Mke wangu alinifanya niwe Mchawi -1

Mke wangu alinifanya niwe Mchawi -1

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Joined
Feb 3, 2009
Posts
43,037
Reaction score
34,742
Katika maisha yangu sikuwahi kuwaza kuua hata nzi kutokana na huruma niliyokuwa nayo.
Watu wengi walipenda kuniita mlokole japo historia yangu yote niliishi maisha ya kutokuwa na dini nikiamini Mungu wa Wakristo ndiye Mungu wa Waislamu kutokana na mafundisho ya dini zote niliyoyafuatilia.

Utashangaa kwa nini niliishi bila kuwa na dini ikiwa wazazi wangu wana dini, tena dini tofauti, baba Muislamu na mama Mkristo. Katika maisha yao hakuna aliyekubali kumfuata mwenzake na kukubaliana, kila mmoja aishi katika imani yake. Hivyo basi, nikawa mtoto wa wazazi wa dini mbili, pamoja na wazazi wangu kuishi kila mmoja na dini yake, waliishi katika upendo wa hali ya juu kwa kila mmoja kuheshimu imani ya mwenzake.


Nilipopata ufahamu nilijikuta nipo njia panda kwa vile sikutaka kumuudhi mmoja wa wazazi wangu kwa kumpendelea mmoja. Halafu kitu cha ajabu nilikuwa mtoto mmoja kama roho, hivyo niliamua kusimama katikati ya wazazi wangu kwa kutochagua dini yoyote. Lakini nilikuwa nafahamu kipi mwanadamu anatakiwa kukifanya ili usimuudhi Mungu.

Katika maisha yangu yote niliamini tofauti ya dini mbili ni ndogo sana lakini anayetakiwa kuabudiwa ni Mungu mmoja. Tokea hapo niliishi nikiwa sina dini na kuishi kama mpagani, tofauti yangu nilikuwa najua Mungu ni mmoja na ndiye anayetakiwa kuabudiwa, lakini sikwenda msikitini wala kanisani na malumbano ya dini hizi mbili mimi yalikuwa hayanihusu.


Wazazi wangu nao walikubaliana na mimi baada ya ushawishi wa kila mmoja kugonga mwamba. Huu ulikuwa muktasari wa maisha yangu ya awali ya kunifanya nisiwe na dini kwa ajili ya mapenzi ya wazazi wangu.

Kutokana na malezi mazuri ya wazazi wangu, niliweza kuishi sehemu yoyote na mtu wa aina yeyote, siku zote heshima na ucheshi ndivyo vilinifanya watu wanipende.


Kama nilivyosema awali, nilikuwa mtu wa huruma na heshima kwa wakubwa na wadogo, lakini mateso ya mapenzi yalinifanya nigeuke niwe na roho mbaya kukiko shetani.


Kuna maelezo niliwahi kusikia wakati nakua kwamba kuna matendo mengine shetani anakimbia akimuona mwanadamu anatenda. Baada ya kuteswa sana na mapenzi ilifikia hatua kutoa roho ya mtu kwangu ilikuwa kitu cha kawaida hata kwa kosa dogo la kuombana msamaha kwa kuamini hakuna kiumbe kibaya duniani kama mwanadamu ambaye hatakiwi kupewa nafasi kwa vile kama ukimchekea basi atakuumiza wewe.

Mkasa wangu unaanzia pale nilipotimiza miaka 21, nilitoka kwa wazazi wangu na kusafiri nje ya mkoa kwenda kufanya kazi baada ya rafiki yangu kupata kazi ya ujenzi.

Hivyo, hakutaka kuondoka peke yake, alinichukua na mimi huku wazazi wangu wakiniasa niishi na watu kwa heshima na taadhima. Nami niliwaahidi wazazi wangu kuwa nitaishi kama walivyonielekeza.

Nilitengana na wazazi wangu kwa mara ya kwanza toka nitoke tumboni kwa mama wangu. Nilifika mkoani na kufikia kwa ndugu wa rafiki yangu. Kwa vile tulifika Jumamosi jioni sana, tulilala na kesho yake tulipumzika na kupata nafasi ya kupelekwa sehemu ya kazi.


Ulikuwa mradi mkubwa sana ambao tuliambiwa utachukua miaka mitano kwisha, siku ile tulipumzika na kesho yake tulikwenda kuanza kazi. Siku ya pili tuliamka asubuhi na mapema na kwenda eneo la ofisi ambapo ndipo mnapangiwa kazi. Ilikuwa kuna tofauti kubwa na vijana wengi tuliowakuta nje ya geti wakisubiri kuitwa, lakini sisi tulikuwa na mwenyeji, mjomba wa rafiki yangu ambaye alikuwa ndiye msimamizi mkuu wa mradi ule ambao ulikuwa chini ya Wataliano, tuliingia bila kuitwa.

Basi huo ndiyo ukawa mwanzo wa kuanza maisha ya kujitegemea, tulianza kwa kulipwa kwa kutwa kama wenzetu kwa wiki mbili, baada ya hapo tulichaguliwa vijana kama ishirini tuliopewa mkataba na kulipwa kwa mwezi na posho yetu kuongezeka tofauti na wenzetu waliokuwa wakilipatwa kwa kutwa.

Maisha yalikwenda vizuri huku mimi na mwenzangu tukihama kwa ndugu zake na kupanga chumba kimoja na kukaa wawili. Wazazi wangu nao walikula jasho langu kila mwezi kwani niliwatumia robo ya mshahara wangu nao walizidi kuniombea kwa Mungu ili niendelee kupata zaidi.


Siku zilikatika huku nami nikipevuka kiakili na mawazo kufikia hatua ya kuhitaji mwenza. Nyumba tuliyokuwa tumepanga kulikuwa na binti mmoja ambaye Mwenyezi Mungu alimjalia umbile dogo lakini nzuri na sura jamili (nzuri). Binti yule alitokea kunipenda sana kiasi cha kumueleza mama yake angependa aolewe na mimi.

Moja ya njia ya kuonesha ananipenda aliniomba mambo yote ya kike ayafanye yeye kama vile kunipikia chakula cha jioni baada ya kazi, kufua nguo na kusafisha chumba lakini sikumpa nafasi ile kwa kuhofia wazazi wake.

Pamoja na mimi kumpenda sana bado sikumkubalia kutokana na kuwaheshimu sana wazazi wake ambao siku zote walinilea kama mtoto wao.

Siku moja usiku baada ya kutoka kazini, mama mwenye nyumba ambaye ni mama mzazi wa yule binti aliniita kwa kumtumia yule binti. Nami niliitikia wito ule, baada ya kuingia sebuleni kwao, nilikaribisha kwenye kochi lililokuwa karibu na alipokaa mama mwenye nyumba.

Itaendelea baadae kidogo......
 
Mke Wangu Alinifanya Niwe Mchawi-2.........

ILIPOISHIA;

Siku moja majira ya usiku baada ya kutoka kazini mama mwenye nyumba ambaye ni mama mzazi wa yule binti aliniita kwa kunmtumia yule binti. Nami niliitikia wito ule, baada ya kuingia sebuleni nilikaribisha kwenye kochi lililokuwa karibu na alipokaa mama mwenye nyumba.
SASA ENDELEA...

“Kazala,” mama aliita kwa sauti ya chini.
“Naam mama,” niliitikia kwa unyenyekevu mkubwa.
“Nimekuita mwanangu nikueleze jambo moja la muhimu sana.”
“Sawa mama.”
“Kwanza wewe dini gani?”
“Sina dini,” nilimjibu kwa mkato.
“Muongo, hebu niambie ukweli wewe ni dini gani?”
“Kweli mama sina dini.”
“Sasa kama ukipata mwanamke mwenye dini utafanya nini?”
“Sitafanya chochote nitaiheshimu dini yake, lakini mi nitabakia sina dini?”
“Kwa nini?”

Sikumficha nilimuelezea maisha ya wazazi wangu na kitu gani kilichonifanya nisiwe na dini.
“Lakini hata kiserikali mtu anapotimiza miaka kumi na nane ana haki ya kuamua chochote bila kuingiliwa, hivyo ulikuwa na nafasi ya kuchagua dini yoyote ya baba au ya mama.”
“Ni kweli, lakini bado kwa mimi sikutakiwa kufanya hivyo.”
“Kwa nini?”

“Nimesimama kati ya baba na mama yangu wote nawapenda na sitaki kumuudhi mmoja kati yao.”
“Sasa mwanangu kuna kitu nimekuitia, mdogo wako Suzana anakupenda sana tena sana kapitiliza kukupenda. Siku zote amekuwa akikuonesha kwa vitendo imeonekana kama umuelewi. Mpaka kuja kunieleza mimi mama yake basi ujue yamemfika shingoni. Kutokana na tabia yako ambayo imekuwa
tofauti na wavulana wengi nimeamini unafaa kuwa mkwe wangu.

“Nakuomba uwe mkwe wangu muoe Suzy kwa kweli ni mwanamke mzuri ambaye atajivunia katika maisha yako. Najua utashtuka mama kumpigia debe mwanaye lakini kwa hili sikuwa na jinsi.”
“Nimekusikia mzazi wangu naomba unipe muda ili nami niwasiliane na wazazi wangu.”
“Kuwasiliana na wazazi wako si vibaya, lakini kwanza ni wewe kukubaliana na mwenzako.”
“Mimi nimekubali.”

“Nashukuru kwa majibu yako mazuri, basi nakuruhusu, uwasiliane na wazazi wako, usihofu gharama nitakusimamiane mpaka mwisho wa harusi yenu.”
“Nashukuru mzazi wangu.”

Baada ya kutoka kwa mama mwenye nyumba nilirudi chumbani kujipumzisha, haikupita muda mlango iligongwa alikuwa Suzy.
“Karibu,” nilikabiribisha bila kunyanyuka kitandani.
Alisukuma mlango na kuingia ndani akiwa na sinia lililofunikwa kawa.
“Karibu chakula Kazala.”

Sikutaka kubisha lakini nilitaka tule pamoja Suzy hakukataa tulikuwa pamoja. Tokea siku ule Suzy akawa na uhuru wa kuja kwangu lakini sikuwa na tamaa ya mwili kwa kujiapia mpaka nimuoe kabisa. Mipango ilienda vizuri na Suzy akawa mke wangu ndoa ilifungwa kwa mkuu wa wilaya kila mtu akiwa na imani yake.

Namshukuru Mungu maisha yalikuwa mazuri kwa mke wangu kuonesha mapenzi ya kweli nami pia nilimpenda mapenzi ya dhati. Miezi sita baada ya kuoana tulihama nyumba ya wazazi wa mke wangu na kwenda kukaa kwenye nyumba nyingine ya familia yao iliyokuwepo umbali kidogo toka kwetu, wakati huo mke wangu alikuwa na ujauzito wa miezi minne.

Nyumba tuliyohamia ilikuwa na wapangaji wawili na sisi tulikuwa sehemu ya nyumba mbele iliyokuwa ya kifamilia. Kazi nayo iliendelea vizuri kila siku kuondoka asubuhi na kurudi usiku. Maisha yalisoga muda ulipofika mke wangu alijifungua mtoto wa kike.

Mwenetu alikuwa vizuri mpaka alipofikisha mwaka mmoja na miezi saba nilipatwa na mshtuko kushindwa kutembeza zaidi ya kukaa na kujibuta kwa ------. Katika maisha yangu pamoja ya kutokuwa na dini bado sikuuamini uchawi hata kidogo japo niliusikia kuwa upo. Hali ya mwanangu ya kutotembea ilinishtua sana. Katika kuulizia kwa watu waliomuona mtoto wangu walisema mtoto wangu inawezekana amebemendwa.

Kauli ile ilinishtua sana baada ya kuelezwa maana ya kubemenda ni mtu kutoka nje ya ndoa, kwa upande wangu sikuwa na shaka kwa vile sikuwa na mpenzi mwingine zaidi ya mke wangu mama Zawadi. Pia kwa upande wa mke wangu hata kwa mtutu nisingekubali kutoka nje ya ndoa kwani nilimuamini sana.

Itaendelea baadae............
 
kumbe unazitoa kwa shigongo!! leo nimekukamata mkuu!! hadithi hii ninayo kwenye gazeti la Risasi!! ha! ha! haaaaa!!
 
kumbe unazitoa kwa
shigongo!! leo nimekukamata mkuu!! hadithi hii ninayo kwenye gazeti la
Risasi!! ha! ha! haaaaa!!

Usipige kelele,Mzizi Mkavu anaumwa na ataendelea na utunzi J'piliiii!
 
Mke Wangu Alinifanya Niwe Mchawi-3


ILIPOISHIA:Kauli ile ilinishtua sana baada ya kuelezwa maana ya kubemenda ni mtu kutoka nje ya ndoa, kwa upande wangu sikuwa na shaka kwa vile sikuwa na mpenzi mwingine zaidi ya mke wangu mama Zawadi. Pia kwa upande wa mke wangu hata kwa mtutu nisingekubali kutoka nje ya ndoa kwani nilimuamini sana.

SASA ENDELEA...


Nikawa njia panda kuelewa hali iliyomkuta mwanangu kama inatokana na mtu kutoka nje ya ndoa basi walikuwa wamekosea nikiamini huenda tatizo alilonalo mwanangu huenda linafanana na hilo.
Jumapili moja niliyokuwa nyumbani, nilitoka na mwanangu ambaye nilimpenda sana pamoja na kuchelewa kutembea. Nikiwa natoka dukani nilikutana na mama mmoja wa makamo na kusalimiana naye. Nilipishana naye lakini sikupiga hatua mbili aliniita.
“Baba Zawadi.”
“Naam mama,” niliitika huku nikigeuka kumsikiliza.
“Samahani mwanangu.”
“Bila samahani mama.”
“Basi naomba tusogee pembeni tuzungumze.”
“Hakuna tatizo mama yangu.”

Nilisogea pembeni kidogo ya barabara na kusimama kwenye uchochoro wa kutokea mtaa wa pili.
“Naam mama,” nilianzisha mazungumzo.

“Mwanangu nimekuita ili tuzungumze kitu kimoja, nina imani hukijui kinachofanyika nyuma kwa vile unatoka asubuhi na kurudi usiku kinachotendeka mchana hukijui.”
“Ni kweli mama.”
“Unamuonaje mjukuu wangu Zawadi?”
“Kwa kweli mama hata mimi nashindwa kuelewa.”
“Unashindwa kuelewa nini ikiwa mwanao mnamtesa bila kosa.”
“Mama tunamtesa kivipi?”

“Unaona hii miguu ya mwanao ipo sawa?” aliniuliza huku akiishika miguu ya mwanangu iliyokuwa haina nguvu.
“Haipo sawa, kwa kweli nachanganyikiwa hata sijui sababu ni nini japo watu wananiambia kitu ambacho naamini si kweli.”
“Kitu gani hicho?”

“Achana nacho hakina umuhimu,” sikutaka kumuambia habari ambazo mimi niliona ni za kizushi.
“Kitu gani?”
“Utayaweza maneno ya watu mama, kila kukicha hawakosi ya kusema.”
“Maneno gani?” yule mama alikazania swali lake.
“Achana nayo hayana umuhimu.”
“Inawezekana uliyoambiwa ndiyo nitakayokueleza leo.”
“Nina imani si hayo.”

“Haya, tuachane na hayo, unajua matatizo ya mtoto kuchelewa kutembea yanatokana na nini?”
“Kwa kweli sijui.”
“Yapo mambo mengi, moja kuchezewa na walimwengu na lingine ni kubemendwa.”
“Kwa hiyo tatizo la mwanangu linatokana na nini?”

“Mkeo atamuua mtoto huyu, kwa nini unakuwa na moyo wa kikatili kiasi hiki, kama hawezi kumlea basi mumpeleke kwa bibi yake kuliko kumtesa bila sababu.”
“Mama sijakuelewa, mke wangu amemfanya nini mtoto?”
“Anambemenda.”
“Eti?”
“Anambembenda na mwisho wake atamuua.”
“Mmh! Una maana gani?”

“Mkeo si muaminifu, wote mtaani wanajua, ukitoka na yeye nyuma anatoka anarudi muda umekaribia kurudi.”
“Sasa mama kutoka kwa mke wangu inaingiliana vipi na mwanangu kuchelewa kutembea?”

“Baba jasho la janaba ni baya kwa mtoto hasa ikiwa mliyekutana si wazazi wa mtoto, mmoja wenu akikosa uaminifu na akamshika na uchafu wake lazima mtoto atadhurika.”
“Sasa mama mke wangu mbona muaminifu?” kauli ile ilinishtua.

“Baba acha kusema hivyo, sisi ndiyo tunayejua, isingekuwa huyu mtoto wala nisingenyanyua mdomo wangu, ningekuacha ili siku moja ujionee mwenyewe uchafu wa mkeo.”

“Kwa hiyo chanzo cha matatizo ya mtoto ni mke wangu?” nilijikuta nikikosa amani moyoni.

“Baba usiandikie mate, kwa vile mkeo hata aibu hana, siku moja rudi nyumbani mchana utajionea mwenyewe. Kabla ya kufanya lolote fanyia kazi haya niliyokueleza. Ukipata majibu ndiyo utajua mkeo muaminifu au siyo, utapata kiini cha matatizo ya mkeo.

“Ila nakuomba kabla ya yote mtoto wako mpeleke kwa bibi yake kisha fanya uchunguzi wako.”
“Asante mama kwa maelezo yako.”

“Ila nakuomba ukienda kwako usioneshe mabadiliko yoyote, kuanzia Jumatatu siku yoyote rudi nyumbani ghafla mchana utaniambia niliyokueleza ni kweli na maendeleo ya mwanao utayaona kwa muda mfupi akiwa mbali na mama yake.”
“Asante mama.”

Niliagana na yule mama ambaye alikuwa mtu wa heshima na nilimuheshimu sana pale mtaani. Nikiwa narudi, njia nzima nilikuwa na mawazo mazito juu ya maneno niliyoelezwa na sababu ya matatizo yanayomfanya mwanangu ashindwe kutembea.

Kingine ambacho sikutaka kukikubali mara moja ni kuhusu kutoka kwa mke wangu nje ya ndoa. Kwa kweli sikuamini mke wangu kama angeweza kutoka nje ya ndoa hasa kutokana na ukimya pia kuonesha mapenzi mazito kwangu.

Itaendelea baadae .......................
 
Mke wangu alinifanya niwe mchawi-4...

ILIPOISHIA;

Kingine ambacho sikutaka kukikubali mara moja ni kuambiwa kuwa mke wangu huwa anatoka nje ya ndoa.
Kwa kweli sikuamini kama mke wangu angeweza kufanya hivyo, kutokana na ukimya wake na jinsi anavyoonesha mapenzi mazito kwangu.
SASA ENDELEA...


Nilifikiria kama ni kweli mke wangu ndiye chanzo cha matatizo ya mtoto, ina maana hajui au anafanya makusudi. Nilipofika nyumbani nilijitahidi kuficha mabadiliko mke wangu alinichangamkia huku akimchukua mtoto ambaye siku zote alimuonesha mapenzi makubwa.
Siku hiyo nilikuwa nyumbani kimwili lakini kiakili nilikuwa mbali sana, kwa kuwa nilikuwa nikiwaza yote niliyoelezwa na wote walioguswa na hali ya mwanangu kuchelewa kutembea kiasi cha watu kumtania kwa kumwita fundi majiko.

Japokuwa mwanangu alikuwa hatembei lakini alikuwa akiongea maneno yote akiwa amekaa kama fundi anayetengeneza majiko.

Kila nilipomuangalia mke wangu sikummaliza, nilivyomuamini na maneno yale nilichanganyikiwa huku upande mwingine nikiona kama maneno yale yalikuwa ni njama za kutaka kuivunja ndoa yangu.

Mke wangu alikuwa mpole na wala hakuwa muongeaji kabisa, muda wote alikuwa kimya mpaka miye nianze kumsemesha.
Niliificha siri ile moyoni mwangu japokuwa kuna wakati moyo ulikubali na wakati mwingine ulikataa kuamini kile kilichokuwa kikisemwa.
Siku ya pili ilikuwani ni Jumatatu nilitakiwa kwenda kazini nilipanga kurudi mchana ili nishuhudie kile kinachosemwa kama ni kweli au la.

Siku ya siku nilipofika kazini, nilisingizia kuumwa kwa vile sikuwahi kuomba ruhusa kutokana matatizo yoyote nilikubaliwa na kurudi nyumbani saa sita kasorobo mchana.

Nilipofika nilikuta mlango ukiwa umefungwa, nilipiga simu ya mke wangu lakini haikuwa hewani. Nilizunguka upande wa pili nilimkuta mtoto wangu Zawadi akichezea matope bila kuwa na mtu yeyote wa kumwangalia.

Nilibisha hodi chumba cha jirani, alitoka jirani yangu ilhali akiwa amepatwa na mshtuko mkubwa sana kwa kuniona muda ule.

“Ha! Shemeji leo umerudi mchana?” alisema huku akimtoa Zawadi kwenye matope na dalili zote zikionesha kwamba kwa kipindi cha mchana, mtoto yule huwa anaachwa peke yake na tayari alikwisha kula kiasi kikubwa cha matope kutokana na mdomo ulivyoonesha.

“Sijisikii vizuri,” nilimjibu kwa sauti ya chini huku roho ikiniuma kwa malezi mabaya aliyokuwa akipewa mwanangu.
Hali ile ilianza kunipa picha ya maneno niliyoelezwa, jirani yangu mama Sonono alianza kumsafisha matope kisha aliingia ndani kwake na kutoka na ufunguo na kunipa huku akisema:
“Shem naomba unitolee na nguo za Zawadi.”
“Hakuna tatizo.”

Niliingia ndani huku nikijiuliza mke wangu atakuwa amekwenda wapi, pia kama nisingekuja mwanangu angekula matope na kuwa mchafu mpaka saa ngapi. Baada ya kumtolea nguo nilimuuliza:
“Mama Zawadi ameenda wapi?”
“Amesema ameitwa na mama yake.”

“Kila siku huwa anaitwa na mama yake?” Nilimshtukiza kwa swali ambalo nilijua hakulitegemea.
“Siku nyingine huwa sijui anaenda wapi.”
“Kwa hiyo akiondoka wewe ndiye unakuwa mlezi wake au siyo?”
“Kwani vipi shem?”

“Nakuuliza wewe ndiye mlezi wake, hebu angalia nimemkuta mtoto anakula matope, kwa siku zote anazoondoka kazi yako ni kumlisha mwanangu matope?” Nilimuuliza kwa hasira.

“Ha...ha...pana shem.”
“Niambie ukweli mke wangu amekwenda wapi maana nimetoka kwao?”
“Si...si...jui akiondoka huniachia mtoto.”
“Huwa anarudi saa ngapi?”
“Jioni kabla hujarudi.”
“Asante.”

Nilimchukua mwanangu na kumpeleka kwa mama mzazi wa mke wangu na kumuuliza kama mke wangu alifika pale nyumbani kwake.
Majibu yalikuwa ni tofauti na nilivyoelezwa, nilimuomba nimuachie mtoto. Alikubali kitu cha ajabu hakuniuliza swali lolote zaidi ya kumchukua mtoto.
Nilirudi nyumbani kumsubiri mke wangu aniambie alikokuwa amekwenda.

Nini kiliendelea? Usikose kusoma baadae
 
Leta story nakesha na wewe mpaka asubuhi nipate somo la wanawake wapole kumbe
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom