Niliua kwa Kukusudia -22-
ILIPOISHIA
Niliingia ofisini, lakini nilishtuka kumkuta bosi akiwa ameshika bastola huku akiifuta kwa kitambaa, nikabaki nimetoa macho.
SASA ENDELEA…
PAMOJA na kwamba ilikuwa ni mara yangu ya kwanza kuona bastola ana kwa ana, hali ile ilinishtua sana. Nishtuka kwa mengi, kwanza sikuwahi kuwaza au kufikiria kuwa yule Mwarabu alikuwa akimiliki silaha ya aina hiyo.
Nikabaki nimetoa macho mithili ya mjusi aliyekuwa amebanwa na mlango. Huku mwili ukinitetemeka, nilijikaza na kumuamkia.
"Shikamoo bosi."
"Marahaba," aliitikia huku akiendelea kuifuta ile bastola na kuigeuza mara kwa mara. Hakuonekana kabisa kujali uwepo wangu ofisini kwake.
Kila mara, uoga wangu ulizidi kuongezeka. Hali hiyo ilichangiwa na kumuona akiwa katika uso wa hasira sana. Hakika niliogopa kuliko maelezo.
"Vipi, mbona unashtuka na kuonesha woga kiasi hicho?" aliniuliza na kunisogelea kitendo kilichozidisha woga maradufu moyoni mwangu. Bila kutarajia nikaanza kutetemeka.
"Hii inaitwa bastola aina ya Beretta, inanisaidia kujilinda kwa mambo mengi sana," akasema na kuisogeza karibu yangu. Ilitisha kwa kuitazama tu. Akazidi kunisogelea, aliponifikia akanishika begani kwa kutumia mkono mmoja. Hapo nikazidi kujawa na hofu kubwa. Kijasho chembamba kikawa kinanichuruzika.
"Usiogope, hii ni silaha ya kawaida sana, ukitaka kuitumia unafanya hivi," alianza kunielekeza namna ya kuitumia.
Akanifundisha kila kitu. Nikajikuta nikivutiwa na jinsi ya kuitumia ile bastola. Ghafla hofu na woga wa awali ulianza kunitoka. Sijui ni kwa nini lakini huenda ni kutokana na lugha laini ambayo alikuwa akiitumia huyo Mwarabu yaani bosi Elhakimu.
Baada ya maelekezo yake, nikamweleza shida yangu ambapo tofauti kabisa na matarajio yangu, alikubali kirahisi mno kunisaidia kiasi cha pesa kilichohitajika kukamilisha upangaji wa chumba.
Akarudi kwenye kiti chake. Taratibu akafungua droo iliyokuwa chini kabisa ya meza yake. Akaiweka ile bastola kisha akanitazama usoni huku akitabasamu.
Alinitazama sana usoni hali ambayo ilinifanya nione aibu na kuishia kuinama na kuanza kupikicha vidole vyangu.
Akachukua kalamu na kikaratasi kidogo na kuanza kuandika maandishi ambayo sikuyaelewa kutokana na umbali uliokuwepo kati yetu.
"Sikiliza Tunu, mimi siwezi kukukopesha pesa ila nimeamua kukusaidia, sawa binti mzuri?" akasema na kunifanya nishtuke tena. Kilichonishtua si kitendo cha kunisaidia ila ni ile kauli ya kuniita binti mzuri. Kwa jinsi ambavyo nilikuwa nikiheshimiana na huyo Mwarabu, tena akiwa bosi wangu, hakuwahi kuniita jina kama hilo tofauti na Tunu.
Akachukua simu yake ya mezani na kupiga namba fulani. Muda mfupi baadaye, aliingia msichana mrefu mwembamba, mweupe na mchangamfu sana.
"Tunu," aliniita yule bosi.
"Bee," nikaitika na kumtamza usoni.
"Huyu ni mhasibu wetu, anaitwa Zulekha, naomba uongozane naye ili akupatie hiyo pesa ambayo naamini itasaidia mahitaji yako."
Licha ya kutomtajia bosi ni kiasi gani cha pesa nilichohitaji, nilishangaa akisema kuwa anaamini kitasaidia kukidhi mahitaji yangu. Nikaongozana na yule mhasibu hadi ofisini kwake.
Wakati tunaondoka, yule bosi Mwarabu akaniambia nipitie tena ofisini kwake kuna maagizo aliyotaka kunipa.
Tulipofika ofisini kwa mhasibu huyo, alichukua bahasha na kuanza kunihesabia pesa alizoagizwa na bosi anipatie. Akanikabidhi kisha nikaondoka. Nilipofika nje, nikaanza kuzihesabu zile pesa ambazo zilikuwa ni shilingi laki mbili na nusu. Sikuamini hata kidogo. Kwa mbali nikaanza kumuona yule Mwarabu kama mkombozi wangu maishani. Niliamini hata kitendo chake cha kunigonga na gari kule Chalinze, ulikuwa ni mpango wa Mungu.
"Nimeamini kila jambo hutokea kwa makusudi, kumbe huyu Mwarabu kunigonga na gari ulikuwa ni mpango mkubwa wa Mungu, ahsante Mola wangu," nilijikuta nikitamka maneno hayo.
Baada ya kuzihesabu, nikazirudisha kwenye bahasha kisha nikaelekea ofisini kwa bosi ili nikamsikilize tena alichoniitia. Moyoni nilijawa na furaha ya ajabu mno.
Kila aliyeniona kwa wakati huo, aliweza kung'amua kwa haraka sana furaha niliyokuwa nayo. Hakika nilifurahi, nashindwa hata kuelezea ni furaha ya kiwango gani.
Nikafungua mlango wa bosi na kumkuta akizungumza na simu. Alipomaliza alinigeukia akiwa na uso wa huzuni.
Usinione nina uso wa huzuni hivi, nina habari kutoka kwa yule mdogo wangu, zinamhusu mdogo wako," akasema na kunikazia macho kauli iliyonifanya nishtuke kwa nguvu.
Je, Inana amepatwa na nini? Fuatilia