Bishop Hiluka
R I P
- Aug 12, 2011
- 7,150
- 14,724
- Thread starter
- #41
HADI LINI! 25
Na Bishop Hiluka
“Hivi jema kwako ni lipi, tuendelee kugombana na hatimaye tuachane ili watoto wetu wateseke au tusameheane na tuanze ukurasa mpya?” Ibrahim alimuuliza Pamela huku akionesha mshangao mkubwa.
“Ukurasa mpya kauanze na mwanamke mpya, na mimi niache nianze ukurasa mpya kivyangu.” Pamela alisema na kumfanya Ibrahim ashtuke sana.
“Kama umekusudia kuachwa hapa sahau, mimi najua kuoa tu sijui kuacha,” Ibrahim aling’aka kwa hasira.
“Na ulipotaka kuniacha hukujua kama hujui kuacha? Naona unajitekenya na kucheka mwenyewe! Nasema hivi, leo bila talaka yangu humu ndani hakukaliki wala hakulaliki,” Pamela alisema kwa ukali huku akimkazia macho Ibrahim.
“Hivi uko yakini Pamela?” Ibrahim alimuuliza Pamela kwa mshangao.
“Niko yakini kabisa, nafahamu ninachokisema!” Pamela alijibu huku akiendelea kumtulizia macho Ibrahim.
Ibrahim akazidi kuchanganyikiwa, alimtazama Pamela kwa kitambo kirefu na kushusha pumzi, kisha akatingisha kichwa chake kwa masikitiko na kuondoka, akaelekea kwenye mlango, akaufungua na kutoka nje kimya kimya huku akiufunga ule mlango nyuma yake.
Pamela alimtazama kwa mshangao wakati akiondoka na kushusha pumzi, kisha akaketi pale kwenye kiti cha kupumzikia pale kwenye balcony. Baada ya muda mfupi alisikia hodi inabishwa mlangoni, akainuka na kwenda kufungua mlango na kuchungulia nje, akamuona Mama Bigirimana akiwa amesimama pale mlangoni akiwa na sura iliyosawajika kidogo.
“Mama yangu, kulikoni! Mbona tumepata taarifa za kutatanisha?” Mama Bigirimana alimuuliza Pamela huku akiwa bado katika sura iliyosawajika.
“Habari zipi za kutatanisha, mama?”
“Tumeambiwa eti hutaki kumsamehe mumeo ila unachodai ni talaka tu?”
Pamela akaachia mguno ulioambatana na tabasamu, alipotaka kusema neno Mama Bigirimana akamkatiza.
“Kama hutajali wazazi wako wanakuhitaji mara moja huko sebuleni. Najua hivi sasa ni usiku wa manane na ungependa kupumzika lakini nia yetu ni njema tu, mama yangu,” Mama Bigirimana alisema huku akishusha pumzi.
“wala usijali mama, nakuja sasa hivi,” Pamela alisema na kurudi chumbani huku akiufunga mlango nyuma yake.
Mama Bigirimana aliutazama ule mlango kwa wasiwasi kisha akazifuata ngazi na kuanza kushuka akielekea sebuleni. Pale sebuleni kimya kizito kilikuwa kimetawala, watu walikuwa wameketi wakiwa wametahayari huku kila mmoja akiwaza lake na wakionekana kusubiri kwa hamu kusikia kilichokuwa kinaendelea. Ibrahim alikuwa ameketi akiwa kajiinamia kwa huzuni.
Mama Bigirimana alifika pale sebuleni peke yake bila Pamela huku akiwa anatembea taratibu na kuwafanya wote wageuze shingo zao kumtazama kwa wasiwasi.
“Anakuja!” Mama Bigirimana alisema huku akiketi juu ya kochi baada ya kuona macho yote yalikuwa yanamtazama kwa wasiwasi.
Haikuchukua muda Pamela akafika pale sebuleni na kusimama akiwatazama wale wazee kwa mashaka kidogo. Mama Bigirimana alisogea na kuacha nafasi kidogo huku akimuashiria Pamela aketi jirani yake. Pamela alikwenda kuketi pale na kubaki kimya akiwatazama wale wazee kwa wasiwasi.
Kisha macho yake yakatua kwa Ibrahim ambaye alikuwa ameinamisha uso wake kutazama chini, hofu ikaanza kumtambaa Pamela mwilini mwake. Kitambo kifupi cha ukimya kikazuka pale sebuleni huku wale wazee wakitazamana kwa makini, kisha Mzee Tugiramahoro akakohoa kidogo kurekebisha sauti yake.
“Haya mama, hebu tuambie, kulikoni! Mbona tumepata taarifa za kutatanisha?”
Pamela alimtazama baba yake kwa makini kisha macho yake yakahama na kuwatazama wale wazee wengine, na mwisho akamalizia kwa Ibrahim na kushusha pumzi.
“Ndiyo baba, nadai talaka, ni Ibrahim ndiye anayeleta utatanishi kwa kutotoa talaka!” Pamela alisema na kuwafanya wale wazee wamwangalie kwa mshangao mkubwa.
Mzee Tugiramahoro alionekana kukerwa mno na ile kauli, hasira iliyochanganyika na mshangao mkubwa ikaibuka ndani yake.
“Hivi u mzima kweli wewe, au una wazimu?” Mzee Tugiramahoro alimuuliza Pamela kwa sauti kali.
“Mungu apishe mbali, sina wazimu, sikupagawa, sikurogwa na wala sina kichaa. Najua ninachokifanya baba! Nisaidieni kumwambia Ibrahim kuwa nataka talaka yangu sasa hivi!” Pamela alisisitiza huku akionekana kujiamini.
Mzee Tugiramahoro alitaka kusema lakini akasita na kugeuza shingo yake kumtazama mkewe kisha akainua mabega yake juu na kuyashusha akionekana kuchanganyikiwa huku akiwa hana la kufanya.
Wazee wote walionekana kuchanganyikiwa, walimtazama Pamela wakiwa hawaelewi ni kipi kilichomfanya awaite, maana mwanzoni walidhani alikuwa amewaita pale kuja kutatua mgogoro wa ndoa yao lakini sasa alionesha kuwa alitaka wamsaidie kudai talaka! Mama Bigirimana alimwangalia Pamela kwa huzuni.
“Mama, ni sababi zipi hasa zimekufanya utake mumeo akutaliki?” Mama Bigirimana alimuuliza Pamela kwa sauti tulivu.
Pamela alimtazama yule mama huku aking’atang’ata midomo yake na kufikicha ncha ya nguo aliyokuwa amejitanda kichwani.
“Ni kwa sababu nampenda sana na ninathamini maendeleo yake… mama!” Pamela alijibu huku akiiangalia ile ncha ya nguo na kuwafanya watu wote wamwangalie kwa mshangao.
Wale wazee waliendelea kumwangalia Pamela kwa muda kisha wakaangaliana wenyewe kwa wenyewe. Ibrahim aliduwaa na kubaki akimwangalia Pamela kwa mshangao zaidi.
“Sasa, kama unampenda sana na unathamini maendeleo yake mbona unataka akuache?” Mama Bigirimana alimuuliza Pamela huku mshangao ukiwa haujamtoka usoni kwake.
Pamela alinyanyua uso wake na kuwaangalia kwa makini wale wazee, hasa Mzee Tugiramahoro na Mzee Bigirimana. Akaonekana kusita na kumeza mate huku akimtupia jicho Ibrahim. Muda ule Ibrahim alionekana kuchanganyikiwa zaidi, jasho lilikuwa linamtoka.
“Kwa sababu sioni sababu kwa nini tumlazimishe kuishi na mtu aliyepanga kumtaliki badala ya kuheshimu maamuzi yake, mbona yeye haulizwi kwa nini alitaka kuniacha na kuoa mwanamke mwingine na kwa nini sasa hivi ananiona nafaa?”
Kauli ile ikafanya pazuke tena ukimya, wale wazee wote wakabaki kimya wakimtazama Pamela kwa makini. Mama Bigirimana akashusha pumzi ndefu huku akibetua kichwa chake akionekana kumwelewa Pamela na kuafikia naye.
“Hilo nalo neno! Mimi nipo upande wako mama, wanaume wanapaswa watambue kuwa mwanamke si mtumwa, tena wewe umekuwa muungwana sana, mwanzo alipokuja hapa alisema yake lakini sasa hayasemi… kwa nini tumuonee haya mtu asiyetuonea haya?”
Ibrahim aliwaangalia wale wazee huku akionekana kugwaya sana. Aliinamisha uso wake akiwa hana la kusema, machozi yalianza kumlengalenga. Pamela alimtazama Ibrahim kwa makini huku akijitahidi kuyazuia machozi ambayo yalianza kumtoka.
“Baba Samantha, nakupenda sana, kwa nini nisikuache huru ukaishi na mwanamke unayempenda. Ulipanga kuniacha ili uoe mwanamke anayekufaa na sasa unaniomba msamaha kwa kuwa wazee wamekulazimisha kufanya hivyo, sijui hapa pendo liko wapi? Hivi utalazimishwaje kuishi na mwanamke uliyemchoka eti kwa kuwa wazee wamekulazimisha? Ndiyo maana nataka unitaliki ili uwe huru kutafuta pendo la kweli…” Pamela alimwambia Ibrahim kwa sauti tulivu.
“Mwambie mama, mwambie mpumbavu huyu,” Mama Bigirimana alidakia na kuwafanya watu wengine wageuke kumwangalia kwa mshangao.
Sasa machozi mengi yalikuwa yanamtoka Ibrahim, alitaka kusema neno lakini akashindwa kuwa kuwa maneno yalikuwa hayatoki, akaanza kulia kilio cha kwikwi. Muda ule ule aliinuka, akamfuata Pamela na kuanguka miguuni kwake kisha akaishika miguu yake huku akiendelea kulia kwa uchungu.
Pamela alimtazama Ibrahim kwa huzuni, akajitahidi kuyazuia machozi yake. Mzee Tugiramahoro aliinuka na kumfuata Ibrahim, akamshika mabega na kumnyanyua kutoka pale alipokuwa amelala, kisha akampa ishara Mama Bigirimana akimtaka ainuke na kumpisha Ibrahim.
Mama Bigirimana alitii na kupisha, Mzee Tugiramahoro akamkalisha Ibrahim kando ya Pamela na kunyanyua kiganja cha mkono wa Pamela kisha akakikutanisha na kiganja cha mkono wa Ibrahim.
“Pamela, mumeo amejua makosa yake na sasa anataka muanze upya, sioni kwa nini usimsamehe…” Mzee Tugiramahoro alisema na kuwatazama wazee wengine.
“Na ikiwa mimi ni mzazi wenu, basi kwa niaba ya wazazi wenzangu wote naiombea kwa Mungu ndoa yenu idumu zaidi na zaidi, isiwe na migogoro tena wala visasi,” Mzee Tugiramahoro alisema na watu wote pale sebuleni wakaitikia, “Amina!”
MWISHO.
Na Bishop Hiluka
“Hivi jema kwako ni lipi, tuendelee kugombana na hatimaye tuachane ili watoto wetu wateseke au tusameheane na tuanze ukurasa mpya?” Ibrahim alimuuliza Pamela huku akionesha mshangao mkubwa.
“Ukurasa mpya kauanze na mwanamke mpya, na mimi niache nianze ukurasa mpya kivyangu.” Pamela alisema na kumfanya Ibrahim ashtuke sana.
“Kama umekusudia kuachwa hapa sahau, mimi najua kuoa tu sijui kuacha,” Ibrahim aling’aka kwa hasira.
“Na ulipotaka kuniacha hukujua kama hujui kuacha? Naona unajitekenya na kucheka mwenyewe! Nasema hivi, leo bila talaka yangu humu ndani hakukaliki wala hakulaliki,” Pamela alisema kwa ukali huku akimkazia macho Ibrahim.
“Hivi uko yakini Pamela?” Ibrahim alimuuliza Pamela kwa mshangao.
“Niko yakini kabisa, nafahamu ninachokisema!” Pamela alijibu huku akiendelea kumtulizia macho Ibrahim.
Ibrahim akazidi kuchanganyikiwa, alimtazama Pamela kwa kitambo kirefu na kushusha pumzi, kisha akatingisha kichwa chake kwa masikitiko na kuondoka, akaelekea kwenye mlango, akaufungua na kutoka nje kimya kimya huku akiufunga ule mlango nyuma yake.
Pamela alimtazama kwa mshangao wakati akiondoka na kushusha pumzi, kisha akaketi pale kwenye kiti cha kupumzikia pale kwenye balcony. Baada ya muda mfupi alisikia hodi inabishwa mlangoni, akainuka na kwenda kufungua mlango na kuchungulia nje, akamuona Mama Bigirimana akiwa amesimama pale mlangoni akiwa na sura iliyosawajika kidogo.
“Mama yangu, kulikoni! Mbona tumepata taarifa za kutatanisha?” Mama Bigirimana alimuuliza Pamela huku akiwa bado katika sura iliyosawajika.
“Habari zipi za kutatanisha, mama?”
“Tumeambiwa eti hutaki kumsamehe mumeo ila unachodai ni talaka tu?”
Pamela akaachia mguno ulioambatana na tabasamu, alipotaka kusema neno Mama Bigirimana akamkatiza.
“Kama hutajali wazazi wako wanakuhitaji mara moja huko sebuleni. Najua hivi sasa ni usiku wa manane na ungependa kupumzika lakini nia yetu ni njema tu, mama yangu,” Mama Bigirimana alisema huku akishusha pumzi.
“wala usijali mama, nakuja sasa hivi,” Pamela alisema na kurudi chumbani huku akiufunga mlango nyuma yake.
Mama Bigirimana aliutazama ule mlango kwa wasiwasi kisha akazifuata ngazi na kuanza kushuka akielekea sebuleni. Pale sebuleni kimya kizito kilikuwa kimetawala, watu walikuwa wameketi wakiwa wametahayari huku kila mmoja akiwaza lake na wakionekana kusubiri kwa hamu kusikia kilichokuwa kinaendelea. Ibrahim alikuwa ameketi akiwa kajiinamia kwa huzuni.
Mama Bigirimana alifika pale sebuleni peke yake bila Pamela huku akiwa anatembea taratibu na kuwafanya wote wageuze shingo zao kumtazama kwa wasiwasi.
“Anakuja!” Mama Bigirimana alisema huku akiketi juu ya kochi baada ya kuona macho yote yalikuwa yanamtazama kwa wasiwasi.
Haikuchukua muda Pamela akafika pale sebuleni na kusimama akiwatazama wale wazee kwa mashaka kidogo. Mama Bigirimana alisogea na kuacha nafasi kidogo huku akimuashiria Pamela aketi jirani yake. Pamela alikwenda kuketi pale na kubaki kimya akiwatazama wale wazee kwa wasiwasi.
Kisha macho yake yakatua kwa Ibrahim ambaye alikuwa ameinamisha uso wake kutazama chini, hofu ikaanza kumtambaa Pamela mwilini mwake. Kitambo kifupi cha ukimya kikazuka pale sebuleni huku wale wazee wakitazamana kwa makini, kisha Mzee Tugiramahoro akakohoa kidogo kurekebisha sauti yake.
“Haya mama, hebu tuambie, kulikoni! Mbona tumepata taarifa za kutatanisha?”
Pamela alimtazama baba yake kwa makini kisha macho yake yakahama na kuwatazama wale wazee wengine, na mwisho akamalizia kwa Ibrahim na kushusha pumzi.
“Ndiyo baba, nadai talaka, ni Ibrahim ndiye anayeleta utatanishi kwa kutotoa talaka!” Pamela alisema na kuwafanya wale wazee wamwangalie kwa mshangao mkubwa.
Mzee Tugiramahoro alionekana kukerwa mno na ile kauli, hasira iliyochanganyika na mshangao mkubwa ikaibuka ndani yake.
“Hivi u mzima kweli wewe, au una wazimu?” Mzee Tugiramahoro alimuuliza Pamela kwa sauti kali.
“Mungu apishe mbali, sina wazimu, sikupagawa, sikurogwa na wala sina kichaa. Najua ninachokifanya baba! Nisaidieni kumwambia Ibrahim kuwa nataka talaka yangu sasa hivi!” Pamela alisisitiza huku akionekana kujiamini.
Mzee Tugiramahoro alitaka kusema lakini akasita na kugeuza shingo yake kumtazama mkewe kisha akainua mabega yake juu na kuyashusha akionekana kuchanganyikiwa huku akiwa hana la kufanya.
Wazee wote walionekana kuchanganyikiwa, walimtazama Pamela wakiwa hawaelewi ni kipi kilichomfanya awaite, maana mwanzoni walidhani alikuwa amewaita pale kuja kutatua mgogoro wa ndoa yao lakini sasa alionesha kuwa alitaka wamsaidie kudai talaka! Mama Bigirimana alimwangalia Pamela kwa huzuni.
“Mama, ni sababi zipi hasa zimekufanya utake mumeo akutaliki?” Mama Bigirimana alimuuliza Pamela kwa sauti tulivu.
Pamela alimtazama yule mama huku aking’atang’ata midomo yake na kufikicha ncha ya nguo aliyokuwa amejitanda kichwani.
“Ni kwa sababu nampenda sana na ninathamini maendeleo yake… mama!” Pamela alijibu huku akiiangalia ile ncha ya nguo na kuwafanya watu wote wamwangalie kwa mshangao.
Wale wazee waliendelea kumwangalia Pamela kwa muda kisha wakaangaliana wenyewe kwa wenyewe. Ibrahim aliduwaa na kubaki akimwangalia Pamela kwa mshangao zaidi.
“Sasa, kama unampenda sana na unathamini maendeleo yake mbona unataka akuache?” Mama Bigirimana alimuuliza Pamela huku mshangao ukiwa haujamtoka usoni kwake.
Pamela alinyanyua uso wake na kuwaangalia kwa makini wale wazee, hasa Mzee Tugiramahoro na Mzee Bigirimana. Akaonekana kusita na kumeza mate huku akimtupia jicho Ibrahim. Muda ule Ibrahim alionekana kuchanganyikiwa zaidi, jasho lilikuwa linamtoka.
“Kwa sababu sioni sababu kwa nini tumlazimishe kuishi na mtu aliyepanga kumtaliki badala ya kuheshimu maamuzi yake, mbona yeye haulizwi kwa nini alitaka kuniacha na kuoa mwanamke mwingine na kwa nini sasa hivi ananiona nafaa?”
Kauli ile ikafanya pazuke tena ukimya, wale wazee wote wakabaki kimya wakimtazama Pamela kwa makini. Mama Bigirimana akashusha pumzi ndefu huku akibetua kichwa chake akionekana kumwelewa Pamela na kuafikia naye.
“Hilo nalo neno! Mimi nipo upande wako mama, wanaume wanapaswa watambue kuwa mwanamke si mtumwa, tena wewe umekuwa muungwana sana, mwanzo alipokuja hapa alisema yake lakini sasa hayasemi… kwa nini tumuonee haya mtu asiyetuonea haya?”
Ibrahim aliwaangalia wale wazee huku akionekana kugwaya sana. Aliinamisha uso wake akiwa hana la kusema, machozi yalianza kumlengalenga. Pamela alimtazama Ibrahim kwa makini huku akijitahidi kuyazuia machozi ambayo yalianza kumtoka.
“Baba Samantha, nakupenda sana, kwa nini nisikuache huru ukaishi na mwanamke unayempenda. Ulipanga kuniacha ili uoe mwanamke anayekufaa na sasa unaniomba msamaha kwa kuwa wazee wamekulazimisha kufanya hivyo, sijui hapa pendo liko wapi? Hivi utalazimishwaje kuishi na mwanamke uliyemchoka eti kwa kuwa wazee wamekulazimisha? Ndiyo maana nataka unitaliki ili uwe huru kutafuta pendo la kweli…” Pamela alimwambia Ibrahim kwa sauti tulivu.
“Mwambie mama, mwambie mpumbavu huyu,” Mama Bigirimana alidakia na kuwafanya watu wengine wageuke kumwangalia kwa mshangao.
Sasa machozi mengi yalikuwa yanamtoka Ibrahim, alitaka kusema neno lakini akashindwa kuwa kuwa maneno yalikuwa hayatoki, akaanza kulia kilio cha kwikwi. Muda ule ule aliinuka, akamfuata Pamela na kuanguka miguuni kwake kisha akaishika miguu yake huku akiendelea kulia kwa uchungu.
Pamela alimtazama Ibrahim kwa huzuni, akajitahidi kuyazuia machozi yake. Mzee Tugiramahoro aliinuka na kumfuata Ibrahim, akamshika mabega na kumnyanyua kutoka pale alipokuwa amelala, kisha akampa ishara Mama Bigirimana akimtaka ainuke na kumpisha Ibrahim.
Mama Bigirimana alitii na kupisha, Mzee Tugiramahoro akamkalisha Ibrahim kando ya Pamela na kunyanyua kiganja cha mkono wa Pamela kisha akakikutanisha na kiganja cha mkono wa Ibrahim.
“Pamela, mumeo amejua makosa yake na sasa anataka muanze upya, sioni kwa nini usimsamehe…” Mzee Tugiramahoro alisema na kuwatazama wazee wengine.
“Na ikiwa mimi ni mzazi wenu, basi kwa niaba ya wazazi wenzangu wote naiombea kwa Mungu ndoa yenu idumu zaidi na zaidi, isiwe na migogoro tena wala visasi,” Mzee Tugiramahoro alisema na watu wote pale sebuleni wakaitikia, “Amina!”
MWISHO.