Nusu Siku Ndani ya Jeneza-16-
ILIPOISHIA JANA:
"Pia ukasema kwamba unataka kuhakikisha kuwa wanawake kwa kudai hali ya usawa wanaivunja tena kwa mara ya pili ile mari ya Mungu wao kwamba wao wameumbwa kuwa wasaidizi.
"Jingine kubwa ulisema kwa kudai huko haki lazima ndoa zitavunjika kwa sababu ya usawa kwani wanaume nao hawatakubali kutawaliwa na wanawake ambao watakuwa wanataka kuwatala."
SASA ENDELEA
"Sawasawa Humuli. Je, kuna dalili ya mafanikio kwa kiwango kikubwa?"
"Sana mkuu. Nchi kubwa na tajiri zote zinatetea wanawake, taasisi mbalimbali zimeanzishwa kwa ajili ya kuwatetea wanawake, baadhi ya nchi kwa sasa duniani zinatawaliwa na wanawake, yapo makanisa ambayo wanawake ndiyo viongozi, lakini pia tumehakikisha kwamba kila serikali inaweka wizara ya kutetea wanawake."
"Je, mmefanyaje ili serikali zisishtuke kwamba ni mkakati wetu?"
"Tumehakikisha tunaongeza, mfano wizara ikiwa ya wanawake tunaongeza na watoto au jinsia au walemavu."
"Je, mkakati mpya mnaokwenda nao mkiwa na huyo binadamu ni upi?"
"Huyu tutamtumia katika maeneo ambayo akifika yeye wanadamu watalainika kuliko sisi tukijifanya wanadamu."
"Sawa. Lakini huyu bado sijakubaliana naye kurudi huko, napenda sana akakae kwenye chumba cha tabia za wanadamu na sifa za nyota ili ajifunze, nataka akiondoka ame amejifunza kazi hiyo akawasaidie wenzake kule."
Aliposema hivyo, kiumbe mmoja alinishika mkono tukaondoka eneo hilo. Tulitembea umbali wa kama nusu saa tena kwa miguu lakini sikutokwa na jasho wala kuhusu joto maana kama nilivyosema, kule kuna mwanga mkubwa lakini hautokani na jua.
"Tunakwenda wapi?" nilimuuliza yule kiumbe, akanijibu kwa mkato:
"Chumba cha tabia na sifa za nyota."
"Ndiyo nini?"
"Utakwenda kuona."
Nilifunga mdomo, tukatembea mpaka kwenye jumba kubwa sana kama godauni, tukaingia ndani yake. Mle ndani nilikuta wanadamu wenzangu wamekaa kwenye madawati halafu kuna kiumbe kama anawafundisha bila kutumia ubao.
Nilipoingia tu, yule kiumbe aliyenipeleka akageuza na kurudi alikotoka. Yule kiumbe aliyekuwa akifundisha aliponiona alisimama kufundisha akanionesha sehemu ya kukaa.
"Una bahati somo letu ndiyo kwanza linaanza."
Nilikaa mkao wa kusikiliza.
"Karibu sana bwana, hiki ni chumba cha tabia za wanadamu na sifa za nyota zao. Eee, mara zote binadamu anakuwa na tabia ya kubadilika kutokana na siku aliyozaliwa. Binadamu aliyezaliwa mwezi wa Januari hawezi kuwa na tabia moja na yule aliyezaliwa mwezi wa Novemba.
Kila mwezi unatawaliwa na nyota yake. Ndiyo maana katika kuishi au kufanya kazi zenu mnatakiwa sana kuhakikisha zinalingana na nyota.
"Ziko nyota kumi na mbili na zote hizi zinatawaliwa na mkuu wa huku mliko. Sisi tunazijua nyota hizi kwa majina ya huku ambayo nyie hamuwezi kuyajua, ila kwenu mnaita hivi: Nyota ya kwanza, Punda au Aries kwa lugha ya kigeni.
"Hii nyota kama wewe unajijua unayo au unajua mwanao anayo ni nzuri kumkuza au kumuandaa kwa kazi kama za jeshini, uokoaji wa majanga mbalimbali, michezo, mfanyabiashara, ualimu na mambo yote yanayohusu usimamizi wa fedha kwa ujumla.
"Binadamu mwenye nyota hii akifanya moja ya kazi hizo atatajirika, atang'ara na atavuma sana. Kama ni mpira ndiyo binadamu wenzake husema f'lani ana kipaji. Huwezi kumkuta mhasibu mwenye nyota ya Punda anapata shoti kazini au anafungwa kwa wizi wa fedha.
"Mfanyabiashara mwenye nyota ya Punda mafanikio yake ni makubwa mno. Anaweza kutajirika mpaka watu wakasema ameroga au anafanya biashara na misukule. Lakini si kweli bali ameongozwa kwenye kazi ambayo ina nyota yake.
"Huwezi kumkuta mfanyabishara ana nyota ya Punda halafu anafilisika. Ile nyota peke yake inalinda fedha zake za kazi. Kwa wanajeshi, wengi wao hufikia kiwango cha kuwa mkuu wa majeshi, mkuu wa polisi, mkuu wa magereza na mambo mengine yenye mazingira hayo.
"Hata hivyo, wanajeshi wenye nyota hii ni rahisi kupindua nchi kwa mafanikio makubwa endapo hakutakuwa na uhusiano mzuri kati yake na serikali iliyopo madarakani.
"Pia wengi wenye nyota ya Punda hupenda kimiliki silaha lakini matumizi yao hayaendi kinyume na sheria ya nchi kama wengine. Ila akilenga mahali lazima apige. Wana shabaha sana.
Itaendelea Kesho wakati kama huu