Niliuwa kwa kukusudia-1

Niliuwa kwa kukusudia-1

Niliua kwa Kukusudia-17-

ILIPOISHIA:
Bosi na yule mgeni walinisisitizia kwa hamasa kubwa. Nikajikuta nimekubali na kunawa. Yule mhudumu akatumiminia kahawa na kutuwekea sawa vitafunwa. Akatukaribisha. Alipoondoka tu, bosi Elhakimu alinigeukia.

"Tunu."
"Abee, bosi."
"Huyu mdogo wangu ana shida ambayo naamini utaweza kumsaidia, najua huwezi kuniangusha."
SASA ENDELEA...


SIKUWA na haraka ya kuitikia. Nikabaki kimya huku nikiwatazama kwa zamu mmoja baada ya mwingine. Mapigo ya moyo yakawa yananienda mbio kwa kuwa sikujua kabisa jambo ambalo walitaka niwasaidie.
"Unasikia Tunu," Bosi alinishitua kutoka kwenye lindi la mawazo ambalo lilikuwa limenivamia ghafla kwa wakati ule.

"Nakusikia bosi."
"Shida yenyewe ni ndogo sana," bosi akazidi kusisitiza na kunifanya nimuangalie usoni hasa baada ya kusema kuwa shida yenyewe ilikuwa ni ndogo sana.
Alipofika hapo akatulia kidogo, akakohoa kisha kuendelea;
"Shida yenyewe ni kwamba anahitaji mtumishi wa ndani," alisema na kumtazama usoni yule mgeni ambaye alitingisha kichwa kuashiria kukubaliana na alichokisema bosi.

"Sasa, nakumbuka uliwahi kuniambia kuwa una mdogo wako kule kijijini, naona anaweza kufaa."
"Naomba utusaidie kumshawishi aje kufanya kazi kwa huyu mdogo wangu, naamini ni msichana aliyetulia kama wewe hivyo hawezi kuleta usumbufu," alisema Bosi Elhakimu na kunifanya nitabasamu kwa furaha.

Hakika alikuwa amegusa kwenye furaha yangu. Kwa siku nyingi sana nilikuwa nikiwaza ni kwa jinsi gani nitaweza kumtoa mdogo wangu huko kijijini ili aje kuishi nami Dar es Salaam.
"Umenisikia Tunu?" bosi aliuliza baada ya kuona niko kimya kwa muda.
"Nimekusikia bosi, nitafanya hivyo," nilimjibu huku nikionesha furaha ya hali ya juu kabisa.

"Nimefurahi kusikia hivyo, basi inapaswa uondoke sasa hivi kuelekea Chalinze ili kesho uje naye hapa maana huyu bwana anahitaji mtumishi haraka sana," alisema bosi na kumuangalia tena Ashraf ambaye alitingisha kichwa kama ishara ya kuunga mkono alichokizungumza bosi Elhakimu.
"Sawa, niko tayari."

Baada ya kauli yangu, bosi alimgeukia Ashraf.
"Umesikia bwana, yuko tayari kutusaidia."
"Nashukuru sana Tunu kwa hilo, sasa chukua hii kama nauli ya kwenda na kurudi pamoja na huyo mdogo wako," alisema Ashraf huku akinipa noti nyekundu ambazo kwa wakati huo sikujua ni kiasi gani.
"Ahsante."

"Sasa utapitia hukuhuku au utaenda hadi Buguruni ukaage nyumbani?"
"Itabidi niende Buguruni nikaage, lakini nitaondoka leo hii," nilimjibu kwa haraka.
Tuliagana, nikatoka nje ambako nilipitiliza hadi kwenye kituo cha mabasi nikarudi Buguruni. Nilipofika nyumbani nilimkuta shangazi akiendelea na shughuli zake. Akashituka na kuacha kila alichokuwa akifanya.

"Kulikoni tena, mbona umerudi asubuhi yote hii?" aliniuliza kwa hamaki kubwa huku akinitazama usoni.
"Nina safari ya kwenda Chalinze tena."
"Chalinze?"
"Ndiyo."
"Kuna kitu ulisahau?"
"Hapana, namfuata Inana."

"Inana! Wa nini?"
"Nimempatia kazi."
"Wapi na kazi gani?" shangazi aliuliza mfululizo.
Ilibidi nikae chini na shangazi ambapo nilianza kumuelewesha kwa kina zaidi. Nashukuru Mungu shangazi alinielewa.
"Kwa hiyo tutakuwa tukiishi naye hapa, siyo?"
"Hapana."

"Sasa atakuwa akiishi wapi?"
"Hukohuko nyumbani kwa bosi wake?"
"Wewe unawaamini hao watu?"
"Hawana shida shangazi."
"Sawa, lakini ni vizuri kuwa makini sana maana kwa sasa ulimwengu umeharibika."
"Sawa shangazi, mimi nawaamini."

"Mimi sina neno, kwa hiyo unasafiri kesho?"
"Hapana, inabidi niende sasa hivi, kesho nitakuwa hapa."
"Sawa."
Niliingia ndani na kuanza kujiandaa. Nikatoka na kushika njia.
"Haya shangazi, naondoka."
"Safari njema mwanangu."
"Ahsante."

Nikaanza safari ya kurudi Chalinze tena. Nikatembea hadi kituoni ambapo nilipanda mabasi ya kwenda Ubungo.
Nilikuta gari la Chalinze likiwa na abiria wachache. Nikakata tiketi na kuingia ndani ambapo nilichagua siti. Nikatulia na kuanza kuyafikiria maisha. Furaha niliyokuwa nayo haikuwa na maelezo, kwani kitendo cha Inana kupata kazi kilinifurahisha mno.

Muda mfupi baadaye, safari ikaanza, tuliwasili Chalinze majira ya saa tisa na nusu. Nikakodi baiskeli hadi nyumbani na kumkuta Inana akipepeta mchele.
Kabla sijamfikia, nilishangaa baada ya kumuona akijiinamia na kuanza kulia.


Je, nini kiliendelea? Usikose kufuatilia usiku wa leo......
 
Niliua kwa Kukusudia-18-

ILIPOISHIA KWENYE IJUMAA:
Muda mfupi baadaye, safari ikaanza, tuliwasili Chalinze majira ya saa tisa na nusu mchana.
Nikakodi baiskeli hadi nyumbani na kumkuta Inana akipepeta mchele.
Kabla sijamfikia, nilishangaa baada ya kumuona akijiinamia na kuanza kulia.
SASA ENDELEA...

Hali ile ilinishtua sana. Nikatembea kwa haraka kuelekea mahali alipokuwa amekaa. Nikamgusa begani na kumfanya ashtuke na kugeuka kuniangalia kwa hali ya uoga.
"Hee, dada Tunu umerudi tena?"
"Ndiyo mdogo wangu, mbona unalia kuna nini?"
"Nimekumbuka ndoto mbaya niliyoiota."
"Ndoto gani iliyokufanya hadi ulie?"

"Niliota tuko na wazazi, maisha ni mazuri na tunaendelea na masomo, sasa wakati nimekaa hapa, ghafla nikakumbuka ile ndoto ndiyo maana umenikuta nalia."
Kauli hiyo ilinifanya ninyongo'nyee sana. Moyoni nilijisikia uchungu na bila kutarajia nikajikuta nikilengwalengwa na machozi.

Sote tukawa katika hali ya maumivu. Kila mtu alilia huku akimbembeleza mwenzake.
"Basi Inana, naomba tuyaache hayo," nilimwambia mdogo wangu huku nikijifuta machozi kwa mkono wa kushoto.
"Sawa dada, lakini inauma sana."
"Achana na habari hizo, sasa tuangalie maisha upya."

"Nimekuelewa dada."
Sikuingia ndani kwa wakati huo, Inana alipeleka kifurushi changu ndani. Akarudi na kuungana nami huku akiendelea kupepeta mchele.
"Ehe habari za huko dada?"
"Nzuri za tangu jana?"

"Nzuri tu, mbona umerudi tena leo, kulikoni?"
"Nina habari njema sana Inana."
"Habari njema?"
"Ndiyo, mbona unashtuka hivyo?"
"Si wewe jamani?"

"Mimi nimefanyaje?"
"Si unanishtua kwa kusema una habari njema!"
"Usiogope, kuna nafasi ya kazi za ndani imepatikana huko hivyo nimekuja kukuchukua."
"Unasemaje?"
"Kama ulivyosikia Inana, kuna mdogo wake na bosi wangu yule Mwarabu, anahitaji msichana wa kazi za ndani."

Inana alivuta pumzi ndefu na kuzishusha taratibu. Furaha aliyokuwa nayo sina maelezo yake. Alifurahi mno. Nikamueleza kila kitu juu ya mpango huo wa kazi.
"Sasa nitakuwa nikiishi na wewe kwa shangazi?"
"Hapana Inana, utakuwa unaishi mahali unapofanyia kazi."

Tulizungumza mambo mengi sana. Inana akaandaa chakula cha usiku. Kilipoiva, tuliingia ndani na kuanza kula. Tulipomaliza nilimwambia Inana ajiandae kwa ajili ya safari kwani nilipanga tuamke mapema ili tuwahi kufika kwa ajili ya maandalizi ya kuonana na bosi.
Akafanya kama nilivyomuagiza, akaandaa kila kitu na kukiweka sawa tayari kwa safari. Alipomaliza aliniita na kuniomba tuombe dua kwa ajili ya kulala. Baada ya kuomba dua tulilala huku kila mtu akiwa kimya kwa kuwaza aliyoyaona yanafaa.
Kulipopambazuka, Inana alikuwa wa kwanza kudamka. Akaniamsha ambapo niliamka na kumkuta akiwa amekaa kitandani.
"Shikamoo dada."
"Marahaba Inana umeamka salama?"
"Salama kabisa dada, sijui wewe?"

"Salama kabisa, basi jiandae tuanze safari."
"Kila kitu kipo sawa dada, kuna kitu najiuliza."
"Kipi tena?"
"Hivi vyombo tunaviacha humuhumu?"

Tulijadili kwa muda kidogo. Baada ya majadiliano tulifikia uamuzi wa kumuachia vyombo mama mmoja aliyekuwa akiishi jirani yetu.
Tulimuita na kumpa maelekezo yote. Bila hiyana akakubali kuvichukua. Alipomaliza kuvisomba vyombo vyote, tuliingia bafuni na kuoga. Tulipomaliza tukaondoka hadi barabarani ambapo tulikodisha baiskeli hadi stendi ya mabasi.

Muda mfupi, lilitokea basi la Kilombero liitwalo Hood ambapo tulipanda na safari ya kuelekea Dar ikaanza.
Tulitumia saa nzima kabla ya kufika stendi ya mabasi ya mikoani ya Ubungo. Tukashuka na mabegi yetu na kuelekea kwenye kituo cha mabasi ya Buguruni. Tukajipakia na kuwasili saa tano na dakika ishirini asubuhi.Wakati tunafika nyumbani, shangazi hakuwepo na nyumba ilikuwa imefungwa hali iliyotulazimu kukaa nje na kumngojea shangazi arudi.

Tukaendelea kusubiri hadi alipowasili.
"Jamani kumbe kuna wageni?"
"Kama unavyoona mwenyewe, nimekuletea mgeni."
"Jamani Inana umekuwa hivi!" Shangazi alisema huku akionesha mshangao wa wazi kwa Inana.

Baada ya kusalimiana, tukaingiza mizigo ndani. Shangazi aliandaa chakula na kutukaribisha. Wakati wa kula nikamweleza shangazi kuwa napanga kumpeleka Inana kwa yule bosi anayemhitaji.
"Hiyo haina shida, ilimradi tu afajitahidi kuwa na heshima pamoja na bidii katika kazi," shangazi alianza kutoa nasaha zake kwa Inana.

"Kwa hayo sina shida naye. Kwa hiyo naamini hataniangusha," nikajibu na kumuangalia Inana.
Wakati tunaendelea na mazungumzo, shangazi alisema kitu ambacho kilitufanya mimi na Inana tushtuke.Je, nini kitaendelea?

Fuatilia leo usiku............
 
Back
Top Bottom