Gachuma baada ya wafanyakazi wake wote kuripoti kwake, alibaki peke yake na maburungutu ya fedha zilizopatikana kwa njia mbalimbali, alizihesabu kwa umakini ili kuzihakiki. Alipohakikisha hesabu ziko sawa alichukua kiswaswadu chake na kuzitafuta namba za afisa mmoja ambae kituo chake cha Polisi hakikuwa mbali na shamba, alitaka kumpa mgao wake ili aendelee na ratiba zingine. Wakati akiendelea kufanya mawasiliano macho yake yaliona mlango wake ukisukumwa na kisha mtu asiyemtarajia akasimama wima katikati ya mlango akiwa amemkazia macho. Alizubaa kidogo na asielewe kama alikuwa ndotoni au alikuwa kwenye uhalisia wake.
“Chu..Chu..chuma kingali moto!” Alisema kwa kukwamakwama huku akikata simu iliyokuwa imeunganishwa upande wa pili.
“Chuma hakiwashi moto.” Zuki alisema huku aliusukuma mlango nyuma yake na kuufunga, akapiga hatua na kusogea karibu na uso wa Gachuma.
“Unakumbukumbu kali sana. Imepita miaka mingi na bado unakumbuka utambulisho wetu.” Alisema na kuangusha tabasamu adimu kuonekana usoni mwake hasa awapo kwenye harakati zake zenye mashaka na uhai wake.
“Siwezi kusahau kamwe. Vipo vingi vya kusahau ila siyo harakati za Oparesheni Duma na namna tulivyoteseka mithili ya vikinda vya tai. Nakumbuka sana.” Gachuma alisema na kusimama kumpisha kiti mgeni wake ambae hajapata kuonana nae kwa zaidi ya miaka kumi na tano.
“Umewazeje kunifikia kirahisi namna hii?” Alimuuliza.
“Kwani siku hizi una ulinzi wa Al shabaab? Nitashindwa vipi kumfikia mwendesha baiskeli maarufu hapa Entebe? Hilo ni swali kweli? Halafu umesahau sisi ni wana wa Duma? Umesahau kwamba harufu ya duma waliokulia pamoja haiwatoki hadi kifo? Aah Gachuma!” Zuki alishangaa.
“Najua huna habari njema, nipashe nione namna ya kuzibeba habari zako.” Gachuma aliamua kufupisha maongezi kwa kuwa muda ulizidi kumtupa mkono na hakutaka kuchelewa aendako.
“Kweli Gachuma ni yuleyule wa jana na leo, hapotezi muda kizembe. Anyway, nahitaji taarifa za Plot nambari 607.” Zuki alisema kilichompeleka pale huku akiwa anahangaika kuisachi mifuko yake iliyohifadhi dola kadhaa.
“No! Wewe ni ndugu yangu wa mapito ya hekaya za kweli.” Gachuma alimzuia kuendelea na zoezi lake la kutaka kuzinunua taarifa.
“Unaongelea ule mtaa wa vigogo?” Aliuliza huku akifikiria kidogo, akarejesha macho yake kwa Zuki na kutikisa kichwa.
“Inawezekana nisiwe sahihi lakini hapo anaishi mtu mmoja anaitwa Daudi Nyuso. Huyo jamaa aliwahi kuwa mkuu wa jeshi la polisi hapa nchini, cheo ambacho hakukihudumu sana kabla ya kuondolewa kwa tuhuma za kutumia vibaya madaraka yake. Haikuishia kuvuliwa madaraka bali na jeshini aliondolewa kabisa. Kilichokuwa nyuma yake ni tuhuma za kushirikiana na waasi wa Uganda wanaopigana vita nchini Congo DR. Alikuwa akishirikiana na wanajeshi ambao hawakuwa waaminifu wa jeshi la Congo. Baada ya kuachishwa kazi aliendelea na maisha yake na biashara zake nyingi zinahusu madini. Sasa hivi anajiingiza taratibu kwenye siasa za Uganda na tayari kwa kutumia pesa zake ameanza kupata ushawishi na kiasi fulani ni mtu asiyegusika. Anaulinzi angalau unaelekea kukaribia wa makamu wa rais. Hafikiki kizembe.” Gachuma alitua.
“Unaweza kupata angalau ratiba zake za hivi karibuni?” Zuki aliuliza.
“Hakuna gumu lakini itabidi nipate angalau saa chache za kufuatilia. Mawasiliano yangu ya siri ni yale yale ya miaka nenda rudi, nistue ikifika saa saba ya usiku.” Gachuma alisema huku akimpa nafasi Zuki ya kuinuka kwenye kiti na kuondoka, hakutaka kuendelea kupoteza muda ikiwa ameshatoa taarifa ziliuliziwa. Zuki aliondoka kama mzimu shambani kwa Gachuma Itaro, Gachuma nae akaondoka kuendelea na ratiba zake akiwa na kazi moja ya kufanya kwa saa chache zilizosalia.
********
Wakati Zuki Gadu akihangaika na kupata taarifa za Daudi Nyuso, nchini Tanzania harakati nyingine zilikuwa zinaendelea kama kawaida. Montana alikuwa kwenye kazi aliyoachiwa na Zuki Gadu, kazi ambayo alitakiwa kuikamilisha ndani ya siku sita pekee na taarifa za awali alizopewa ziliishia kwenye namba ya pikipiki na hakukuwa na taarifa za ziada. Dar es laam ni jiji kubwa na lenye idadi kubwa ya watu, vyombo vingi vya Moto hivyo ni ngumu kuitafuta pikipiki moja na kuipata kirahisi. Kwa wengine ingelikuwa ngumu lakini kwa Montana ugumu unapungua kwa kiasi kikubwa, kwa nini? Kwa sababu ni mwanamke anaejuana na kila mtu anaetakiwa kumjua huku silaha yake kubwa ikiwa ni uzuri wake ambao huwachanganya watu wengi bila kujali hadhi zao. Nani alisema kichwa kidogo kikisimama hadhi ya mtu unazingatia? Thubutu yako, kila kizuri kilimezewa mate na kila mtu na hapo ndipo wenye mabavu ya madaraka na fedha hutumia madaraka yao kumega wavitakavyo. Montana alimegwa na kila mwenye pesa jijini Dar es laam, alimegwa na kila mwenye madaraka ili mradi aive kwa tamaa juu yake. Watu wengi hawakuwahi kujua sababu ya Montana kuugeuza uzuri wake kama chambo ya kumnasa amtakae na kingine ambacho hawakujua ni kwamba, hakuwa mwepesi wa kuvua nguo kwa kila aliyemtaka bali alikuwa hodari wa kuvuna taarifa kwa kila aliyeingia kwenye hamsini zake. Mbali na kufanya kazi na Zuki Gadu lakini mwanamke huyo alikuwa ni mtego wa kitengo nyeti sana nchini Tanzania na alifunzwa kwa sababu hiyo. Taarifa nzuri na mbaya za watu mashuhuri zilipitia kwake na kuchujwa kabla ya kufika dawatini. Kitu kimoja alichofundishwa na akafundishika ni kutokurejea alikoiba taarifa na kabla ya kuvua nguo alihakikisha anakufyonza kila alichotaka kusikia na endapo akipata kila kitu unaweza usione maumbile yake na ukaishia kujilaumu huku yeye akiwa mbali na uso wako, ukifanikiwa kumgusa utakavyo ina maana kuna kitu amekwama kukipata bila kukuonesha utupu wake na akikuonesha atakikisha anakufanyia yote ambayo si kahaba wala kungwi amewahi kuyafanya kitandani, baada ya hapo anakumega taratiibu na utampa atakacho kisha anatokomea na usijue alipoelekea. Licha ya utaalamu wake huo uliogharimu pesa nyingi wakati wa mafunzo yake, lakini hakuwahi kuvuna chochote kutoka kwa Zuki Gadu na badala yake alijikuta akitumika yeye kuvuna taarifa alizohitaji Zuki. Alifanya kila jihadi kuhakikisha anajua njia zote za Zuki lakini aliambulia patupu na akaishia kuisubiri siku ambayo hajui itatokea lini ili amjue vema mtu huyo ambae kumuona huwa ni kama kumuona Kakakuona, itokee bahati tu. Montana alikuwa na mitego yake kwa Zuki lakini kitu kimoja ambacho hakujua ni kwamba, Zuki alishazihesabu hatua zake siku nyingi sana na alijua uhatari wa kuweka ukaribu nae, hiyo ni moja ya sababu iliyomfanya Zuki awe anajitokeza kwake mara chache sana na hujitokeza awapo na ishu ya maana ambayo ni lazima Montana ahusike na baada ya hapo hupotea kama vile hakuwahi kuonana nae maisha yake yote. Montana alitaka uaminifu kwa Zuki hivyo kila kazi aliyokuwa akiifanya alikuwa anataka kuwa karibu zaidi yake na aliifanya kwa juhudi kubwa. Baada ya kupewa namba za pikipiki hakulaza damu, alimtembelea kwa kushitukiza mtu wake wa zamani ambae alikuwa ni kigogo mmoja ndani ya ofisi za TRA. Aliyetembelewa aliona ni bahati ya mtende kuota jangwani, kupita muda mrefu bila kumuona Montana kisha ghafla tu anajitokeza akiwa na uzuri ulioongezeka maradufu, hiyo ilikuwa ni bahati ambayo hajawahi kuiota. Kutokea kwa Montana kulisimamisha kazi za kibosile kwa dakika kadhaa, walipiga soga nyingi hadi pale kibosilea aliponasa kwenye mtego, akaombwa kuitambua pikipiki hiyo ambayo ilisadikika mmiliki alihusika kumwibia Montana. Kibosile akafanya alichoombwa na ndani ya muda mfupi jina la mmiliki wa pikipiki likapatikana, makazi yake nayo yakapatikana. Montana alipopata alichotaka akaaga, akasindikizwa na noti nyingi za elfu kumi huku yeye akiacha namba ambayo aliizima dakika tatu baada ya kutoka ofisini. Malima Bilali lilikuwa jina la kwanza kukaa kichwani mwake punde alipoziacha ofisi za mamlaka ya mapato. Kwa taarifa za haraka haraka alitambua jamaa alikuwa ni mmliki wa kituo cha kuoshea magari maeneo ya Mkwajuni, Kinondoni.
Saa tatu baadae gari aina ya Toyota Crown ilikuwa inaingia kwenye maegesho ya kituo cha kuoshea magari kilichokuwa Mkwajuni. Kabla hata gari haijasimama tayari vijana wawili walikuwa wameizunguka wakiomba kumsikiliza mteja wao. Gari ikazimwa na aliyekuwa ndani ya gari hakushuka wala kushusha vioo kuwasikiliza wenyeji wake, alitulia kwa zaidi ya dakika tatu akiwa anayasoma mazingira ya eneo lile,mbali na wale vijana wawili waliokuwa wakigombea kutoa huduma, kulikuwa na mabarobaro wengine watatu ambao walikuwa wameliegemea gari moja huku wakionekana kuwa katikati ya kikao cha kusimuliana yaliyokuwa yakiendelea mjini. Kwa namna walivyokuwa wanajiamiani kusimama eneo walilokuwepo moja kwa moja alihisi watakuwa wanahusika na kituo kile. Akashuka kuijaribu bahati yake. Montana alikuwa kwenye vazi fupi lililoacha maungo yake wazi, nywele zake ndefu aliziachia ziufunike mgongo wake, macho yake aliyafunika kwa miwani ya bei kubwa na mwilini alipulizia uturi wa bei ghari. Kwa namna alivyoshuka aliacha watu wote na mshangao wa sekunde kadhaa, nae akaamua kuwamaliza kabisa kwa kuzungusha kichwa chake na kuzifanya nywele zake nyeusi zitawanyike huku na huko kwa namna ya kuvutia.
“Mtatumia muda gani kulisafisha gari langu?” Aliwauliza vijana waliokuwa kando ya gari lake.
“aah..ahh.. dakika ishirini tu..” Mmoja alijibu kwa mashaka kama vile hakuwa na uhakika na kile alichokuwa amekijibu, lakini kigugumizi chake ni kwa sababu ya kiumbe aliyekuwa mbele yake, alimtamani lakini alijiua hataweza kumpata hata kwa dawa. Hadhi yake hakuona kama inaendana hadhi ya mwanamke aliyekuwa akitazamana nae. Si vijana hao pekee waliokuwa wakijitenga na daraja la mwanamke aliyekuwa mbele yao, hata wale vijana wengine waliokuwa bize na maongezi walikuwa wameacha kila walichokuwa wanafanya, macho yao yakahamia kwa malaika mweusi aliyekuwa mbele yao, walikuwa wakijipima daraja lao kwa kiumbe aliyependelewa na Mungu uzuri wa ajabu na siyo uzuri tu, hata nyota alikuwa ya kupendwa alikuwa nayo.
Wakati gari ikiendelea kuhudumiwa, Montana aliomba kukaa kando ili asubiri gari lake, hiyo ikawa nafasi nzuri kwa vijana wakware kupanga vema karata zao na hatimae wakaamua kumwacha mmoja kati yao ajaribu bahati yake huku wengine wakisubiri kuona kama watapata ushemeji au watatoswa. Vijana waliosalia waliamua kumuacha mwenzao Kwa sababu waliamini anafaa kuhangaika na binti mzuri na aliyeonekana kuwa na kipato, walimsusia kwa sababu alikuwa na kipato kikubwa kuliko wao. Aliyesusiwa alikuwa ni Malima Bilali.
Montana alizihesabu vema hatua za kijana mjivuni mwenye kuonekana kuwa na pesa za kurungishia warembo, alitembea kwa kujiamini na mikogo ya hapa na pale. Alitabasamu kwa kuwa alijua ni kitu gani kingelifuata kwenye maongezi yao.
“Habari yako mrembo..” Jamaa alisabahi.
“Nzuri.” Montana alijibu kwa ufupi na kuendelea na kuperuzi kwenye simu yake.
“Naitwa Bilali ni mmiliki wa hiki kituo cha kuoshea magari.” Alijitambulisha.
“Ahsante kwa kunifahamisha.”Montana alijibu na kuinua uso wake kumtazama Malima, aligundua jambo ambalo alishalitilia shaka tangu alipoisikia lafudhi ya Malima. Uso wa Malima ulikuwa na matokeo ya utumiaji wa vipodozi vikali, lafudhi yake pia haikuwa ya Mtanzania halisi wala jamii ya jina alilojiita. Malima hutoka ukanda wa kanda ya ziwa hasa mkoani Mara kwenye jamii za wavuvi pamoja na visiwa vya Ukerewe. Bilali pia halikuwa jina la ukanda huo bali ni jina linalotumiwa na watu wenye asili ya bara Hindi ni nadra majina yenye asili mbili kuchangamana ijapokuwa inawezekana. Lakini ni ngumu zaidi mtu anaeonekana kuwa na asili ya nchi ya Congo kuwa na vinasaba na jina la Malima na ubini wa Bilali kisha akawa anaejichubua. Hilo lilimtia shaka Montana na likamfanya avutiwe zaidi na kutaka kumjua Malima ni nani.
“Gari inaweza kuchukua muda mrefu kuoshwa, hapa hapakufai kusubiri.” Jamaa alisema kwa mikogo huku akiligeukia eneo la jirani ambalo lilitunza mgahawa na watu wachache walikaa wakiburudika na mlo.
“Naomba tukae pale angalau upate maji wakati gari lako likiendelea kuhudumiwa, ahsante kwa kuchagua ofisi yangu.” Malima alisema.
Montana hakutaka kuongeza neno kwa sababu moja ya silaha yake kubwa ya kumsoma mtu ni kumpotezea wakati akibwabwaja, alitaka amuelewe vema mtu huyo na tabia zake. Aliinuka bila kusema lolote kisha akaanza kupiga hatua kuelekea mgahawani, nyuma yake alifuata Malima ambae aliwageukia wenzake na kuwanyooshea alama ya dole la ushindi kwa kumuinua mwanamke mrembo.
“Agiza chochote nitalipa.” Malima alisema baada ya kufika mgahawani.
“Niitakunywa maji tu.” Montana alijibu na kuendelea kuperuzi simu.
“Ningependa kulijua jina lako mrembo.” Malima alianza kurusha ndoano bila kujua alishatupiwa yeye na alikaribia kunasa.
“Naitwa Marry Mariam.” Montana alidanganya.
“Kwa hiyo nikuite Marry au Mariamu?” Aliulizwa.
“Niite hivyohivyo, Marry Mariam.” Alisema na kuiweka simu kwenye mkoba, akamtazama kwa macho malegevu yaliyoenda kuvuruga mfumo wa akili wa mtazamwaji. Baada ya macho yaho kutua kwenye fikra za Malima, kilichofuata ni raha za muda mfupi na karaha ya muda mrefu. Lakini nani angelijua yajayo? Ninge hubaki kauli ya kila kiumbe hai mwenye kauli na hutamkwa yakishatokea. Ninge ni kauli ya majuto. Nani alijuta kati yao? Mi sijui.