Mke wangu alinifanya niwe Mchawi -1

Mke wangu alinifanya niwe Mchawi -1

Mke Wangu Alinifanya Niwe Mchawi - 26...

ILIPOISHIA;
“Kuna kazi ya ziada inatakiwa kufanyika tuliyoifanya ilikuwa ya kawaida sana.”
“Sasa itakuwaje?”
“Safari imekufa, tutarudia tena leo jioni.”
Kauli ile ilinitisha na kuiona kama vita yangu na mwanaume aliyemchukua mke wangu ni kubwa sana tofauti na matumaini niliyopewa.
SASA ENDELEA...


Hatukuwa na jinsi tulikubali kushinda pale kijijini mpaka jioni tulipongia kwenye kazi nyingine. Safari ile alichemsha maji kwenye chungu,yalipokuwa yakichemka aliweka dawa na kunieleza nishike kisu na kukiingiza ndani ya yale maji yaliyokuwa yakichemka.

Japokuwa ndani ya chungu hakukuwa na kitu kingine lakini kila nilipoingiza kisu kiligoma.
“Vipi mbona huingizi kisu?” mzee Kidereko aliniuliza.
“Kimegoma kunaonesha kuna kitu ndani ya chungu,” nilimweleza mganga baada ya kisu kugoma kuingia.
“Hebu toa kisu,” aliniamuru.

Nilikitoa kisu, mganga alichukua dawa ya unga na kuiweka kwenye yale maji yaliyokuwa yakichemka kisha aliweka maji yaliyokuwa kwenye chupa ndogo na kunieleza nikiingize tena kisu.

Kisu kiliingia kama kinaingia sehemu iliyokuwa ngumu, ghafla maji kwenye chungu yalibadilika na kuwa damu.
“Endelea kukiingiza kisu kwa nguvu,” mganga alinieleza.
Kila nilivyojitahidi kukiingiza ilifika sehemu kikagoma kabisa kwenda mbele wala kutoka nje.
“Chomoa kwanza.”
Nilipochomoa kiligoma kutoka.
“Kimegoma.”

“Hebu,” ilibidi akitoe mwenyewe ndani ya maji ambayo yalikwishaanza kutoa harufu ya damu mbichi. Baada ya kukitoa kisu maji yalirudi katika hali ya kawaida. Hali ile ilimshtua mganga na kumsikia akishusha pumzi nzito na kusema:
“Mmh! Hapa ipo kazi.”
Nilimuona akikuna kichwa na kukitazama chungu ambacho muda huo kiliacha kuchemka ghafla kiliacha kuchemka japo moto ulikuwa bado unawaka. Nilijikuta nikichanganyikiwa hata Shedu naye alionekana kushtushwa na tukio lile ambalo bado sikuelewa.

Nilisikia mganga akisema, hapa lazima turoge kazi hii ifanyike saa nane za usiku hatuna jinsi mtu tunayepambana naye si mtu mdogo, kajidhatiti ndiyo maana ameamua kufanya aliyotaka. Lakini muda si mrefu atanijua mimi ni nani sijawahi kushindwa na kitu japokuwa hili ni tukio langu kubwa kunisumbua lakini lazima nitamaliza kazi.

Kazi hii sasa hivi ninatakiwa kuifanya mwenyewe kwa vile wewe ni mwepesi, nitaondoka mwenyewe usiku nikirudi kila kitu kitakuwa kama kilivyopangwa.”

Kulikuwa na dalili za siku inayofuata kulala palepale, nikaanza kuingiwa na wasiwasi kwamba mganga kazi ile imemshinda.
Nikaona tutachelewa hata kazini, lakini sikuwa na jinsi siku ile tulilala palepale mpaka siku ya pili.
Siku ya pili baada ya kufungua kinywa nilipelekwa porini ambako nilichanjwa juu ya kichuguu kupewa kinga kwa ajili ya kupambana na adui yangu ambaye alionekana amejidhatiti katika nguvu za kiza.

Baada ya kupewa kinga ambayo nilielezwa hakuna mtu wa kunigusa hata mambo yangu yatakuwa mepesi tofauti na mwanzo.

Kutokana na kazi kuwa nzito nilitakiwa kununua mbuzi mwekundu. Nilifanya hivyo kwa kutoa fedha kisha mganga aliwatuma watoto wake kwenda kumtafuta mbuzi huyo mwekundu asiye na baka lolote.
Watoto walirudi jioni wakiwa na mbuzi mwekundu kwa ajili ya kafara yangu ya usiku ya kumkomesha mbaya wangu. Siku ile tuliendelea kusota kwa mganga mpaka usiku.

Ilipotimu saa mbili ndipo mbuzi yule alipovishwa sanda na kuchinjwa na damu yake kumiminiwa ndani ya shimo lililochimbwa kama kaburi kisha tulimzika yule mbuzi ndani ya shimo lile akiwa ndani ya sanda na kuelezwa tukalale kwa ajili ya kujiandaa na safari ya siku ya pili alfajiri.

“Vijana wangu kazi imekwenda vizuri kesho safari ya kurudi mjini ipo kama kawaida.”
“Tutashukuru mzee wangu,” nilishukuru kwa vile nilikuwa nimeishaanza kuchoka kukaa pale kijijini.
“Kazi imekwenda vizuri inaoneka hata tiba niliyokupa asubuhi imekusaidia sana.”
“Kwa hiyo mzee kazi itakwenda kama ilivyopangwa?” nilimuuliza.

“Shaka ondoa, japo kazi ilikuwa ni kubwa bado usiku nitatoka peke yangu kwenda kumaliza kazi ndogo iliyobakia.”
“Je, ikienda kinyume?” bado nilimdadisi mganga.
“Haiwezi, nilichokifanya ni uchawi mkubwa sana,” mganga alinihakikishia alichokifanya.
Kauli ile ilinishtua na kujiuliza uchawi na uganga una tofauti gani, sikutaka kuuliza kitu lakini moyoni niliomba basi kafara yake ifanikiwe ili turudi mjini.


Je, kafara itafanikiwa? ili kujua fuatilia baadae
 
Mke Wangu Alinifanya Niwe Mchawi - 27


ILIPOISHIA;
“Haiwezi, nilichokifanya ni uchawi mkubwa sana.” Mganga alinihakikishia alichokifanya.
Kauli ile ilinishtua na kujiuliza uchawi na uganga una tofauti gani, sikutaka kuuliza kitu lakini moyoni niliomba kafara yake ifanikiwe ili turudi mjini kwani maeneo yale yalikuwa yameanza kunikera.
SASA ENDELEA...


Tulilala mpaka siku ya pili ambapo tuliamshwa alfajiri, saa kumi na moja, baridi lilikuwa kali sana, nilijua tulitakiwa kujiandaa kwa safari, kumbe tulipewa taarifa iliyonivunja nguvu na kutamani kulia.

Mzee Kidereko tangu alipoondoka jana yake hakurudi, hivyo tulitakiwa kuingia porini kumtafuta.
Kwangu yale yalikuwa mapya na kujiuliza tunakwenda kumtafutia sehemu gani huko porini. Hatukuwa na jinsi tuliondoka zaidi ya watu sita wakiwemo watoto wawili wa kiume wa mganga na wasaidizi wake, huku msaidizi wake akitangulia mbele na usinga ili kutuelekeza mzee Kidereko alipo.

Tulitembea porini kwa saa mbili bila kupumzika wala kujua mzee Kidereko alikuwa wapi. Lakini muda wote msaidizi wake alitueleza kuwa muda si mrefu tungemuona.

Baada ya mwendo kidogo tulishtuka kuyaona matone ya damu.
Ningekuwa peke yangu ningetimua mbio au kubadili njia lakini msaidizi wa mganga huyo alielekea upande uleule.
Mimi na Shedu tuliwafuata nyuma huku nikijiuliza zile damu zilikuwa ni za nini? Tuliendelea kuzifuata, ziliongezeka kila tuliposogea mbele huku majani yakionekana kuvurugika kama kulikuwa na vita nzito.

“Huyu hapa,” sauti ya mtoto wa mzee Kidereko ilitushtua na kutufanya sote tugeuke kwenye majani yaliyoonekana kulala kama kulikuwa na ugomvi wa tembo.

Tuliposogea nilishtuka kumuona mzee Kidereko akiwa amelala ameshikilia pembe nyeusi iliyokuwa imefungwa na kitambaa chekundu kwa chini na mwili wake hasa sehemu za kifuani na tumboni zikionesha damu iliyoanza kuganda.
Nilijua mzee Kidereko ngoma ilimshinda na kusababisha mauti yake, baada ya kumuona, msaidizi wake alitueleza turudi nyuma. Alitoa unga mweupe na kuanza kuurusha eneo lote, kisha alitoa maji kwenye chupa ndogo na kummwagia kichwani mzee Kidereko ambaye bado alikuwa ametulia kama tulivyomkuta.

“Kazi ilikuwa nzito,” alisema msaidizi wake aliyekuwa akifungua kichupa kidogo na kutoa dawa aliyoiweka kwenye pua za mzee Kidereko. Baada ya sekunde chake alipiga chafya mfululizo na kuamka, alikaa kitako na kututazama kisha alimuuliza msaidizi wake.
“Umekuja na utanduo?”
“Ndiyo”
“Nipe.”
Alitoa pembe ndogo na kumkabidhi, aliichukua na kuifungua kwa chini kisha alitoa unga mweusi na kuuweka mkononi na kupuliza kidogo, uliobakia aliutupia wote mdomoni na kunyanyuka. Tuliongozana naye kurudi nyumbani.
Tulipofika alikuwa amechoka sana, baada ya kuoga na kula aliingia ndani kwake kulala.

Tulibakia njia panda na Shedu bila kujua nini kilikuwa kinaendelea, kwani tulikuwa tumemaliza siku ya nne tofauti na ruhusa ya siku mbili tulizoomba kazini. Nikiwa nimekaa na Shedu chini ya mti nilimuuliza rafiki yangu.
“Shedu nini kinaendelea mbona sielewi?”
“Kazala hata mimi nimechanganyikiwa hata sijui kinachoendelea.”
“Shedu usipojua wewe mimi si ndiyo nitazidi kuchanganyikiwa kabisa.”
“Kazala haijawahi kutokea tangu nimemfahamu mzee Kidereko.”
“Sasa hii ni nini?”
“Yaani sielewi ni wazi aliyemchukua mkeo ni mtu aliyejizatiti sana.”
“Kwa hiyo kazi imemshinda?”
“Mmh! Sijajua hebu tusubiri aamke.”
“Kwa kweli nimekwisha kata tamaa.”

“Kazala huwezi kuamini hata mimi nimechanganyikiwa, tangu nimfahamu huyu mzee na sifa zake kwa kazi nzito alizowahi kuzifanya hii yako imekuwa ya kwanza kwa haya yanayomtokea. Hajawahi kushindwa na kitu hata wasaidizi wake nao wamechanganyikiwa.”

“Sasa huku tutakaa siku ngapi wakati tumezidisha siku moja?”
“Tumsubiri aamke ili tujue nini kinaendelea kama ameshindwa tujue moja.”
“Na akisema hajashindwa tutafanyaje maana hawezi kukubali kirahisi namna hii, lazima anaweza kutueleza tuongeze siku.”
“Tutamuomba tuondoke kuwahi kazini ili tupange siku nyingine ya kurudi.”
“Siamini kama ataiweza tena, kama ametaka kufa nina wasiwasi akilazimisha anaweza kufa bure.”

“Kweli nimeamini mwenye uwezo wa juu ni Mungu peke yake, nilivyomuamini mzee Kidereko amechemka kwa siku nne. Kweli hakuna marefu yasiyo na ncha.”

Maneno ya Shedu yalinikatisha tamaa na kurudiwa na imani yangu ya awali kuwa hakuna uchawi bali kuna mazingaombwe. Nilijikuta nikianza kumuwaza upya mke wangu na kuamini hakukuwa na suluhu ya kumrudisha zaidi ya kuendelea kuteseka.
Mpaka jioni inaingia mzee Kidereko alikuwa bado hajaamka.

Pale nyumbani palikuwa kimya kila mtu aliendelea na shughuli zake kama hakikutokea kitu chochote cha hatari. Jioni ya siku ile mimi na Shedu tulizunguka baadhi ya vijiji, giza lilipoingia tulirudi nyumbani.

Tulimkuta mzee Kidereko akiwa bado hajaamka, kitu kilichotutia wasiwasi ni mtu kulala asubuhi mpaka jioni. Nilijiuliza ni usingizi wa aina gani huo au ndiyo kapitiliza kabisa.

Hali ya utulivu iliyokuwepo ilizidi kutupa wasiwasi na kujiuliza nini hatma ya yote. Majira ya saa tatu usiku tulifuatwa na yule binti aliyetupokea siku ya kwanza tuliyofika.
“Mzee anawaita.”
“Mzee gani?” niliuliza.
“Jamani kaka Kazala hapa nyumbani kuna wazee wangapi?’
“Mmoja.”
“Basi ndiye anayewaita.”
“Ameamka?”
“Ndiyo.”
“Saa ngapi?”
“Muda mrefu, ameoga amekula na kupumzika.”
“Lakini hajambo?”

“Hajambo mbona hali ile ni ya kawaida, tumeizoea kazi hii inataka moyo la sivyo utaiacha.”
Tuliongozana na yule msichana hadi ndani ya nyumba ya mzee Kidereko, hali ilikuwa tofauti na siku zote ambazo huzungumzia pale chini ya mwembe au kilingeni kwake. Alipotuona alitukaribisha.
“Karibuni vijana wangu.”
“Asante mzee, shikamoo.”
“Marahaba karibu mketi.”
“Asante.”

Tulikaa kwenye viti vya kukunja na kusubiri alichotuitia. Baada ya ukimya mfupi alizungumza.
“Vijana wangu.”
“Naam mzee,” tuliitikia kwa pamoja.
“Kwanza poleni kwa kuwachelewesha tofauti na tulivyokubaliana.”

“Kawaida mzee tukupe pole wewe kwa matatizo uliyokutana nayo,” nilimpa pole kwa kuamini hata kama angekufa mimi ndiye ningekuwa chanzo.

Itaendelea baadae ...
 
Mke Wangu Alinifanya Niwe Mchawi - 28..


ILIPOISHIA:
“Vijana wangu.”
“Naam mzee,” tuliitikia kwa pamoja.
“Kwanza poleni kwa kuwachelewesha tofauti na tulivyokubaliana na matarajio yenu.”
“Kawaida mzee tukupe pole wewe kwa matatizo uliyokutana nayo,” nilimpa pole kwa kuamini hata kama angekufa mimi ndiye ningekuwa chanzo.
SASA ENDELEA...


“Wala usihofu ile ni moja ya kazi zetu, kazi nyingine lazima ujitolee uhai ufe wewe au afe yeye.”
“Kwa hiyo kazi imekuwa nzito?”
“Ilikuwa nzito si nzito tena japo kidogo iondoke na roho ya mtu.”
“Unamaanisha nini?”

“Baada ya kafara ya mbuzi mwekundu kazi iliyobakia ni kummaliza kabisa, kumbe katika sehemu ya uhai wake kuna ulinzi mkubwa uliomzunguka yaani atakayegusa lazima aondoke.

“Baada ya kuingia porini ili kumalizia kazi kilikuja kitu cha ajabu ambacho nimepambana nacho mpaka alifajiri. Ilikuwa vita nzito ambayo kwangu ilikuwa mara ya pili japo hii ilikuwa kubwa kidogo. Lakini mpaka naishiwa nguvu nilikuwa nimemaliza kazi. Kama ningeishiwa nguvu kabla sijammaliza ningekufa mimi.”
“Mungu wangu,” nilishtuka.”
“Usishtuke ni jambo la kawaida kwetu waganga.”
“Kwa hiyo?”
“Kesho mnaweza kurudi kazi imeisha.”
“Kuhusu yule jamaa itakuwaje?”
“Kazi imeisha hivi mkirudi mtakuta msiba.”
“Msiba?”
“Ndiyo.”
“Wa nani?”
“Wa adui yako.”
“Kafa lini?”
“Alfajili ya leo.”
“Mmh! Umejuaje?”

“Ndiyo kazi yangu, wewe umeleta si juu yako kujua kila kitu kinachofanyika zaidi ya kufanikisha kilichokuleta.”
“Nini kilichomuua?”
“Wewe ulitaka afe kwa nini?”
“Ajali.”
“Basi kafa kwa ajali leo alfajiri, asingekufa ningekufa mimi.”
“Mmh!”

“Basi nina imani kazi imekwisha japo ilikuwa nzito nashukuru imeisha salama, japokuwa kuna wakati nilianza kuchanganyikiwa. Lakini niliamini nitamuweza tu asingeweza kushindana na mimi huku ndiko Tewe hakujawahi kushindwa kitu.”
“Basi tunashukuru. Vipi kuhusu mke wangu?”
“Atarudi mwenyewe wala hakuna haja ya kutumia dawa kwa vile aliyekuwa akimzuzua ameshakufa.”
“Mmh! Mzee kweli atarudi?”
“Baada ya kifo atafukuzwa na ndugu wa huyo mwanaume na kumuona yeye ndiye nuksi.”
“Kwa hiyo?”

“Utamuona mwenyewe anarudi kuomba radhi, nina imani atatulia, kama adhabu atakuwa ameipata.”
Tuliagana na mzee Kidereko nikiwa siamini na kuona kama vile mzee kazi imemshinda na kuamua kutuondoa kijanja. Tulikwenda kulala baada ya kujiandaa na safari ya kesho alfajiri kurudi tulipotoka ili tuwahi kazini japo tulikuwa tumepitisha siku mbili.

Tuliamshwa alfajiri ya siku ya pili kwa ajili ya safari. Kwa vile kulikuwa na baridi kali hatukuweza kuoga, tulinawa uso tu.
“Kazala mwanangu kazi yangu japo ilikuwa ngumu lakini nimeimaliza vizuri sana. Ningekuwa mtu mwepesi pale uliponikuta mngekuta mzoga.”
“Ukisema mzoga una maana gani?” nilimuuliza.
“Mngekuta nimekufa.”
“Dah! Pole sana mzee wangu, ahsante sana kwa msaada wako.”
“Nawe pia. Ila nina ombi moja naomba unisaidie!”
“Ombi gani tena?”

“Nakuomba jambo tulilofanya huku libakie siri yako, watu wao ndiyo watakaozungumza yao kuhusu kifo cha ugoni wako. Kifo hiki ni vigumu mtu kujua kwa vile mazingira yake hakuna atakayekuwa na wasiwasi kwa kuamini amri ya Mungu.”
“Sawa mzee wangu nitafanya hivyo.”
“Haya nawatakieni safari njema,”

Mzee Kidereko alimpatia Shedu kifurushi kidogo na kumwambia:
“Hii zawadi yako.”
“Asante,” Shedu alipokea kile kifurushi, nikajua cha dawa japo sikutaka kujua dawa ya nini. Sikutaka kuhoji kapewa nini kwa vile ile ilikuwa hainihusu.
Baada ya kila kitu kwenda kama kilivyopangwa tulisindikizwa na vijana wa mzee Kidereko kwa baiskeli mpaka Mlalo ambako tulifika muda wa saa moja hivi za asubuhi.

Ilikuwa ni saa moja kabla ya magari ya kuelekea Dar kuondoka. Tulibahatika kupata tiketi kwenye basi la Umba, basi la Shambalai lilikuwa limejaa. Tuliingia na kukaa kwenye siti ya watu wawili.
Saa mbili gari liliondoka Mlalo na kuelekea Dar es salaam, Shedu alionesha alikuwa na usingizi sana, safari ilipoanza tu aliuchapa usingizi mimi niliendelea kuangalia mji wa Mlalo.

Akili yangu ilikuwa njia panda nisipate jibu kuhusu mwanaume aliyemchukua mke wangu kufariki dunia kwa ajali kama ni kweli.
Akili yangu haikuamini nilijua yule mzee katutoa kisiasa ili tu tusiondoke tukiwa hatuna imani naye. Sifa alizonipa Shedu na niliyoyakuta niliona kuna tofauti kubwa. Lakini sikutaka kuumiza kichwa, ukweli na uongo wa mganga nilijua ningeupata baada ya kufika mjini.

Fuatilia baadae....
 
Mke Wangu Alinifanya Niwe Mchawi - 29...

ILIPOISHIA;
SAA mbili asubuhi gari liliondoka Mlalo na kuelekea Dar es Salaam, Shedu alichukuliwa na usingizi na safari ilipoanza aliuchapa vya kutosha.

Miye niliendelea kuangalia mji wa Mlalo huku akili yangu ikiwa njiapanda nisipate majibu kuhusu mwanaume aliyemchukua mke wangu kama atakuwa amefariki dunia kwa ajali.

Akili yangu haikuamini, nilijua yule mzee aliamua kututoa kisiasa ili tusiondoke tukiwa hatuna imani naye.
Sifa alizonipa Shedu na mambo niliyoyakuta kule niliona kulikuwa na tofauti kubwa lakini sikutaka kuumiza kichwa zaidi, nilijua ukweli na uongo wa mganga nitaujua baada ya kufika nyumbani.
SASA ENDELEA...


KWA vile ilikuwa ni alfajiri nami usingizi ukaanza kuninyemelea lakini jambo hilo lilikuwa limechangiwa na mazingira ya sehemu tuliyofikia, siku zote sehemu usiyoizoea huwezi kulala vizuri, basi nami usingizi ukanichukua bila ya kujijua.
Shedu ndiye aliyenishtua kutoka usingizini, yeye aliamka muda ambao usingizi ulikuwa umeshanikolea.

“Kazala amka tupate chakula cha mchana.”
“Wapi hapa?” nilimuuliza baada ya kuona tumefika kwenye kituo cha basi.
“Korogwe.”
“Sasa ni saa ngapi naona jua ni kali?”
“Saa saba.”
“He! Kumbe nimelala sana!”

Tuliteremka Korogwe na kupata chakula cha mchana, kisha tukarudi kwenye basi na kuendelea na safari ya kurudi kwetu. Tulifika Chalinze saa tisa na nusu alasiri, tulipanda basi lililokuwa likitoka Dar saa kumi na nusu jioni tuliingia makwetu saa nne usiku.
Kwa vile muda ulikuwa bado Shedu alikwenda kwake na mimi nilirudi kwangu.
Nilishukuru kwa kuwa siku ya pili ilikuwa Jumamosi ambayo kwa kawaida huwa siendi kazini, hivyo niliamini ningekuwa na muda mrefu wa kupumzika.

Baada ya kula chakula nilichonunua, nilioga na kujitupa kitandani kutokana na kutawaliwa na uchovu usingizi haukuchelewa kunichukua.
Nilishtuka siku ya pili tena baada ya kugongewa na jirani yangu, nilifungua mlango na kutoka nje.
“Vipi jirani za asubuhi, ulisafiri?”
“Nzuri, eeh nilitoka kidogo.”
“Mbona hukuaga?”
“Ilikuwa ni safari ya ghafla sana samahani kwa hilo.”
“Mkeo alirudi,”
“Eeh!” nilishtuka kusikia vile.

“Alikuja juzi pamoja na mwanao, walikusubiri mpaka usiku bila kutokea, ilipofika usiku ilibidi alale kwenye korido asubuhi ya jana ndiyo kaondoka.
“Jana tena alikuja hapa bila mtoto alikaa mpaka saa tatu usiku akaamua kuondoka,” aliendelea kunifahamisha jirani yangu.
“Atakuwa amekwenda wapi?”

“Mmh! Kwa kweli siwezi kujua ila ameondoka na kuniomba nimuwekee mizigo yake vizuri na kusema atarudi kesho. Nia yake ilikuwa ni kuingia ndani, amesema anaweza kuja na fundi ili amfungulie mlango. Kwa nini hukuacha funguo?”
“Kama nilivyokwambia safari ilikuwa ya ghafla sana.”
“Basi kwangu kuna mizigo ya mkeo,”
“Sawa,” nilichukua mizigo ya mke wangu na kuiingiza ndani.

Baada ya kuweka vitu vya mke wangu vizuri nilikaa kwenye kochi na kuanza kuwaza na kuwazua kama kauli ya mganga na niliyoyasikia muda mfupi kuhusu mke wangu kurudi nyumbani yalikuwa na uhusiano.
Nilijiuliza kama mke wangu amerudi ina maana ni kweli yule mwanaume amekufa kwa ajali kama alivyonieleza mganga au kuna lingine lililotokea.

Nikiwa katikati ya mawazo Simon alibisha hodi, nilimkaribisha ndani kwa vile mlango ulikuwa wazi. Simon aliingia akionekana kuwa na jambo alilotaka kuniambia, baada ya kuketi alisema:
“Pole na safari.”
“Asante.”
“Mmh! mzee unatisha.”
“Kivipi?”
“Jamaa tumemzika jana.”
“Jamaa gani?”
“Si mgoni wako.”
“Muongo!”

“Kweli tumemzika jana, kwa kweli mimi na wote tuliosikia sababu ya kifo chake tulijua ni kifo cha kawaida lakini aliyonieleza Shedu nimeshtuka sana.”
“Unashtuka nini wakati hata mgoni wa Shedu naye alilamba udongo.”

“Ni kweli alilamba udongo, kifo chake wengi walijua kilitokana na kumchukua mke wa mtu, kulikuwa kama kuna miujiza fulani hivi, lakini kifo cha mbaya wako kilikuwa cha ajali, tena baada ya gari lake kugongana uso kwa uso na gari la mafuta. Waliofika kwenye tukio wanasema wala hakuomba maji, alikufa palepale.

“He! Kumbe kweli?” nilijikuta nikishtuka baada ya kusikia vile.
“Unashangaa nini?”
“Unajua aliyosema yule mzee mimi nilijua anatudanganya, nilidhani alikuwa anatupa moyo baada ya kuona kazi imemshinda.”
“Kaniambia yote Shedu yaliyotokea huko, lakini ukweli unabaki palepale yule mzee ni tishio, hasa kwenye kazi za kulipa visasi.”
“Lakini naamini adhabu aliyopewa ni kubwa sana,” nilisema.
“Si ndiyo uliyochagua?” Simon aliniuliza akinikazia macho.
“Adhabu hii sikuichagua bali walinichagulia ili kumkomesha.”
“Basi tena ni kujipanga upya, shemeji amerudi?”

“Nasikia amerudi juzi jioni na kulala hapa, asubuhi ameondoka inaonekana labda ameenda kwao.”
“Sasa ndiyo mkeo atulie kama umemuua huyo, akiendelea na tabia yake utaua wangapi?” Simon aliniuliza.
“Kwanza Simon hebu ondoa hilo neno la kusema nimeua, kazi yote imefanywa na mganga,” nilijitetea.
“Kwa sababu ya nani?”

“Kwa sababu yangu, lakini kwa uamuzi wa wengine, mi nilikuwa namtaka mke wangu tu.”
“Basi ndiyo hivyo mkeo atarudi jipange kuhakikisha kosa la awali halijirudii tena.”

Tukiwa katikati ya mazungumzo mara mlango wa mbele uligongwa, ilikuwa sauti ya mke wangu. Nilitamani ninyanyuke nikampokee lakini niliona aibu mbele ya ya rafiki yangu Simon.
Nilimkaribisha aingie ndani.

Mke wangu alipoingia alikuja moja kwa moja hadi nilipokuwa nimekaa na kupiga magoti kuomba msamaha.
Nini kitaendelea? Usikose baadae ....
 
Mke Wangu Alinifanya Niwe Mchawi - 30...

ILIPOISHIA...
Mke wangu aliingia na kuja moja kwa moja nilipokuwa nimekaa na kupiga magoti akiomba msamaha.
SASA ENDELEA...


“Samahani mume wangu najua nimekukosea kwa yote niliyokutendea, nimeamini yote ni matawi shina ni wewe. Najua nimekuumiza mume wangu kiasi cha kukufanya uchanganyike. Yote ni kiburi cha nazi kushindana na jiwe, leo hii nimegeuka bundi kila kona nafukuzwa familia ya nilipokwenda hawataki hata kunisikia mama naye hataki kuniona nitakuwa mgeni wa nani?
“Mume wangu Kazala nakuomba nipo chini ya miguuu yako, wewe ndiye kimbilio langu la mwisho, nawe ukinifukuza sina pa kwenda. Kazala mume wangu naomba unipokee tumlee mtoto wetu Zawadi. Najuta kukukimbia, nimeamini si wajinga waliosema usiache mbachao kwa msala upitao...

“Shemeji Simon nakuomba niombee msamaha kwa mume wangu Kazala ambaye nilimkosea kwa kuondoka bila kuaga, zilikuwa ni hasira lakini leo hii zimekuwa hasara kwangu.

“Kazala bado nakuhitaji katika maisha yangu, rudisha moyo wako nipokee tena, nakuahidi kuwa mke mwema katika maisha yangu yote yaliyobaki chini ya jua, nakupenda Kazala, nakupenda baba Zawadi nipo chini ya miguu yako,” mke wangu alilia kilio cha uchungu kuonesha kweli ameumizwa na yaliyotokea.

Yote yaliyotokea kwangu hayakuwa tatizo kwangu zaidi ya mke wangi kurudi tena mikononi mwangu. Nilimnyanyua na kumkumbatia na kumweleza nimemsamehe. Nilimkumbatia mwanangu ambaye alikuwa kwenye afya nzuri na mke wangu.

Pamoja na kuumizwa roho na kifo cha mgoni wangu, lakini nilipata faraja ya ajabu mke wangu kurudi mikononi mwangu. Kwa mara ya kwanza niliamini uchawi upo na unafanya kazi.

Maisha yalianza upya huku mke wangu kila kukicha akijutia alichokifanya, nami nilimweleza yote aliyofanya nimemsamehe toka moyoni mwangu. Hali ya utulivu ilirudi ndani bila mtu kunitilia wasiwasi juu ya kifo cha mgoni wangu kuwa nimekisababisha mimi, wengi waliamini ile ilikuwa amri ya Mungu.

Maisha nayo yaliendelea huku nikirudi katika hali yangu ya zamani kutokana na mapenzi mazito niliyopewa na mke wangu. Haikuchukua muda toka arudi, akabeba ujauzito mwingine ambao haukuwa na matatizo nao, hakuzungumzia kuutoa zaidi ya kuulea kwa ajili ya kusubiri siku ya kujifungua.

Hali ile ilinifanya niamini mke wangu kweli tukio lililotokea limempa fundisho. Muda ulipofika alijifungua mtoto mwingine wa kike ambaye nilimwita Happy kutokana na furaha ya kurudi kwa utulivu ndani ya nyumba yetu.

Watoto wetu Zawadi na Happy walikua vizuri huku mama yao akionesha kuwapenda na kuwajali tofauti na Zawadi alipokuwa mdogo alivyobemendwa na mama yake.

Siku zilizidi kwenda nami nikizidi kuyafurahia maisha, mke wangu alichukua miaka mitatu na nusu toka arudi kuanza mambo yake. Nakumbuka aliniomba sana tutafute msichana wa kazi kwa ajili ya kumsaidia kazi za nyumbani.

Kwa vile sikutaka kubishana na mke wangu nilikubaliana naye na kumpa ruksa ya kutafuta mfanyakazi.
Haikuchukua hata siku tatu msichana wa kazi alipatikana kuonesha alimuandaa hata kabla ya kunieleza. Tuliendelea na maisha huku familia yetu ikiwa imeongezeka mtu mwingine.

Waswahili wanasema kaniki hata ukiifua na mito na bahari zote dunia na sabuni zote hata siku moja haiwi nyeupe. Pia hawakukosea kusema la kuvunda halina ubani. Toka aliporudi alikuwa na tabia ya kunywa pombe kitu ambacho mwanzo nilikikemea lakini alinibembeleza kwani alikuwa amezoeshwa na alipokwenda.

Kwa vile nilikuwa nampenda nilimkubalia awe anakunywa siku mojamoja. Sehemu tuliyokuwa tukiishi kulikuwa na Grosari karibu. Mara nyingi alimtuma msichana wa kazi na kumletea ndani na kunywa.

Siku nyingine niliporudi sikumkuta ndani, msichana wa kazi alinieleza kwamba, mke wangu alimwambia, kama nitarudi kabla hajarudi akamwite.
Nilimtuma akamwite japo muda ule alitakiwa kuwa nyumbani, alimfuata na baada ya muda alirudi akiwa amechangamka kidogo.

“Vipi mume wangu umerudi zamani?”
“Kama dakika tano, vipi umeanza lini kwenda baa kunywa?”
“Samahani mume wangu, leo jirani yetu God alinipa ofa hapo nje kwenye Grosari.”
“Hakuna tatizo ila usiiendekeze sana pombe.”
“Mume wangu si leo tu, tena nimepewa ofa na jirani.”
“Hakuna tatizo ila usiendekeze sana, kunywa siku mojamoja siyo mbaya.”

Kumbe ukaribu na jirani yangu ulikuwa na maana pana zaidi ya ujirani, mke wangu alianzisha uhusiano na jirani yangu ambaye nikiwa kazini alimgeuza mke wangu wake.
Nakumbuka siku moja usiku nilishtuka kitandani na kujikuta nipo peke yangu. Sikuwa na wasiwasi kwa kuamini huenda amekwenda msalani.
Kwa vile choo na bafu vilikuwa nje nilijua amekwenda kujisaidia tu, nilijilaza tu pale kitandani. Sikuchelewa, nikapitiwa na usingizi.

Itaendelea baadae........
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom