Verily Verily na Mkandara, Nafurahia michango yenu. Wakati naendelea kutafakari juu ya changamoto mlizo toa, na post makala ya BW. Masinde(MwanaCHADEMA) ambayo inatoa uchambuzi wa kina wa sera ya Majimbo.
Tembelea:
http://www.chadema.net/nyaraka/sera/majimbo1.php
WATANZANIA TUKUBALI KUWA KUNAHITAJIKA KUWEPO MABADILIKO KATIKA MFUMO NA MUUNDO WA TAWALA ZA MIKOA!
TUONDOKANE NA MAZOEA TU
Mheshimiwa Sylvester K. Masinde anafafanua Sera ya Utawala wa Majimbo na kutoa mtazamo wake juu ya Sera hii baada ya kufuatilia kwa makini malengo ya Chama na maoni ya Watanzania.
Miaka 44 sasa baada ya nchi yetu kuwa huru, hatuna haja wala ulazima wa kuendelea kukumbatia mfumo na muundo wa Tawala za Mikoa tuliorithi kutoka kwa wakoloni. Ni muundo wa kuwa na mamlaka (Rulership) juu ya watu kama ilivyokuwa wakati wa Tanganyika ya Ukoloni. Utawala wetu sasa unatakiwa kuwa wa kuongoza watu (Leadership).
Nyakati za mfumo wa siasa za Chama Kimoja na Dhana ya Chama kushika hatamu za utawala wa nchi, muundo wa tawala za mikoa uliendelezwa kwa maslahi ya kiitikiadi. Wakati huu wa zama na udikiteta wa kisiasa, muundo huu ulitumika kuunganisha mamlaka na madaraka ya utawala na shughuli za chama. Kwa ajili hii chama kiliweza kudhibiti Nguvu ya Umma kwa kuwanyima watu fursa ya kupata na kujua maoni na mitazamo tofauti ya kisiasa. Chama kilichukua nafasi ya kuwa kiunganishi cha jamii ya Watanzania badala ya serikali. Serikali ilifanywa chombo cha kutumiwa na chama badala ya kuwa chombo cha watu, raia huru wa nchi.
Leo CCM na Serikali zake vinatetea na kuukumbatia mfumo na muundo huu kwa maslahi ya kisiasa tu na siyo kwa sababu ya ufanisi wa kuwaendeleza wananchi kimaisha. Mkuu wa Mkoa na Mkuu wa Wilaya kama watu binafsi hawawezi kuwaendeleza watu zaidi ya kuwatawala.
Serikali za Mitaa na siyo Tawala za Mikoa ndilo jibu sahihi katika kuleta ufanisi wa kuwaendeleza Watanzania. Wakuu wa Mkoa na Wakuu wa Wilaya wako na wanajishughulisha zaidi na maslahi ya kisiasa ya chama chao na ndio maana uteuzi wao ni wa kiitikadi zaidi ya taaluma, ujuzi na uzoefu wa maswala ya utawala. Ni vema ikumbukwe kuwa Wakuu wa Mikoa na Wilaya ndiyo nguzo za kuwezesha CCM kushinda uchaguzi. CCM na Serikali zake hawako tayari kuzifanya nyadhifa hizi kuwa za kitendaji katika utumishi Serikalini. Hii ni kwa sababu wanaogopa kupoteza nguvu hii kubwa ya kisiasa.
MANENO JIMBO NA MKOA
Maneno Jimbo na Mkoa kimsingi yana maana moja. Yote yana maana ya eneo katika mgawanyo wa nchi kwa ajili ya uendeshaji wa shughuli za Serikali/utawala. Maneno haya yanatumika kwa kubadilishana (Interchangeably).
Katika lugha ya kiingereza neno Jimbo lina tafsiri ya Province na neno Mkoa lina tafsiri ya Region lakini kiutawala yote yana maana ya aina moja ile ile ya eneo la kiutawala. Wakati Tanganyika (Tanzania Bara) inapata uhuru, neno Jimbo ndilo lilikuwa linatumika na Tanganyika ilikuwa imegawanywa katika majimbo nane. Neno Jimbo lilibadilishwa baada ya uhuru na neno Mkoa. Huenda kubadilisha matumizi ya neno Jimbo kuwa Mkoa ulikuwa uamuzi wa kisiasa tu ili kuondoa fikra za utawala wa kikoloni. Kwa bahati mbaya kubadili neno Jimbo kuwa Mkoa hakukuenenda na mabadiliko ya misingi ya utawala wenyewe, yaani misingi ya mamlaka juu ya jamii chini ya mtu mmoja. Hiyo mtu anaweza kutumia Tawala za Mikoa au Tawala za Majimbo kwa maana moja ile ile.
UONGOZI DHIDI YA UTAWALA
Kabla ya kujadili misingi na malengo ya dhana ya Uongozi wa Kijimbo dhidi ya Tawala za Mikoa ni budi tuelewe tofauti ya kuongoza na kutawala. Kuwatawala watu au jamii fulani ya watu kunaweza kutokana ama kutotokana na ridhaa ya watu hao. Lakini kuwaongoza watu au jamii wakati wote kunahitaji na kunatokana na ridhaa ya aina fulani ya watu husika.
Machifu wetu na wakoloni walitutawala bila ridhaa yetu. Majeshi yanapotumia nguvu ya mtutu wa bunduki kushika mamlaka na madaraka ya kuendesha nchi hayapati kwanza ridhaa ya watu. Husimika utawala wa kijeshi bila ridhaa ya watu. Gavana wa Kiingereza na Makamishena wa Majimbo yake manane ya Tanganyika walikuwa watawala wa Watanganyika kwa niaba ya mamlaka ya utawala wa Uingereza, utawala wa Kifalme.
Kutawala, kimsingi, ni kuwa na mamlaka na madaraka juu ya watu wengine hata kama watu hao hawahiari hivyo. Utawala ni kuwa na madaraka juu ya jamii na mtawala anaweza kuwa mtu binafsi au kundi la watu. Kwa lugha ya kiingereza utawala wa aina hii ni Rulership, Lakini neno utawala linatumika pia kwa maana ya uendeshaji (Administration). Ndiyo maana sheria ya Tawala za Mikoa kwa kiingereza inaitwa Regional Government Administration Act".
Kwa upande mwingine, neno Uongozi unatokana na ridhaa ya watu au jamii husika. Mamlaka na madaraka ya kiongozi yanatokana na ridhaa ya watu/jamii moja kwa moja ama kupitia uwakilishi wao. Watawala wa aina ya Rulership huendesha mambo kwa kutumia zaidi sheria na kanuni walizoziweka wao wenyewe. Lakini viongozi watawala huendesha mambo kwa kutumia sheria na kanuni zilizowekwa na jamii yenyewe kwa utaratibu maalumu, uliokubalika.
Tanzania ni nchi inayofuata misingi ya kidemokrasia. Kwa mantiki hii Watanzania wanaongozwa, hawatawaliwi tena.
Rais wetu ni Kiongozi Mkuu wa Nchi, siyo Mtawala Mkuu kama alivyokuwa Gavana wa Kiingereza. Hii ni kwa sababu Rais anatokana na ridhaa ya Watanzania kupitia uchaguzi wa kidemokrasia. Rais wetu ana kofia mbili za uongozi. Ana uongozi wa kisiasa (Government Political Leadership) na ana uongozi wa uendeshaji Serikali (Government Administration Leadership).
Katika kuendesha uongozi wa nchi na watu wake, Rais huteua timu kuu mbili za kumsaidia. Timu ya kwanza inapewa jukumu la uongozi wa kisiasa. Timu hii ni Baraza la Mawaziri. Timu ya pili inapewa jukumu la uongozi wa uendeshaji shughuli za serikali. Hawa ni Makatibu Wakuu wa Wizara, Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama, Wakuu wa Idara na Wakala Kuu za Serikali zinazojitegemea/zinazojiendesha na Maafisa wengine waandamizi kama Makamishna na Wakurugenzi katika utumishi wa Serikali.
Baraza la Mawaziri huteuliwa kutoka miongoni mwa wabunge ambao wana ridhaa ya jamii kupitia uchaguzi. Rais pia ana ridhaa ya kuteua watu kuwa Wabunge na kisha kuwapa dhamana ya Uwaziri. Rais hufanya hivyo kwa kutumia mamlaka aliyopewa kikatiba na kisheria kupitia Bunge, chombo kinachotegemewa kuwakilisha sauti ya watu.
Rais anategemewa kuteua viongozi wa uendeshaji wa shughuli za Serikali kutoka miongoni mwa Watanzania walio katika utumishi wa umma kwa kuzingatia taaluma zao, uzoefu na ujuzi wao na uadilifu wao katika jamii na katika utumishi wa umma.
Kwa hiyo kimsingi mfumo wa uendeshaji shughuli za nchi yetu ni wa Ki-uongozi na siyo kwa Ki-utawala; Vivyo hivyo Mikoani kunahitajika kuwepo uendeshaji wa ki-uongozi badala ya utawala wa Wakuu wa Mikoa na wa Wilaya.
UKAMISHNA WA MAJIMBO NA WILAYA WAKATI WA UKOLONI NA
UKUU WA MKOA NA WILAYA WA LEO
Makamishna wa majimbo na wilaya waliteuliwa na mamlaka ya utawala wa Uingereza kupitia Ofisi ya makoloni. Makamishna wa majimbo waliwajibika kiutendaji kwa Gavana. Makamishna wa majimbo walikuwa na mamlaka na madaraka ya kisiasa, ya kiuendeshaji/kiutendaji, ya kipolisi na hata ya kimahakama. Walikuwa watawala wa kweli kweli.
Wakuu wa Mikoa wanateuliwa na Rais. Kiutendaji wanawajibika kwa Rais kupitia Waziri Mkuu. Kama walivyokuwa Makamishna wa Majimbo, Wakuu wa Mikoa pia wana mamlaka na madaraka ya kisiasa na kiuendeshaji/kitendaji na ya kipolisi (kama kutoa amri mtu kukamatwa na kushtakiwa) ila hawana madaraka ya kimahakama tu. Kwa hiyo nao ni watawala tu siyo viongozi.
Kama alivyo Waziri kwa Wizara yake ndivyo alivyo pia Mkuu wa Mkoa kwa Mkoa wake. Wote wanamwakilisha Rais katika maswala ya kisiasa na ya uendeshaji shughuli za Serikali. Lakini tofauti na Waziri, Mkuu wa mkoa hatokani na ridhaa ya wananchi kupitia uchaguzi wa kidemokrasia. Hii ndiyo kasoro ya kwanza kubwa na ya msingi sana inayokusudiwa kuzibwa na Dhana ya Uongozi wa Kijimbo.
UTAWALA WA KIJIMBO NA TAWALA ZA MIKOA
DHIDI YA SERIKALI ZA MITAA
Serikali za mitaa zilikuwapo hata kabla na wakati wa ukoloni. Wakoloni wa Kijerumani walikuta tawala za Jadi nchini Tanganyika. Hawakuziamini na kwa hiyo wakaweka mawakala wao walioitwa MAAKIDA.
Baada ya vita kuu ya kwanza ya Dunia, wakoloni wa kiingereza walichukua nafasi ya Wajerumani. Lakini tofauti na Wajerumani, wao walizitambua Tawala za Jadi za Machifu. Wakoloni hawa wa Kiingereza walithubutu hata kusimika machifu wa Jadi pale ambapo hawakuwepo. Mwaka 1926, Gavana Donald Cameron aliyetawala Tanganyika kati ya mwaka 1925 na 1931 alipitisha sheria ya Mamlaka ya Wenyeji (SURA YA 72). Mnamo mwaka 1947, kutokana na vuguvugu za kudai uhuru zilizoendeshwa na waafrika waliorejea kutoka vitani, Waziri wa makoloni wa Serikali ya Kiingereza, Bw. A. Creech Jones, alitoa waraka maalum kwa magavana wa kiingereza na kuwaagiza waanzishe mfumo wa kidemokrasia wa Tawala za Serikali za Mitaa katika makoloni yao. Kwa kuzingatia waraka huo mnamo mwaka 1950 Gavana wa Tanganyika aliifanyia marekebisho sheria ya mamlaka ya wenyeji ya mwaka 1926, marekebisho ambayo yaliunda MABARAZA YA MACHIFU kama mamlaka ya kuwashauri wakuu wa majimbo na Wilaya.
Mamlaka hizi za Mabaraza ya Machifu zilipewa kibali cha kutumia mapato yao kwa shughuli za utawala, maendeleo na ustawi wa Jamii. Kamati za Fedha ziliundwa kusimamia mapato na matumizi ya mamlaka hizo.
Mwaka 1953, sheria ya serikali za mitaa (sura ya 333) ilipitishwa kwa kufuta sheria ya Mamlaka ya wenyeji (Sura ya 72) ya 1926 na kuanzisha Halmashauri za Serikali za Mitaa zenye madaraka kamili ya utendaji juu ya watu ndani ya maeneo yake. Sheria hii ilianzisha pia utaratibu wa uchaguzi wa madiwani na kutoa uhuru zaidi wa utendaji kwa Halmashauri zilizoundwa.
Kwa hiyo chimbuko la Tawala za Serikali za mitaa za sasa ni Serikali za aina hiyo za wakati wa ukoloni.
Kuwepo kwa makamishna wa mikoa na wilaya wakati wa ukoloni kama wawakilishi wa utawala wa kikoloni chini ya Gavana, lilitokana na wakoloni kutowaamini wenyeji kujiongoza. Kwa hiyo Tawala hizi za Serikali za Mitaa ziliwajibika kwa wakuu wa majimbo na wilaya. Hata sisi leo bado wakuu wa mikoa na wa wilaya wamepewa mamlaka na madaraka fulani juu ya Serikali za Mitaa. Tumeendeleza mtazamo huo huo wa kikoloni wa kutokuwaamini wananchi kujiongoza. Hii ni kasoro kubwa ya pili ya mfumo wa Tawala za Mikoa.
Leo Watanzania ni watu huru. Serikali za Mitaa na watu chini ya Mamlaka hizi ni sehemu ya Jamii ya Tanzania huru. Ni kweli kuwa uendashaji na utendaji wa Serikali za mitaa vinahitaji kuratibiwa na kudhibitiwa kwa kiasi fulani na Serikali Kuu. Lakini hii haihalalishi kuendeleza mfumo wa Tawala za Mikoa wa enzi za ukoloni kama ulivyo sasa. Uratibu na udhibiti unaweza kuendeshwa bila ya kuwa na Ofisi za Wakuu wa Mikoa na Wilaya katika mfumo wa sasa. Rais siyo mtawala kama Gavana wa Kiingereza na Serikali ya Muungano wa Tanzania siyo sawa na Serikali ya Mfalme wa Kiingereza iliyoitawala Tanganyika. Uongozi wa Kitaifa na ule wa Serikali za mitaa unatokana na jamii ile ile ya Watanzania katika mtandao wao Mkoani na Wilayani.