MAMA YANGU ADUI YANGU -37-
ILIPOISHIA:
Ilikuwa baada ya kupoteza fahamu kwa siku mbili, kilichositisha kuzikwa kwangu ni joto la mwili ambalo wazee walisema wanaweza kunizika nikiwa bado hai.
Baada ya hapo sikuelewa kilichokuwa kikiendelea mpaka niliposhtuka pale nilipopiga chafya mfululizo.
Nilipofumbua macho nilijikuta sehemu ambayo haikuwa ngeni lakini bado sikuwa na uhakika nayo.
Nilipojaribu kunyanyuka nilishindwa, nilipojipapasa bado nilikuwa mifupa mitupu. Kutokana na harufu niliyokuwa nikiisikia nilijua pale ni kwa mganga.
Nilijiuliza kwa nini wamenipeleka tena kwa mganga ikiwa tulikubaliana nisubiri mauti yangu. Nikiwa bado katikati ya mawazo kwa nje ya chumba nilichokuwa nimelala, nilisikia sauti ya watu wakizungumza nje ya chumba.
SASA ENDELEA...
Nilisikia sauti ya mama akizungumza na sauti nyingine ambayo ilinishtua. Ilikuwa ya mtu ninayemfahamu lakini nilijua labda zinafanana na nyingine ilinishtua zaidi ilikuwa kama ya mama Amina mganga aliyenitibu mwanzo.
Nilimsikia akizungumza:
"Mmesikia chafya atakuwa amerudiwa na fahamu."
"Hata mimi nimesikia."
"Mmh! Akipona nitashukuru," nilimsikia mama akisema.
"Tumuombe Mungu, lakini mwanao yote kayataka mwenyewe, nilimueleza arudi akadharau. Wagonjwa wengi wakipata nafuu huwa hawajali kumalizia tiba na kujiona wapo sawa matokeo yake ugonjwa unamrudia tena kwa kazi kubwa kwa vile vita inakuwa mara mbili."
"Hakuniambia, kama angenieleza haya mapema ningemleta pengine hata ujauzito wake usingetoka."
"Nilimwambia arudi niufunge lakini akadharau matokeo yake ni haya. Lakini nakuhakikishia Mwaija atatembea na kurudia katika hali yake ya kawaida."
"Kweli?" mama aliuliza.
"Tatizo alilonalo likitoka mbona mwanao mzima, hilo nina uhakika wa kulitoa."
Nilishangaa kusikia mganga akijiamini kupita kiasi, kwani hata mganga wa Yombo alisema hivyo lakini mwisho wa siku alichemka.
"Ngoja nikamuangalie."
Baada ya kimya cha dakika chache nilisikia sauti za nyayo za miguu zikija ndani.
Nilitulia nikitizama juu kwa vile sikuwa na nguvu ya kujigeuza, nilivyolazwa ndivyo nilivyolala.
Baada ya muda nilisikia nikiitwa.
"Mwaija."
"Abee," niliitikia.
Baada ya kuitikia aliyeniita alisogea karibu yangu ndipo nilipomtambua vizuri kuwa ni mama Amina.
"Pole."
Badala ya kuitikia nilianza kulia, mama Amina alinibembeleza:
"Mwaija utapona japo umechelewa sana."
Lakini kumbe sikuwa nalia kwa maumivu bali aibu ya kumkimbia baada ya kupata ujauzito na kuondoka bila kurudi, pia kuwa muongo kwa niliyomuahidi.
"Silii hilo dada."
"Unalia nini?"
"Nimekuwa muongo na hii ndiyo adhabu yangu."
"Hebu achana na hayo, naomba nikupe uji wa dawa kwa vile sasa hivi huwezi kula chakula kigumu ili niendelee na tiba yako."
"Sawa."
Mama Amina alitoka na kuniacha nikiwa na maswali mengi, huku nikijiuliza ni nani aliyenipeleka kwake.
Baada ya muda alirudi na bakuli la uji akiwa ameongozana na mama pamoja na da' Suzy hapo ndipo nilipojua aliyenileta kwa mama Amina ni da' Suzy.
Nilijikuta nikisahau ugonjwa wangu na kutabasamu baada ya kumuona da' Suzy japokuwa niliamini sura yangu ilikuwa kama ya mzee kutokana na kukonda kwa ugonjwa.
"Mwaija," da Suzy aliniita
"Abee."
"Pole mdogo wangu."
"Sijapoa."
"Utapona tu dada."
"Mmh! Nitashukuru japokuwa imani yangu imekuwa ndogo sana."
"Mwaija kwa uwezo wa Mungu utapona tu mdogo wangu," mama Amina alinipa moyo.
Walisaidiana kunikalisha kisha nilipewa uji uliochanganywa na dawa. Japokuwa nilikuwa mgonjwa niliweza kuunywa wote uliokuwa kwenye bakuli.
Baada ya kunywa waliniacha nipumzike kwa muda. Baada ya muda nilifuatwa na kutolewa nje, ilionesha ni majira ya jioni inayokimbilia usiku kutokana na kigiza kuanza kuimeza nuru ya mchana.
Kama kawaida nilitolewa kwa kubebwa, ilikuwa yataka moyo kwani kila aliyenishika alishika mifupa. Nilitolewa uani na kulazwa kwenye mkeka.
Nilielezwa natolewa mdudu (jini) niliyetupiwa, kazi ya kumtoa ilianza mara moja.
Nilipewa dawa ya maji ambayo nilielezwa ni miti zaidi ya nane iliyokuwa imechangwanywa pamoja.
Baada ya kunywa nilianza kujisikia vibaya tumbo likaanza kunichanganya na kusikia kichefuchefu. Nilianza kutapika lakini hakuna kilichotoka nilipoanza kujigogoa, mama Amina alikuja na kuingiza vidole mdomoni kwangu kama anatafuta kitu na kukitoa kwa kukwangua.
Aliingiza vidole mpaka kwenye koromeo na kukwangua na kutoa vitu kama malenda na kusema anatoka. Sikuelewa anatoka nani, aliendelea kufanya vile na kutupa nje yale malenda.
Alifanya vile zaidi ya mara tano kisha alisema:
"Lilikuwa limeanza kukomaa lakini bahati nzuri limetoka lote."
Bado sikuelewa lilikuwa limekomaa nini. Baada ya muda nilipewa uji wa dawa ambao ulinifanya niharishe mpaka nguvu ziliniishia. Mauti niliyaona mbele yangu, baada ya zoezi lile nilirudishwa ndani.
Kutokana na mshikemshike nilioupitia usingizi mzito ulinichukua.
Niliamshwa usiku sana na kupewa ndizi zilizopondwa na kulazimishwa kula japo mwili haukuwa na nguvu hata kidogo.
Baada ya kula nilirudi kitandani kulala. Siku ya pili niliamshwa na kupewa uji wa dawa na kupumzika. Majira ya saa nne nilipata kifungua kinywa cha nguvu. Nilishangaa siku ile nilikula vizuri.
Mama Amina aliniambia mdudu aliyekuwa akinisumbua ametoka. Japokuwa nilikuwa naumwa lakini nilikuwa na uwezo wa kuzungumza.
"Mdudu ndiyo nini?"
"Jini ulilotupiwa."
"Unamaanisha limetoka?" sikuamini.
"Ndiyo."
"Mbona yule mganga wa mwanzo alisema limetoka na kupata nafuu lakini matatizo yalizidi?"
"Hakumtoa."
"Alifanya nini?"
"Alimpoza, waganga wengi huwapoza tu lakini hawawatoi."
"Kwa hiyo wewe umemtoa?"
"Ndiyo."
"Hatarudi tena?"
"Ndiyo."
"Kwa hiyo nimepona."
"Kwa vile kilichokuwa kikikumaliza tumekitoa nina imani sasa hivi afya yako itaimarika."
Kauli ya mama Amina niliiamini kwa asilimia ndogo sana, niliamini alikuwa akinitia moyo tu. Ajabu mwili wangu ulikuwa
mwepesi tofauti na siku za nyuma ambapo nilikuwa nikiusikia kuwa mzito kama nimebebeshwa mzigo, hata kuhema
kwangu kulikuwa kwa shida lakini baada ya zoezi lile nilihema vizuri.
Nilikaa kwa mama Amina kwa siku kadhaa huku nikiendelea kutumia dawa zake. Alinieleza jini nililotupiwa lilitaka kufanya
viungo vyangu kupooza, kama ningechelewa mwili mzima ungekufa ganzi na kupooza kabisa.
Je nini kitaendelea? Fuatilia Jumapili ijayo