Mitambo ya IPTL yawashwa,megawati 10 zaingia gridi ya taifa

Pdidy

JF-Expert Member
Nov 22, 2007
50,720
21,779
Na Mussa Mkama

HATIMAYE mtambo mmoja wa kufua megawati 10 za umeme wa kampuni ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL), umewashwa jana na kuingizwa kwenye gridi ya taifa.

Mtambo huo ni kati ya mitambo kumi ya IPTL inayofanyiwa matengenezo na kampuni kandarsi ya Wartsila kwa ajili ya kutoa jumla ya megawati 100 za umeme.

"Tayari megawati kumi zimeshaingizwa kwenye gridi ya taifa na hii ni kutokana na kuwashwa kwa mtambo mmoja baada ya kukamilika kwa matengenezo," alisema meneja mkuu wa IPTL, Dk Magesvaran Subramaniam.

Kukamilika kwa mtambo huo kunatokana na juhudi za mafundi wa hapa nchini wakishirikiana na wengine kutoka Uhoranzi.

Alisema kuwa mtambo huo uliwashwa jana (juzi) usiku, lakini kwa bahati mbaya ukazima kutokana na hitilafu za kiufundi na sasa umewashwa tena na unaendelea kufanya kazi bila matatizo.

Tathmini ya mafundi na wataalam hao inaonyesha kuwa mitambo hiyo haina ubovu mkubwa hivyo kuna matumaini ya kuwashwa kwa mashine zote kwa awamu baada ya mafanikio ya mtambo huo namba moja.

"Mafundi wanaendelea na juhudi ya kuhakikisha mitambo yote inawashwa kwa kufanyia matengenezo na kukagua mtambo mmoja mmoja kwa umakini ili kuhakikisha kuwa ikikamilika na kuwashwa haisababishi matatizo madogo madogo" alisema Subramaniam.

"Kukamilika kwa mtambo huo ni ishara nzuri ya kuendelea kukamilika kwa mingine tisa iliyobaki."

Kuwashwa kwa mtambo huo ni kielelezo tosha kwa wananchi kuwa maumivu ya mgao ulioanza Septemba kuisha hivi karibuni.

Mtambo huo umewashwa zikiwa zimepita siku 18 tangu Rais Jakaya Kikwete aagize kuwashwa mara moja kwa mitambo ya kampuni hiyo iliyo katika mgogoro na serikali kiasi cha kupelekana mahakamani.

Kikwete aliingilia kati tatizo la umeme Oktoba 20 baada ya makali ya mgawo kuzidi na kusababisha wananchi na wafanyabiashara kumtaka afanye hivyo. Baada ya agizo lake, ilitangazwa kuwa mitambo hiyo ingewashwa Novemba mosi, lakini ilibainika baadaye kuwa serikali haikuwa imeilipa IPTL na hivyo matengenezo ya mitambo kuchelewa.

Mitambo hiyo ilifungwa nchini mwaka 1998, lakini serikali ikaamua kutoitumia kutokana na gharama za uzalishaji na kuagiza kampuni hiyo iangalie uwezekano wa kuibadili ili iendeshwe kwa kutumia nguvu za gesi na hivyo kupunguza makali ya bei.

Hata hivyo, IPTL ilifungua kesi nchini Marekani ikidai kulipwa gharama za uzalishaji, huku utekelezaji wa agizo la kuigeuza mitambo hiyo ili iwe inatumia gesi asilia likionekana kusuasua.

Mgao wa umeme wa safari hii umetokana na kuharibika kwa mtambo wa kuzalisha umeme kwa kutumia gesi asilia wa kampuni Songas na mingine miwili ya kuzalisha umeme kwa kutumia nguvu ya maji iliyo kwenye mabwawa ya Kihansi na Pangani.

Sababu nyingine ilielezwa kuwa ni kupungua kwa uzalisha umeme kwenye mabwawa ya Kihansi, Hale na Pangani kulikotokana na kupungua kwa kiwango cha maji.
 
na Na Halima Mlacha;
Tarehe: 8th November 2009

Habari Leo

HATIMAYE mtambo mmoja kati ya mitambo 10 ya Kampuni ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL), umewashwa na kuanza kuingiza mewagati za umeme 10 katika gridi ya Taifa.

Akizungumza na HabariLeo, Mkurugenzi Mkuu wa kampuni hiyo, Dk. Magesvaran Subramanian, alikiri kuwashwa kwa mtambo huo na kuongeza kuwa uliwashwa rasmi jana saa 6.04 mchana.

“Tumeanza kufanya kazi na mtambo mmoja namba moja ndio uliowashwa na mpaka sasa kila kitu kinakwenda vizuri tunatarajia mpaka kesho (leo), utakuwa umeshaanza kuzalisha megwati zote kumi,” alisema Dk. Subramanian.

Naye Mfilisi wa kampuni hiyo, Rugonzibwa Mujunangoma, alisema mtambo huo uliwashwa jana, lakini kwa wakati ule haukuweza kuzalisha umeme wote wa megawati 10 na kwamba kadri ulivyokuwa ukiendelea kuzalisha umeme, ndipo megawati zilipokuwa zikiendelea kupanda na kufika 10.

“Tangu mtambo uwashwe na hadi ninaondoka muda wa saa saba mchana, mtambo tayari ulishaanza kuingiza megawati 1.5, lakini hadi kesho (leo)), utakuwa tayari unazalisha megawati kumi, ikumbukwe hii ni mashine,” alisema Rugonzibwa.

Kuhusu mitambo mingine tisa, alisema mafundi na watalaamu wa masuala ya umeme wanaendelea na ukaguzi ambapo nayo haitochukua muda mrefu itawashwa wakati wowote.

“Kuwaka kwa mtambo huu ni dalili nzuri kuwa mitambo mingine nayo haitochukua muda itawaka, mafundi wanaendelea vizuri na kazi yao na kwa kweli hali inatia matumaini,” alisema mfilisi huyo.

Kampuni hiyo ya IPTL ina mitambo 10 ambayo kila mmoja ukiwaka utatoa megawati 10 na hivyo mtambo mzima wa IPTL unatarajiwa kutoa megwati 100, na hivyo kupunguza tatizo la mgawo wa umeme ambalo limeikumba nchi kutokana na kuharibika kwa mitambo ya Kihansi na Songas.

Rais Jakaya Kikwete aliagiza katikati ya mwezi uliopita kwa mamlaka husika kuwa mitambo hiyo ya IPTL iwashwe ifikapo Novemba mosi, mwaka huu ili kukabiliana na tatizo la mgawo. Imechelewa kuwashwa kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo za kuchelewa kwa malipo kwa taasisi zitakazohusika kuendesha mitambo hiyo.

 
Back
Top Bottom