SEHEMU YA 23
Siku zikakatika. Kwa Fareed, maisha yalikuwa burudani lakini hakutaka kuendelea kuwa na mwanaume mmoja tu. Alitaka kila mwanaume mwenye mwili mzuri awe wake. Hakuacha kujiremba, alijipamba, alijua kujisafisha na kila alipokuwa, alikuwa akinukia maradhi ya Zenji, alijua kurembua macho, alijua kubinua midomo na zaidi ya yote alijua sana kuzungumza hasa kwa sauti ile ya kike.
Kwa wakati huo, alikuwa akijiandaa kwa safari ya kwenda Dubai. Alikuwa akimsindikiza mpenzi wake huyo aliyekuwa akienda kwa mambo ya kibiashara. Alichukua ndege pamoja naye, alivalia mavazi ambayo ilikuwa ni vigumu kugundua kama alikuwa mwanaume, alijiremba, alivalia dela na kichwani alivalia kiremba.
“Unakwenda Dubai?” aliuliza wakala wake aliyeitwa Asteria Kimaro, mwanamke aliyekuwa akiwaunganisha wanawake na wanaume tata kwa wanaume wengi waliokuwa wakiishi Ulaya, Asia na Marekani. Alijenga nyumba nyingi, kununua magari ya kifahari kwa biashara hiyo tu.
“Ndiyo!”
“Kuna wateja wawili wanakuhitaji huko. Nishafanya mawasiliano nao, nakutumia namba zao. Wanakuhitaji sana,” alisema Bi Asteria.
“Haina shida! Ila wana hela?” aliuliza Fareed, yeye alikuwa akifikiria hela tu.
“Eeh! Mtu aishi Dubai, awe mfanyabiashara mkubwa halafu asiwe na pesa! Umeona wapi hiyo! Hao wana hela mpaka wanaumwa!” alisema Bi Asteria.
“Basi sawa.
Naomba namba zao!” Akatumiwa namba hizo. Mwili wake ulikuwa ukiwasha mno, kila alipokaa, akili yake ilikuwa ikifikiria pesa tu. Hakutaka kuona akiishi maisha ya kimasikini, alijitoa maishani mwake, hapokuwa alikuwa akifanya jambo gumu, lenye kujidharirisha lakini hakuwa na jinsi, hayo yalikuwa maisha ambayo aliyachagua na alipaswa kuishi katika maisha hayohayo.
Walipofika Dubai, wakateremka ndani ya ndege, haikuwa mara yake ya kwanza, alikwishawahi kufika mara kadhaa hapo, wakatoka nje na kuchukua gari kisha kuelekea hotelini. Walipofika huko, ilikuwa ni kujiachia tu, walikuwa wakiyafurahia maisha, Godfrey alisahau kama alikuwa na mke, kwake, mwanaume huyo tata alimridhisha mno.