SEHEMU YA 30
Alikuwa mzuri wa sura, msafi, mwenye umbo maridhawa na sauti ya kuvutia. Alipoambiwa kwamba na huyo alikuwa mmoja wa wanaume tata waliotaka awe wakala wake, alichanganyikiwa kwani aliamini kwamba angepata kiasi kikubwa cha fedha kama tu angekubaliana naye na kuingia mkataba.
Wakakaa chini na kuzungumza, halikuwa tatizo, alitaka kupanua biashara yake hivyo akasaini naye mkataba na ndiye alikuwa mtu wa kwanza kufikiriwa kila dili la nje lilipokuwa likifika mezani kwake.
Akaanza kumnadi kwa wateja wake, akawatumia picha kwa kuwaambia kwamba mali mpya iliwasili, kila aliyemuona, alichanganyikiwa, hawakuamini kama kungekuwa na mtoto mashalaah kama alivyokuwa Fareed.
“How much?” (kiasi gani?) aliuliza mwanaume aliyekuwa akiishi Qatar.
“Three thousand dollars?” (dola elfu tatu)
“I want her,” (namuhitaji)
Hiyo ndiyo biashara iliyokuwa ikifanyika, Asteria aliendelea kutengeneza utajiri, serikali haikumgundua kile alichokuwa akikifanya. Wale waliopata hela, wakawaambia wenzao na hatimaye idadi ya wanaume tata ikazidi kuongezeka nchini Tanzania, hasa katika Jiji la Dar es Salaam.
Asteria aliijua biashara ya uwakala, alijitoa, alihangaika huku na kule kuwatafuta wateja, alikuwa akiwapata na malipo kufanyika. Mpaka kipindi hicho, Fareed alikuwa amekwenda nchini nyingi, hasa za Uarabuni ambapo matendo hayo yalishamiri kwa kiasi kikubwa sana.
Baada ya miezi kadhaa, Asteria akampata bilionea Saed na kumwambia kuhusu Fareed. Mwarabu huyo alichanganyikiwa zaidi baada ya kutumiwa picha. Akapata uroho, udenda ukamtoka na kuhitaji kuwasiliana naye.
Walifanya yao na siku chache mbele, wakala huyo akapokea simu kutoka nchini Marekani, kwa Bilionea Cotton Keith ambaye alimwambia kwamba alisikia mambo mengi kuhusu yeye hivyo alihitaji msichana.
“Msichana?” aliuliza Bi Asteria.
“Ndiyo!”
“Sawa. Una dola elfu tano?”
“Swali la kitoto sana hilo. Unajua unazungumza na nani?” aliuliza bilionea huyo.
“Hapana!”
“Hebu angalia Google jina la Cotton Keith,” alisikika mwanaume huyo na kukata simu.
Je, nini kitaendelea?