Polisi wamtaja jamaa anayesakwa kwa mauaji ya mke na binti zake
Polisi wametoa picha ya CCTV ya mshukiwa wa mauaji anayeaminika kumuua mkewe na binti zake wawili kabla ya kutoroka Uingereza.
Miili ya Nothabo Zandile Tshuma, 42, na binti zake Natalie, 15, na Nala, 5, ilipatikana baada ya polisi kuingia kwa nguvu katika nyumba moja karibu na Bedford siku ya Jumatatu baada ya ripoti kwamba familia hiyo haikuwa imeonekana kwa siku kadhaa.
Polisi wa Bedfordshire wanamtafuta Ndodana Mkhanyisi Tshuma mwenye umri wa miaka 45, anayejulikana pia kama Mark, ambaye aliondoka nchini kupitia Uwanja wa Ndege wa Heathrow kwa pasipoti ya Uingereza siku ya Jumamosi.
Inspekta Mkuu wa Polisi Lee Martin alisema: "Tunajua kwamba Mark Tshuma aliondoka nchini Jumamosi na sasa inaaminika yuko Zimbabwe."
Aliongeza kuwa kikosi hicho kilikuwa kikifanya kazi na mashirika ya kitaifa na kimataifa ili kumtafuta Tshuma.
"Tunafanya kazi ya haraka kumtafuta na kumkamata, na tutamwomba moja kwa moja ajisalimishe."
Alitoa wito moja kwa moja kwa mshukiwa, akisema: "Mark, madhara yasiyofikirika yamesababishwa kwa wale walio karibu nawe na hii imewaacha jamaa na marafiki zako wakiwa wamevunjika moyo kabisa. Uchunguzi wa jinai haujui mipaka."
"Tafadhali fanya jambo sahihi, jitokeze na ujisalimishe kwa mamlaka za mitaa."
Jeshi la polisi la Zimbabwe limeiambia BBC kwamba nchi hiyo bado haijapokea taarifa yoyote rasmi kutoka kwa Interpol kuhusu uwezekano wa kuwepo kwa Mark Thsuma nchini humo.
Msemaji wa polisi Paul Nyathi alisema jeshi hilo lilikuwa linajua kuhusu kisa hicho kupitia vyombo vya habari na limeweka miundo ya kutoa taarifa kwa yeyote atakayeona tukio hilo.
Nyumba iliyoko Carnoustie Drive, Great Denham, imezungushiwa uzio na mashada ya maua yamewekwa kwenye ua nje.
Mwanamke mmoja ambaye alikuwa miongoni mwa watu walioweka maua huku akitokwa na machozi alisema: "Tunasikitika sana kumpoteza."
"Alikuwa mama mkarimu sana."
Majirani wengine waliozungumza na BBC walisema walishangaa kwamba tukio hilo lilitokea katika "eneo zuri na salama".
Shule zao ziliwapa wasichana hao wawili salamu za rambirambi, huku mkuu wa Shule ya Maandalizi ya Mahujaji, Jo Webster, akimtaja Nala kama "mwanga wa jua" anayejulikana kwa tabia yake ya kudadisi na "ucheshi mzuri".
Alisema: "Wengi wa wafanyakazi wetu walikuwa wakimjua tangu akiwa na miezi saba tu na walikuwa na fursa ya kumwona akikua."
Mkuu wa Shule ya Wasichana ya Bedford, Gemma Gibson, alimkumbuka mwanafunzi wa Darasa la 10, Natalie, kama "mwenye akili na mafanikio" huku akisisitiza vipaji vyake kama dansi, mwanamuziki na mwanamichezo.
Msaidizi Mkuu wa Polisi John Murphy hapo awali alisema kuwa ni "tukio la kuhuzunisha sana ambapo mama mmoja na watoto wake wawili wanaaminika kuuawa".
Kikosi hicho kilisema hakuna kinachoonyesha kuwa kuna hatari kubwa zaidi kwa umma, lakini kitakuwa ni kuongeza doria katika eneo hilo.
Mtu yeyote mwenye taarifa kuhusu tukio hilo, au ambaye aliona shughuli zozote za kutiliwa shaka katika eneo hilo Ijumaa au Jumamosi, ameombwa kuwasiliana na Polisi wa Bedfordshire .
Source:BBC
cc loose Nut