..naona Mjengwa ameanza kampeni za Uraisi za Kikwete 2010.
..tatizo ni kwamba hawezi hata kutaja achievement moja ya Kikwete tangu hajaingia madarakani, na mpaka sasa hivi 3 years as the President.
..Mjengwa ameishia kumsifa Kikwete kwa kuwa "karibu" na wananchi kwasababu hutembea kwa miguu kwenye viuchochoro vya Bagamoyo.
..Kikwete yuko karibu na wananchi kwa namna gani wakati aliitelekeza shule yake ya msingi aliposomea? shule hiyo ilionyeshwa ktk gazeti la Uhuru wakati wa kampeni za 2005 ikiwa na hali mbaya imechoka mithili ya zizi la ng'ombe.
..halafu kidogo kidogo Mjengwa anachombeza kuhusu hizi kesi mbuzi zilizofunguliwa majuzi na serikali. inavyoelekea zimempa imani kubwa sana na utawala wa Kikwete.
..Mjengwa anasahau kwamba Kikwete alimteua Chenge kuwa waziri wa afrika mashariki, baadaye akafanya mabadiliko na kumpeleka miundo mbinu. Kikwete huyo huyo alimteua Basili Mramba mara mbili ktk baraza lake la mawaziri. Baada ya Dr.Msabaha kuvuruga Nishati, Kikwete akajaribu kumficha wizara ya afrika mashariki. zaidi, kulifanyika mabadiliko mawili ya makatibu wakuu na yote hayakumgusa Gray Mgonja.
..sasa hii imani ya Majid Mjengwa kwa uongozi wa Raisi Kikwete inatoka wapi?
..Watanzania kwanini tunakumbukumbu fupi namna hii?
Majid Mjengwa said:
NAENDELEA na tathmini yangu binafsi ya miaka mitatu ya Uongozi wa Awamu ya Nne wa Rais Jakaya Kikwete.
Naam. Linapotokea jambo jema na zuri katika nchi, basi, ni vizuri jema hilo likaelezwa, vivyo hivyo kinyume chake. Kubwa kabisa linalotokea sasa ni ukweli kuwa Watanzania wameanza kurejewa na imani na uongozi wa juu pale wanaposhuhudia baadhi ya ‘vigogo' wakifikishwa mahakamani.
Hata kama ni chache kwa sasa, lakini hizi ni hatua za maana za uongozi wa Awamu ya Nne. Kwa Jakaya Kikwete, huu ni mtaji wa imani anaoanza kuuwekeza kwa umma. Kwa mwendo huu, mtaji huu unaweza kulipatia taifa mavuno makubwa, pengine si katika awamu yake, bali kwa awamu zijazo.
Katika kutathmini miaka mitatu ya Jakaya Kikwete madarakani bado nitarudi nyuma alikoanzia, maana huko nilipata pia kuandika fikra zangu kwa jinsi nilivyomwona akiianza awamu yake. Nilikuwa Bagamoyo siku tatu kabla ya Jakaya Kikwete kuhutubia Bunge la kwanza la Uongozi wa Awamu ya Nne, Desemba 30, 2005.
Nikiwa Bagamoyo nilipata wasaa wa kuzungumza na baadhi ya wananchi, kusikia maoni yao juu ya mtu huyu, Jakaya Kikwete. Nilitaka kupata maoni ya watu wa kawaida juu ya matarajio yao kwake.
Nakumbuka kuzungumza na kijana mwuza ‘chipsi' pale sokoni Bagamoyo. Huyu aliniambia; " Braza, Jakaya huwa anapita hapa kwa miguu akienda nyumbani kwake. Na kichochoro anachopita hiki hapa. Ukimaliza kichochoro hiki nyuma hapo utaukuta mti wa mkungu, mbele kidogo kuna kiwanja cha watoto, nyumba yake inaonekana kwa mbele".
Watu kadhaa walinipa simulizi zenye kufanana juu ya Jakaya Kikwete aliye karibu na watu. Jakaya waliyezoea kumwona akikatisha mitaa ya Bagamoyo kwa miguu na kuzungumza na wananchi. Kwa namna moja au nyingine, simulizi hizi zilionyesha ni kwa jinsi gani mtu huyu Jakaya Kikwete asivyo na makuu.
Na hakika, kiongozi wa watu hatakiwi awe mtu mwenye makuu, mbinafsi, mwenye tamaa ya mali na fisadi. Na katika hili la kuwa upande wa wananchi, Kikwete, kama mtu aliyekuwa na ndoto ya muda mrefu ya kushika nafasi ya ukuu wa nchi, naamini amesoma kwa kina maandiko ya wanafalsafa mbalimbali kama vile Niccolo Machiaveli na hata Plato.
Na kwa kupitia maandiko ya Machiavelli, " The Prince", yaani, "Mwana Mfalme", Kikwete ana mengi ya kujifunza . Machiaevelli anamtaka kiongozi kuwa makini na tabaka la waliomsaidia kuingia madarakani na hata wenye kumzunguka. Kwa mujibu wa Machiavelli, hutokea kwa Mwana Mfalme "kuwajeruhi" waliomsaidia kupata utawala. Hii ni kwa kutowatimizia yote yale waliodhani kuwa ni haki yao kutimiziwa.
Badala yake, Mwana Mfalme huwaingiza kundini wawe kama wengine. Katika manung'uniko yao, Mwana Mfalme hawezi kutumia dawa chungu dhidi yao kwa vile hujihisi ana deni kwao. Lakini, cha msingi kwa Mwana Mfamle ni kuzingatia ukweli, kuwa, hata kama atakuwa na maadui wachache, katika kuchukua nchi, muhimu ni kuwaridhisha walio wengi, na hapa ni wananchi.. Huwezi kutawala kwa amani bila upendo na utashi wa walio wengi. Ni kwa sababu hizi, Mfalme Louis XII wa Ufaransa aliweza kwa kasi ya ajabu kuitwaa Milan na kwa kasi ya ajabu kuipoteza Milan. Hakukidhi matakwa na matarajio ya wananchi walio wengi waliomfungulia milango.
Mtawala aliye mbali na asiyejali maslahi ya watu wake walio wengi ni mtawala mwenye hofu. Na mtawala mwenye hofu zaidi na watu wake kuliko adui wa nje, basi, hujijengea kasri ama ngome imara ya kujihifadhi ingawa hilo halitamsaidia kuzuia nguvu za umma za kumwondoa madarakani. Kwa mtawala, kasri ama ngome iliyo imara ni kuepuka kuchukiwa na wananchi, kuacha ubinafsi na kujali maslahi ya wengi.
Katika ubinafsi wa viongozi wetu, kiongozi wa Kiafrika, mara nyingi hapendi kukosolewa. Hana busara ya kutambua, kuwa, hakuna mwelevu wa kila jambo, kwamba sote hatujakamilika, tuna mapungufu yetu. Kwa kiongozi wa staili hii, akitamka jambo, basi hakuna wa kufikiri jingine. Fikra zake siku zote ni sahihi.
Plato, mwanafalsafa wa Uyunani ya kale anasema; katika nchi, kiongozi wa namna hii, hufikia kukoma kuwa kama wanadamu wengine, hugeuka mbweha. Atawaandama "wapinzani" wake. Wengine atawaua kwa kuwapachikia mashitaka batili, na wengine atawalazimisha kwenda kuishi uhamishoni.
Haya ni masuala ya kimaadili. Katika machapisho yake ya "Republic", yaani , "Jamhuri", Plato anazungumzia kwa kina juu ya ubinafsi na maadili. Je, kuna sababu gani nzuri na za kimsingi za kuwa mtenda haki na si kinyume chake, yaani mtenda maovu? Glaucon, ndugu wa Plato anajibu; "Binadamu wote kwa asili yetu tu wabinafsi, tunajijali sisi wenyewe kila tunapopata nafasi ya kufanya hivyo. Bila kujali kama jambo hilo si la haki kiasi gani kwa wengine. Lakini, kwa bahati mbaya, nasi pia hufikwa na hali kama hiyo kwa kufanyiwa yasiyo haki na wengine. Jambo hilo huwa si la kufurahia."
Maana. mlevi wa madaraka hupungukiwa haraka maadili ya uongozi. Basi, ghafla huwa mla rushwa mkubwa kwa kutumia ofisi aliyokabidhiwa . Na hatimaye, ghafla huwa tajiri mkubwa, bilionea! Vyote hivi huweza kumtokea kiongozi wa Kiafrika kwa kasi ya kutisha sana. Leo unapishana na Mwafrika mwenzako akiendesha baiskeli, kesho anaukwaa uongozi. Baada ya miaka 10 tu, anajenga "ikulu" yake mwenyewe ya kifahari, anaweza kuwa nazo mbili au tatu za namna hiyo na magari kadhaa ya kifahari. Je, yote haya ni kwa kipato halali cha "mteule" huyu kutokana na kazi yake?!
Mtu wa namna hii kamwe hawezi kukupa historia yenye kueleweka juu ya utajiri wake wa ghafla. Huyo si mhalifu kama walivyo wezi wa kuku au wenye kuvunja madirisha usiku. Huyo ni jambazi, ni mhalifu mkubwa anayetishia usalama wa taifa husika.
Hivyo basi, ili kuwapo na mazingira ya kuishi kwa amani na usalama ni vema, kwa mujibu wa mwanafalsafa Plato, kukawapo na taratibu za kuishi kistaarabu. Ndipo hapa dhana ya kuwapo kwa Mkataba wa Kijamii (Social Contract) ikaingia akilini kwa mwanadamu. Ndilo chimbuko la katiba za nchi. Chimbuko la misingi ya utawala bora.
Na hii ni changamoto kwa Rais Jakaya Kikwete na uongozi wake wa Awamu ya Nne. Ana nafasi ya kuwawekea Watanzania misingi na taratibu za kistaarabu za kuishi katika nchi yao. Aendelee na juhudi za kukirekebisha chama chake ili apate msingi wa kufanya marekebisho ya Katiba ya nchi. Ni kazi ngumu, lakini inawezekana, na hususan anapokuwa na umma nyuma yake.