Bishop Hiluka
JF-Expert Member
- Aug 12, 2011
- 7,148
- 14,716
- Thread starter
- #21
HADI LINI! 15
Na Bishop Hiluka
Hata mzigo wa majukumu juu ya wazazi wake na wadogo zake ungemuelemea sana Pamela kama angeamua kuondoka kwa Ibrahim, ni afadhali basi angekuwa anafanya kazi mahali walau angeweza kupata faranga mbili tatu ambazo zingeweza kukidhi mahitaji yake na ya wazazi wake, lakini wakati ule hakuwa na kazi, mume wake alikuwa hajamruhusu kufanya kazi kwa kauli ya kwamba yeye alikuwa anao uwezo wa kumhudumia kwa kila kitu. Na kama mume amesema hivyo, je, mke angebisha nini?
Hali ilipozidi kuwa mbaya zaidi Pamela aliamua kupigania haki yake, kwanza kwa kumkabili Ibrahim na kumtaka wakae, wayazungumze na kutatua matatizo ya ndoa yao, lakini Ibrahim alimpuuza. Kuona hivyo Pamela akaamua kwenda kuitafuta haki yake kwenye taasisi mbalimbali za watetezi wa jinsia na hata katika taasisi za kisheria lakini kote huko ilishindikana kwa sababu Ibrahim alidharau mwito kutoka katika taasisi hizo, alipata jeuri kwa sababu ya nafasi yake iliyomfanya kukutana na wakubwa wa nchi.
Pamela alipoona kote huko imeshindikana, ndipo akafikia uamuzi kuwa “liwalo na liwe!” maana alijiuliza, je, angeendelea kuvumilia mateso yale hadi lini? Ndiyo maana aliamua kukata mzizi wa fitina kwa kuwaita wazazi wa pande zote ili sasa aweke wazi kuhusu msimamo wake juu ya ndoa yake na Ibrahim. Kama noma na iwe noma!
Na sasa Ibrahim alikuwa amesimama akimtazama mkewe katika ule usiku usiosahaulika kamwe kwenye kumbukumbu zake, ulikuwa usiku wa kizaazaa! Ibrahim aliendelsa kumkodolea macho Pamela ambaye alikuwa chumbani kwake akiwa kasimama kwenye kibaraza cha ghorofa (balcony) akiangalia mbingu kwa unyonge.
Kilikuwa chumba kikubwa na chenye nafasi ya kutosha ambacho upande wa kulia na wa mbele wa kile chumba kulikuwa na madirisha mapana yenye vioo yaliyokuwa yamefunikwa kwa mapazia marefu na mepesi. Dirisha moja lilikuwa limeungana na mlango uliokuwa unatokea kwenye balcony, sehemu alipokuwa amesimama Pamela.
Upande wa kushoto ukutani kulikuwa na kabati kubwa la nguo la ukutani na kando ya kabati lile kulikuwa na meza nzuri nyeusi ya kioo. Juu ya meza hiyo kulikuwa na seti moja ya runinga kubwa Flat screen katikati ya spika mbili za sistimu ya muziki wa Home threatre.
Katikati ya chumba kulikuwa na kitanda kikubwa cha futi sita kwa sita chenye nakshi nzuri za kupendeza, upande wa kulia wa chumba. Upande huo wa kulia kulikuwa na mlango mwingine wa chumba kidogo cha maliwato.
Upande wa kushoto wa chumba kulikuwa na seti moja ya makochi ya sofa nadhifu na ya kisasa juu ya zulia zuri lenye rangi za ngozi ya Pundamilia. Katikati ya makochi hayo kulikuwa na meza ndogo ya mbao iliyokuwa na umbo la nusu duara. Juu ya ile meza kulikuwa na kibakuli kidogo cha majivu ya sigara, kibiriti kimoja cha gesi, kasha tupu la miwani ya macho na simu ya mezani.
Dirishani kwenye balcony kulikuwa na ua kubwa zuri kwenye chungu cha udongo na kando ya ua hilo kulikuwa na kiti kimoja cha kupumzikia kilichokuwa kinatazama nje. Pembeni ya kile kiti kulikuwa na meza fupi ya mbao yenye droo mbili.
Ibrahim alimtazama Pamela kwa makini na kushusha pumzi za ndani kwa ndani kisha akaachia tabasamu la kebehi.
“Naona unatazama juu kama vile unatarajia Mungu akushushie mume mwingine zaidi yangu!”
Pamoja na kutambua uwepo wa Ibrahim mle chumbani lakini Pamela hakugeuka kumtazama bali aliendelea kutazama kule juu bila kuonesha dalili yoyote ya kumsikia mumewe.
Ibrahim alionesha kukerwa mno, akaiweka briefcase yake sakafuni na simu zake akaziweka juu ya meza ndogo ya mbao yenye umbo la nusu duara, kisha akaanza kupiga hatua kumfuata Pamela. Alimfikia na kusimama nyuma yake huku akimwangalia kwa hasira iliyokuwa imechanganyika na jeuri.
“Mapokezi gani haya, halafu eti mwanamke anataka apendwe!” Ibrahim alisema huku akimtazama Pamela kwa dharau.
Pamela aligeuza shingo yake kumtazama Ibrahim kupitia juu ya bega lake bila kuonesha hisia zozote za kumjali, kisha akageuzia shingo yake upande mwingine akionekana kumpuuza. Ibrahim akapandwa zaidi na hasira na kushika mabega ya Pamela, akamgeuza kwa nguvu.
“Naona wewe na hao wazee sasa mnanitafuta kwa jambo, nasema hamtaniweza!” Ibrahim alibwata kwa hasira huku akimkazia machp Pamela.
Pamela alimkazia Ibrahim kwa chuki kubwa na kukunja sura yake, akaitoa mikono ya Ibrahim kwenye mabega yake na kurudi nyuma hatua moja akiwa bado kakunja sura yake.
“Nitashukuru iwapo utauacha moyo wangu utulie, tafadhali sana niache!” Pamela alisema huku akimtazama Ibrahim kwa makini.
Ibrahim alimsogelea tena na kumshika mabegani kisha akaanza kumtingisha kwa nguvu akionekana kupandwa zaidi na hasira. “Unanifanyia kiburi siyo? Nitakupiga sasa hivi au unadhani nawaogopa hao wazee?” Ibrahim alizidi kubwata huku akimtazama Pamela kwa hasira.
“Ni heri uniue kabisa maana nimechoshwa na maisha haya. Nitaishi hivi hadi lini?” Pamela alisema huku akiitoa tena mikono ya Ibrahim mabegani kwake. Ibrahim alimkazia macho akimtazama kwa makini na kucheka kwa dharau huku akitingisha kichwa.
“Huna lolote, najua ni wivu tu unakusumbua, tena wivu wa kijinga,” Ibrahim alisema huku akishusha pumzi.
“Sikuolewa nikuonee wivu bali nikupende na kukutumikia, na wala si kugeuzwa kijakazi wa mahaba!” Pamela alisema huku akimwangalia Ibrahim kwa makini na kutingisha kichwa chake kwa huzuni. Kisha alipiga hatua taratibu kujitenga na Ibrahim, akasimama hatua chache na kumwangalia kwa makini kuanzia chini hadi juu, kisha anaangua kicheko hafifu kilichokuwa kimebeba uchungu.
“Eti wivu! Utoke wapi katika unyumba duni kama huu!” Pamela alisema huku akiendelea kucheka kwa uchungu.
Kauli ile ikaonesha kumchukiza zaidi Ibrahim, alimsogelea Pamela kwa hasira na kunyanyua mkono wake akitaka kumzaba kibao, lakini Pamela alikinga mkono wake kwa ujasiri aakionesha kutomuogopa mumewe. Ibrahim akamwangalia Pamela kwa hasira na kusonya.
“Kama unyumba wangu ni duni, unangoja nini basi nyumbani mwangu? Si uondoke ukatafute anayeona anakutosheleza!” Ibrahim alisema huku akimtazama kwa hasira.
“Nangoja talaka! na itapendeza zaidi ikiwa ni kifo!” Pamela alijibu kwa dharau. Ibrahim alimkazia macho Pamela na kuachia kicheko cha dharau, kisha anasonya.
“Yaani ufedhuli wako ndiyo unanifanya nikuone kinyaa siku hizi,” Ibrahim alisema huku akishushas pumzi za ndani kwa ndani.
ITAENDELEA...
Na Bishop Hiluka
Hata mzigo wa majukumu juu ya wazazi wake na wadogo zake ungemuelemea sana Pamela kama angeamua kuondoka kwa Ibrahim, ni afadhali basi angekuwa anafanya kazi mahali walau angeweza kupata faranga mbili tatu ambazo zingeweza kukidhi mahitaji yake na ya wazazi wake, lakini wakati ule hakuwa na kazi, mume wake alikuwa hajamruhusu kufanya kazi kwa kauli ya kwamba yeye alikuwa anao uwezo wa kumhudumia kwa kila kitu. Na kama mume amesema hivyo, je, mke angebisha nini?
Hali ilipozidi kuwa mbaya zaidi Pamela aliamua kupigania haki yake, kwanza kwa kumkabili Ibrahim na kumtaka wakae, wayazungumze na kutatua matatizo ya ndoa yao, lakini Ibrahim alimpuuza. Kuona hivyo Pamela akaamua kwenda kuitafuta haki yake kwenye taasisi mbalimbali za watetezi wa jinsia na hata katika taasisi za kisheria lakini kote huko ilishindikana kwa sababu Ibrahim alidharau mwito kutoka katika taasisi hizo, alipata jeuri kwa sababu ya nafasi yake iliyomfanya kukutana na wakubwa wa nchi.
Pamela alipoona kote huko imeshindikana, ndipo akafikia uamuzi kuwa “liwalo na liwe!” maana alijiuliza, je, angeendelea kuvumilia mateso yale hadi lini? Ndiyo maana aliamua kukata mzizi wa fitina kwa kuwaita wazazi wa pande zote ili sasa aweke wazi kuhusu msimamo wake juu ya ndoa yake na Ibrahim. Kama noma na iwe noma!
Na sasa Ibrahim alikuwa amesimama akimtazama mkewe katika ule usiku usiosahaulika kamwe kwenye kumbukumbu zake, ulikuwa usiku wa kizaazaa! Ibrahim aliendelsa kumkodolea macho Pamela ambaye alikuwa chumbani kwake akiwa kasimama kwenye kibaraza cha ghorofa (balcony) akiangalia mbingu kwa unyonge.
Kilikuwa chumba kikubwa na chenye nafasi ya kutosha ambacho upande wa kulia na wa mbele wa kile chumba kulikuwa na madirisha mapana yenye vioo yaliyokuwa yamefunikwa kwa mapazia marefu na mepesi. Dirisha moja lilikuwa limeungana na mlango uliokuwa unatokea kwenye balcony, sehemu alipokuwa amesimama Pamela.
Upande wa kushoto ukutani kulikuwa na kabati kubwa la nguo la ukutani na kando ya kabati lile kulikuwa na meza nzuri nyeusi ya kioo. Juu ya meza hiyo kulikuwa na seti moja ya runinga kubwa Flat screen katikati ya spika mbili za sistimu ya muziki wa Home threatre.
Katikati ya chumba kulikuwa na kitanda kikubwa cha futi sita kwa sita chenye nakshi nzuri za kupendeza, upande wa kulia wa chumba. Upande huo wa kulia kulikuwa na mlango mwingine wa chumba kidogo cha maliwato.
Upande wa kushoto wa chumba kulikuwa na seti moja ya makochi ya sofa nadhifu na ya kisasa juu ya zulia zuri lenye rangi za ngozi ya Pundamilia. Katikati ya makochi hayo kulikuwa na meza ndogo ya mbao iliyokuwa na umbo la nusu duara. Juu ya ile meza kulikuwa na kibakuli kidogo cha majivu ya sigara, kibiriti kimoja cha gesi, kasha tupu la miwani ya macho na simu ya mezani.
Dirishani kwenye balcony kulikuwa na ua kubwa zuri kwenye chungu cha udongo na kando ya ua hilo kulikuwa na kiti kimoja cha kupumzikia kilichokuwa kinatazama nje. Pembeni ya kile kiti kulikuwa na meza fupi ya mbao yenye droo mbili.
Ibrahim alimtazama Pamela kwa makini na kushusha pumzi za ndani kwa ndani kisha akaachia tabasamu la kebehi.
“Naona unatazama juu kama vile unatarajia Mungu akushushie mume mwingine zaidi yangu!”
Pamoja na kutambua uwepo wa Ibrahim mle chumbani lakini Pamela hakugeuka kumtazama bali aliendelea kutazama kule juu bila kuonesha dalili yoyote ya kumsikia mumewe.
Ibrahim alionesha kukerwa mno, akaiweka briefcase yake sakafuni na simu zake akaziweka juu ya meza ndogo ya mbao yenye umbo la nusu duara, kisha akaanza kupiga hatua kumfuata Pamela. Alimfikia na kusimama nyuma yake huku akimwangalia kwa hasira iliyokuwa imechanganyika na jeuri.
“Mapokezi gani haya, halafu eti mwanamke anataka apendwe!” Ibrahim alisema huku akimtazama Pamela kwa dharau.
Pamela aligeuza shingo yake kumtazama Ibrahim kupitia juu ya bega lake bila kuonesha hisia zozote za kumjali, kisha akageuzia shingo yake upande mwingine akionekana kumpuuza. Ibrahim akapandwa zaidi na hasira na kushika mabega ya Pamela, akamgeuza kwa nguvu.
“Naona wewe na hao wazee sasa mnanitafuta kwa jambo, nasema hamtaniweza!” Ibrahim alibwata kwa hasira huku akimkazia machp Pamela.
Pamela alimkazia Ibrahim kwa chuki kubwa na kukunja sura yake, akaitoa mikono ya Ibrahim kwenye mabega yake na kurudi nyuma hatua moja akiwa bado kakunja sura yake.
“Nitashukuru iwapo utauacha moyo wangu utulie, tafadhali sana niache!” Pamela alisema huku akimtazama Ibrahim kwa makini.
Ibrahim alimsogelea tena na kumshika mabegani kisha akaanza kumtingisha kwa nguvu akionekana kupandwa zaidi na hasira. “Unanifanyia kiburi siyo? Nitakupiga sasa hivi au unadhani nawaogopa hao wazee?” Ibrahim alizidi kubwata huku akimtazama Pamela kwa hasira.
“Ni heri uniue kabisa maana nimechoshwa na maisha haya. Nitaishi hivi hadi lini?” Pamela alisema huku akiitoa tena mikono ya Ibrahim mabegani kwake. Ibrahim alimkazia macho akimtazama kwa makini na kucheka kwa dharau huku akitingisha kichwa.
“Huna lolote, najua ni wivu tu unakusumbua, tena wivu wa kijinga,” Ibrahim alisema huku akishusha pumzi.
“Sikuolewa nikuonee wivu bali nikupende na kukutumikia, na wala si kugeuzwa kijakazi wa mahaba!” Pamela alisema huku akimwangalia Ibrahim kwa makini na kutingisha kichwa chake kwa huzuni. Kisha alipiga hatua taratibu kujitenga na Ibrahim, akasimama hatua chache na kumwangalia kwa makini kuanzia chini hadi juu, kisha anaangua kicheko hafifu kilichokuwa kimebeba uchungu.
“Eti wivu! Utoke wapi katika unyumba duni kama huu!” Pamela alisema huku akiendelea kucheka kwa uchungu.
Kauli ile ikaonesha kumchukiza zaidi Ibrahim, alimsogelea Pamela kwa hasira na kunyanyua mkono wake akitaka kumzaba kibao, lakini Pamela alikinga mkono wake kwa ujasiri aakionesha kutomuogopa mumewe. Ibrahim akamwangalia Pamela kwa hasira na kusonya.
“Kama unyumba wangu ni duni, unangoja nini basi nyumbani mwangu? Si uondoke ukatafute anayeona anakutosheleza!” Ibrahim alisema huku akimtazama kwa hasira.
“Nangoja talaka! na itapendeza zaidi ikiwa ni kifo!” Pamela alijibu kwa dharau. Ibrahim alimkazia macho Pamela na kuachia kicheko cha dharau, kisha anasonya.
“Yaani ufedhuli wako ndiyo unanifanya nikuone kinyaa siku hizi,” Ibrahim alisema huku akishushas pumzi za ndani kwa ndani.
ITAENDELEA...