Ndoa Yangu

Ndoa Yangu

SEHEMU YA 31

"One, hakika nakupenda sana na nilikuamini kila ulichonambia katika maisha yako. Nilikusikiliza na wala sikuwahi kukuhisi vibaya. Hakika ulipendeza machoni mpaka moyoni mwangu kila nilipofumba mboni zangu niliiona taswira yako. Sikuwahi kutegemea wala kuwaza kama nitakuja kuingia katika mkosi wa mapenzi tena katika wakati muhimu zaidi. Wakati wa kuunganishwa kuwa mwili mmoja. Hakika umeniumiza na kunitia aibu kuu mimi na wazazi wangu. Sijajua kwanini uliamua kudanganya lakini sitaki kukuhukumu kwa hilo. Ua hili nililokuletea ni ishara ya upendo wangu wa dhati kwako lakini sina uhitaji wowote tena. Nakusihi uishi na mkeo. Kwanza ni mzuri sana mwenye kuvutia pia ni msomi. Wazazi wangu wamekusamehe na hata mimi sina kinyongo zaidi nimekuja kukuaga zimebaki siku chache nasafiri kuelekea London kwa mapumziko ya muda na sidhani kama tutaonana tena One. Sitamani wala siwezi kuvumilia maumivu haya hapa nyumbani. Naelekea kwa mjomba London One baki na mkeo na usije thubutu kufanya kinyume kama ulivyotaka kufanya kwangu. Kumbuka ni dhambi hata Mungu hapendi. Kwaheri One huna haja ya kunihadithia chochote nishayasikia yote ya nyuma kwenye maisha yako. Hakika mkeo Atuganile bado anakupenda sana nakusihi umpende na umuheshimu. Ahsante!"
Hayo yalikuwa ni baadhi ya maneno kati ya mengi aliyoongea Rose siku hiyo na kunifanya midomo inicheze na kuzungumza kwa hisia na uchungu.
"Ro...Ro...Rose tafadhali aaah! Rose hujui kitu. Mimm...." Kabla hata sijamalizia kusudi langu la kusema mara niliwashuhudia wazazi wa Rose nao wakiingia wakiwa sambamba na baba mchungaji. Ilibidi nimung'unye tu maneno na kujikaza.
Rose alinitazama kwa na kuniaga kwa ishara ya macho huku akiwapisha wazazi wake ambao niliwaonea aibu na kujisikia viabaya moyoni. Ingawa wao walionesha utu na kunifariji lakini niliona ndio kwanza utu wanaonionesha unazidi kuniumiza na kunidhihirishia dhambi zangu kwao. Mchungaji alifanya maombi na kuniombea pale huku wakimshukuru Mungu kwa kuzidi ifanya afya yangu kutengemaa.
"Onesmo mwanangu. Hupaswi kuumia kichwa kufikiria yaliyopita. Najua na nina hakika lengo lako halikuwa baya nafsini mwako kutokana na ukomo wa fikra tu. Mimi nimekusamehe pia nakupa pole kwa gharama zote zilizoenda bure pasipo kutimia jambo kusudiwa. Tumefanya mawasiliano na mkeo zaidi ya mara tatu na tumejaribu kuzungumza na uongozi wa kanisa Iringa wamewaita na wamezungumza nao na nina hakika sasa atarudi kuwa mke mpya bora na mzuri katika maisha yote ya hapa suniani. Hakuna kitu cha kuwatenganisha zaidi ya kifo tu. Nitaporudi London baada ya kumpeleka Rose akatulize kichwa chake. Nitakutimizia nusu ya yale yote niliyoyakusudia kukupa pindi utapomuoa binti yangu ili maisha yenu yaendelee kuwa katika mstari mzuri. Najua kwa hali uliyo nayo hupaswi kuumiza sana kichwa kufikiria vipi maisha utakabiliana nayo. Tuliza tu kichwa One wewe bado utaendelea kuwa mwanangu. Bwana ameipa mamlaka sauti yako usiache kumuimbia na kumsifu. Ugua pole mwanangu uponywe kwa damu ya yesu katika jina la baba, la mwana na la roho mtakatifu. Ameen."
Aliongea baba Rose maneno yaliyonitoa machozi nikishindwa jua nimshukuru vipi. Nilishindwa kabisa nimuweke kwenye kundi la wema kiasi gani baba yule. Daaah! hakika nilijiona mwenye bahati niliyevikwa joho la mikosi. Baba Rose alisema nami pasipo kuonesha kinyongo wala maono mabaya dhidi yangu.
*******
Saa zilikatika na siku tatu mbele zikapita nikizidi kuwa mzima na hatimaye nikaruhusiwa hospitalini. Kila siku mtu mwengine ambaye hakukauka hospitali alikuwa ni Sulu. Alinifariji sana kwa kweli zaidi ya sana. Hata siku naruhusiwa yeye ndiye aliiendesha gari yangu ambayo nilipewa na baba Rose. Tukiwa sambamba na dada zangu tulifika nyumbani kule nilipokuwa naishi. Watu wengi walionijua na wale waliopata mkasa wangu hawakukauka kunipigia simu na kuja nijulia hali. Ingawa nilidhoofika kimwili kwa kupungua mpaka uzito wangu wa kawaida lakinikupona kwangu wengi hawakuamini kwa vile wapo ambao walishazusha kuwa nilifariki kule hospitali. Wengi walishazoea kuwa wakisikia mtu amelazwa wodi ya wagonjwa mahututi basi imani zao huwapelekea kuwa huyo ni mtu wa kufa tu. Si hivyo! walisahau kuwa kuugua si kufa. Nilipona japo furaha ilienda likizo. Muda wote nilikuwa mkimya nikiwa sina hata hamu ya kwenda kuliona kaburi la mamaangu. Wala hakuna mtu aliyenigusia msiba wa mama kwa haraka hata niliporuhusiwa hospitali na kuwa nyumbani. Dada zangu walinifariji kwa maneno ya hekima na kutia nguvu huku Sulu akiendelea kunisisitizia kuchangamka kama ilivyokuwa kawaida yangu. Ucheshi wote uliniisha. Sikuwa mtu wa maneno ya utani wala mchangamfu tena. Muda wote nilikuwa mkimya kama kobe. Moyo wangu pekee ndio ulikuwa unanijua nini nafikiria na vipi najisikia.
"Lazima nilipe kisasi! hapana! Atuganile sikuachi wewe na mamaako mtaiipa roho ya mamaangu kwa roho nzenu." Nilisema na akili zangu huku mawazo yakinituma kufunga safari ya Kyela kwenda kulipa kisasi hata kwa kuwachomea moto ndani kina Atuganile. Hakuna cha zaidi nilichofikiria zaidi ya hiko.
Usiku wa siku niliyoruhusiwa hospitalini ndiyo siku ambayo baba Rose alikuwa anampeleka bintiye London kwa mjombaake. Walisindikizwa hadi uwanja wa ndege salama.
Sikuwa najua kama siku hiyo ndiyo walisafiri hadi pale majira ya saa kumi jioni niliposikia sauti ya dadaangu mmoja akija akilia huku ameshika mikono kichwani.
"Dada vipi?" Niliuliza kwa mshtuko wakati huo nilikuwa nimekaa sebuleni na Sulu tukitazama mkanda wa video.
Dadaangu yule ambaye alikuwa mwanakwaya pia aliendelea kulia pasipo kunyamaza hata alipokuwa anabembelezwa na wenzake.
"Dada Angel kwani vipi? mbona Sara analia sana?" Aliuliza Sulu ambae alikuwa anaijua familia yetu yote vizuri tu nao walikuwa wanamtambua vyema.
"Alikuwa ametoka kuelekea kanisani kwenye mazoezi ya kwaya muda si mingi. Sasa ndio amerudi saa hizi akilia hata sisi anatutisha kwanini hasemi kimlizacho."
Alijibu dadaaangu yule mwengine. Moyo wangu uliripuka muda huo na kuhisi naikosa amani. Nilichukua simu yangu iliyokuwa pembeni lakini kabla sijafanya chochote ziliingia meseji tatu kwa mpigo kutoka kwa watu tofauti.
Moja ilisema.
'ROSE MASIKINI..'
Nyengine ikaandikwa.
'HIVI NI KWELI KAKA HIKI TUKIONACHO BECKER TV DAAAH SIAMINI'
Nilistushwa zaidi na kujikuta naisoma nyengine ambayo nayo ilisomeka
'POLE SANA ONE KWA MITIHANI MIZITO. R.I.P ROSE'
hii sasa ndiyo ilinichanganya kila kitu wakati huo na kukurupuka kuwasha king'amuzi huku nikibadili chaneli haraka na kuiweka Becker TV pasipo kumwambia chochte Sulu aliyebaki akinishangaa.
Machozi tayari yalianza kunitoka huku nikiwa naikodolea macho tv kuona habari gani hiyo. Dada aliyekuwa analia wakati huo naye alijitahidi kutuliza mzka na kuanza wahadithia kwa kwikwi na shida wenzake kilichokuwa kimemfanya alie vile.
Laaaaa haulaa! ama kweli ng'ombe wa masikini hazai na wa moja havai mbili. Taarifa ya habari iliyokuwa inatangazwa Becker TV wakati ule ilimstua kila mtu hata Sulu alijikuta anashika mikono kichwa.
"....................ndege hiyo pekee kutoka shirika la ndege Tanzania iliyokuwa inafanya safari kuelekea London ilikuwa na abiria takribani 35, marubani 3 na wahudumu 6 na wote wanaripotiwa kufariki katika mlipuko huo unaosemekana umesababishwa na kikundi cha kigaidi waliodhani ni ndege ya kijeshi iliyokuwa inakatiza kwenye anga yao. Mungu azilaze roho za marehemu wote peponi. Becker TV tunatoa pole kwa wanafamilia wote na watanzania kwa ujumla."
Habari ilikuwa inaishia lakini tayari ilitosha kutuzibua macho na masikio kwa kilichotokea ambacho sikutaka kukiamini kabisaaa.
"Ndiooo! ndege waliyosafiri nayo ndiyo iliyolipuliwa jamani wifiii yangu Roseeee"
sauti ya dada mkubwa nayo niliisikia ikilia kwa uchungu na hapo ndipo simu yangu ilipozidi kuita na kuingia meseji za watu tofautitofauti na kunivuruga.
Ooooh! yaani Rose ndio awe ametutoka hivi hivi? Aaaaah! sikutaka kuamini hata nilipompigia simu baba mchungaji ambae naye alithibitisha kutokea kwa ajali hiyo mbaya ambapo ndege iliripuliwa na kubaki majivu. Hakuna kilichotoka ndani yake. Magaidi waliua watu wasio na hatia. Rose na babaye walisafiri kwa ndege ile iliyogeuka kuwa kaburi lao.
"Roseee! hapana Roseee oooh Rose wanguuuuu?"
Nilianza kulia taratibu huku Sulu naye akinifariji kwa kunizuia pasipo kufanikiwa.
Niliyakumbuka maneno ya Rose na yale ya babaake siku chache nyuma hospitalini. Ina aana yale yalikuwa maneno yao ya mwisho na sitowaona tena? Niliumia zaidi kila nilivyotafakari chanzo cha yote hasa kinarudi palepale kuwa ni NDOA YANGU.
Ndoa iliyosababisha sasa vifo vya watu watatu sambamba na mamaangu. AaaH
'Asante One. Kwa sababu ya ndoa yako imelazimisha mwanangu asafiri kwenda mbali kutafuta pumziko na kuipata faraja. Na kweli sasa amepata pumziko la milele. Umenisababishi ukiwa sina mke sina mtoto. Asante One kwa kuisambaratisha familia yangu.'
"ROOOOOOOOZZIIIIIIIIIIIIIIIIIIIIIIIIIIIIII"
Nililia kwa sauti kuu ya maumivu huku nikisujudu na kupigapiga mikono chini baada ya kupokea ujumbe wa kuthibitisha ajali ile kutoka kwa mama Rose mwenyewe ambae alionesha wazi amenichukia na kuniweka kuwa chanzo cha ma5tatizo yote. Aaaah! ingawa inaweza nisiwe kwenye chanzo lakini kwenye ndoa yangu kuna chanzo. Oooooopppphhhh!!!! Buriani Rose wangu. Nisamehe uko ulipo aaaah!
 
SEHEMU YA 32

Ama kweli jeraha linapochimba sana maumivu hupitiliza na mwili kuingiwa ganzi. Na ndivyo ilivyokuwa. Safari hii baada ya kulia sana na kupiga piga sakafu huku nikibembelezwa na kutulizwa na Sulu mwishowe nilijikuta nikicheka badala ya kulia.
Sikucheka eti kwa sababu nimefurahi! bali nilijikuta nikicheka kwa kujishangaa na kupagawa.
"Sulu haya ndio maisha na hii ndio ndoa yangu. Imenifanya nimkose mama, imenifanya nimkose Rose, ona nimemkosa mpaka babaake ambae alijitoa kunisaidia na kunirudisha katika mstari niliopotea. Sulu usihuzunike rafiki yangu."
Niliongea kana kwamba si mimi niliyekuwa nalia muda mfupi uiopita. Niliwanyamazisha daa zangu ambao walipagawa sana kwa taarifa za msiba ule uliotuumiza kwa namna yake. Nilijua sasa sina msaada tena. Mama Rose tayari amejenga chuki akiamini laiti ingekuwa si mimi kusema uongo na kuleta kizaazaa cha ndoa kanisani hadi kumvuruga akili bintiye ambae alizimia siku nzima hospitali, basi safari ile isingekuwepo hivyo aliamini bintiye na mumewe wangeendelea kuishi. Hata mwenyewe nilijiona kweli ni mkosaji. Lakini majuto mjukuu na niliyokosewa kwenye ndoa yangu hakuna aliyetaka nimsimulie tena kwa kuwa nilishawahiwa na wanafiki kina Atuganile wachawi walioshindika.
Habari za ajali ile ya ndege zilisambaa kama upepo kwenye vyombo vya habari na majina ya abiria waliokuwamo ndani ya ndege kila yalipotajwa yalizidi kuniumiza moyo pale nilipolisikia jina la Rose. Picha yake ilijirudia kwenye fahamu zangu tokea namuona mara ya kwanza pale kanisani. binti mcheshi aliyeishiba dini. niliamini atakuwa kwenye mikono salama ya malaika akistarehe mawinguni. Niliumia na kulia na moyo wangu nafsini ingawa ujasiri wa hali ya juu safari hii ulinivaa. Sulu alirudi kwake usiku huo tukikubaliana mapema kufika msibani mapema kesho yake kujua taratibu zitazofnyika katika msiba ule mkubwa ambao ilionesha thabiti hakutakuwa na maiti kutokana na miili yote kuteketea vibaya kwa mlipuko huo uliosababishwa na kombola la magaidi. Nilimuitikia Sulu na kumsindikiza ihali kichwani mwangu nilishaamua mambo mengine. Nilijiona nisiyestahili kuvuta kuendelea kuvuta pumzi ihali nimekuwa chanzo cha kuwakatisha maisha watu niwapendao ambao walionesha upendo wa kweli kwangu.
Nilikitamani kifo. Hakika nilitamani kufa lakini si kwa kuwapa mzigo ndugu zangu. Nillifikiria nikafe mbali na pale lakini kabla ya kuondoka niwe nimeacha msaada mkubwa kwa niaba ya maisha yao. Nilimkumbuka mtotowa dada ambae alishindwa kuendelea na masomo kwa kufeli la saba ihali alikuwa na akili za shule. Nilirudi nyumbani nan kujifungia chumbani kwangu na hapo ndipo nilipochukua kalamu na karatasi na kuandika barua hii niliyoiacha mezani sambamba na viambatanisho kusudiwa vya barua ile.
'Dada zangu wapendwa. Kabla ya yote napenda kuwakumbusha kuwa nawapenda sana. Awali nilikuwa na ndoto ya kuwa na maisha mazuri baada ya tabu tulizopambana nazo tangia kifo cha baba etu. Niliamini ndoto hizi zinaenda kutimia mara baada ya kupata kazi za miradi ya umeme hususani nilipoajiriwa na kwenda jijini Mbeya. Lakini ndoto hizi zimebaki kuwa ndoto endelevu. Furaha ya kupata mke bora ambae nyote mlimsifu ndio imegeuka kuwa mwiba mkali uliopasua puto la ndoto za maisha yangu. Kwa sasa sina tumaini tena katika ulimwengu isipokuwa nina haki ya kwenda kupumzika kwa baba nikisubiri hukumu. Hukumu juu ya ndoa yangu. Siyaandiki haya eti kwa kuwa nimechanganyikiwa, la hasha bali naomba msome mpaka mwisho barua hii wala msichanganyikiwe.
Kwa moyo wangu mkunjufu nimeamua kumfata Rose huko aliko huenda mambo yakawa mazuri na tukaishi pamoja baada ya kushindikana hapa kwenye ulimwengu wa kina Atuganile. Dada mkuu. Nimeambatanisha kadi ya gari yangu juu ya barua hii kwa lengo moja. Mfanye hima kuliuza ili pesa mtayopata basi itumike kumsomesha mpwa wangu. Hii ni ahadi ambayo nilishindwa itekeleza awali lakini sasa inapaswa iwe hivyo. Kila kilicho changu nimekiandika hapa na kuanzia sasa ni halali yenu. Naomba mfikishe salamu nyingi kwa rafiki yangu Sulu. Mmwambie kuwa nimeenda safari isiyo mrejeo. Msihangaike kunitafuta wala kuutafuta mwili wangu popote kwani hamtauona zaidi mtapoteza muda na pesa. Sina cha kuwapa ndugu zangu zaidi nadhani kwa umri huu unatosha. Msiache kuwalea wajomba zangu katika maadili maazuri na siku zote mkumbuke kuwa hakuna chochote kilichopelekea haya zaidi ya kusudio la Mungu mwenyewe. Kupitia NDOA YANGU msisikitike wala kutafuta kulipa kisasi kwani.... chozi langu litalipwa.
Ni mimi kaka enu mpendwa. Onesmo'
Niliihitimisha barua ile huku machozi yakichukua nafasi kubwa usoni mwangu. Nilijifuta na kufanya kama nilivyokusudia kabla ya kutoka usiku huo huku nikichukua kiasi kidogo cha pesa na kuanza safari ambayo kila nilivyopiga hatua ndivyo nilivyopata wazo wapi nielekee.
*********
|MIAKA MITANO BAADAE|
"Amefaulu vizuri sana tena ameongoza kimkoa na yupo katika kumi bora za kitaifa."
"Bwana anaweza hakika nashukuru sana. Sasa nitatuma milioni tano kwenye akaunti yako ya benki moja ya kwako nne wapelekee ila usisahau kumuelewesha dada kuwa na hao wengine wahamishiwe shule za kulipia ili wawe wasomi wa ukweli kama mwenzao. Vipi nymba nayo imefikia wapi? naomba unitumie picha whatsapp."
"Usijali One, ila nakusihi kaka usiyamalize maisha yako huko."
"Nakubaliana nawe na niko tayari kubatirisha ile barua punde wakati ukifika."
"Sawa kila la kheri kaka."
"Ahsante."
Nilikata simu na kushusha pumzi ndefu nikiwa nimeketi sofani miguu nimeitandaza mezani. Nilifurahishwa na habari zile alizokuwa ananipasha rafiki mwema wa muda wote Sultani Rwambo aliyekuwa Tanzania jirani kabisa na ndugu zangu ambao wote kwa wakati huo walishanisahau wakiamini nilifariki miaka mitano nyuma siku zilezile walizofariki Rose na babaake kwa ajali ya ndege.
Naam haikuwa hivyo walivyodhani na hapa si Tanzania tena kama awali ingawa mimi ndiye Onesmo yuleyule. Kilichotokea siku ile usiku nilipotoka bila kujua yeyote ni hadithi nyengine ndefu sana ambayo ilijaa misukosuko ya kutisha lakini kwa neema za bwana nilifanikiwa kuvuka vikwazo vyote mpaka kudondokea kwenye ardhi ya nchi hii ya kiafrika iliyo kama ulaya. Nakumbuka usiku ule ilivyokuwa kabla hakujapambazuka alfajiri na kupanda basi la kuelekea Mbeya nia na madhumuni nifike Kyela mpaka Ipinda kwa kina Atuganile nikalipe kisasi kwa kuwakata mapanga wote popote hata kama nami nitapigwa na kijiji nife basi itakuwa safi. Hilo ndilo wazo nililokuwa nalo siku hiyo.
Lakini kitu cha kushangaza kwa kuchanganyikiwa kwangu nikajikuta nakata tiketi ya basi ya Tunduma badala ile ya Kyela na matokeo yake nakosa wzo la kushuka Mbeya mjini na mwishowe nikajikuta naingia Tunduma nikiwa sina akiba za pesa ya kutosha. Hapo ndipo songombingo nyengine ikaanza. Wazo la kutafuta pesa niende Kyela Ipinda nikatimize lengo langu kabla ya kifo changu. Nilikusudia kuwafanyia unyama kina Atu huku nikiumizwa na habari za redioni na magazeti yaliyokuwa yanaonesha picha za ndege ya Tanzania iliyolipuliwa na zaidi niliumizwa kwa picha za wasafiri ambapo kila nilipoiona picha ya Rose na babaake ndivyo nilizidi kudata na kuamua kutimiza jambo. Nilijua kwa wakati huo ndugu zangu tayari watakuwa wameusoma ujumbe na wanahaha kunitafuta ama wameshaweka matanga kwa niaba yangu. Nilikuwa tayari kufa lakini moyo wangu ulikuwa na kisasi.
"Kama wao wachawi basi mimi nitawamaliza kwa mkono wangu." hivyo ndivyo nilivyosema na mopyo wangu siku zote.
 
SEHEMU YA 33

"Kama wao wachawi basi mimi nitawamaliza kwa mkono wangu." hivyo ndivyo nilivyosema na mopyo wangu siku zote.
Lakini baada ya kusota Tunduma kwa miezi kadhaa nikifanya kazi za ukuli kupakia mizigo kwenye maroli na kujichanganya na watu wa pale ndipo nikajikuta nazoea mazingira hata kuvuka boda na kuingia nchi ya Zambia badala ya kurudi nyuma kuelekea Kyela. Huko nilivutiwa na show moja kubwa iliyokuwa inasimamiwa na watu wa marekani kutoka nchi ya afrika kusini. Show hiyo ilihusu nyimbo za injili na kutafuta vipaji vipya. Hapo ndipo nilipojichomeka nami kujiandikisha kushiriki ingawa sikuwa mzungumzaji mzuri wa kiingereza lakini niliamini uimbaji ni lugha tofauti ambayo inaweza kusikiwa na mtu wa lugha yoyote. Na kweli niliimba nyimbo za kiswahili lakini kwa weledi na hisia za hali ya juu. Mungu amtupi mja wake. Kweli sauti yangu huenda ilikuwa na mwito wa mamlaka kwani mbali ya ugeni niliokuwa nao na lugha tofauti lakini bado mwisho wa siku niliiibuka kidedea na hapo ndipo milango ya kuikanyaga afrika kusini ilipofunguka baada ya kuhangaikia pasipoti ya kusafiria ambapo ilinibidi nichukue ya uraia wa Zambia huku mambo mengine yakimalizwa na watu wale wa kanisa. Hivyo ndivyo safari yangu ilipogeuka na kufika Afrika kusini ambapo nilikutana na waimbaji wa kia aina na kwa bahati nilikutana na mtu anayekijua vizuri kiswahili pale kanisani naye akawa chachu ya kunifunza vitu vingi. Nilianza kuimba kama mwana kwaya kwenye kanisa na kuzunguka kwenye matamasha mbalimbali siku hadi siku. Nilijikuta moyo wangu ukibadilika na kuachana na yale yaliyopita hususani kisasi cha ndoa yangu. Miaka mitatu baadae nikapata udhamini ambao ndio niko nao hadi sasa naandika mkasa huu. Udhamini huu ulifanikisha nikarekodi albamu nzima ya nyimbo za dini ambayo iliuza sana na kufanya vizuri hadio bara la ulaya. Sikuwa kwenye kwaya sasa nikawa mwimbaji wa kujitegemea wa nyimbo za kumsifu bwana. Siku zote ninapoimba nakuwa na hisia za mengi mazito yaliyonisibu na kunifanya niimbe kwa moyo mmoja huku nikiamini chozi langu litalipwa. Baada ya maisha yangu kurudi kwenye mstari mzuri tena ndipo hapo nilpomtafuta Sulu ambae naye alishaamini nimekufa baada ya jiihada za kupatikana kwangu kugonga mwamba. Nilimuhadithia kila kitu Sulu na kumuomba anisaidie kuwa karibu na ndugu zangu ambapo kupitia yeye nilianza kutuma misaada mbalimbali. Nilifurahi niliposikia dada zangu walifanya kama nilivyoandika kwenye baruqa na yule mjobaangu amefanya vizuri sana kwenye mtihani wa kidato cha pili kwa kuongoza kishule na kiwilaya huku akiwa ndani ya kumi bora kimkoa. Mambo ndio yakawa hivyo na nilihakikisha kupitia Sulu nawanunulia kiwanja ndugu zangu na kuwajengea nyumba ambayo wao waliamini ni ufadhili alioupata mpwa wangu kama nilivyomuelekeza Sulu kuwa atumie kigezo cha akili za huyo mtoto zimesababisha atokee mfadhili kutoka nje ya Tanzania ambae amejitolea kumsaidia kwa kutuma pesa mbalimbali. Walifurahi na kushukuru pasipo kujua kama kaka yao nipo na ndiye ninayefanya hivyo. Maisha yangu yanaenda vizuri na nina heshima kubwa sana hapa Afrika kusini kwa sasa. Hata uraia tayari nishachukua wa hapa. Sauti yangu imekuwa lulu kila ninaposimama kuimba na kumsifu bwana. Hakika ingawa nina furaha machoni lakini bado moyoni nina kovu kubwa na kila ninapomshuhudia mtu akioa basi naikumbuka ndoa yangu. Sina hamu ya kuoa tena wala siko tayari na maisha hayo. Ndoa yetu ni moja na ndoa yangu edhulumiwa kwa hila. Sikupanga ivunjike lakini ndio imetokea hivyo. Nilibakiza kumshukuru Mungu nikifuta kisasi ila nikiuacha msamaha lupango. Sikuwa tayari kuhukumu wala kusamehe kwa niliyotendwa.
********
"Mfanya biashara maarufu wa mafuta toka Senegal Sheikh Abdulaziz Razaq leo hii amefunga ndoa ya kihistoria nchini Tanzania ambako ameanza kuwekeza sheli zake huko. Kwa habari kamili tujiunge na muandishi wetu."
Hiyo ilikuwa sauti ya msoma habari kwenye TV na hapo ndipo macho yangu yalihamaki baada ya kuliona tukio ambalo nililiona miaka mitano nyuma. Nilimshuhudia bibi harusi akiwa si mwengine bali mke wangu Atuganile Mwakyusa. "Ina maana utabiri umekuwa kweli? basi bila shaka na yale niliyoyaona yote ni kweli! Atuganile unajidanganya. Ila kwa hila uliyofanya kwenye NDOA YANGU basi amini CHOZI LANGU LITALIPWA." Niliongea mwenyewe kwa ghadhabu kidogo na kupooza koo kwa funda la maji. Atuganile aliolewa kweli na maisha yake sikutaka kuyajua yakoje huko kwa huyo shehe bilionea. Nilitamani siku moja nilale nimuote yule mtu walau nimuulize kuhusu binti yule mzuri Suyrashfatina aliyenisaidia kupambana na nguvu za kichawi za kina Atuganile je, alikuwa nani? Jini au Malaika? Na kwanini alifanya vile kwangu? Hakika ni swali ambalo sijawahi kupata jibu zaidi ya kuendelea kushukuru leo hii bado mzima. Mungu awalaze pema peponi na awape raha za milele wote waliotangulia mbele za haki hususani mamaangu, Rose na babaake. Hakika hawa waliponzwa na ndoa yangu. Sitaki kuoa tena ijapo Atu ameshaolewa kwengine. Ninachosubiri ni malipo ya chozi la ndoa yangu. Mimi bado naendelea na kazi ya kuimba na kumsifu Mungu na furaha niliyo nayo inanitosha. Siku yoyote tokea sasa nitarudi kuwasalimia ndugu zangu wakae waelewe ukweli kama sijafa. Ila kabla ya hapo napenda kitabu hiki kitangulie kuwafikia watanzania wenzangu na vijana kote ulimwenguni wajifunze kuhusu mapito ya maisha ya NDOA YANGU lakini pia wasambaze kitabu hiki mpaka kimfikie ATUGANILE huko alipo na nduguze wakae wajue kwamba CHOZI LANGU LITALIPWA. Naitwa Onesmo.
|||||||||||||||||||||||||| ******TAMATI****** |||||||||||||||||||
 
Shukraanii Madame S""
Mwisho wa Ndoa yangu ndo mwanzo wa simulizi nyingine""" hakika tumejifunza mengi kupitia kisa hiki naamini bundle zetu umezitendea haki"""

Stay blessed dear
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom