Majigo
JF-Expert Member
- Feb 23, 2012
- 5,519
- 1,831
1--Katika familia ya watoto Matulanya wengi hakuwakupenda elimu hasa walionitangulia akiwemo kaka yangu mkubwa na dada zangu yupo aliyeishia darasa la pili mpaka leo hata kusoma hajui. Mwingine aliishia darasa la sita baada ya kupata ujauzito.
Maisha tuliyokuwa tukiishi yalikuwa ya hali ya chini kutokana na ukubwa wa familia na udogo wa kipato...
Kwa kweli tulitegemea kilimo na mifugo ambayo kwa kiasi kikubwa vilituwezesha kupata chakula na pesa za kimaendeleo. Kwa upande wangu nilijiona kama nabii fulani niliyeshushwa ndani ya familia ya mzee Matulanya. Naweza sema nilikuwa na tofauti kubwa na ndugu zangu wote walionitangulia na walionifuata. Toka nikiwa darasa la kwanza nyota yangu ilionekana, nilikuwa na uwezo mkubwa kuliko hata wanafunzi walionizidi umri.
Shuleni sikupelekwa nilijipeleka mwenyewe kwani umri wangu ulikuwa mdogo sana, siku aliyopelekwa kaka yangu nami nilikuwepo. Kutokana na michezo ya watoto waliokuwa wamekwenda kuanza darasa la kwanza, nilivutiwa nayo na kungangania kubakia shule. Mwalimu aliamini ningeweza kushindwa kurudi siku ya pili kwa kumwambia mama aniache tu nikichoka nitarudi nyumbani.
Siku hiyo nilishinda pale hadi muda wa kurudi nyumbani, siku ya pili nilikuwa wa kwanza kuamka kuwahi shule tofauti na kaka aliyetakiwa kuamka kwa vile yeye ndiye aliyekuwa muhusika mkuu. Mama alitaka kunikataza lakini baba alimwambia aniache kwa vile ile ilikuwa nguvu ya soda.
Lakini siku zilikatika nikiwa mwanafunzi mwenye bidii na mdogo darasa zima, katika mtihani wa darasa la kwanza nilikuwa wa sita katika darasa la watu 45. Hiyo iliwashtua wengi hasa walimu ambao siku zote walinidharau kwa kuamini hasa kuandika kwangu nilisaidiwa na kaka yangu. Ajabu ilikuwa kaka yangu alikuwa wa thelathini mimi mdogo wake wa sita, ilikuwa kioja na kuwashtua watu wengi. Ukweli ulibakia pale pale katika mtihani wa kufunga muhula nilikuwa wa pili, nilizidi kujijengea heshima na kuwashangaza watu wengi.
Kila penye zuri hapakosekani wabaya , watu walianza kusema eti kwetu wachawi tunatumia uchawi mimi kushinda. Hawakuchoka kuzusha kwa kusema kwa vile kaka yangu alionekana yupo yupo, walisema eti familia yetu tumemgeuza ndondocha ili mimi nionekane nasoma zaidi.
Maneno yale nilipowapelekea wazazi wangu walinieleza niachane na maneno ya kunikatisha tamaa. Niliwasikiliza wazazi wangu kuanzia hapo nilianza kushika nafasi ya kwanza mpaka naingia sekondari. Nilichaguliwa kujiunga na sekondari ya kutwa. Nikurudisheni nyuma kidogo, tulipofika darasa la tatu, wakati mimi nashika nafasi ya kwanza kaka yangu alikuwa kifunga darasa yaani wa mwisho, imani ya uchawi ndani ya familia yangu ndipo ilipoanza kutawala na kuonekana wazi tunamtumia kaka yangu kama msukule ili mimi niwe na akili sana.
Hawakuamini mtoto mdogo kama mimi kuwazidi akili watu wazima niliokuwa nao darasa moja. Kutokana na ufinyu wa akili iliyotawala vijijini vingi visivyojua elimu ni nini, waliamini mwenye umri mkubwa ndiye mwenye akili. Kila kona nilipotembelea niliitwa mtoto wa kichawi
Itaendelea....