwa wenyewe licha ya kuonywa mara kwa mara na viongozi wa kidini.
Nilianza kumwamini yule kiumbe kwamba anajua mengi kuhusu ulimwengu na asili zake, nikamuuliza.
Sasa wale malaika walioshindwa kwenda peponi walikwenda wapi?
Kabla ya kunijibu alinisahihisha kwa kusema:
Kwanza kabisa napenda kukwambia awali hao malaika hawakutoka peponi bali mbinguni.
Nilimshangaa sana, nikamuuliza:
Kwani kuna tofauti kati ya peponi na mbinguni?
Ipo kubwa tu.
Ipi hiyo?
Mbinguni ndiko kwenye makazi ya Mungu, peponi ni makazi ya watu wema.
Sijawahi kusikia hilo, lakini nimeamini sasa.
Basi, sikuwa na maswali tena, nikaanza kuwaona wale viumbe wakihangaika huku na kule wakitweta kama vile wana jasho jingi kwa kazi kubwa waliyoifanya, hali zao zilikuwa za kutisha.
Niliweza kuwaona wakitoa meno marefu kiasi cha kuweza kuzidi urefu wa mkono wa binadamu, wengine masikio yao makubwa yalipita zaidi vichwani, ungeweza kusema wamejifunga miavuli vichwani mwao.
Karibu wote weusi wao ulifanana sana na wa jongoo, lakini meno yao yalikuwa meupe sana tena sana. Niliwaona wawili wakitembea, walikuwa kama watu wanene sana kwamba wanashindwa kutembea sawasawa kutokana na unene.
Baada ya hapo kiumbe alinishika mkono na kunipeleka sehemu nyingine bila kuniambia ni wapi na kuna nini, ikabidi mimi nimuulize.
Huku tunakokwenda sasa ni wapi?
Utapajua tu tukifika.
Ni kama hapa tulipotoka?
Usiwe na haraka sana.
Itaendelea .......