Jamani wana JF,
Naombeni mnisaidie labda mimi ndio sijaelewa kauli ya waziri wa utumishi mhe.Hawa Ghasia alipokuwa kikao cha kamati ya kudumu ya bunge ya katiba na sheria alipokuwa akijibu maswali/maoni ya baadhi ya wabunge;eti serikali inajiaandaa kuanza utaratibu wa kuwalipa wafanyakazi wa serikali mishahara kupitia dirishani
Soma hapa, angalia mistari ya mwisho hapo kwenye RED
Mbunge amwambia Waziri Mkurugenzi hafai
Imeandikwa na Shadrack Sagati;
Tarehe: 24th February, 2011
MBUNGE wa Temeke, Abbas Mtemvu (CCM), amemshitaki Mkurugenzi Mtendaji wa Manispaa ya Temeke, Steven Kongwa kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma), Hawa Ghasia, akidai ni mtu ambaye hana uwezo wa kiutendaji wa kuongoza manispaa hiyo.
Akichangia katika taarifa ya Waziri Ghasia wakati wa kikao cha Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala jana Dar es Salaam, Mtemvu alidai kutokana na uwezo mdogo wa mkurugenzi huyo, manispaa ya Temeke imerudi nyuma kimaendeleo.
Alisema, kuna miradi inayotekelezwa katika manispaa hiyo, lakini mkurugenzi huyo hajishughulishi kwenda kushuhudia, jambo ambalo alisema mfano huo unaonesha namna mkurugenzi huyo asivyo na sifa za kuongoza manispaa kubwa kama hiyo ya Temeke.
Kongwa aliteuliwa kushika wadhifa huo baada ya kifo cha aliyekuwa Mkurugenzi wa Manispaa hiyo, Iddi Nyundo. Mtemvu alisema wananchi wa Temeke wanamkumbuka Nyundo kwani chini ya uongozi wake, Temeke ilipiga hatua kubwa kimaendeleo.
Akijibu hoja hiyo, Ghasia alisema wabunge wanapokuwa na malalamiko yenye ushahidi juu ya utendaji mbovu wa watendaji kwenye halmashauri ni vyema wapeleke kwenye ofisi yake ili hatua zichukuliwe.
Kuhusu suala hilo la Mkurugenzi wa Temeke, Ghasia alisema wananchi wa Temeke wenyewe wana uwezo wa kumkataa mtendaji yeyote katika halmashauri hiyo kama wataona hawafai.
"Kwa mfumo wa sasa hivi wa utumishi wa umma, wananchi wenyewe wana mamlaka ya kumkataa mkurugenzi huyo sio lazima suala hilo lifikishwe utumishi," alisema Ghasia.
Mbunge wa Karagwe, Gosbert Blandes (CCM) alilalamikia hatua ya baadhi ya halmashauri kuwanyima ruhusa walimu kwenda kujiendeleza, akidai uamuzi huo unawafanya walimu wasiwe na ari ya kufundisha.
Alisema ana mifano ya walimu ambao wameamua kwenda kujisomesha kwa gharama zao, lakini halmashauri zinawazuia hivyo akataka kupata mwongozo kutoka kwa waziri huyo.
Mbunge wa Manyoni Magharibi, Paul Lwanji (CCM), alitaka kufahamu Serikali inavyoshughulikia tatizo la watumishi hewa na kuhoji sababu ya kuwepo watumishi hao wakati tayari kuna sensa ilishafanywa miaka ya nyuma.
Akijibu hoja za wabunge hao, Ghasia alisema walimu kwenda kusoma, kwa sasa Serikali imeweka utaratibu kuwa wakajiendeleze kwa kufuata utaratibu uliopo na sio kila mtu kujigharamia na kwa muda anaotaka.
Alisema utaratibu uliopo ni walimu wanaruhusiwa kwenda kujiendeleza kufuatana na uzoefu kazini kwamba aliyetangulia kazini ndiye anapewa kipaumbele kwanza.
Alisema iwapo walimu wataruhusiwa kila mtu akajiendeleze shule zitaendelea kukumbwa na ukosefu wa walimu.
Kuhusu watumishi hewa, alisema kwa sasa kila taasisi ya Serikali inasafisha benki yake ya takwimu ili kujiridhisha kuwa fedha wanazoomba za mishahara ya bajeti ijayo ni kwa watumishi walioko kazini tu.
Alisema baada utaratibu huo kukamilika, Serikali itaandaa malipo ya mishahara ya watumishi kupitia dirishani, jambo ambalo linaweza kutekelezwa ndani ya miezi miwili ijayo.
"Kwa sasa tunaendelea na maandalizi kwani ni suala ambalo linahitaji fedha," alisema Ghasia.