Tuache siasa, bandarini tunaua uchumi
Mwandishi wetu
WAZIRI wa Uchukuzi Dk. Harrison Mwakyembe sasa ametangaza kupokea ripoti ya
tume aliyoiunda kuchunguza tuhuma ambazo zimekuwa zikidaiwa kuwa chanzo cha
kuzorota kwa huduma za bandari zetu na hasa Bandari ya Dar es Salaam.
Tuhuma za Dk. Mwakyembe wakati akiunda tume yake na hata sasa, zinaelekezwa
tu kwa uongozi wa Mamlaka ya Bandari Tanzani (TPA) na zaidi viongozi maalumu
anaowalenga yeye tu na mfumo mzima katika sekta husika.
Kwa kuwa waziri hana taaluma katika maswala ya usafiri kwa njia ya majini bandari
nikiwa kama mmoja wa wadau kwenye sekta hiyo naamini sasa atakuwa amepata
ufahamu wa kuifahamu vema sekta nzima ikiwa ni pamoja na mfumo mzima wa
kupokea, kuhifadhi na kusafirisha mizigo ipitayo kwenye bandari zetu zikiwamo zile
za maziwa.
Kwa wadau waliobobea kwenye eneo hili na ambao biashara zao za kila siku
hutegemea ufanisi endelevu wa kila mdau kwenye eneo hili wanategemea kuona
ripoti yenye weledi na muonekano wa kitaaluma kuliko ya kutafuta makosa ndani
ya mdau mmoja.
Kwa maelezo ya Dk. Mwakyembe na wanaoungana naye, kwa sasa inaonekana
tuhuma zinaelekezwa TPA ili kuhalalisha mbele ya umma kwamba Bandari ya Dar es
Salaam kuna uozo, wizi, rushwa na kila aina ya uovu unaofahamika duniani.
Baadhi ya wadau wanaona matamshi kama haya na ambayo hayajahusisha wadau
wote kwa kina yanatoa taswira ambayo inaweza kuwapoteza wateja kabisa hata
wateja wachache tulionao Tanzania.
Waziri anadiriki kusema eti amehakikishiwa na mawaziri wenzake wa uchukuzi wa
nchi jirani kwamba nchi hizo zitaendelea kuzitumia bandari zetu hasa ya Dar es
Salaam.
Baadhi ya wadau na wafanyabiashara wanasema kwamba mawaziri siyo wanaofanya
biashara ila kazi yao ni kuweka na kusimamia sera ya biashara husika.
Tunafahau na waziri lazima afahamu kwamba bandari haiwezi kufanya kazi zake bila
kuhusisha kwa umakini sekta nyinginezo na mfanyabiashara mmoja anayemiliki meli
kubwa duniani ameliambia gazeti hili wazi kwa kusema, Bandari haiwezi kufanya
kazi kivyakevyake kama kitu kilichojitenga bila vifaa, watu au taasisi na mitandao
inayopaswa kufanya nayo kazi!
Hali kadhalika bandari haiwezi kufanya kazi ikawa na ufanisi bila kuwa na
viunganishi thabiti kwa maana ya barabara, reli na mabomba ya mafuta.
Pia bandari haiwezi kuwa na ufanisi wa kupokea mizigo mingi kwa wakati mmoja
kama haina miondombinu ya kutosha na ya kisasa kama gati za kutosha na zenye
kina kinachoweza kuegesha meli kubwakubwa ambazo zinaweza kutia nanga hapa
kama zilivyo kwenye bandari zinazoshindana na Bandari ya Dar es Salaam.
Ikumbukwe baada ya uchaguzi wa mwaka 2007 wa Kenya kugubikwa na vurugu,
wafanyabiashara wa Uganda walipata shida kutokana na mizigo yao kukwama
kwenye Bandari ya Mombasa kwa zaidi ya miezi mitatu mpaka hali ilipotengemaa.
Ni wakati huo ujumbe mzito ulikuja kutoka Uganda ukiongozwa na Waziri wa
Uchukuzi, kuja kuona uwezekano wa kutumia Bandari ya Dar es Salaam na kuahidi
kwamba Uganda ingetumia kupitisha asilimia 30 ya mizigo yake hapa kama mbadala
wa Bandari ya Mombasa.
TPA ilibidi iweke wakala kule Uganda kama njia ya kuwavutia Waganda lakini
wafanyabiashara wamekuwa wanasita kutokana na ukweli kwamba miundombinu
yetu bado ni hafifu.
Kukosekana kwa reli kumefanya Waganda waghairi kutokana na gharama kubwa kwa
njia ya barabara wakilinganisha na umbali wa kutoka Mombasa mpaka Kampala.
Hoja hapa ni kwamba pamoja na kuhakikishiwa na Waziri wa Uchukuzi wa Uganda
wa kutoa ahadi ya asilimia 30 ya mizigo ya Uganda kupitia hapa imekuwa ni
kitendawili kutokana na changamoto za mapungufu katika mtandao wetu wa njia za
usafirishaji mpaka mzigo ufike Uganda au utoke Uganda mpaka bandarini Dar es
Salaam.
Kama wadau, tunaona changamoto za uendeshaji bandari ziangaliwe kitaaluma zaidi
kuliko kuchukua mrengo wa kisiasa.
Inashangaza kuona inachukua zaidi ya miaka mitano kuamua namna ya kuongeza
gati mbili kwa nia ya kuongeza ufanisi kwenye sekta nzima kwa njia ya bahari
ambayo faida yake yake ni kuongeza pato la taifa kwa kuwa kila mdau kwenye
biashara inayohusiana na Bandari ya Dar es Salaam atakuwa anachangia kwa kiasi
kikubwa kwenye GDP!
Mombasa wanaongeza gati nne kwenye katika bandari yao na mkandarasi yuko
kazini mwaka wa pili sasa.
Pia wanajenga bandari mpya ya Lamu ambayo pia mkandarasi yuko kazini; hapa
tunalumbana wakati wenzetu wanashangilia kwa ujinga wetu.
Waziri anahusisha vipi TPA peke yake na wizi wa makontena?! Mizigo hutolewa
bandarini kwa njia ya nyaraka ambazo zina mlolongo mrefu.
Je, kama nyaraka za mzigo husika zimeghushiwa wakati mzigo unapotolewa
bandarini au toka kwenye eneo linalomilikiwa TICTS, bandari au mkaguzi mkuu wa
bandari atajuaje?
Tumeona kwenye vyombo vya habari kwamba kuna makontena yameshikwa huko
Hongkong yakiwa na pembe za ndovu zikitokea Dar na Mombasa.
Je, hapa TPA inahusika vipi wakati anayetakiwa kufungua na kukagua makontena
kabla hayajapelekwa kwenye meli kupakiwa ni ofisa forodha?
Ni vema wanasiasa wakajifunza kwanza jinsi bandari inavyofanya kazi kwa
kushirikiana na taasisi nyingine ndani ya mfumo kabla ya kufanya maamuzi ambayo
kwa kiasi kikubwa yatakuwa hayajengi zaidi ni kuuvuruga mfumo wote wa
usafirishaji kwa njia ya majini na kuua uchumi wetu kwa maslahi ya kisiasa.
juu
Habari Mpya | Matangazo | Bei zetu | Wasiliana nasi
Tuache siasa, bandarini tunaua uchumi