Hili nalo linahitaji mabadiliko ya Katiba au laweza kufanyiwa kazi bila kubadili katiba? Naona itakuwa hatua nzuri...
Mameya sasa kuchaguliwa kwa kupigiwa kura na wananchi
2006-10-23 17:24:17
Na Abdul Mitumba, Mbezi
Halmashauri za Manispaa na majiji barani Afrika, zimekubaliana kubadili mfumo wa sasa wa kuwapata wastahiki mameya kutoka kuchaguliwa na madiwani hadi kupigiwa kura na wananchi.
Kwa sasa mameya wa manispaa na majiji katika nchi nyingi za Afrika wanapatikana kwa kuchaguliwa na madiwani kutoka eneo husika.
Naibu Meya wa Manispaa ya Kinondoni, Bwana Julian Bujugo, amesema kuwa makubaliano hayo yalifikiwa katika mkutano wa mameya, wakurugenzi na watendaji wengine wa serikali za mitaa, uliomalizika hivi karibuni jijini Nairobi, Kenya.
"Ilionekana hakuna ugumu kwa wananchi kutoka eneo husika kuwapigia tena kura wagombea wa umeya.
Hii itasaidia kupunguza uwezekano wa baadhi ya wagombea kutumia fursa ya uchache wa madiwani kunyakua kiti hicho kwa 'ulaini,' alisema.
Amesema hatua hiyo pia itaongeza heshima ya Meya katika eneo lake kwani ataongoza kwa baraka za walio wengi, tofauti na mfumo wa sasa wa kuwatumia madiwani wachache kupiga kura.
Bwana Bujugo amesema tayari Uganda wameanza kufuata utaratibu huo unaoaminika kuwa ni bora zaidi katika kufikia malengo ya demokrasia ya kweli na utawala bora.
Hata hivyo, Bwana Bujugo amesema ili nchi za Afrika zifikie hatua hiyo, zinahitaji muda wa kujipanga upya kwa faida ya nchi zao na bara zima la Afrika.
Katika mkutano huo wa wiki moja ambao ulihutubiwa na Waziri Mkuu wa Tanzania, Bwana Edward Lowassa, Bwana Bujugo alimwakilisha Mstahiki Meya wa Manispaa ya Kinondoni, Bwana Salum Londa.
SOURCE: Alasiri 23 Oktoba 2006