Kuhusu Escrow; Sehemu ya hotuba ya Mnyika, mwaka jana Bunge la Bajeti....
Ufisadi katika akaunti ya Escrow
Mheshimiwa spika, kutokana na mgogoro wa IPTL na TANESCO ilifunguliwa akaunti inayojulikana kwa jina la "Escrow". Akaunti hii ilifunguliwa ili fedha ambazo Tanesco ilipaswa kuilipa IPTL kwa ajili ya Capacity Charge ziwekwe kwenye akaunti hiyo hadi pale mgogoro huo utakapomalizika, kwa mjibu wa taarifa zilizopo akaunti hii ilikuwa na Dola milioni 122 ambazo ni zaidi ya billion 200 pesa ambazo ni zaidi ya zile zilizoko kwenye kashifa nyingine ya EPA ambazo sasa zimepotea katika mazingira ya kutatanisha.
Kwa mjibu wa taarifa ya Gavana wa benki kuu ya Tanzania aliyotoa katika kikao cha kamati ya uchumi ya bunge kilichofanyika Bagamoyo, Gavana huyu alikiri kuwa alibanwa na viongozi wa juu kiasi cha kushindwa kufurukuta.
Kwa maneno yake anasema "mnanionea bure, kulikuwa na presha kubwa sana kuhusu fedha hizi…ukweli ni kwamba IPTL inabadilishwa tu rangi na watendaji ni walewale" Ikumbukwe kuwa Tuhuma dhidi ya Gavana wa Benki kuu zinatolewa kwa kuwa hawezi na hana mamlaka ya kuingia Bungeni kujitetea kwa sababu wanajua kuwa fedha ile ilishaliwa na wajanja wachache.
Tayari viongozi waandamizi wa serikali na shirika la umeme nchini kwa nyakati tofauti wameshatoa kauli mbalimbali zenye nia na malengo tofauti pia, serikali kupitia kwa waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospiter Muhongo alinukuliwa na baadhi ya vyombo vya habari kwa mfano gazeti la mwananchi Tanzania lilikuwa na habari inayosema Muhongo aongeza utata wa mabilioni IPTL .
Katika muendelezo wa kile kinachoonesha kuwa watendaji wa serikali hii ya chama cha mainduzi hawana nia njema na Taifa hili kama ambavyo historian a mazingira ya IPTL yameonesha tangia mwanzo, katika sakata hili pia, Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo amesema fedha hizo hazikuwa za Serikali. Waziri amenukuliwa na vyombo vya habari akisema
"Hizo fedha hazikuwa za Serikali, Tanesco ilitakiwa kulipa Capacity Charge (gharama za uwekezaji) kwa IPTL kama inavyolipa karibu Sh27 bilioni kwa kampuni nyingine zinazozalisha umeme,"
Profesa Muhongo alisahau kuwa Tanesco iliyoweka fedha hizo ni shilika la umma na hivyo ni fedha za serikali, pili madhumuni ya fedha hizo hayajafikiwa na Tanesco wenyewe wanasema kupitia taarifa kwa umma iliyotolewa na Ofisi ya Uhusiano Tanesco Makao Makuu, kuwa hukumu kati ya Tanesco na IPTL inasema: "Mahakama hiyo (ya Kimataifa ya Usuluhishi wa Migogoro ya Uwekezaji) haikutangaza aliyeshinda wala kushindwa.
"Ilichofanya ni kutoa muda wa miezi mitatu kwa pande zote mbili, (Standard Charted Bank Hong Kong (SCB-HK)) na Tanesco kwenda kukubaliana nje ya Mahakama… kwa sasa kuna mazungumzo yanayoendelea kuhusu taratibu za kukokotoa gharama halisi.
Mheshimiwa spika, huku nyuma tayari mafisadi wa Taifa hili wameshakwapua fedha hizo, mbaya zaidi hakuna anayekanusha kuhusu kuibiwa kwa fedha hizo isipokuwa mkazo unatiliwa kuliaminisha taifa kuwa fedha hizi hazikuwa za serikali, ni lazima watanzania tukumbuke kuwa viongozi waandamizi wa serikali ya chama cha mapinduzi huwa na kawaida ya kauli hizi pale wanapokuwa wamefanya ufoisadi, kwa mfano katika kasata la kashfa ya rada, mwanasheria wa serikali alisema hakukuwa na mazingira ya rushwa lakini baadaye sote tulishuhudia chenji za rada, pili katika sakata la Richmond sote tulishuhudia ofisi ya mwanasheria mkuu wa serikali ikikanusha kuwepo kwa mazingira ya rushwa na hivyo TAKUKURU ikashidwa kufanya kazi yake, hali siyo tofauti pia katika sakata hili la bilioni zaidi ya 200.
Mheshimwa spika kambi rasmi ya upinzani bungeni inalitaka bunge hili kuunda tume kuchunguza kashfa hii, kamati hii kwa kuwa itakuwa na uwezo wa kujua mbivu na mbichi dhidi ya sakata hili ambalo inasadikika wezi wa fedha za Escrow wako ndani ya bunge hili tukufu.
Mheshimwa spika maelezo yoyote kuwa taasisi ya kupambana na kuzuia rushwa TAKUKURU ifanye uchunguzi haitaungwa mkono na kambi ya upinzani bungeni kutokana na historia ya TAKUKURU kutumika kusafisha sakata la Richmond, kwa upande wingine ofisi ya CAG nayo ilihusika katika kumsafisha sakata la aliyekuwa katibu mkuu Jairo.
Aidha historia inaonesha kuwa magavana wanapokuwa na taarifa kama hizo hupotea katika mazingira ya utatanishi kama ilivyokuwa kwa Balali, kambi rasmi ya upinzani bungeni inatoa angalizo la kutojirudia kwa hali hiyo