NUSU SIKU NDANI YA JENEZA - 10-
ILIPOISHIA JANA :
Mara nyingi anaanza mwanaume kutoka. Ile ni aibu kwa sababu ujasiri wa lile pepo la ngono unakuwa umeshatoka, mtu anakuwa ana ufahamu wake mwenyewe.
Hapa naomba nifafanue kwamba ninaposema kila mtu ana pepo la dhambi moja ninamaanisha kufanya jambo kupita kiasi na lenye madhara, binadamu anayevuta sigara kupitiliza ile ni roho chafu yake na binadamu huyo utamuona akikosa sigara hata nguvu zinamwishia au zinamtoka kabisa, kama alilala anatoka kwenda kununua na kuvuta ndiyo roho yake inatulia.
ENDELEA SASA
Si rahisi kwa binadamu wa kawaida kuishinda roho hii, mara nyingi inatanguliza uwezo wa mtu kutenda hilo kosa. Ndiyo maana mtu akizini, hawezi kufikiria kuzini tu lazima kuna muda ataisikia sauti nyingine ikimzuia kufanya tendo hilo kwamba ni dhambi.
Sisi tulishahukumiwa, yaani hatuna tena msamaha hata iweje, ndiyo maana tunakazana kila sekunde kuhakikisha wanadamu wanaopotea ni wengi kuliko wanaokwenda kwenye njia za Mungu wenu.
Kuna pepo la maafa na vilio, kazi yao ni kuhakikisha binadamu wanalia na kufa kila sekunde. Haya mapepo yapo kwa kitengo, mfano wapo wa ajali, wapo wa sumu, wa magonjwa, wa vifo vya ghafla, lakini mwisho wa kazi zao ni kuua na kusababisha vilio.
Napenda nikupe mfano mmoja, nyinyi binadamu mtu akifa mna kawaida ya kusema ni mapenzi ya Mungu au ni mipango ya Mungu, mnakosea sana kwa sababu hamjui lolote na tena hamjui maandiko.
Mungu alipanga binadamu azaliwe, akue, aishi mpaka miaka ya uwezo wake wa kimwili ndipo afe. Kwa sasa Mungu amesema mnatakiwa muishi miaka 75, kupita hapo ni lazima muwe na nguvu. Kwa hiyo mtu akifa mapema, yaani kabla ya miaka hiyo, mfano mtoto mdogo, kijana wa miaka 25 au mtu mzima wa miaka 45, hicho kifo si mpango wa Mungu, ni sisi.
Watumishi wote wa Mungu waliishi miaka mingi hadi uzeeni mwao, wakalala kwa mapenzi ya Mungu wenu. Kama umesoma kitabu cha Biblia utaona kizazi cha Adamu na Eva ambacho ni Kaini, Abeli, Enoko, Noa, Abrahamu, Sarah, Loti, Isaka na kuendelea walilala pale walipofikisha umri wa kufanya hivyo.
Sasa nitoe mfano wa pepo la ajali, hili pepo lina tabia ya kuwaangalia binadamu katika kundi moja tu, mkusanyiko. Mfano, pepo limeona basi limebeba watu wengi, hapohapo linaamua kuingilia kati na kuua.
"Kama unataka kuuliza kitu, uliza tu."
"Ina maana mtu akifa tunavyosema siku yake ilifika tunakosea?"
"Mnakosea sana, siku ya binadamu kufa ni kufika kwa umri alioupanga Mungu wenu. Wapo binadamu waliishi miaka mingi sana, kama sijakosea Methusela ndiye aliongoza, aliishi miaka 969 ndipo akafa. Baadaye Mungu wenu alipunguza umri wa kuishi, ilishuka polepole hadi kufikia miaka 75 ndiyo maana ajali nyingi haziwakuti wazee wenye miaka hiyo, we fuatilia utagundua hilo.
Kinachotuumiza sisi huku ni jinsi nyinyi mlivyojaaliwa kuwa na maandiko ili msome lakini hamfanyi hivyo ndiyo maana mnapitwa na utambuzi wa mambo mengi sana. Nyoka zamani alikuwa na miguu kama mjusi, kwenye maandiko yenu ipo lakini wengi hamjui.
"Kivipi? Si kweli," nilidakia.
"Si hilo tu, hivi mnajua kama mwanamke mwanzoni kabisa alikuwa akizaa bila uchungu?"
"Hamna bwana," nilidakia tena.
Sikiliza wewe, maandiko yenu wenyewe yanasema Mungu wenu alipoibaini dhambi iliyotendwa na Eva na mumewe Adam kwa kushawishiwa na mmoja wetu ambaye alijifanya nyoka, alitoa adhabu kali.
Katika adhabu hiyo, kila mmoja alipewa ya kwake. Adamu aliambiwa adhabu yake itakuwa kutoa jasho ili apate chakula ndiyo maana mpaka sasa kule duniani kwenu mwanaume ndiye anayelisha nyumba kwa kufanya kazi, tena wengine wanafanya kazi ngumu na nzito.
Mwanamke yeye kufanya kazi anapenda mwenyewe kwa sababu si adhabu yake. Yeye aliambiwa adhabu yake itakuwa kuzaa kwa uchungu. Pia akaambiwa atatawaliwa na mwanaume.
"Kwa hiyo ina maana wanawake wanaposema usawa wanakosea?" nilimuuliza.
Wanakosea sana kwani wanavunja maagizo ya Mungu wenu. Kwetu sisi wanawake ndiyo tunaowatumia kuuvunja utaratibu wa Mungu wenu, mifano ipo mingi sana.
Ukianzia na mwanzo kabisa wa maandiko kwenye kitabu chenu cha Agano la Kale ambacho kiliandikwa mwaka wa 1688 kabla ya kuzaliwa mkubwa wenu (Kabla ya Kristo).
Adamu alimkosea sana Mungu kwa kutumiwa na mke wake. Nyoka alimdanganya Eva kuhusu tunda akalila akampa na mumewe naye akalila, Mungu akakasirika.
Ukitoka kwa Adam utakutana na Samson yule mnadhiri wa Mungu wenu, naye alimkosea Mungu kwa kupitia kwa mwanamke ambaye ni Delila.
Ukiachana na Samson, Mfalme Suleiman naye alimkosea Mungu kupitia kwa wanawake. Kuna mtu alikuwa anaitwa Hamani, mfalme aliamuru akatwe kichwa kwa sababu ya mwanamke.
Yusufu kama unamkumbuka, alikwenda jela kwa sababu mke wa mfalme alimsingizia uongo kwamba alitaka kumbaka.
Kifupi kazi zetu nyingi za kwenda kinyume na mapenzi ya Mungu wenu sisi huwa tunazipitishia kwa wanawake kwa vile wao ni viumbe dhaifu sana lakini wana nguvu ya ushawishi. Majambazi wengi wanakamatwa kwa sababu ya kutegewa wanawake.
Nataka kuuliza swali, tangu umekuja huku kutoka duniani unadhani una muda gani?
"Mh! Kama wiki moja," nilimwona yule kiumbe akicheka, nikashangaa anacheka nini wakati ni kweli.
Haiko hivyo huku kwetu. Tunaishi kama watawala wakuu wa kwenye nguvu za giza. Siku moja kwetu kama miaka miaka kumi na miaka kumi pia inaweza kuwa siku moja.
Tangu umekuja huku, kule duniani leo ni siku ya pili tena asubuhi kumekucha lakini jua halijaanza kutoka. Kwaheri tutaonana siku nyingine kwani nimepewa amri ya kukuacha.
Nilitaka kusema kitu lakini kufumba na kufumbua sikumwona yule kiumbe mbele ya macho yangu, nikajikuta nimesimama mbele ya kiumbe mwingine aliyekaa kwenye kiti cheupe, pembeni yake walisimama viumbe wengine wanne, wawili kila upande.
"Karibu ukae," yule kiumbe aliniambia. Alionekana yeye ni bosi wa wote kwani eneo alilokaa ni zuri, mahali pazuri, panavutia na hali yake pia.
"Wapi?" nilimuuliza.
"Si ukae."
Niligeuka kuangalia pa kukaa, nikaona kiti kingine kidogo lakini kizuri sana, cheupe, nikakaa kwa kujiachia.
Ili kujua zaidi usikose kusoma leo jioni.....