Maisha bana yana
raha yake na karaha zake, kwenye ujana nako kuna mambo haya pia.
Leo nimekutana na mtu ambae alinisababisha nikakumbuka mbali
sana,nimekutana na binti mmoja ambae alinipa "wehu sana" miaka hiyo ya
2000.
Binti huyu nilimpenda" sana, wakati huo nilikuwa mwoga kiasi kwa wadada
lakini huyu nilijikuta namvagaa na kumweleza shida yangu, wakati huo
alikuwa anasoma kidato cha 5, aliniambia atafikiria na atakuja kunipa
jibu.
Nilikaa huku kiroho kikinidunda kusubiria jibu, kwa namna nilivyokuwa
siwajui wadada kwa kipindi kile nilijidanganya kuwa kweli atakuja kunipa
jibu, nilisubiri sana huku nikijipitisha pale kwao na kumsalimia bila
kuuliza chochote nikitarajia atakuja kuniambia mwenyewe.
Ulipita mwezi mmoja kimya, kuna jamaa yangu akanishauri nimvagae kwenda
kumuuliza, kiukweli mimi kwa tabia nina aibu kwenye kufa hamna jambo
ambalo litaonekana sio la kistaarabu, nilijifikiria sana kuhusiana na
jambo hili na nikajipa wiki na kusema kama hatanijibu basi namvagaa,
wakati huu alikuwa akimuagiza mara kwa mara rafiki yake shida ya fedha
mara kwa mara na mimi nilikuwa natoa, si nilipenda bana?
Wiki ilikatika bila majibu yoyote yale, niliamua kumuandikia kabarua
kwasababu wakati huo sikuwa na simu ya mkononi kwani zilikuwa ndio
zinaingia ingia na zilikuwa ghali kweli kweli, baada ya kuandika
nilimuagiza rafiki yake ampelekee, kesho yake nilipokutana na huyu
rafiki yake baada ya kutoka shule nilimuuliza na aliniambia kuwa alimpa
na hakumjibu chochote hata baada ya kusoma.
Nilijiuliza na niliona kama hanitaki hivi, sikujisikia vizuri kwa kweli
nakumbuka kuanzia siku hiyo nilikuwa napata hamu ya kula kwa taabu sana,
ulipita muda huku nikiteseka kwa penzi la huyu dada na ilifikia wakati
nikawa silali kabisa kwa kukosa usingizi, maisha yalikuwa magumu sana na
siku moja niliamua kumfuata ili nijue hatma yangu.
Nilimkuta akipika kwao na nilimuita na hakuja wala hakunijibu chochote,
roho iliniuma sana na nakumbuka hadi nililia siku hiyo nilipofika
nyumbani, nakumbuka kaka yangu aliniuliza kulikoni na nilimuambia na
alinicheka sana, aliniambia kama mwanamke hanitaki si niachane nae?
Nilimwambia kuwa nampenda na hakunielewa na aliniambia kuwa nitakuja
kufa kwa sababu ya mapenzi.
Nilikonda kwa kweli, muda uliendelea kupita na hali yangu kiafya na
kifikra haikuwa nzuri kwa kweli, siku moja niliamua kumvaa wakati
anatoka shule na kumuuliza kulikoni na aliniambia ataniandikia ujumbe na
atamtuma yule rafiki yake,kidogo nilifarijika kwasababu alinijibu
vizuri.
Baada ya kuniambia hivyo nilihisi na njaa maana sikuwa hata nasikia njaa
kwa mawazo, nilikwenda kula na nilirudi nyumbani na kusubiri majibu,
muda wa saa moja usiku ulifika na niliona yule rafiki yake akija na
kijibahasha, nilijipa matumaini kuwa huenda nimetunukiwa "dhahabu".
Nilichokikuta humo yalikuwa ni majonzi tu, kwa kifupi binti huyu
aliniambia kuwa ana mtu na hana kabisa mpango na mimi na nikiendelea
kumfuatilia atamuambia huyo jamaa yake ili aninyooshe, kiukweli mimi
huwa sipendi mavurugu, nilinyong'onyea na nilihuzunika sana siku hiyo,
nakumbuka sikuweza kula vizuri kwa mwezi mmoja na nilipata ugumu sana
kwenye shughuli zangu za kila siku kwa mwezi mzima ule.
Lakini nashukuru sana kwani kwa tukio hili na mengine nilikuja kujifunza
mengi sana kuhusiana na hawa wadada kwani ni viumbe wa kustaajabisha
sana kwa asiewajua hasa hawa wavulana na wanaweza hata kujiua kabisa.
Binti huyu kwa sasa ni mke wa mtu na nilipokutana nae leo alinichekesha
baada ya kunikumbusha yale ya kipindi kile na nilimuuliza sababu ya
kunipa kile kibuti na aliniambia kuwa mimi mwenyewe ndio nilisababisha
kwa kuonesha nampenda kupita kiasi.
Mnaweza kuona kuwa kuna cha kujifunza za hapo kuhusu hawa wadada.
Wewe una kipi unakumbuka kuhusu kibuti cha nyakati hizo ambacho
kilikupelekesha na ambacho ulijifunza?