"
Vigezo vya kuteuliwa
"Wametaja vigezo vyao vyote, nimeangalia mimi ninavyo. Kama ni muda wa kutumikia chama nimejiunga na Chadema tangu mwaka 2004, tena nimeanza katika ngazi ya chini ya uongozi mpaka nikafikia hatua ya kuaminika na wanawake wenzangu na kunipa nafasi ya uenyekiti wa Taifa. Nimekuwa diwani kwa miaka mitano, nimekuwa mweka hazina wa madiwani wote wa Chadema."
Mbali na uongozi ndani ya chama, anasema amekuwa katibu wa mitandao ya asasi zilizo za kiserikali katika Wilaya ya Tarime, Mwenyekiti wa Wanawake wa Kanisa Katoliki Jimbo la Ukonga, Mratibu wa Asasi ya Mkamilishano Trust Fund iliyokuwa na makao makuu yake Ujerumani na Mwenyekiti wa Tukamilishane Women Association.
Elimu
Ni mhitimu wa kidato cha nne aliyepata pia mafunzo ya uuguzi nchini Ujerumani kwa muda wa miaka minne katika ngazi ya stashahada.
"Naweza kuzungumza vyema lugha tatu, Kiswahili, Kiingereza na Kijerumani, najiuliza kati ya wabunge wote wa viti maalumu kwa nini waniache wakati wapo wabunge waliochaguliwa ambao nawazidi elimu, michango katika chama, uwezo na hata muda wa kukitumikia?" anasema.
Mchango katika Chama
"Nimetoa michango mingi ndani ya chama. Mwaka 2006 nililipia pango la ofisi ya chama kwa pesa zangu mwaka mzima. Nilitoa pesa zangu nikanunua kiwanja kwa ajili ya kujenga ofisi ya chama huko Tarime. Kiwanja hicho kilikuwa katika Kata ya Nyanungu. Sasa hivi hiyo kata imegawanywa na kipo katika Kata ya Ikiryo."