Niliuwa kwa kukusudia-1

Niliuwa kwa kukusudia-1

Mzizi mkavu ukiiweka unibeep ili isije ikapitiliza maana haina siku wala saa maalum. Unashtukia tu episode ya 17, 18...imeshapita!
 
Niliua kwa Kukusudia - 19


ILIPOISHIA:

"Kwa hayo sina shida naye. Naamini hataniangusha," nikajibu na kumuangalia Inana.
Wakati tunaendelea na mazungumzo, shangazi alisema kitu ambacho kilitufanya mimi na Inana tushituke.
ENDELEA SASA…


Ndiyo. Mimi na Inana tulishituka sana hasa kutokana na ukweli kwamba hatukutegemea kusikia maneno kama hayo kutoka kwa mtu kama shangazi.
Alisema: "Maisha hayawezi kutafutwa kwa kuajiriwa na watu hasa weupe." Ni kauli ambayo hakika ilinikata maini. Nikamwangalia Inana kwa macho ya huruma, naye alionesha kuumizwa na kauli hiyo.

"Hata hivyo, siwakatishi tamaa, endeleeni kupambana, huenda mkafikia malengo na ndoto zenu," aliendelea kutuambia shangazi au mama Shufaa kama wengi walivyozoea kumuita licha ya mtoto wake huyo kufariki dunia miaka mingi iliyopita.
Tuliendelea kula japo si kwa hamu ya chakula bali kwa kushiba na kuondoa njaa.

Muda mfupi, niliamua kujitenga pembeni na kisha kunawa.
"Mbona mapema sana?" shangazi aliniuliza kwa sauti ya chini.
"Nimetosheka shangazi," nikamjibu.

Ukimya ukazidi kutawala. Si shangazi, Inana wala mimi aliyefunua mdomo kwa wakati huo. Baadaye Inana naye alishiba na kuungana nami mahali nilipokuwa nimejiegesha.
Shangazi alipomaliza kula, akaingia ndani na kulala bila hata ya kutusemesha tena, hali ambayo ilizidi kutuchanganya mimi na Inana. Lakini hata hivyo, hatukutumia muda mwingi sana kuwaza juu ya kitendo kile.

Mimi na Inana tukalala pamoja na kujifunika shuka moja huku tukitandika jingine. Tukaukaribisha usingizi kwa ukimya wa ajabu. Katika ndoto ya usiku ule, niliota kuwa mimi na mdogo wangu tunaishi maisha ambayo ni ya kifahari sana. Katika ndoto ile, tulikuwa tumepata karibu kila kitu tulichokikosa utotoni.
Kulipopambazuka, nilikuwa wa kwanza kuamka na kumkuta Inana bado akiwa anaufaidi usingizi wa asubuhi uliokuwa ukisindikizwa na sauti za ndege wa asubuhi. Hakika alionekana kukolea kwa usingizi.
Ilipotimu saa moja kamili, nilimuamsha ajiandae ili nimpeleke kazini akakutane na mdogo wake na bosi ili waelewane jinsi gani ataanza kazi.

"Inana," niliendelea kumuita lakini alionekana kuzidiwa kwa usingizi. Lakini kutokana na kumuita kwa nguvu, aliamka na kukaa kitako kwenye kigodoro huku akijifuta usoni kama ishara ya kuyaweka sawa macho kwa ajili ya kukabiliana na hali ya mwanzo wa siku mpya.
"Shikamoo dada," alinisabahi huku akijiandaa kuvaa.

"Marhaba, umeamka salama?"
"Salama kabisa sijui wewe?"
"Salama, basi jiandae nikupeleke ukaonane na huyo bosi anayehitaji mtumishi, sawa?"
"Sawa dada."

Kwa muda huo shangazi alikuwa akiendelea na shughuli yake ya kukaanga chapati kwa ajili ya umama ntilie. Nikaenda kumsalimia kisha nikaingia bafuni.
Baada ya kuoga, Inana naye akaenda kuoga na alipomaliza tulivaa na kumuaga shangazi kwa ajili ya kwenda kazini.

"Haya nawatakia mafanikio mema," alijibu shangazi huku akituangalia mmoja baada ya mwingine.
"Haya, ahsante sana, nawe kazi njema," Inana alijibu kwa uchangamfu, japo si kwa hali ya kujiamini kwa asilimia zote kutokana na maneno ambayo shangazi alikuwa ameyatoa jana yake.
Tukaongozana hadi kwenye kituo cha mabasi ya Mwananyamala ambapo tulipanda na kukaa siti za karibu sehemu ya nyuma kabisa.

Safari ya kuelekea Mwananyamala ikaanza huku Inana akionekana kushangaa kila mahali tulipopita kutokana na ugeni wake ndani ya Jiji la Dar es Salaam. Kutokana na foleni kubwa iliyokuwepo kwa siku hiyo, tulitumia muda mwingi sana njiani.
Tulitumia mwanya huo wa urefu wa foleni kujadili mambo mengi ikiwemo mustakabali wa maisha yetu. Hatimaye foleni ilipungua na magari yakaanza kwenda japo kwa mwendo wa taratibu sana.
Mara itembee mara isimame, hakika siku hiyo kulikuwa na foleni ndefu sana. Lakini sikushangazwa sana na jambo hilo, kwani ni kawaida kwa Jiji la Dar es Salaam kuwa na foleni ndefu ya magari hasa kwa siku kama hiyo ambayo ni Jumatatu.

"Kwani dada, kwa kuwa mimi nitakuwa naishi mahali nitakapoanza kufanya kazi, wewe utaendelea kuishi na shangazi hadi lini?" Inana aliniuliza huku akiwa amenikazia macho.
"Kwa nini umeniuliza hivyo Inana?" nilimuuliza kwa shauku kubwa.
"Jibu swali dada Tunu, kuna kitu nimekiona kwa shangazi, ndiyo maana nimekuuliza," alisema Inana kwa msisitizo.


Je, nini kitaendelea? Usikose kufuatilia baadae .....
 
asante MziziMkavu kwa kijizawadi cha pasaka japo kimechelewa kuja ila shukrani sana Mungu akuzidishie
 
Last edited by a moderator:
Niliua kwa Kukusudia -20-

ILIPOISHIA:
“Kwa nini umeniuliza hivyo Inana?” nilimuuliza kwa shauku kubwa.
“Jibu swali dada Tunu, kuna kitu nimekiona kwa shangazi,” alisema Inana kwa msisitizo.
SASA ENDELEA…


ikuwa na haraka ya kuzungumza kitu. Nikabaki nimemtazama Inana kwa umakini wa hali ya juu sana. Alionekana kumaanisha alichokisema. Hapo nikabaki kimya na kuendelea kumtazama.
“Mbona huongei kitu na kubaki unanitazama tu dada Tunu jamani?” Inana alisema na kunishika begani huku akinitazama machoni kwa ukaribu zaidi.

“Nakusikiliza Inana, bado sijajua unamaanisha nini kwa maneno yako.”
“Hujaelewa nini Tunu?”
“Umesema kuna kitu umekiona kwa shangazi?”
“Ee dada, huamini?”
“Ni kipi hicho Inana?”

“Shangazi hataki uendelee kuishi hapo kwake, sasa anatafuta njia ya kukuondoa lakini hajaipata,” alisema Inana huku akiniangalia kwa umakini bila kupepesa macho.
“Mh!” Niliishia kuguna.

“Ndiyo hivyo dada,” Inana akaendelea kusisitiza zaidi.
Wakati huo foleni ikawa inatembea na muda mfupi baadaye tukawa tumefika kwenye kituo cha daladala cha Peace Mwananyamala. Tukashuka na kuanza kutembea kuelekea mahali ilipokuwa hoteli niliyokuwa nikifanyia kazi.

Tuliwasili na kuwakuta baadhi ya wafanyakazi wenzangu wakiwa wanajiandaa kwa ajili ya kuanza kazi. Tukasabahiana na baadhi yao huku mimi na Inana tukiingia upande wa mapokezi ambapo tulimkuta msichana wa mahali pale akiendelea na shughuli zake za kila siku.
“Habari za saa hizi dada?” nilimsabahi kwa uso wa uchangamfu wa hali ya juu.

“Salama kabisa Tunu, habari za siku nyingi jamani?”
“Nzuri tu, sijui wewe?”
“Salama, karibu.”
“Ahsante sana.

“Shikamoo,” Inana naye akamsalimia.
“Marahaba jamani, mzima?”
“Salama tu, pole kwa kazi.”
“Ahsante sana, Tunu huyu ni mdogo wako? Maana mnafanana sana!” aliniuliza yule dada wa mapokezi baada ya kujuliana hali na Inana.

“Eee, ndiye anayenifuata.”
“Sawa, mnafanana kama mapacha.”
Baada ya kuzungumza na dada huyo, nilimuuliza kama tayari bosi Elhakimu alikwisha wasili ofisini. Alinitaarifu alikuwepo.

Mimi na Inana tuliongozana hadi ofisini na kumkuta bosi akiwa anaandika kitu kwenye tarakishi yake ya mkononi (laptop).
“Oooh, karibuni sana Tunu,” alitukaribisha yule bosi huku akionesha uchangamfu ambao hapo awali sikuwahi kumuona nao.
“Ahsante sana, shikamoo bosi.”

“Marahaba Tunu, habari za huko nyumbani?”
“Salama.”
“Shikamoo,” Inana alimsabahi.
Baaada ya kusalimiana na kujuliana hali, nikamtambulisha Inana kwa bosi huku nikichombeza kwa utani jinsi alivyonigonga na gari lake kule Chalinze.

Tukazungumza kwa uchache. Baada ya muda yule bosi akachukua simu yake ya mkononi na kubonyeza namba fulani kisha akaipeleka simu sikioni.
Muda mfupi kidogo akaanza kuzungumza na mtu wa upande wa pili ambaye mimi na Inana hatukumjua.

“Eee, tayari wameshafika, sasa uko wapi Ashraf?” alisema bosi katika mazungumzo hayo ndipo nikajua kuwa alikuwa akizungumza na yule mdogo wake aliyehitaji mtumishi wa ndani.
“Amesema anakuja muda si mrefu, hivyo huyu anaweza kungojea, wewe Tunu unaweza kuendelea na majukumu yako kama kawaida, akija unaweza kuja tena.”

Nikaondoka na kwenda nje ambako nilipitiliza hadi kwenye chumba cha kubadilishia nguo. Nikaungana na wafanyakazi wenzangu kufanya usafi ambapo siku hiyo nilipangiwa kukatakata maua na kuyamwagia maji.
Baada ya muda, alikuja msichana mmoja na kuniambia kuwa ninaitwa ofisini kwa bosi. Nikamfuata na kuingia moja kwa moja hadi ofisini kwa bosi ambako nilimkuta yeye, mdogo wake pamoja na Inana.
Nikamsabahi Ashraf kisha nikaketi kwenye moja ya viti.
Utambulisho ukafanyika na Ashraf akaridhika na Inana kuwa anafaa kuwa mtumishi wake wa ndani japokuwa sikujua alitumia kigezo gani kujiridhisha na Inana.
“Anaonekana ni mchapakazi sana, nimeridhika naye kwa kila kitu,” alisema Ashraf huku akitutazama usoni kwa zamu.

“Kweli kabisa, hata mimi naona,” alidakia bosi Elhakimu na kumfanya Inana atabasamu na kutazama chini kwa aibu ya kike.
Tukakubalina kuwa waondoke hadi nyumabani kwa Ashraf. Lakini kabla hawajaondoka, yule Mwarabu alilala ubavu na kutoa pochi yake ambapo alichomoa noti nyingi nyekundu na kuanza kuzihesabu mbele yetu. Hakika zilikuwa pesa nyingi.

Akanikabidhi huku akinishukuru kwa kumtafutia msichana wa kazi kwani alikuwa akihangaika sana.
Wakati akinikabidhi zile pesa, Inana aligeuka na kutuangalia lakini walipokutanisha macho na Ashraf, wote wakatabasamu na kunifanya nishtuke.


Usikose kufuatilia leo usiku....
 
Hapo ndo penye ile nyimbo ya kiswahili chenye lafudhi ya kiarabu inapogonga mu kichwa cha mbalu "Kama madaka tende nunua kama madaka khalua nunua h'alah'ala makun.u fanuaaa... thank MziziMkavu
 
Last edited by a moderator:
Niliua kwa Kukusudia-21-

ILIPOISHIA :
Akanikabidhi huku akinishukuru kwa kumtafutia msichana wa kazi kwani alikuwa akihangaika sana.
Wakati akinikabidhi zile pesa, Inana aligeuka na kutuangalia lakini walipokutanisha macho na Ashraf, wote wakatabasamu na kunifanya nishituke.
SASA ENDELEA…

NIKAWATAZAMA tena usoni kwa zamu. Kila mmoja alijawa na furaha, nikazidi kubaki njia panda. Nilijiuliza maswali mengi ikiwemo inawezekana vipi watu ambao hawajawahi kuonana waweze kuzoeana kwa muda mfupi namna hiyo hadi kufikia hatua ya kuachiana tabasamu murua kama lile.
Mshangao wangu uliongezeka kutokana na uchangamfu wa ajabu aliouonesha Inana kwa Ashraf. Nilishangaa kwa kuwa namjua vyema mdogo wangu Inana. Si mtu wa kutabasamu hovyo. Hasa kwa mtu asiyemjua hata kama atamfurahisha vipi.
"Ahsante sana jamani, Mungu akubariki," nilimshukuru Ashraf.
"Wala usijali Tunu, mimi napaswa nikushukuru kwa msaada wako," alisema Ashraf na kumgeukia tena Inana ambaye awamu hii aliinama chini kwa aibu.

Baada ya mazungumzo ya hapa na pale, Bosi Elhakimu aliwaruhusu waondoke nami nikaendelea na majukumu ya kazi za siku hiyo. Inana na Ashraf waliondoka. Nikawa namuangalia mdogo wangu kwa macho ya huzuni ingawa sikujua hasa huzuni ilitokana na nini.
Wakatembea hadi nje ambako Ashraf alikuwa ameegesha gari lake la kifahari aina ya Toyota Land Cruiser V8. Lakini kabla hawajapanda, nikamuita Inana na kuzunngumza naye kidogo.
"Inana mdogo wangu," nilimuita kwa sauti ya chini na ya upole mno hali ambayo hata yeye ilimfanya anitazame usoni kwa mshangao.

"Bee dada."
"Nakutakia kazi njema, lakini kuwa mwangalifu sana."
"Sawa dada, nitafanya hivyo."
"Jitahidi kufanya kazi kwa bidii na juhudi kubwa, si unayaona maisha tunayoishi kwa sasa?"
"Ndiyo dada yangu, nitajitahidi."

Baada ya mazungumzo hayo, Inana na Ashraf waliondoka na kuniacha nikiwa nawasindikiza kwa macho hadi walipopotea kabisa kwenye upeo wa mboni zangu.
Moyo uliniuma sana. Uliniuma kwa mengi lakini kubwa ni kuwa nimewezaje kumruhusu Inana aende mahali ambako hata mimi sikupajua, hata kama nilimuamini sana Bosi Elhakimu.

Nilirudi na kuendelea na majukumu yangu kama kawaida. Siku nzima nilishinda bila raha kabisa. Muda mwingi nilikuwa nikimuwaza Inana. Moyoni nikawa namuomba Mungu amtangulie na kumuepusha na mabaya yote.
Muda wa chakula ulipowadia, mimi na wafanyakazi wenzangu tuliongozana hadi kwenye bohari la chakula. Nilikula huku nikiwa nimezongwa na mawazo tele kichwani.
"Tunu vipi, mbona kama hauko sawa kulikoni?" alikuwa msichana mmoja ambaye ni mfanyakazi mwenzangu aliyetaka kujua kilichonisibu kutokana na hali yangu.

"Hapana, niko sawa Misoji," nikamjibu huku nikionesha uchangamfu wa bandia.
"Nimeona kama hauko sawa, unaonekana mwenye mawazo."
"Hapana, ni ukimya wa kawaida tu."
"Sawa, lakini naona kama hauko sawa kabisa."

Sikuendelea kumjibu zaidi ya hapo. Ni kweli kabisa sikuwa sawa licha ya kujilazimisha kuchangamka.
Tulipumzika kidogo, lakini kichwa kilianza kuniuma kwa mbali. Nikajilazimisha kufanya kazi. Hatimaye ukawadia muda wa kuondoka. Nikaenda kubadili nguo na kuanza safari ya kurudi Buguruni kwa shangazi.

Nikiwa ndani ya basi kuelekea nyumbani, maneno ya Inana kuhusu matendo ya shangazi yakaanza kujirudia. Hakika yalionekana kuwa na ukweli ndani yake.
"Lazima nitafute chumba cha kuishi peke yangu. Tena maeneo haya haya ya karibu na kazini kwangu.

Nilipofika nyumbani sikutaka mazungumzo ya aina yoyote na shangazi zaidi ya salamu. Nikajilaza kwenye kile kigodoro changu cha kila siku. Kutokana na wingi wa mawazo na uzito wa kichwa, nilijikuta nikipitiwa na usingizi.
Niliamka ikiwa ni saa nne usiku, shangazi alikuwa ameshalala, nikaenda kujisaidia na kurudi kulala. Asubuhi niliamka mapema na kwenda kazini. Jambo la kwanza kufanya ni kuuliza mahali kulipokuwa na chumba cha kupanga maeneo hayo ya Mwananyamala.
Nilipata chumba na kuridhika nacho. Nikaamua kuomba kiasi kidogo cha pesa ili niongeze nilipie chumba.
Nikaamua kwenda ofisini kwa bosi ili kumuomba pesa hiyo. Moyoni nilipanga kuhamia kabisa siku iliyofuata. Nikapanga kumbembeleza bosi kwa kiwango kikubwa ili aweze kunipa pesa hiyo.
Niliingia ofisini, lakini nilishituka kumkuta bosi akiwa ameshika bunduki aina ya bastola huku akiifuta kwa kitambaa, nikabaki nimetoa macho.

Je, nini kiliendelea? Fuatilia leo jioni
 
Ivi sasa ivi sio jioni eeh?inaanzia saa kumi basi mzizi ufanye kweli
 
Back
Top Bottom