69--"Hawajanipiga si umewakataza." "Shija wangu jamani," Helena alinikumbatia huku akibubujikwa na machozi. "Usilie Helena," nilijikuta nikimuonea huruma. "Siwezi kuacha kulia, Shija upo sehemu mbaya."
"Ni kweli, lakini sina jinsi." "Shija nimepata kazi sana kukutetea, mama yangu ana roho mbaya aliitamani damu na nyama yako," Helena alisema huku akiketi kwenye mkeka wangu. "Kwani nimemkosea nini?" "Toka siku tulipogombana shuleni bado nipo na Sabina, ulipotuambia sisi wachawi alikasirika sana.
Kingine kukingiwa kifua na marehemu mzee Manoni, kitendo kile kilimuuma sana hasa siku ile tulipokuwa tunakutorosha na kushtukiwa na mzee Manoni na kupewa adhabu ya kutoa nyama ya mtu katika familia. Aliapa kuwa mzee Manoni aishi milele lakini akitangulia basi cha moto ungekiona."
"Lakini mbona aliona mimi na wewe tumepatana?" "Hata sijui kwa nini alikuchukia kiasi hicho." "Kwa hiyo ndiyo kasemaje?" "Shija, wana bahati siku ile nilijikwaa na kuumia, lakini nisingekubali wakukamate kirahisi vile. Baada ya kukufikisha hapa walipanga kukula siku ile ile usiku.
Lakini nilimuapia mama kuwa wakikula nyama atafuata yeye au mimi. "Mama alinibembeleza sana nikubali wakutie adabu, ujinga wa mara ya kwanza nilivyo kusaliti, lakini niliapa sitarudia tena kutenda kosa la kinyama kama lile.
Niliapa sitakusaliti mpaka nakufa. Pamoja na kunitisha nilikuwa tayari kwa lolote kuhakikisha wanatula nyama wote. "Ilibidi kifanyike kikao usiku ule ule wakubaliane wakufanye nini, wapo waliopendekeza uwe mchawi kwa vile siri nyingi unazijua.
Lakini ulikosa sifa moja, ulishafanyiwa zindiko la kifo. Wengine walipendekeza uwe msukule, wengi waliunga mkono. Wakati wanajiandaa kukufanya ndondocha, niliendelea kumbembeleza mama wasikutie undondocha, wakuache msukule freshi.
Mama alisema analifanyia kazi, ndiyo maana mpaka leo hii upo katika hali hii." "Asante sana Helena." "Shija muda wa kunishukuru bado, mpaka nikutoe humu ndani." "Helena! Bado tu hujakata tamaa?" "Siwezi kukata tamaa, kwanza kukuleta hapa ni nafasi yangu nyingine ya kufanya vitu vyangu kwa uhakika."
"Helena, unaweza kukosea na kusababisha nikageuzwa asusa." "Shija wee acha tu, nitakachokifanya hutanisahau mpaka unaingia kaburini." "Helena unataka kufanya nini?" "Shija ni siri yangu naijua mimi na Mungu wangu." "Hivi wale walioletea chakula misukule wenzangu, kina nani?"
"Wale ni wafanyakazi walioajiriwa kwa ajili ya kupikia misukule." "Nao ni wachawi?" "Si wachawi, ila hujipaka dawa ili kuwaona misukule wakati wa kuwapa chakula."
"Hawawezi kutoa siri nje?" "Wapo waliojaribu lakini walikufa na wengine kuwa vichaa siku siri ilipovuja."
"Eti mama Suzana alikufa au ndiyo wamemfanya kama mimi?" "Mama Suzana kweli amekufa baada ya kutupiwa uchawi, lakini kaburi lake ndugu zake walizindika. Mwili wake haukuchukulika." "Kwa hiyo walitaka kumfanya nini?" "Shija kuna kitu kingine zaidi ya kumla nyama."
"Mh! Kweli wamepania." Siku ile tulizungumza mpaka kulipokaribia kupambazuka ndipo Helena aliponiaga na kuniachia kipande cha shuka. "Shija utajifunika hiki." "Asante Helena."
Helena aliondoka na kuniacha nizidi kumfikiria na msaada wake mkubwa kuokoa maisha yangu.
Haukupita muda Misukule wenzangu walirudi toka kwenye mashamba ya mama Helena. Siku zilikatika nikiwa naishi maisha ya kimsukule, tofauti yangu na misukule wengine ilikuwa, wao hawaongei lakini mimi nilikuwa naongea pia nilikula chakula kizuri, nililala kwenye kipande cha mkeka na kujifunika shuka.
Lakini wenzangu walilala chini vifua wazi. Hata ulaji wao ulikuwa tofauti nmimi, wakati wa kula
waligombea chakula kama nguruwe, hata chakula chao kilikuwa bora chakula, siku nyingine walikula mapumba au ugali ambao haufai mwanadamu kula. Helena naye alipona na kuweza kuingia ndani mle wakati wa kuwatoa misukule kwenda shamba. Siku nyingine alinichukua kwenda kuangalia kazi ya misukule mashambani.
Asikuambie mtu wanadamu tunateseka, walilima kama trekta na anayetegea hutandikwa kama ng'ombe. Kuna kipindi Helena aliwatandika mpaka nikawa nafumba macho, kingine kilichonishangaza ni ukubwa wa shamba la mama Helena. Nilijiuliza shamba lile lipo wapi.
Nini hatma ya maisha ya Shija?
ITAENDELEA BAADAYE.... NIKIWA MAPUMZIKONI KTK BIASHARA YANGU YA KARANGA!