....Profesa Baregu na Marando ni miongoni mwa waliomtetea Zitto na hoja yao kubwa ilikuwa kwamba kwa vile walikiri makosa yao, kukubali kujiuzulu kwao kulitosha kulimaliza suala hilo badala ya kuliendeleza kwa kuwataka wajieleze kwa maandishi kuhusu makosa yao.
Dalili za mpasuko
Kuanzia wiki iliyopita, yamekuwepo matamko mbalimbali kutoka mikoani na taasisi mbalimbali kuhusiana na hatua ya akina Zitto kuvuliwa nyadhifa zao.
Matukio hayo yanaonyesha kwamba uamuzi huo haujakubaliwa na wanachama wote na ndiyo maana wiki iliyopita, makao makuu ya CHADEMA yalianza kutuma baadhi ya makada wake kwenda mikoani kwa ajili ya kueleza maamuzi hayo ya Kamati Kuu kwa wanachama wake.
Katibu Mkuu wa CHADEMA, alikuwa amepanga kufanya ziara katika mikoa ya Tabora na Kigoma inayotajwa kuwa ngome kuu ya kisiasa ya Zitto, kuanzia kesho lakini tayari baadhi ya viongozi wa mikoani wameonyesha kutokuwa tayari kuandaa mikutano hiyo.
Katika taarifa yake iliyotolewa kwa vyombo vya habari juzi, Mwenyekiti wa CHADEMA mkoa wa Kigoma, Jafari Kasisiko, alisema ingawa ziara ya Slaa ina lengo la kujenga chama, mazingira yaliyopo sasa hayatoi fursa ya kufanya hivyo.
Hata hivyo, wana CHADEMA kutoka Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, wametoa taarifa inayoeleza kuunga mkono maamuzi hayo ya Kamati Kuu na taarifa yao ilitolewa na kiongozi wa matawi ya chama hicho, Frank Sumbe.
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili umebaini kwamba maamuzi hayo yanaungwa mkono zaidi katika mikoa ya Kaskazini na Nyanda za Juu lakini kuna upinzani kwenye mikoa ya Kanda ya Kusini na Ziwa Magharibi anakotoka Kabwe.
Jana Mwenyekiti wa CHADEMA mkoa wa Singida, Wilfred Kitundu, naye alitangaza kujiuzulu wadhifa wake huo akipinga maamuzi hayo ya Kamati Kuu. Pamoja na mambo mengine, Kitundu ndiye mwanachama wa kwanza kujiunga na chama hicho kutokea mkoani Singida.