Mara nyingi nimekuwa nikisema kuwa nchi hii ina wananchi wanaopenda na kushabikia uongo na uzushi bila hata kujipa muda wa kufanya uchunguzi kidogo wa mambo wanayoelezwa na kiongozi ama wa serikali au wa siasa, na hasa mtu huyo akiitwa Profesa au Dokta, au akisema ana elimu ya chuo kikuu ya shahada au shahada ya uzamili (masters). Watanzania wanadanganyika na makaratasi ya chuo yanayoitwa shahada. wanaamini mtu mwenye shahada basi anajua kila kitu na msema ukweli, kumbe wapi, hao ndiyo wezi wakubwa wa rasilimali za nchi yetu. Huyu waziri anayeitwa muhogo sijui muhongo ni kibaraka mkubwa wa wazungu, ni mtumwa wa wazungu ambaye hatamani hata uhuru, yeye anamwamini mzungu kuliko hata baba na mama yake, anatamani angezaliwa na baba na mama wazungu, shame on him! Huyu waziri tangu ateuliwe kushika wizara hiyo kazi yake ni moja tu, kuwapiga vita wafanyabiashara wazawa, kuwapiga vita watanzania wanaojishughulisha kukuza uchumi wao na wa nchi, kazi yake kuwashambulia na kuwazuia wazawa kushiriki katika kujenga uchumi wa nchi yao, anawazuia watanzania kunufaika na rasilimali za nchi yao, anataka kila kitu wamiliki wageni, mabwana zake wazungu, huyu si adui wa Reginald Mengi pekee bali ni adui wa wafanyabiashara wote wazawa, ni adui wa watanzania wote wazawa, na anapaswa kupigwa vita na kila mtanzania mzawa mpaka atakapobadili mtazamo wako dhidi ya watanzania wenzake au mpaka atakapoondolewa katika utumishi wa umma. Mimi kwa upande wangu kama mwandishi wa habari, mwaka huu niliandika makala ya kumsema huyu waziri ikiwa ni mchango wangu wa kuhakikisha hili joka tunalitimua katika nyumba yetu, nimeamua kuiweka makala hii ndani ya JF ili watanzania wenzangu wenye mapenzi mema na nchi yetu wachangie. ............................................................................................................................................................................. WAZIRI wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo ametutukana na kutudhalilisha Watanzania. Amesema eti sisi hatuna haki wala hatustahili kushirikishwa katika kujua na kuamua sera na hata kupatiwa fursa ya kumiliki miradi ya gesi yetu kwa kile alichodai kuwa hatuna uwezo wa kuivuna. Amesema eti sisi ni hohehahe ambao uwezo wetu hauruhusu kupewa fursa ya kufanya biashara ya kuwekeza katika gesi, bali tunaweza kujihusisha na biashara za soda, juisi, machungwa, maembe, mapeasi na uchuuzi mwingine usiohitaji mitaji mikubwa. Matusi hayo ya Profesa Muhongo dhidi ya Watanzania ameyatoa kupitia kwa mfanyabiashara mzalendo Reginald Mengi. Matusi na udhalilishaji huo dhidi ya Mengi vilikuja baada ya mfanyabiashara huyo mwenye mapenzi ya dhati kwa Watanzania na taifa kwa ujumla kuitaka serikali kusitisha zoezi la kugawa vitalu vya gesi hadi pale sera ya taifa ya gesi itakapokuwa tayari imeandaliwa. Mengi alikuwa akitoa rai hiyo kwa serikali kwa niaba ya Taasisi ya sekta binafsi nchini (Tanzania Private Sector Foundation TPSF) ambayo yeye ni mwenyekiti wake. Katika maoni yake, TPSF ilisisitiza umuhimu wa ushirikishwaji wa Watanzania katika uchumi wa gesi na kuishauri serikali kusitisha ugawaji wa vitalu vya gesi hadi sera ya gesi itakapokuwa tayari na taasisi hiyo iliomba kukutana na Waziri Muhongo kwa mashauriano zaidi. Katika kumdhalilisha zaidi Mengi, Waziri Muhongo amediriki kumuita kuwa si mzawa wa kweli bali ni mbinafsi, dalali, na mlanguzi wa rasilimali za Watanzania. Waziri Muhongo amedai kuwa Mengi na kundi lake wanataka vitalu ili wafanye ulanguzi wa gesi na mafuta ya Watanzania. Kama nilivyotangulia kusema hapo juu, kwamba matusi na dharau za Waziri Muhongo havikumlenga Mengi tu, bali Watanzania wote. Kwamba, mtazamo wa Waziri Muhongo ni juu ya Watanzania wote, ndiyo maana akasema: Watanzania uwezo wao ni biashara za soda, juisi na maembe, siyo gesi wala mafuta. Hebu jiulize Mtanzania mwenye akili sawa sawa, hivi kama Mengi katukanwa na kudharauliwa kwa kiwango hicho, nani kabakizwa? Hivi kama waziri hawezi kumheshimu Mengi, ataweza kweli kumheshimu babu na bibi zangu wanaolima kule kijijini kwetu kwa kutumia jembe la mkono? Hivi Waziri Muhongo atawaheshimu kweli wamachinga wanaoshinda kutwa nzima wakitembea jiji lote la Dar es Salaam wakitembeza mashati mawili? Waziri Muhongo anawaheshimu, kuwanyenyekea, kuwaabudu wageni wanaokuja hapa nchini kwa koti la wawekezaji, huku wakiwa hawana chochote, lakini hutajirika ghafla kwa kutumia rasilimali zetu. Mtazamo wa Waziri Muhongo ni kwamba uwekezaji mkubwa ukiwemo ule wa sekta ya gesi, mafuta, dhahabu, almasi na vingine hauwezi kufanywa na Watanzania wazawa. Kwamba hiyo ni biashara ya Wazungu, Wachina au Wahindi. Waziri Muhongo hawaamini waswahili wenzake, anawaona wababaishaji, madalali na walanguzi! Waziri Muhongo hayuko pekee yake katika mtazamo huu. Baadhi ya viongozi katika serikali, katika chama tawala na hata katika chombo cha kutunga sheria, yaani Bunge, wamekuwa watetezi wakubwa wa wafanyabiashara wageni. Kibaya zaidi, baadhi ya viongozi wamekuwa wakitumiwa na baadhi ya wafanyabiashara wa kigeni kuwakwamisha wafanyabiashara wazawa. Wamo watu ndani ya serikali yetu, Bunge na chama tawala (CCM) ambao ni mawakala wa wageni hawa. Wanawapa kandarasi mbalimbali za mabilioni ya fedha na kuwanyima Watanzania wazawa. Wakati mwingine baadhi ya wabunge wanatumwa kwenda bungeni kuwashambulia wafanyabiashara wazawa kwa lengo la kuwakwamisha. Nimeambiwa hata baadhi ya taasisi za fedha nchini kama benki nazo zimekuwa zikitumiwa na wafanyabiashara wageni kuwakwamisha wazawa kwa kuwanyima mikopo au kuwawekea mazingira magumu ya kuipata. Ikumbukwe kuwa hakuna benki hata moja nchini inayomilikiwa na wazawa, nyingi ni za wageni. Waziri Muhongo na viongozi wengine wa serikali wenye mtazamo hasi dhidi ya Watanzania wazawa wanapaswa kujua kuwa hao wafanyabiashara wa kigeni siyo matajiri kiasi hicho, bali huwezeshwa na serikali zao kuja kuwekeza hapa kwetu kwa kupewa dhamana ya mikopo katika mabenki ya kwao. Makampuni yote yaliyowekeza leo katika sekta ya madini nchini yamekopa mabilioni ya dola katika mabenki ya kwao kwa dhamana ya serikali zao. Hata hayo makampuni yanayoomba vitalu vya gesi na mafuta pia yamekopa huko kwao. Hakuna kampuni inayoweza kuja hapa kuwekeza bila kukopa, haiwezekani. Na hapa ndipo hoja ya waziri wa zamani wa viwanda na biashara, Idd Simba ya kutaka uanzishwe utaratibu wa kisera na kisheria wa kuwawezesha Watanzania wazawa kibiashara inapopata nguvu. Simba alianzisha hoja hiyo kutokana na ukweli usiopingika, kwamba mfumo wa kiuchumi wa kikoloni uliwapendelea Wazungu, Wahindi na Waarabu kwa kuwapa fursa za kufanya biashara zote kubwa na kuwaacha pembezoni wenye nchi. Hata hivyo, hoja ya Simba ilipata upinzani kutoka kwa wafanyabiashara wenye asili ya kigeni pamoja na mawakala wao, hususan wanasiasa watawala wenye mtazamo kama wa Waziri Muhongo, ambao kwa kiasi kikubwa wananufaika na mfumo wa sasa. Hoja iliyokuwa ikitolewa na wapinzani wa mtazamo wa Simba ni kwamba kuanzisha upendeleo maalumu wa kiuchumi kwa jamii fulani ya watu katika nchi kwa kuzingatia rangi au tofauti nyingine yoyote, ni tangazo la wazi la sera ya ubaguzi, jambo walilosema ni kinyume cha katiba na sera ya nchi yetu. Hata hivyo, naamini kuwa Simba alikuwa na hoja nzito iliyopaswa kufanyiwa kazi, si hoja ya kubishaniwa kwamba umaskini unaowakabili Watanzania wengi wazawa si wa bahati mbaya, bali ni wa kutengenezwa. Mfumo wa kiuchumi wa watawala wa kikoloni uliwabagua Waswahili na kuwapendelea Wazungu, Wahindi na Waarabu. Wakati wa ukoloni, biashara zote kubwa zilimilikiwa na Wazungu na zile za kati zilikuwa mikononi mwa Wahindi na Waarabu. Kwa mfano, viwanda na mashamba makubwa vyote vilikuwa vikimilikiwa na wafanyabiashara wa Kizungu na serikali ya kikoloni iliwapa kila aina ya msaada ikiwamo ruzuku ili kuwawezesha kupata mafanikio ya kiuchumi, hivyo kuwasaidia kututawala. Wahindi na Waarabu nao walipewa fursa ya kufanya biashara zote za kati na kupata mafanikio ya kiuchumi kwa sababu wakoloni hawakuwa na hofu yoyote ya kuhatarisha utawala wao kwani walijua wazi kuwa hawakuwa wenyeji wa Tanganyika, hivyo wasingejihusisha na harakati zozote za kupinga utawala wao. Wakoloni waliwatenga wazee wetu na mfumo wa kiuchumi kwa hofu kuwa kama wangepata nguvu za kiuchumi wangeanzisha harakati za kisiasa za kupinga kutawaliwa na wageni, hivyo kuhatarisha mamlaka yao ya kuendelea kuwatawala na kuwanyonya Watanganyika. Matokeo yake, leo hii uchumi wa nchi unadhibitiwa na wageni. Biashara zote kubwa hapa nchini zinamilikiwa na wageni. Angalia orodha ya matajiri zaidi ya 10 nchini iliyotolewa hivi karibuni ambayo Waswahili ni wawili tu. Kwahiyo, ni hoja yenye mashiko leo kutaka kuanzishwa kwa mfumo wa kisera na kisheria wa kutoa upendeleo maalumu wa kiuchumi kwa wazalendo, kwa lengo la kurekebisha dhambi ya ubaguzi waliyotendewa wazee wetu wakati wa ukoloni, ambayo madhara yake yanaendelea hadi sasa. Kukataa hoja hii ni kujifanya vipofu wa ukweli, huko ni sawa na kuendeleza ubaguzi wa wakati wa ukoloni, ni mwendelezo wa kuwazuia na kuwatenga na mfumo wa kiuchumi Watanzania weusi ambao ndio wengi nchini, jambo ambalo ni hatari kwa amani ya taifa. Mwaka 1994, serikali ya kizalendo ya Chama cha African National Congress (ANC) ilichagua kutekeleza sheria ya affirmative action kwa lengo la kurekebisha ubaguzi wa zamani. mwisho.