Mke wangu alinifanya niwe Mchawi -1

Mke wangu alinifanya niwe Mchawi -1

Mke wangu alinifanya niwe mchawi-5

ILIPOISHIA; NILIMCHUKUA mwanangu na kumpeleka kwa mama mzazi wa mke wangu na kumuuliza kama mke wangu alifika kwake. Alijibu kuwa hajamuona, nilimuomba nimuachie mtoto. Alikubali kitu cha ajabu hakuniuliza swali lolote zaidi ya kumchukua mtoto. Nilirudi nyumbani kumsubiri mke wangu aniambie alikwenda wapi.

SASA ENDELEA... Majira ya saa kumi na mbili na nusu mke wangu alirudishwa na gari, kwa vile nilishaelezwa muda wake wa kurudi, nilitoka na kukaa nje, ufunguo nilimpatia mama Sonono na kumwambia akija amwambie kuwa mtoto amechukuliwa na mama yake mzazi. Alipofika aliteremka na kukimbilia kwa mama Sonono kuulizia ufunguo. Baada ya muda nilimuona akitoka barabarani akiwa kama anayetafuta kitu, huku akiwa anapiga simu, baada ya muda gari lililomleta lilirudi. Kabla hajapanda kwenye gari nilijitokeza na kumwita. “Mke wangu.” Alishtuka kuniona mpaka simu ikamponyoka chini huku akisema kwa sauti kubwa: “Ha! Mume wangu!” “Vipi mpenzi ingia twende nina safari nyingine,” sauti kutoka ndani ya gari ilimhimiza aingie kwenye gari. “John nenda tu, mume wangu.” “Mumeo kafanya nini tena mpenzi?” “John ondoka mume wangu huyu hapa.” “He!” Sauti ilitoka kwenye gari na gari kuondoka kwa kasi bila kufunga mlango mmoja. Sikutaka kutaharuki nilimuuliza: “Unatoka wapi?” “Kwa mama.” “Yule nani?” “Bwana wa shoga yangu alinipa lifti.” “Mmh! Sawa.” “Vipi mbona mapema?” “Kawaida tu kwani kuna ubaya?” “Hakuna, Samahani mume wangu, nilikwenda kwa mama na kupishana naye huku nyuma alikuja na kumchukua Zawadi, nilikuwa naomba nimfuate.” “Sawa, hakuna tatizo, utanikuta.” Alisogea mbele na kukodi teksi iliyompeleka kwao, niliingia ndani nikiwa nimefura kwa hasira nikiwa siamini nilichokiona na kuanza kuamini yote niliyoelezwa juu ya uchafu wa mke wangu. Nilimsubiri kwa hamu kubwa arudi anieleze sababu ya kujifanya kondoo mwenye ngozi ya chui. Kitu cha ajabu mezani kulikuwa kumeandaliwa kila kitu kuonesha kwamba mke wangu kabla ya kuondoka hufanya kila kitu kwa ajili ya chakula cha jioni ili akirudi hata kama amechelewa chakula kionekane kuwa ni tayari. Miye nilipokuwa narudi niliamini kuwa mke wangu hakutoka kwa vile chakula kilikuwa kimeshatayarishwa. Nilikwenda hadi chumbani na kujilaza kitandani miguu ikiwa chini bila ya kuvua viatu, niliweka mikono kichwani huku macho yangu yakitazama juu nisiamini nilichokisikia, hata nilichokiona kwa macho yangu. Nilipatwa na mtikisiko wa moyo kwa mara ya kwanza tangu niwe na akili timamu japokuwa niliishawahi kuona na kusikia usaliti ndani ya ndoa za watu. Nikiwa katikati ya mawazo mke wangu alirudi akiwa na mtoto na moja kwa moja alikuja kukaa pembeni yangu huku akijichekesha. Nilijiuliza mama yake amemwambia nini kutokana na kuwa katika hali ya kawaida tu. “Vipi mume wangu?” “Poa.” “Mbona kama haupo sawa?” “Nipo sawa,” nilimjibu kwa sauti ya chini. “Hapana mume wangu lazima utakuwa na tatizo.” “Nipo sawa.” “Nakuja,” mke wangu alisema huku akinyanyuka na kwenda nje akimuacha mtoto pembeni. “Baba,” mwanangu Zawadi aliniita. “Mama,” nilipenda kumwita hivyo kwa kuwa alikuwa akitumia jina la mama yangu mzazi. “Pipi api?” “Nitakwenda kukununulia.” “Tende dukani baba kanunue pipi,” mwanangu alisema huku akijivuta kwangu na kunishika mkono, niliamua kumpelekea dukani. Nilimuangalia mwanangu na kujikuta nikitokwa na machozi ya uchungu, alizidi kunilazimisha ninyanyuke. Nilinyanyuka kitandani na kumbeba mpaka dukani ambako nilimnunulia pipi na biskuti. Wakati napita kurudi ndani nilimsikia mke wangu akizungumza na mama Sonono. Kwa jinsi walivyokuwa wakizunguza niliamini kabisa alijua bado nilikuwa chumbani. “Dada umeniangushia jumba bovu,” nilisikia sauti ya mama Sonono ikilalamika. “Jumba bovu vipi, kwani anajua nilikwenda wapi?” “Kurudi kwa mumeo kuna sababu, hata maswali yake yalionesha anajua mengi juu yako, hata mtoto kwa mama yako alimpeleka yeye.” “Wewee usiniambie!” sauti ya mke wangu ilionesha kushtuka. “Kweli, kabisa ila alinikataza nisikuambie.” “Jamani kwa nini umenigeuka?” “Sikuwa na jinsi nilihofia kupigwa na mumeo kwa jinsi alivyokuwa angeweza kumtafuna hata mtu.” “Akupige kwani wewe ndiye uliyetoka nje ya ndoa, wa kupigwa ni miye, kwanza jeuri hiyo ataitoa wapi?” mke wangu alizungumza kwa sauti ya kujiamini. Maneno yale yalionesha dhahiri kwamba mke wangu alifanya yote yale kwa vile alikuwa na kitu alichokuwa akikitegemea. “Dada ukitoka tena uondoke na mwanao sitaki ugomvi na mumeo, kwani ataona labda mimi ndiye ninayekufanyia mipango.” Itaendelea
 
Mi ilipotoa wazo kuwa nami nitakuwa mwandhishi wa stori, ilijifanya kunishushua... Ona sasa mzizimkavu ameshaniwahi...

mambo Tuko miss you miss you sana mkuu
tupo wote mashabiki aisee.......dah huchezi mbali!!!
 
Last edited by a moderator:
Mke wangu alinifanya niwe mchawi-6

ILIPOISHIA;

“Akupige kwani wewe ndiye uliyetoka nje ya ndoa, wa kunipiga ni mimi, kwanza jeuri hiyo aitoe wapi?” Mke wangu alizungumza kwa sauti ya kujiamini.
Maneno yake yalionesha kabisa kuwa mke wangu alikuwa akifanya mambo yake huku akijua kuwa kulikuwa na kitu anachokitegemea.
“Dada ukitoka tena uondoke na mwanao sitaki ugomvi na mumeo na ambaye anaweza kuona labda miye ndiye ninayekufanyia mipango.”
SASA ENDELEA...


“Mi mtoto mdogo? Nitaondoka naye kwani kazi anafanya yeye? nitamuweka kwenye kochi kisha namaliza haja zangu, hilo shoga lisikupe shaka, basi baadaye.”
Kwa vile ilikuwa giza mke wangu alitupita mimi na mwanangu bila ya kutuona na kuingia ndani.
Nami niliingia ndani na kukutana naye mlangoni, aliponiona aliniuliza:
“Vipi umetoka wapi?”
“Dukani.”
“Eti, kwani mume wangu leo umerudi saa ngapi?”
“Kwani vipi?”
“Nasikia umerudi mapema?”
“Tatizo ni nini?”
“Sasa umerudi mapema ili iweje?”
“Sina ruhusa ya kurudi nyumbani kwangu mapema?”
“Siyo hivyo.”
“Sasa tatizo nini?”
“Ujaji wako umeonekana umekuja kwa sababu.”
“Ndiyo umekuja kwa sababu maalum.”
“Sababu gani?”
Nilijikuta nikipata nafasi ya kufungua yaliyo moyoni mwangu.
“Niambie ulikwenda wapi?”
“Kutembea.”
“Kwa ruhusa ya nani?”
“Nilisahau kukuaga naomba unisamehe kwa hilo.”
“Aliyekurudisha ni nani?”
“Ni rafiki wa shoga yangu.”
“Naomba uniambie ukweli la sivyo leo nitakufanyia kitu kibaya sana,” nilimtisha.
“Unataka kunifanyia kitu gani?” alishtuka.
“Usiponieleza ukweli nitakufanyia kitu kibaya ambacho hutakisahau maisha mwako.”
“Unataka ukweli gani mume wangu?” mke wangu aliingia woga.
“Ninajua kila siku nitokapo nawe huku nyuma unatoka, huwa unakwenda wapi?”
“Nani kakuambia?”
“Si kujua aliyeniambia, bali ni wewe kunieleza ninapotoka nawe unatoka, unakwenda wapi?”
“Waongo hao mi sijawahi kutoka, ni leo tu.”
“Mama Zawadi naomba uniambie ukweli,” nilipandisha sauti.
“Nilikwenda kwa shoga yangu na wakati wa kurudi mpenzi wake alinipa lifti kwenye gari lake.”
“Huyu mtoto kakukosea nini?”
“Kwa vipi?”
“Mbona unamfanya kama yatima, kama unafanya uchafu wako basi mhurumie mtoto, unaridhika na hali ya mtoto ya kuteseka hivi?”
“Nimemtesa kivipi?” majibu ya mke wangu hayakuonesha kushtushwa na hali ya mtoto wetu.
“Kila ukiondoka unamwacha kwa mama Sonono mtoto hana matunzo, leo tu nimemkuta akila matope, kwani nini umekuwa mkatili kiasi hiki mke wangu?”
“Mume wangu mtoto kuchezea matope ni kitu cha kawaida tu.”
“Uchafu unaoufanya umesababisha mtoto aendelee kuteseka chini kama fundi majiko, au unataka azeeke akiwa amekaa?”
“Mwanao mvivu tu wala si mimi.”
“Taarifa zako za kumharibu mtoto kila mtu mtaani anazijua, wanamuonea huruma mtoto, ona miguu ilivyolegea kwa umalaya wako.”
“Sawa mimi malaya, basi nipe talaka yangu.”
“Tatizo si talaka bali kumuonea huruma mtoto.”
“Mi si malaya naomba talaka yangu.”
“Hapa talaka haitoki kuanzia leo mtoto atakaa kwa mama na siku nirudi halafu nisikukute utanitambua.”
Kwa kweli mke wangu nilikuwa nampenda sana, sikumfanya lolote tulilimaliza kwa kuniomba msamaha kwa kuondoka bila kuaga lakini suala ya kutoka nje ya ndoa alilipinga kwa nguvu zote huku akiniuliza:
“Lini tulipokutana kimwili ulikuta nimetumika? Mara nyingi mimi ndiye ninayekulazimisha kufanya mapenzi kama ningekuwa si mwaminifu kulikuwa na haja gani ya kulazimisha mapenzi kwako?”
Kwa kweli sikuwa na jibu, kwa upande mwingine nilimuona kama mke wangu yupo sawa kutokana na tangu nimuoe hakuwahi kutoa udhuru kitandani. Tena kwa upande mwingine nilikuwa namuonea huruma kutokana na kazi zangu ambazo hunilazimu kurudi nikiwa nimechoka. Suala la mtoto kumpeleka kwa bibi yake alikubaliana nalo.
***
Maisha yaliendelea huku nikiamini kabisa kuwa mke wangu amejirekebisha, alipokuwa akitaka kutoka nyumbani alikuwa lazima aage ndipo atoke.


Nini kiliendelea baadae................
 
Mke Wangu Alinifanya Niwe Mchawi-7


ILIPOISHIA:
Maisha yaliendelea huku nikiamini kabisa mke wangu kajirekebisha, ikawa akitaka kutoka nyumbani ni lazima aage ndipo aondoke.
SASA ENDELEA...


Na safari zake nyingi zilikuwa kwenda kumuona mtoto kwa bibi yake. Hilo halikunipa shida, nilijua ni sehemu ya upendo kwa mwanaye.
Miezi minne baada ya tukio lile, hali ya mtoto ilibadilika, akawa anaweza hata kusimama na kunyanyua mguu mmoja. Hali ile ilinifanya niamini kabisa mke wangu hakuwa mwaminifu katika ndoa yetu licha ya kujitetea kwa kuapa kwa miungu yote.
Kama kawaida, siku moja nikiwa kazini majira ya saa nane mchana, mke wangu alinipigia simu na kunieleza kuwa ameitwa na mama yake mara moja, nilimkubalia. Jioni niliporudi sikumkuta, sikuwa na wasi, nikaingia ndani na kuoga, baada ya hapo nilijipumzisha sebuleni kwenye kochi kumsubiri mke wangu arudi.
Kwa vile nilikuwa nimechoka, nilipojilaza kidogo usingizi mzito ulinipitia. Nilishtuka usiku na kujiona nimelala muda mrefu, saa ya kwenye simu ilionesha ni tayari saa tatu za usiku. Nilishtuka na kwenda nje kulipokuwa na kiza kinene, nilijaribu kupiga simu ya mke wangu, iliita kwa muda bila kupokelewa na niliporudia, simu haikupatikana tena.
Nilirudia zaidi ya mara tano, nikaamini huenda chaji imekwisha, niliendelea kumsubiri nikiamini yupo njiani na angerudi muda wowote. Mpaka saa tano inaingia, bado alikuwa hajarudi. Wasiwasi ulikuwa mwingi, nikaamua kwenda nyumbani kwao kujua kuna kitu gani kilichomfanya mke wangu mpaka muda ule awe hajarudi.
Kabla ya kwenda, nilijaribu kupiga simu yake lakini bado haikuwa hewani. Niliondoka na kwenda ukweni kwa kukodi gari lililonipeleka mpaka nyumbani kwao. baada ya kuteremka, nilielekea nyumbani kwa wazazi wa mke wangu, sehemu niliyokuwa nimepanga wakati naanza maisha.
Nyumba ilikuwa kimya na taa zote zilikuwa zimezimwa kuonesha walikuwa wamelala, akili ya haraka ilinifanya nifikiri kuwa huenda nimepishana na mke wangu ambaye ameondoka muda si mrefu na kufanya wazazi wake walale. Nilitaka kugeuza kurudi lakini niliona ni vizuri niulize ikiwezekana nijue kilichomchelewesha mke wangu.
Nilisogea kwenye nyumba na kugonga mlango, baada ya kugonga kwa muda sauti kutoka ndani iliuliza:
“Nani?” ilikuwa sauti ya mama mkwe.
“Mimi mama.”
“Nani... baba Zawadi?” aliifahamu sauti yangu.
“Ndiyo mama.”
Baada ya muda mlango ulifunguliwa na kutoka huku akionesha alikuwa ameshapitiwa na usingizi.
“Karibu baba.”
“Asante mama.”
“Vipi mbona usiku?”
“Nimekuja kumuulizia mwenzangu.”
“Nani, mama Zawadi?”
”Ndiyo mama.”
“Alikuaga anakuja huku?”
“Ndiyo, alinipigia simu akisema umemwita, niliporudi nyumbani sikumkuta, nimemsubiri tangu nimerudi mpaka muda huu sijamuona na kunifanya niingiwe na wasiwasi.”
“Amekuomba ruhusa saa ngapi?”
“Saa nane mchana.”
“Mmh! Sasa atakuwa wapi, simu yake umempigia?”
“Iliita mara moja bila kupokelewa, niliporudia haikupatikana tena.”
“Ulipiga saa ngapi?”
“Majira ya saa tatu usiku.”
“Mmh! Mbona mtoto huyu ana matatizo!”
“Mama hukumwita?” nilimuuliza bibi Zawadi baada ya kuona hakukuwa na mawasiliano na mwanaye.
“Sijamwita,” alinijibu kwa mkato.
“Sasa atakuwa amekwenda wapi?”
“Kwa kweli sijui.”
“Bora simu yake ingekuwa hewani ingekuwa afadhali lakini ndiyo hivyo haipatikani.”
“Mtoto huyu kawaje jamani, hebu baba rudi nyumbani kamuangalie huenda amerudi.”
“Sawa mama.”
“Basi lolote litakalotokea nijulishe.”
“Sawa mama.”
Niliagana na mama mkwe na kurudi nyumbani, njia nzima nilikuwa na maswali mengi juu ya ombi la ruhusa ya mke wangu kuwa ameitwa na mama mkwe. Ilionesha wazi msamaha alioomba mke wangu ulikuwa ni danganya toto. Nilijiuliza tabia ile mke wangu kaitoa wapi? Tangu nilipomfahamu alikuwa msichana mpole, mkimya tena mwenye heshima.
Nilipofika nyumbani sikumkuta mke wangu, niliingia ndani na kukaa kwenye kochi kwa kuhofia kama nitakwenda kulala na kupitiwa na usingizi mzito, labda mke wangu anaweza kurudi muda wowote na mimi kushindwa kumfungulia na kupata sababu ya kulala nje.

Nilirudisha mlango na kuzima taa ya sebuleni, nikakaa kwenye kochi ili kumsubiri mke wangu ambaye sikujua atarudi muda gani. Mpaka muda ule ilikuwa ni saa saba na nusu usiku usiku.
Itaendelea baadae.........................
 
Mke Wangu Alinifanya Niwe Mchawi-8....

ILIPOISHIA;
MLANGO nilirudisha na kuzima taa ya sebuleni na kukaa kwenye kochi ili kumsubiri mke wangu ambaye sikujua atarudi muda gani.

Mpaka muda ule ilikuwa ni saa saba na nusu za usiku.
SASA ENDELEA...


Nilijitahidi kukaa macho ili mke wangu akirudi na kugonga, niweze kumuona. Kuna kipindi nilipitiwa na usingizi niliposhtuka nilitoka mpaka nje kuangalia kama labda nitamuona mke wangu akiwa amerudi na kuniita na kushindwa kumsikia.
Nilizunguka nyumba nzima bila kumuona mke wangu na kurudi tena sebuleni kumsubiri.
Siku ya pili ilinikuta nikiwa bado nipo sebuleni nikimsubiri mke wangu, nikiwa najiandaa kwenda chumbani, mke wangu aliingia akionesha amekunywa pombe kitu ambacho hakuwahi kukifanya katika maisha yake yote niliyomjua na nywele zake zilikuwa timtim.
“Ooh! Mume wangu, habari za asubuhi?”
“Nzuri, habari za wapi?”
“Nilikwenda kwa mama wakati narudi shoga yangu alinipigia simu kuwa kuna harusi ya ndugu yake. Nilijua nitawahi kurudi kumbe sherehe ni sherehe kuja kushtuka muda umekwenda na usafiri ulikuwa wa tabu nikaamua kulala huko huko.”
“Kwa nini hukunipigia simu?”
“Wakati unanipigia simu ilizimika hata kabla sijakujulisha.”
“Na mbona umekunywa pombe, umeanza lini?”
“Mume wangu sherehe ina vishawishi vingi, lakini sikunywa sana.”
Nilijikuta kwa mara nyingine nikishindwa kumhukumu mke wangu, niliamua kumsamehe kwa vile nilikuwa nampenda sana. Ila nilimuomba asiondoke nyumbani bila kuaga pia asiwe anakunywa pombe.
Mke wangu kama kawaida yake aliniomba msamaha na kuniahidi kuwa hataweza kuondoka bila ya kuaga, pia hatarudia tena kunywa pombe.
Nilimsamehe mke wangu kwa vile nilikuwa nampenda sana na sikutaka kumpoteza maishani mwangu kwa kuamini kuwa yeye ni kila kitu kwangu.
Baada ya tukio lile mke wangu alitulia na heshima ya ndoa ikarudi ndani kama kawaida.
Wakati huo mtoto wetu alikuwa amekazana kutembea, kwa kitendo cha mwanangu kutembea niliwashukuru sana majirani. Wiki moja baada ya tukio la mke wangu kulala nje aliniomba tuhame mtaa ule.
“Mume wangu naomba tuhame hapa.”
“Tuhame hapa twende wapi?”
“Sehemu yoyote lakini mbali na hapa.”
“Kodi si itatusumbua?” Nilimwambia kwa kuwa hali yangu ya kiuchumi aliijua.
“Mume wangu unafanya kazi, acha kujilegeza, inatakiwa sasa hivi tuishi maisha ya kwetu wenyewe bila kuwategemea watu,” yalikuwa maneno ya kweli lakini yalitakiwa maandalizi ya muda mrefu hasa nikizingatia kulipa kodi ya miezi sita kwa haraka ulikuwa mtihani mkubwa kwangu.
“Lakini mbona mama alisema hii ni nyumba yako amekupa baada ya kuoana?” Ilibidi nihoji baada ya mke wangu kulazimisha kuhama.
“Kazala, husikii tunavyosimangwa kuhusu hii nyumba, hasa wewe mume wangu maneno yao kwa kweli huwa yananiumiza sana pale wanapokusema vibaya eti nimekuoa badala ya kunioa, hayo ni maneno gani mume wangu?”
“Mmh! Sina jinsi kwa vile ni haraka sana, nipe wiki nijaribu kukopa kazini ili tutafute nyumba.”
“Kuhusu kodi ya kuanzia nitalipa mimi itakayofuata utalipa wewe.”
“Hakuna tatizo,” nilikubaliana naye bila kuhoji fedha ataitoa wapi kwa kuhofia kubadili uamuzi wake.
Siku ya pili nilipokwenda kazini mke wangu alinipigia simu na kunijulisha kuwa amekwisha hamisha kila kitu na kunielekeza nikitoka kazini niende sehemu alipo na siyo pale tena.

Nilipotoka kazini nilikwenda sehemu aliyonielekeza na kushtuka kukuta amepanga kwenye nyumba ya gharama iliyokuwa imo kwenye uzio, kitu kilichonipa wasiwasi na kujiuliza kama kodi aliyolipa mke wangu ikiisha nitaweza kulipa.

Nini kiliendelea baade........
 
Mke Wangu Alinifanya Niwe Mchawi-9....

ILIPOISHIA:

Nilipotoka kazini nilikwenda sehemu aliyonielekeza na kushtuka kukuta amepanga kwenye nyumba ya gharama iliyokuwa ndani ya fensi, kitu kilichonipa wasiwasi na kujiuliza kama kodi aliyolipa mke wangu ikiisha nitaweza kuilipa. Mke wangu alinipokea kwa furaha.
SASA ENDELEA...

"Karibu mume wangu kwenye makazi mapya."
"Asante."
"Mbona kama unashangaa?"
"Nashangaa kwa mambo mawili, kwanza nyumba nzuri sana na pili na wasiwasi kodi yake ni kubwa."
"Ni kweli kodi ni kubwa lakini ni sehemu nzuri tutakayoishi bila bughuza za watu."
"Nyumba yote kwa mwezi shilingi ngapi?"
"Laki moja na nusu."
"Mke wangu laki moja na nusu kwa mwezi umelipa kwa muda gani?"
"Mwaka mzima."
"Ndiyo shilingi ngapi?"
"Hesabu unajua, zidisha laki na nusu mara kumi na mbili."
"Sasa mimi nitaweza kulipa fedha zote hizo?"
"Nitakusaidia, kuwa na amani moyoni mwako."
Sikutaka kuhoji sana fedha zote hizo kazipata wapi, kwani Waswahili wana msemo wao kuwa ukimchunguza sana bata huwezi kumla na ukimchunguza sana mkeo hutaweza kuishi naye. Tuliyaanza maisha ya Uzunguni, sehemu waliyokuwa wakiishi watu wenye uwezo. Kwa kweli maisha ya makazi mapya yalikuwa mazuri sana yenye furaha na amani.
Kwa muda mfupi, afya yangu ilirudi katika hali ya kawaida baada ya kuteseka kwa muda mrefu kutokana na vituko vya mke wangu. Kutokana na kuonesha mke wangu amejirekebisha tulimchukua mtoto wetu na kuishi naye. Heshima aliyoonesha ilimshtua hata mama yake mzazi.
Maisha yalisonga mbele, mke wangu akashika ujauzito wa pili, kitu kilichozidi kunipa faraja moyoni mwangu. Lakini ilikuwa tofauti kwa upande wa pili, mke wangu hakupenda kubeba ujauzito kwa vile mtoto wetu alikuwa bado mdogo.
"Mke wangu tatizo nini?"
"Huoni Zawadi bado mdogo."
"Miaka mitatu si michache na mpaka unajifungua atakuwa amesogea sana."
"Kwa upande wangu nilipanga kuzaa baada ya Zawadi kufikisha miaka mitano."
"Basi bahati mbaya, itabidi uzae hivyohivyo."
"Siwezi, lazima niitoe hii mimba."
"Usiitoe mke wangu, Zawadi tutampeleka kwa bibi yake ili asipate shida."
"Bado nina hamu ya kumlea mwanangu, kama mtoto utapata tu muda ukifika," mke wangu bado alishikilia msimamo wake.
"Nakuomba usiitoe hiyo mimba, nipo chini ya miguu yako mke wangu," nilimbembeleza mke wangu mpaka nikampigia magoti.
"Kwa hilo siwezi kukusikiliza, sihitaji senti tano yako, nitatoa kwa fedha zangu."
Kwa mara nyingine mke wangu alinizidi nguvu, nikamkubalia kwa shingo upande. Siku ya pili nikiwa kazini, majira ya saa tisa alasiri, mke wangu alinipigia simu kunijulisha kuwa amefanikiwa kuitoa mimba salama. Nilimkubalia lakini upande wa pili moyo uliniuma sana, hata kazi ilinishinda na kwenda sehemu ya peke yangu ambapo nililia sana kumpoteza mwanangu mtarajiwa.
Jioni niliporudi, nilimkuta mke wangu nyumbani, hali yangu ya unyonge ilimshtua mke wangu na kunifuata nilipokuwa nimekaa, akawa ananibembeleza.
"Mume wangu, najua kiasi gani nilivyokuumiza lakini sikuwa na jinsi, nilifanya vile kwa maana kubwa. Kwa sasa ni vigumu kunielewa lakini amini nilichokifanya si kukukomoa bali kumpa nafasi Zawadi. Kumbuka makosa yangu ya awali yalimtesa mwanangu hivyo sasa hivi nina deni la kumlea."
Kutokana na kumpenda sana mke wangu, nilikubaliana naye. Maisha yalisonga huku akionesha mapenzi mazito kwangu, kitu kilichofuta mawazo ya kutoa ujauzito.
Siku zote kimya kingi kina mshindo mkuu. Mwezi mmoja baada ya kutoa ujauzito, asubuhi moja nilidamka kwenda kazini huku hali yangu kiafya ikiwa si nzuri.
Nilijitahidi kwa kuamini mwanaume si mtu wa kujilegeza. Nilipofika kazini, nilijitahidi kufanya kazi lakini kutokana na kufanya kazi juani, hali yangu ilibadilika na kuwa mbaya hivyo niliruhusiwa kwenda hospitali kupata matibabu.
Nilikwenda hadi hospitali ya wilaya na kupata huduma japo dawa nilikwenda kununua duka la kuuza dawa. Nilibeba dawa zangu na kurudi nyumbani kupumzika. Nilipofika nyumbani, ndani ya geti nilikuta kuna gari ambalo kwangu halikuwa geni sana japo sikukumbuka nililiona wapi.
Baada ya kutafakari, niligundua lile gari ndilo lililomshusha mke wangu, nikashtuka kulikuta nyumbani kwangu na kujiuliza limefuata nini pale. Niliingia ndani na kukuta sebuleni kuna pombe kali juu ya meza na glasi mbili.
Sikujishughulisha navyo, nilielekea chumbani, nilipofika kwenye mlango wa chumbani, nilikuta umefungwa kwa ndani, nikasikia sauti mbili ya mwanamke na mwanaume. Sauti ya mwanamke ilikuwa ya mke wangu ya kiume sikujua ni ya nani. Kwa haraka nilitoka mpaka nje na kuzunguka dirishani na kuchungulia ndani.

Itaendelea baadae............
 
Mke Wangu Alinifanya Niwe Mchawi-10.....


ILIPOISHIA;
Sikujishughulisha navyo nilielekea chumbani, nilipofika kwenye mlango wa chumbani nilikuta umefunga na ndani nilisikia sauti mbili ya mwanamke na mwanaume. Sauti ya mwanamke ilikuwa ya mke wangu ya kiume sikujua ni ya nani. Kwa haraka nilitoka mpaka nje na kuzunguka dirishani na kuchungulia ndani.
SASA ENDELEA...


Nilioyaona ndani nusra mapigo ya moyo yasimame ghafla, kitandani kwangu alikuwepo mke wangu na mwanaume mmoja ambaye hakuwa mgeni sana machoni mwangu japo sikukumbuka niliwahi kumuona wapi wote wakiwa watupu kama walivyozaliwa.
Ilionesha walikuwa wamemaliza kufanya uchafu wao muda si mrefu kwa jinsi walivyokuwa wamejilaza. Nilihisi miguu haina nguvu na kurudi chini bila kujieleza na kukaa kama mzigo. Nikiwa nimekaa chini huku nimeegemea ukutani nikisikia homa ikipanda mara mbili na jasho lilinitoka kama maji na kujiona kama nakufa muda si mrefu.
Nikiwa nimekaa chini niliyasikia mazungumzo yaliyokuwa yakiendelea ndani.
“Sasa kwa nini uliitoa ile mimba, si uliniahidi utanizalia mtoto,” sauti ya kiume ilisema.
“Ni kweli, lakini damu yako ni kali sana ningeiacha ingeniletea matatizo katika ndoa yangu.”
“Matatizo gani?”
“Nilikuwa na wazo hilo, lakini siku niliyowaona watoto wako wanafanana kama mayai niliogopa. Nilikueleza niwe mke wako wa pili hutaki unafikiri ningejifungua humu ndani japo mume wangu asingejua kitu lakini walimwengu wangemweleza. Hata kutoka kwangu kuna watu wenye roho mbaya walimueleza.
“Bila kuhama kule mambo bado yangekuwa mabaya, japo inabidi kutokana na kukupenda lakini wakati mwingine namuonea huruma mume wangu. Toka tuhamia huku pamekuwa kama kwako unakuja muda wowote unakula na kuvaa tofauti na kwako.
“Ukitaka nikuzalie mtoto nitoe kwa bwana huyu haichukui hata mwezi nitakubebea mtoto.”
“Nimekuelewa mpenzi wangu, lakini japo tunamfanya yule jamaa ---- huwa sijiamini sana kuja hapa unafikiri akitufumania tutafanyaje?”
“Hawezi kutufumania.”
“Kwa nini unasema hivyo?”
“Nimekueleza haruhusiwi kurudi nyumbani bila kunijulisha.”
“Kwa nini nisikupangie nyumba nyingine au uwe unatoka na kuwahi kurudi huku nani anakufahamu?”
“John hebu acha kuniudhi, nilikulazimisha tuhamie huku ili tujitawale sasa unataka twende wapi?”
“Si unajua wewe mke wa mtu.”
“Hili umelijua leo, tuna muda gani toka tuhamie hapa?”
“Muda mrefu.”
“Basi naomba wazo la kufumaniwa ondoa.”
“Sasa mpenzi wacha nikukimbie.”
“Mbona haraka.”
“Nilipokuja nilikueleza nini?”
“Ooh! Nilisahau kwa hiyo mpaka kesho kutwa?”
“Ndiyo maana yake.”
“Basi twende tukaoge uwahi.”
Niliwasikia watu wakinyanyuka kwa sauti ya kitanda kupiga kelele. Nikiwa nimekaa chini. Niliamini kama mke wangu akigundua nimemfumania angeomba taraka kutokana na kauli aliyokuwa akiitoa ndani. Nilinyanyua pale chini huku miguu ikiwa haina nguvu na kutoka nje ya geti kwa shida huku nikitetemeka mpaka nje. Nilisogea mbali ya nyumbani ili kusubiri jamaa aondoke ili nipige simu kuwa nipo njiani.
Kutokana na hali yangu kuwa mbaya sikufika mbali sana kizunguzungu na kichefuchefu kilikuwa kikali. Nilisogea kwenye mti wa jirani na nyumbani na kutapika sana na kulala kwenye matapishi kwa vile sikuwa na nguvu ya kujinyanyua. Huwezi kuamini usingizi ulinipitia palepale kwenye matapishi mpaka niliposhtuliwa na wasamalia wema mmoja aliyekuwa akipita njia na kunikuta kwenye hali ile.
“Vipi kaka?” aliniuliza akiwa amesimama pembeni yangu.
“Naumwa,” nilimjibu kwa mkato huku nikijinyanyua kwenye matapishi.
“Unakaa wapi?”
“Pale,” nilisema huku nikionesha ninapokaa ambako hapakuwa mbali.
“Unaweza kusimama?”
Nilijaribu kunyanyuka kidogo nilikuwa na nguvu, yule msamalia mwema alinisaidia mpaka nyumbani. Bahati nzuri mke wangu alikuwa nje aliponiona alishtuka na kuja mbio.
“Jamani mume wangu, umekuwaje?”
“Naumwa,” nilimjibu kwa sauti ya chini.
Walisaidiana kuniingiza ndani na kunilaza sebuleni, baada ya kunifikisha msamalia mwema aliaga.
“Jamani mi niwakimbie.”
“Asante ndugu yangu,” nilimshukuru.
“Hakuna tatizo Mungu atakusaidia.”

“Asante kaka yangu.”

Itaendelea baadae nisawachoshe kwa kusoma sana..............
 
Mke Wangu Alinifanya Niwe Mchawi-11...

ILIPOISHIA:
“Hakuna tatizo Mungu atakusaidia.”
“Asante kaka yangu.”
SASA ENDELEA...


“Hakuta tatizo.”
Yule mtu aliondoka na kuniacha na mke wangu ambaye alionesha kushtushwa na hali yangu.
“Mume wangu vipi?” aliuliza huku akitokwa na machozi.
“Naumwa?” nilimjibu huku moyo wangu ukiniuma mpaka machozi yalinitoka kitu kilichomshtua mke wangu na kuzidisha kilio.
“Maskini mume wangu, unaumwa nini baba Zawadi?”
“Malaria.”
Alinichukua hadi bafuni na kunivua nguo zote kisha alinimwagia maji na kunisaidia kurudi ndani. Alinitengenezea uji haraka na kuninywesha, kila kitendo cha upendo alichonifanyia mke wangu kiliuumiza moyo wangu baada ya kubaini unafiki.
Lakini mke wangu ugonjwa wangu ulimgusa sana, muda wote alikuwa karibu yangu mpaka nilipopitiwa na usingizi. Nilipoamka nilimkuta pembeni yangu mkono shavuni.
“Mume wangu,” aliniita kwa sauti ya upole.
“Naam.”
“Poleee.”
“Asante.”
“Inaendeleaje kwa sasa?”
“Sijambo kidogo.”
“Nikutayarishie chakula gani?”
“Sijisikii kula,” pamoja na huruma yake ya mamba sikuipenda zaidi ya kuona unafiki.
“Mume wangu kumbuka umemeza dawa kali, unatakiwa kula ili dawa zifanye kazi.”
“Nitakula baadaye.”
“Hapana kuna ndizi za nyama nimekuandalia, naomba ule kidogo.”
“Hapana sijisikii kula.”
“Mume wangu.”
“Naam.”
“Mimi nani wako?”
“Mke wangu.”
“Unataka nani akubembeleze ili umsikie?”
“Wewe.”
“Kwa nini hutaki kunisikia?”
“Si nimekueleza nitakula baadaye.”
“Ni wazi huna mapenzi na mimi hata kunisamehe kwako kulikuwa kwa uongo.”
“Jamani mi si naumwa?”
“Kuumwa gani, ni wazi najilazimisha kwako huna mapenzi nami.”
Nilishangaa aliyokuwa akizungumza mke wangu kitu ambacho hakikuwepo zaidi ya mimi kutojisikia kula.
Niliamini kama nitaendelea kukataa naweza kuzalisha mapya, nilikubali kula kitu kilichomfurahisha mke wangu.
Baada ya kula nilijitahidi kulala lakini usingizi uligoma kunichukua, kila nilipofumba macho niliyaona matukio yote yakijirudia toka la mwanangu kuchelewa kutembea na siku niliporudi ghafla na kumkuta mwanangu akiwa katika mazingira mabaya.
Pia nilipomshuhudia mke wangu akiteremka kwenye gari na pia siku aliyorudi siku ya pili na kunidanganya kuwa alikuwa kwenye sherehe ya harusi kumbe alikwenda kulala na mwanaume.
Na la siku ile nililoshuhudia kwa macho yangu akiwa na mwanaume kama walivyozaliwa katika kitanda changu na kuonesha walikuwa wameshafanya uchafu wao.
Pia kusikia katoa mimba kwa kusingizio cha kumlea mtoto wetu Zawadi kumbe haikuwa mimba yangu, ilikuwa ya yule mwanaume aliyempangia nyumba.
Kila yalivyojirudia akilini mwangu, moyo uliniuma sana na kujikuta nalia peke yangu kitandani nikiwa nimejifunika shuka ili mke wangu asijue. Niliwaza kuachana naye lakini moyo ulikataa kwa kuamini sitampata mwanamke mzuri kama yule.
Niliamua kufa kizungu na tai shingoni, niliificha siri ile moyoni mwangu kwa kuamini kama ningeisema basi ningeachana naye kwa mazingira niliyoyaona na mazungumzo niliyosikia. Kufuatia kutopenda kuwepo nyumbani kutokana na kuumia kila nilipomuona mke wangu, niliamua kwenda kazini siku ya tatu japo sikuwa nimepona vizuri.
Baada ya tukio lile, lilizidi kunitesa kila alipokuwa kazini, siku ambayo nilijua mume mwenzangu atakuja nyumbani moyo ulinilipuka kwa kujua muda ule nilikuwa nasalitiwa. Kila nilipokuwa peke yangu nilijikuta nashindwa kufanya kazi na kuhama kimawazo na kuiona dunia nzima nimeibeba kichwani mwangu.
Kutokana na kuwa na wasiwasi wa moyo juu ya vitendo vya mke wangu, hali yangu ilianza kubadilika nilikuwa nikipungua mwili kila kukicha, suruali zangu zote niliongeza matundu ya mkanda matatu kurudi nyuma ili suruali ikae kiunoni. Wa kwanza kunigundua hali ile alikuwa mke wangu ambaye alitaka kujua nina tatizo gani.
“Mume wangu mbona upo hivi, una tatizo gani?”
“Nipo sawa,” nilijibu kwa mkato.
“Hapana mume wangu, kuna kitu kinakusumbua.”
“Mbona mimi nipo sawa.”
“Si kweli, toka ulipougua hujarudi katika hali yako ya kawaida, pia hata ule uchangamfu wa ndani umepotea. Kama bado unaumwa turudi hospitali tujue una tatizo gani?”
“Hapana nipo sawa,” niliendelea kumkatalia mke wangu.
Nilimkatalia kwa kuamini chanzo ni yeye, hata kama ningemwambia ningeongeza msumari wa moto kwenye kidonda kuwa nimemuona akifanya mapenzi na mwanaume mwingine kwenye kitanda changu, lazima angeomba talaka kutokana na kunipa masharti kuwa nikirudi nyumbani nimpigie simu, japo nilimpigia zaidi ya mara kumi bila kupokelewa.

Pia niliyafuatilia maneno yake aliyomhakikishia yule mwanaume kuwa siwezi kurudi nyumbani kwa vile alinieleza nirudi kwangu kwa taarifa. Niliamini kama ningemueleza ningekuwa nimevunja masharti ya kurudi nyumbani bila taarifa japo simu haikupokelewa.
itaendelea baadae .............
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom