SEHEMU YA 33
Bilionea Keith hakuamini, alimwangalia vizuri Fareed, ilikuwa vigumu kufahamu kama mtu huyo alikuwa mwanaume, alionekana kukamilika kama mwanamke kamili. Hakutaka kumganda sana, akaendelea kufanya mambo yake na usiku wa siku iliyofauata, sherehe ikaanza kufanyika katika ukumbi wa Hoteli hiyo.
Huo ndiyo ulikuwa mwanzo wa wawili hao kuonana, wakabadilishana namba za simu na kuanza kuwasiliana. Bilionea Keith hakuwa na hofu na Fareed, kwake alikuwa rafiki yake mkubwa, alimsaidia kama rafiki yake na wakati mwingine alimuita mpaka Marekani kwa ajili ya kumtembelea.
Hakufanya naye kitu, kila alipokuwa akimuhoji kwa lengo la kutaka kujua mambo mengi zaidi, hasa kuhusu uhusiano, mwanaume huyo hakumficha, alimwambia kwamba alikuwa kwenye uhusiano na mwanaume mwingine aliyeitwa kwa jina la Godfrey.
“Ni mwanaume mwenye bahati sana,” alisema Keith.
“Kwa nini?”
“Kumpata mrembo kama wewe.”
“Kwani mimi mrembo?”
“Hujioni? Nenda kachukue kioo halafu jiangalie,” alisema Keith huku akimwangalia Fareed.
“Hapana!”
“Niamini!”
Safari zake za kutafuta wanaume hazikuisha, aliendelea kuizunguka dunia, kila alipoambiwa na wakala wake kwamba kulikuwa na mwanaume aliyekuwa akimtaka, alikwenda huko, alizunguka sehemu mbalimbali na hakutaka kabisa Godfrey ajue kile kilichokuwa kikiendelea katika maisha yake.
“Upo wapi Fareed,” aliuliza Keith kupitia ujumbe mfupi kwenye Mtandao wa WhatsApp.
“Ubelgiji!”
“Nahitaji nikuone.”
“Lini?”
“Hata kesho!”
“Mh! Mbona haraka hivyo?”
“Kwa sbabu nimekumisi.”
“Basi naomba tufanye wiki ijayo. Nitakuja tu rafiki yangu,” alisema Fareed.
“Basi sawa. Nakusubiri kwa hamu!”
“Kuna nini lakini?”
“Hakuna kitu! Nataka nikuone tu.”
“Mmh! Sawa,” alisema Fareed na kukata simu, hakuamini kama kulikuwa na kitu cha kawaida, alijua kabisa kwamba kulikuwa na kitu mwanaume huyo alikuwa akikihitaji kutoka kwake. Hivyo akajiandaa.