Mwalimu kutoadhibu ni jambo linalowezekana kwa 100%
Fuatilia mwongozo huu: Mwalimu hakikisha umefika shule muda husika, simamia usafi na kama wanafunzi hawaonyeshi kushiriki kufanya usafi, tafadhali usishike kiboko. Mwalimu kumbuka muda wa vipindi ukifika hata kama mazingira ya shule ni machafu, wanafunzi waingie darasani tayari kwa masomo. Mwalimu fundisha kipindi chako kama mwongozo unavyoonesha, tafadhali usiwafuatilie wanafunzi wasioandika, kwani inaweza kuhamasisha hisia za kutoa adhabu ili kumjenga mwanafunzi husika. Mwalimu, daftari zikikusanywa kwa ajili ya kusahihisha, tafadhali usifuatilie kubaini wanafunzi wasiokusanya daftari kwani kubaini kwako kunaweza kupelekea kuwepo na mazingira yenye kuchochea adhabu.
Mwalimu wakati utakapoita majina, zingatia kuwa wale waliopo darasani kwa wakati huo ndiyo wanaokuhusu, hitaji lako la kutaka kujua mwanafunzi X ana tatizo gani la kutokuja shuleni linaweza kupelekea mazingira yatakayo chochea adhabu, kwani wanafunzi wenzie wakati mwingine watakupa jibu kuwa mwanafunzi X yupo maeneo ya chooni anacheza tu, hivyo jibu ili linaweza kupelekea mazingira ya adhabu. Mwalimu wangu, mara upatapo kesi za mwanafunzi X kuwa amepigana darasani au kutoa lugha chafu, tafadhali tumia neno moja tu kuwa "LUGHA ZA MATUSI SI NZURI " kisha mruhusu kurudi darasani ili kuepusha mazingira ya adhabu. Mwalimu wangu mzazi akikuletea kesi ya mtoto wake kuhusu tabia za nyumbani na hata mwenendo mbovu wa maendeleo yake darasani, tafadhali mueleze mzazi kuwa amalizane na mwanaye kwa namna inayofaa. Mwalimu wangu ukifuata muongozo huu, shutuma na jazba za wana wa nchi hii utaziepuka pia itakusaidia japo kurudisha mwili wako uliopukutika kwa kufuatilia watoto wasiokuhusu, nakutakia kazi njema mwalimu wangu.