SEHEMU YA 22
Hali ilibadilika, mapenzi ya Godfrey kwa mkewe yakapungua, hakutaka kuwa naye karibu kama ilivyokuwa siku za nyuma, mapenzi yalikuwa kwa mwanaume tata ambaye alikutana naye ufukweni.
Walikuwa wakiwasiliana kama kawaida, mara kwa mara walikutana na hata alipokuwa akienda safari zake za Ulaya, Marekani na nchi nyingine alikuwa akiongozana naye ambapo huko uchafu wao uliendelea.
Fareed aliendelea kufanya mambo yake kama kawaida, alimpenda sana Godfrey, alimpa kila kitu alichotaka lakini siku zote alitamani kutembea na wanaume wengine. Aliijua dunia, alijua nchi zilizokuwa na wanaume tata wengi, watumiaji wa watu hao na hata alipokwenda huko, wakati mwingine alikuwa akimtoroka Godfrey na kujiunga na wenzake kufanya ufuska.
Siku ziliendelea kukatika, walipokuwa wakirudi nchini Tanzania, halikuwa jambo la ajabu kumuona Godfrey akiondoka nyumbani na kurudi baada ya siku tatu. Kila alipokuwa akiulizwa, alikuwa mkali, aligombana na mkewe kisa tu alihisiwa kulala na wanawake wengine.
Mkewe akaanza kupeleleza, aliamini kwamba kwa namna moja au nyingine ilikuwa ni lazima kuwe na mwanamke aliyekuwa akimzuzua mume wake hivyo kumfuatilia.
Alifuatilia kwa kuchukua simu yake nyakati za usiku na kuangalia meseji mbalimbali, hakuweza kugundua, hakuacha, aliendelea kufuatilia watu aliokuwa akiwasiliana nao, wengi walikuwa wanaume lakini kulikuwa na mwanaume mmoja ndiye aliyekuwa akiwasiliana naye sana, huyu aliitwa Fareed.
Mara ya kwanza akahisi kwamba alikuwa msichana aliyembadilisha jina, akaangalia katika mtandao wa simu kwenye huduma ya kifedha kugundua kama hilo lilikuwa jina lake au mumewe alimfanyia mchezo, alipoangalia, akakutana na jina hilohilo, Fareed Hassan.
Hakuwa na hofu na mwanaume huyo, aliendelea kutafuta lakini hakumfuma mumewe kuwa na uhusiano wa siri na mwanamke mwingine. Akauachia moyo wake kumwamini mwanaume huyo, akajiondoa hofu, akaona kwamba kila alipokuwa akiambiwa kwamba alikuwa bize na mambo ya biashara, kweli alikuwa bize.